Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ishi Ukifikiria ya Kesho

Ishi Ukifikiria ya Kesho

Ishi Ukifikiria ya Kesho

“MSIHANGAIKE kamwe juu ya kesho,” akasema Yesu Kristo katika mahubiri yake ya mlimani huko Galilaya ambayo yanayojulikana sana. Kulingana na tafsiri ya Union Version, Yesu aliongezea hivi: “Kesho itajisumbukia yenyewe.”—Mathayo 6:34.

Je, unajua maneno, “kesho itajisumbukia yenyewe” yanamaanisha nini? Je, yanadokeza kwamba unapaswa kuishi kwa ajili ya leo tu na kupuuza ya kesho? Je, kweli hilo linapatana na mambo ambayo Yesu na wafuasi wake waliamini?

“Acheni Kuhangaika”

Soma simulizi hilo lote la Yesu katika Mathayo 6:25-32. Kwa sehemu Yesu alisema hivi: “Acheni kuhangaika juu ya nafsi zenu kuhusu kile mtakachokula au kile mtakachokunywa, au juu ya miili yenu kuhusu kile mtakachovaa. . . . Waangalieni kwa makini ndege wa mbinguni, kwa sababu hawapandi mbegu au kuvuna au kukusanya ghalani; na bado Baba yenu wa mbinguni huwalisha wao. . . . Ni nani kati yenu kwa kuhangaika anaweza kuongeza kipimo cha mkono mmoja kwenye uhai wake? Pia, katika lile jambo la mavazi, kwa nini mnahangaika? Jifunzeni kwa mayungiyungi ya shamba, jinsi yanavyokua; hayafanyi kazi, wala hayasokoti . . . Kwa hiyo msihangaike kamwe na kusema, ‘Tutakula nini?’ au, ‘Tutakunywa nini?’ au, ‘Tutavaa nini?’ Kwa maana vyote hivi ndivyo vitu ambavyo mataifa yanafuatilia kwa tamaa. Kwa maana Baba yenu wa mbinguni anajua mnahitaji vitu hivi vyote.”

Yesu anamalizia sehemu hiyo ya mahubiri yake kwa kutoa mashauri mawili. Shauri la kwanza ni hili: “Basi, endeleeni kuutafuta kwanza ufalme [wa Mungu] na uadilifu wake, nanyi mtaongezewa hivi vitu vingine vyote.” La pili ni hili: “Kwa hiyo, msihangaike kamwe juu ya kesho, kwa maana kesho itakuwa na mahangaiko yake yenyewe. Unatosha kila siku ubaya wake.”—Mathayo 6:33, 34.

Baba Yenu Anajua Mnachohitaji

Je, unafikiri kwamba Yesu alikuwa akiwavunja moyo wanafunzi wake, kutia ndani wakulima ili ‘wasipande mbegu, wasivune, au wasikusanye mazao yao katika maghala’? Au alikuwa akiwavunja moyo ‘wasifanye kazi na wasisokote’ mavazi waliyohitaji? (Methali 21:5; 24:30-34; Mhubiri 11:4) Bila shaka hapana. Ikiwa wangeacha kufanya kazi ni wazi kwamba wangekosa chakula na mavazi na hivyo ‘wangeombaomba wakati wa mavuno.’—Methali 20:4.

Namna gani kuhusu kuhangaika? Je, Yesu alimaanisha kwamba wasikilizaji wake hawangehangaika kamwe? Hilo halingepatana na akili. Hata Yesu mwenyewe alihangaika na kufadhaika sana kihisia usiku ambao alikamatwa.—Luka 22:44.

Yesu alikuwa akitaja tu ukweli fulani wa msingi. Kuhangaika kupita kiasi hakuwezi kamwe kukusaidia kutatua matatizo yoyote uliyo nayo. Kwa mfano, hakuwezi kurefusha maisha yako. Yesu alisema kwamba kuhangaika hakuwezi ‘kuongeza kipimo cha mkono mmoja kwenye uhai wako.’ (Mathayo 6:27) Kwa kweli, kuna uwezekano mkubwa kwamba kuhangaika sana kwa muda mrefu kunaweza kupunguza uhai wako.

