Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Isikie Sauti Inayotoka Ndani

Isikie Sauti Inayotoka Ndani

Isikie Sauti Inayotoka Ndani

‘Watu wa mataifa wasio na sheria ya Mungu wanafanya kwa asili mambo ya sheria.’—WAROMA 2:14.

1, 2. (a) Watu wengi wametenda jinsi gani kwa sababu ya kuwajali wengine? (b) Ni mifano gani ya Kimaandiko inayoonyesha jinsi watu fulani walivyowajali wengine?

MWANAMUME mmoja mwenye umri wa miaka 20 na aliye na ugonjwa wa kifafa alianguka kwenye reli ya gari-moshi la chini ya ardhi. Mtu mmoja alipoona hilo aliwaachilia mabinti wake, akaruka na kumvuta mtu huyo mwenye kifafa kwenye nafasi iliyo katikati ya reli hiyo, kisha akajilaza juu yake ili kumlinda asikanyagwe na gari-moshi lililopita juu yao. Watu fulani wangemwita mwokoaji huyo shujaa, lakini yeye alisema hivi: “Unapaswa kufanya mambo mazuri. Nilifanya hivyo kwa sababu ya fadhili. Sikufanya hivyo ili nitambuliwe au kusifiwa.”

2 Labda unajua mtu fulani ambaye alihatarisha maisha yake ili kuwasaidia wengine. Watu wengi walifanya hivyo wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu kwa kuwaficha wageni. Pia, kumbuka yale yaliyompata mtume Paulo na watu wengine 275 meli yao ilipovunjika huko Malta, karibu na Sisili. Wenyeji wa huko waliwasaidia wageni hao kwa kuwaonyesha “fadhili za kibinadamu zisizo za kawaida.” (Matendo 27:27–28:2) Na namna gani yule msichana Mwisraeli ambaye labda hakuwa akihatarisha uhai wake, lakini alihangaikia kwa fadhili afya ya mmoja wa Wasiria ambao walikuwa wamemshika mateka? (2 Wafalme 5:1-4) Pia, fikiria mfano wa Yesu unaojulikana sana kuhusu Msamaria mwema. Kuhani na Mlawi walimpuuza Myahudi mwenzao aliyekuwa karibu kufa. Hata hivyo, Msamaria mmoja alijitahidi isivyo kawaida ili kumsaidia. Mfano huo umegusa mioyo ya watu wa tamaduni mbalimbali kwa muda wa karne nyingi.—Luka 10:29-37.

3, 4. Hisia za kuwajali wengine zinahusiana jinsi gani na nadharia ya mageuzi?

3 Ni kweli kwamba tunaishi katika “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo”; watu wengi ni “wakali” na “wasiopenda wema.” (2 Timotheo 3:1-3) Hata hivyo, je, hatujaona watu wakitenda kwa fadhili, na labda hata sisi wenyewe kufaidika kutokana na matendo hayo? Mwelekeo wa kuwasaidia wengine, hata kwa hasara ya kibinafsi, umeenea sana leo hivi kwamba watu fulani wanauita mwelekeo huo “ubinadamu.”

4 Mwelekeo huo wa kuwa tayari kuwasaidia wengine hata kwa hasara ya kibinafsi unaonekana katika jamii na tamaduni zote, na unapinga dai la kwamba mwanadamu anaongozwa na kanuni ya kwamba unapaswa kutimiza kwanza mahitaji yako mwenyewe, yaani, “viumbe bora ndio wanaosalimika.” Francis S. Collins, mtaalamu wa chembe za urithi ambaye aliongoza jitihada za serikali ya Marekani za kuelewa chembe za urithi za mwanadamu (DNA au ADN), alisema hivi: “Kuwajali wengine bila ubinafsi ni tatizo kubwa kwa mwana-mageuzi. . . . Sifa hiyo haipatani na wazo la kwamba tunachochewa na chembe za urithi zenye ubinafsi.” Pia, alisema: “Watu fulani wanajitolea wenyewe kuwasaidia wale ambao si wa jamii yao na ambao hawana uhusiano wowote nao. . . . Inaonekana kwamba sifa ya kuwajali wengine haiwezi kufafanuliwa na nadharia ya Darwin.”

“Sauti ya Dhamiri”

5. Ni jambo gani ambalo limeonekana mara nyingi kwa watu?

5 Dakt. Collins anaonyesha sababu moja inayotufanya tuwajali wengine: “Sauti ya dhamiri ndiyo inayotuamuru tuwasaidie wengine hata ikiwa hatupati faida yoyote.” * Neno “dhamiri” linalotajwa na Collins huenda likatukumbusha jambo hakika ambalo mtume Paulo alisema: “Wakati watu wa mataifa wasio na sheria wanapofanya kwa asili mambo ya sheria, watu hawa, ijapokuwa hawana sheria, wao ni sheria kwao wenyewe. Wao ndio wanaoonyesha kuwa yaliyomo katika sheria yameandikwa ndani ya mioyo yao, huku dhamiri yao ikiwatolea ushahidi na, katikati ya fikira zao wenyewe, wanashtakiwa au hata kutetewa.”—Waroma 2:14, 15.

6. Kwa nini watu wote watatozwa hesabu na Muumba?

6 Katika barua yake kwa Waroma, Paulo alionyesha kwamba wanadamu watatozwa hesabu na Mungu kwa sababu kuwapo Kwake na sifa Zake zinaonekana wazi kupitia mambo yanayoonekana. Hilo limekuwa hivyo “tangu kuumbwa kwa ulimwengu na kuendelea.” (Waroma 1:18-20; Zaburi 19:1-4) Ni kweli kwamba watu wengi wanampuuza Muumba wao na wanafuatia mwenendo mpotovu maishani. Hata hivyo, Mungu anataka wanadamu watambue uadilifu wake na kutubu matendo yao mabaya. (Waroma 1:22–2:6) Wayahudi walikuwa na sababu nzuri ya kufanya hivyo kwa kuwa walipewa Sheria ya Mungu kupitia Musa. Lakini hata watu ambao hawakuwa na “maneno matakatifu ya Mungu,” walipaswa kutambua kwamba kuna Mungu.—Waroma 2:8-13; 3:2.

7, 8. Hisia ya haki imeenea kadiri gani, na hilo linaonyesha nini?

Sababu yenye kusadikisha zaidi inayopasa kuwafanya watu wote wamtambue Mungu na kutenda kupatana na uhakika huo ni uwezo wao wa ndani wa kutambua mema na mabaya. Hisia yetu ya haki inaonyesha kwamba tuna dhamiri. Fikiria hili: Watoto fulani wanapanga mstari wakingojea kubembea. Kisha, mtoto mmoja anawaruka wengine na kwenda mbele, huku akiwapuuza wale wanaongojea. Watoto wengi wanasema hivi, ‘Hiyo si haki!’ Sasa jiulize, ‘Kwa nini hata watoto wanaonyesha kwa kawaida kwamba wana hisia ya haki?’ Kufanya hivyo kunaonyesha kwamba wana uwezo wa ndani wa kutambua yaliyo sawa kiadili. Paulo aliandika: “Wakati watu wa mataifa wasio na sheria wanapofanya kwa asili mambo ya sheria.” Hakusema, “Iwapo,” kana kwamba jambo hilo lilitukia mara chache. Alisema “wakati,” ili kumaanisha kwamba jambo hilo linatukia mara nyingi. Hivyo, watu ‘wanafanya kwa asili mambo ya sheria’ katika maana ya kwamba wanachochewa na uwezo wao wa ndani wa kiadili kutenda kulingana na yale tunayosoma katika sheria ya Mungu iliyoandikwa.