Shauri lake lilikuwa na faida kubwa. Kwa vyovyote vile, mambo mengi ambayo tunahangaikia hayatukii kamwe. Mwanasiasa wa Uingereza Winston Churchill alitambua hilo kuhusu kipindi chenye kuhuzunisha cha Vita vya Pili vya Ulimwengu. Aliandika hivi kuhusu mahangaiko fulani aliyokuwa nayo wakati huo: “Ninapofikiria mahangaiko hayo yote ninakumbuka hadithi ya mzee fulani ambaye muda mfupi kabla ya kufa alisema kwamba alikuwa na mahangaiko mengi sana maishani, na mambo mengi aliyohangaikia hayakutukia kamwe.” Kwa kweli, ni jambo la hekima kushughulikia matatizo yanayotokea, hasa tunapopata shida na matatizo ambayo yanaweza kutuletea mahangaiko makubwa.

‘Endeleeni Kuutafuta Kwanza Ufalme wa Mungu’

Kwa kweli, Yesu alikuwa akifikiria mambo mengi zaidi ya hali ya kimwili na ya kihisia ya wasikilizaji wake. Alijua kwamba kuhangaikia mahitaji ya lazima ya maisha, na pia tamaa inayopita kiasi ya vitu vya kimwili na raha, inaweza kutuzuia tusikazie fikira mambo yaliyo ya maana zaidi. (Wafilipi 1:10) Huenda ukauliza, ‘Ni nini cha maana kuliko kupata mahitaji ya lazima ya maisha?’ Ni mambo ya kiroho ambayo yanahusiana na ibada tunayomtolea Mungu. Yesu alikazia kwamba jambo kuu katika maisha yetu linapaswa kuwa ‘kuendelea kuutafuta kwanza ufalme wa Mungu na uadilifu wake.’—Mathayo 6:33.

Katika siku za Yesu, watu wengi walikuwa wakitafuta kwa bidii vitu vya kimwili. Jambo kuu zaidi katika maisha yao lilikuwa kujikusanyia mali. Hata hivyo, Yesu aliwahimiza wasikilizaji wake wawe na mtazamo tofauti. Wakiwa watu waliojiweka wakfu kwa Mungu, ‘wajibu wao wote’ ulikuwa ‘kumwogopa Mungu wa kweli na kushika amri zake.’—Mhubiri 12:13.

Wasikilizaji wake wangeangamia kiroho kwa sababu ya kujishughulisha sana na vitu vya kimwili, yaani, kuwa na “mahangaiko ya mfumo huu wa mambo na nguvu za udanganyifu wa utajiri.” (Mathayo 13:22) Mtume Paulo aliandika hivi: “Wale ambao wameazimia kuwa matajiri huanguka katika jaribu na mtego na tamaa nyingi za kijinga na zenye kudhuru, ambazo hutumbukiza watu katika maangamizi na uharibifu.” (1 Timotheo 6:9) Ili kuwasaidia waepuke “mtego” huo, Yesu aliwakumbusha wafuasi wake kwamba Baba yao wa mbinguni alijua kwamba walihitaji vitu hivyo vyote. Mungu angewatunza kama vile tu anavyowatunza “ndege wa mbinguni.” (Mathayo 6:26, 32) Badala ya kuruhusu mahangaiko yawalemee, walipaswa kujitahidi kadiri walivyoweza kutimiza mahitaji yao na kisha kuacha mambo mikononi mwa Yehova wakiwa na uhakika.—Wafilipi 4:6, 7.

Yesu aliposema “kesho itajisumbukia yenyewe,” alimaanisha tu kwamba hatupaswi kuruhusu mahangaiko yasiyo ya lazima kuhusu mambo ambayo yanaweza kutokea kesho yaongeze matatizo yetu ya leo. Maneno yake yametafsiriwa hivi katika tafsiri nyingine ya Biblia: “Msihangaike kuhusu kesho; itakuwa na mahangaiko yake ya kutosha. Hakuna haja ya kuongeza matatizo ya kila siku.”—Mathayo 6:34, Today’s English Version.

“Ufalme Wako na Uje”

Hata hivyo, kuna tofauti kubwa kati ya kutohangaikia kesho kupita kiasi na kupuuza kesho kabisa. Yesu hakuwatia moyo kamwe wanafunzi wake wapuuze ya kesho. Kinyume chake, aliwahimiza wapendezwe sana na wakati ujao. Inafaa wasali kwa ajili ya mahitaji waliyo nayo, yaani, kuhusu mkate wao wa kila siku. Lakini kwanza wanapaswa kusali kwa ajili ya mambo ya wakati ujao, yaani, kusali Ufalme wa Mungu uje na mapenzi ya Mungu yatendeke duniani.—Mathayo 6:9-11.