8 Mwelekeo huo wa kiadili unaonekana katika nchi nyingi. Profesa mmoja wa Chuo Kikuu cha Cambridge aliandika kwamba viwango vya Wababiloni, Wamisri, Wagiriki, na pia Wenyeji wa Asili wa Australia na Wenyeji wa Asili wa Amerika vilitia ndani “sheria zinazoshutumu ukandamizaji, uuaji, hila, na udanganyifu, viwango vilevile kuhusu fadhili kwa waliozeeka, vijana, na walio dhaifu.” Na Dakt. Collins aliandika hivi: “Inaonekana kwamba wazo la mema na mabaya limeenea ulimwenguni pote miongoni mwa wanadamu wa aina zote.” Je, hilo halikukumbushi andiko la Waroma 2:14?

Dhamiri Yako Inafanya Kazi Jinsi Gani?

9. Dhamiri ni nini, na inaweza kukusaidia jinsi gani kabla hujatenda jambo fulani?

9 Biblia inaonyesha kwamba dhamiri ni uwezo wa ndani wa kuona na kuchanganua matendo yako. Ni kana kwamba sauti kutoka ndani yako inakuambia ikiwa tendo fulani ni sawa au si sawa. Paulo alisema hivi kuhusu sauti hiyo iliyokuwa ndani yake: “Dhamiri yangu inanitolea ushahidi katika roho takatifu.” (Waroma 9:1) Kwa mfano, huenda sauti hiyo ikasema kabla hujafanya uamuzi wa jambo lililo sawa au lisilo sawa kiadili. Huenda dhamiri yako ikakusaidia kuamua jambo fulani la wakati ujao na kukuonyesha jinsi ungejihisi ikiwa ungelifanya.

10. Mara nyingi dhamiri inafanya kazi kwa njia gani?

10 Kwa kawaida, dhamiri yako inatenda kazi baada ya wewe kufanya jambo fulani. Alipokuwa akimkimbia Mfalme Sauli, Daudi alipata nafasi ya kutenda jambo fulani lisilo la heshima kuelekea mfalme mtiwa-mafuta wa Mungu, naye alitenda hivyo. Baadaye, “moyo wa Daudi ukaendelea kumchoma.” (1 Samweli 24:1-5; Zaburi 32:3, 5) Neno “dhamiri” halitumiwi katika simulizi hilo; lakini hivyo ndivyo Daudi alivyohisi kwa sababu ya dhamiri yake. Vivyo hivyo, sote tumewahi kusumbuliwa na dhamiri. Tulifanya jambo fulani, na kisha tukafadhaika na kuvurugika kwa sababu ya namna tulivyotenda. Watu fulani ambao hawakulipa kodi walisumbuliwa na dhamiri yao hivi kwamba baadaye walilipa madeni yao. Wengine wamechochewa kuungama kwa wenzi wao wa ndoa dhambi yao ya uzinzi. (Waebrania 13:4) Hata hivyo, mtu anapotenda kulingana na dhamiri, anaweza kuridhika na kupata amani.

11. Kwa nini inaweza kuwa hatari ‘kuiacha tu dhamiri yako ikuongoze’? Toa mfano.

11 Basi, je, tunaweza tu ‘kuiacha dhamiri yetu ituongoze’? Ni vizuri kuisikiliza dhamiri yetu, lakini sauti yake inaweza kutudanganya kabisa. Ndiyo, sauti ya “mtu tuliye kwa ndani” inaweza kutudanganya. (2 Wakorintho 4:16) Fikiria mfano mmoja. Biblia inasema kuhusu Stefano, mfuasi mshikamanifu wa Kristo aliyekuwa “amejaa neema na nguvu.” Wayahudi fulani walimtupa Stefano nje ya Yerusalemu nao wakamuua kwa kumpiga kwa mawe. Sauli (ambaye baadaye alikuja kuwa mtume Paulo) alisimama karibu na “alikuwa akikubaliana na kuuawa” kwa Stefano. Inaonekana Wayahudi hao walisadiki kabisa kwamba walikuwa wakitenda yaliyo sawa na dhamiri yao haikuwasumbua. Haikosi kwamba Sauli pia alisadiki hivyo kwa sababu baada ya hapo, alikuwa “bado akiwatisha wanafunzi wa Bwana na akitaka kuwaua.” Kwa wazi, wakati huo dhamiri yake haikutoa sauti iliyo sahihi.—Matendo 6:8; 7:57–8:1; 9:1.