Hatupaswi kuwa kama watu wa siku za Noa. Walijishughulisha sana na ‘kula na kunywa, wanaume wakioa na wanawake wakiolewa’ hivi kwamba “hawakujali” mambo ambayo yalikuwa yakija. Matokeo yalikuwa nini? “Gharika ikaja na kuwafagilia mbali wote.” (Mathayo 24:36-42) Mtume Petro alitumia tukio hilo la kihistoria kutukumbusha uhitaji wa kuishi tukifikiria mambo ya kesho. Aliandika hivi: “Kwa kuwa hivyo vitu vyote vitayeyushwa jinsi hiyo, ninyi mnapaswa kuwa watu wa namna gani katika matendo matakatifu ya mwenendo na vitendo vya ujitoaji-kimungu, mkingojea na kuweka karibu akilini kuwapo kwa siku ya Yehova!”—2 Petro 3:5-7, 11, 12.

Wekeni Hazina Mbinguni

Ndiyo, acheni ‘tuweke karibu akilini’ siku ya Yehova. Hilo litakuwa na uvutano mkubwa juu ya jinsi tunavyotumia wakati, nguvu, vipawa, mali, na uwezo wetu. Hatupaswi kujishughulisha sana kufuatia vitu vya kimwili, iwe ni mahitaji ya lazima au raha za maisha, hivi kwamba hatuna wakati wa kutosha wa kutenda matendo ya “ujitoaji-kimungu.” Huenda tukapata faida sasa tukikazia fikira mambo ya leo tu, lakini kwa kweli faida hizo zitakuwa za muda mfupi tu. Yesu alisema kwamba ni jambo la hekima zaidi ‘kujiwekea wenyewe hazina mbinguni’ badala ya duniani.—Mathayo 6:19, 20.

Yesu alikazia jambo hilo katika mfano wake kuhusu mtu ambaye alifanya mipango mikubwa sana ya wakati ujao. Mipango yake haikutia ndani uhitaji wa kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Mungu. Shamba la mtu huyo lilizaa sana. Akaamua kubomoa maghala yake na kujenga maghala makubwa zaidi ili aishi maisha ya starehe, ale, anywe, na kujifurahisha. Tatizo lake lilikuwa nini? Alikufa bila kufurahia matunda ya kazi yake. Hata hivyo, jambo baya hata zaidi ni kwamba hakuwa amejenga uhusiano pamoja na Mungu. Yesu alimalizia hivi: “Ndivyo huwa kwa mtu anayejikusanyia mwenyewe hazina lakini si tajiri kwa Mungu.”—Luka 12:15-21; Methali 19:21.

Unaweza Kufanya Nini?

Usifanye kosa lililofanywa na mtu ambaye Yesu alizungumza juu yake. Tafuta kusudi la Mungu kuhusu wakati ujao, na uishi kupatana nalo. Mungu hajawaacha wanadamu gizani wasijue la kufanya. Amosi, nabii wa kale, aliandika hivi: “Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova hatafanya lolote isipokuwa awe amewafunulia watumishi wake manabii jambo lake la siri.” (Amosi 3:7) Leo, unaweza kupata mambo ambayo Yehova amefunua kupitia manabii wake katika Biblia, ambayo ni Neno lake lililoandikwa kwa mwongozo wa roho.—2 Timotheo 3:16, 17.

Biblia inafunua tukio fulani litakalotukia hivi karibuni ambalo litabadili dunia yote kwa njia isiyo na kifani. Yesu alisema: ‘Kutakuwa na dhiki kuu ya namna ambayo haijapata kutukia tangu mwanzo wa ulimwengu mpaka sasa.’ (Mathayo 24:21) Hakuna mwanadamu anayeweza kuzuia tukio hilo. Kwa kweli, waabudu wa kweli hawana sababu yoyote ya kutaka kulizuia. Kwa nini? Kwa sababu tukio hilo litaondoa uovu wote duniani, na litafuatwa na “mbingu mpya na dunia mpya,” yaani, serikali mpya ya kimbingu na jamii mpya ya kidunia. Katika ulimwengu huo mpya, Mungu “atafuta kila chozi kutoka katika macho [ya watu], na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena.”—Ufunuo 21:1-4.

Basi je, si jambo linalopatana na akili kuchunguza kwa makini yale ambayo Biblia inasema kuhusu tukio hilo? Je, unahitaji msaada wa kufanya hivyo? Waombe Mashahidi wa Yehova wakusaidie. Au waandikie wachapishaji wa gazeti hili. Fanya yote uwezayo kuhakikisha kwamba unaishi si kwa ajili ya leo tu bali pia kwa ajili ya wakati ujao utakaokuwa mzuri ajabu.

[Picha katika ukurasa wa 7]

“Msihangaike kamwe . . . Kesho itakuwa na mahangaiko yake yenyewe”