12. Huenda dhamiri yetu ikafinyangwa kwa njia gani moja?

12 Ni nini ambacho huenda kiliifinyanga dhamiri ya Sauli? Jambo moja linaweza kuwa uhusiano wake wa karibu pamoja na wengine. Wengi wetu wamezungumza kwenye simu na mtu ambaye sauti yake inafanana sana na ya baba yake. Kwa kadiri fulani huenda mtu huyo amerithi sauti hiyo, lakini huenda pia ameiga njia ya baba yake ya kuzungumza. Vivyo hivyo, huenda Sauli alifinyangwa na uhusiano wake wa karibu pamoja na Wayahudi ambao walimchukia Yesu na kupinga mafundisho yake. (Yohana 11:47-50; 18:14; Matendo 5:27, 28, 33) Ndiyo, huenda marafiki wa Sauli waliifinyanga sauti aliyosikia ndani yake, yaani, dhamiri yake.

13. Mazingira ya mtu yanaweza kufinyanga dhamiri yake jinsi gani?

13 Pia, dhamiri inaweza kufinyangwa na utamaduni au mazingira ambamo mtu anaishi, kama vile uvutano wa mazingira unavyoweza kumwongoza mtu kuzungumza kwa matamshi au kwa lugha fulani. (Mathayo 26:73) Huenda ilikuwa hivyo kuwahusu Waashuru wa kale. Walijulikana kwa nguvu zao za kijeshi, na kwenye mawe yao yaliyochongwa wanaonyeshwa wakiwatesa mateka wao. (Nahumu 2:11, 12; 3:1) Waninawi wa siku za Yona walisemekana kuwa wasiojua “tofauti kati ya mkono wao wa kuume na wa kushoto.” Hilo linamaanisha kwamba hawakuwa na viwango sahihi vya kuamua yaliyo sawa au yasiyo sawa machoni pa Mungu. Fikiria jinsi ambavyo mazingira hayo yangekuwa na uvutano juu ya dhamiri ya mtu aliyelelewa Ninawi! (Yona 3:4, 5; 4:11) Vivyo hivyo leo, dhamiri ya mtu inaweza kufinyangwa na mtazamo wa watu wanaomzunguka.

Kuboresha Sauti Iliyo Ndani

14. Dhamiri yetu inaonyesha jinsi gani yale yanayosemwa kwenye Mwanzo 1:27?

14 Yehova aliwapa Adamu na Hawa zawadi ya dhamiri, nasi tulirithi dhamiri yetu kutoka kwao. Andiko la Mwanzo 1:27 linatueleza kwamba wanadamu wamefanywa kwa mfano wa Mungu. Hilo halimaanishi kwamba tunafanana na Mungu kimwili, kwa sababu Mungu ni roho na sisi tuna mwili wa nyama. Tumefanywa kwa mfano wa Mungu katika maana ya kwamba tuna sifa zake ndani yetu, kutia ndani ufahamu wa maadili pamoja na dhamiri inayotenda kazi. Ukweli huo unaonyesha njia moja ambayo tunaweza kuitia nguvu dhamiri yetu, na hivyo kuifanya iwe yenye kutegemeka zaidi. Njia hiyo ni kujifunza zaidi kuhusu Muumba, na kumkaribia zaidi.

15. Tunaweza kufaidika kwa njia gani moja tukimjua Baba yetu?

15 Biblia inaonyesha kwamba katika maana fulani Yehova ni Baba yetu sisi sote. (Isaya 64:8) Wakristo waaminifu, iwe wanatumaini kwenda mbinguni au kuishi duniani katika paradiso, wanaweza kumwita Mungu kuwa Baba. (Mathayo 6:9) Tunapaswa kutamani kumkaribia zaidi Baba yetu na hivyo kujifunza maoni yake na viwango vyake. (Yakobo 4:8) Watu wengi hawataki kufanya hivyo. Wao ni kama Wayahudi ambao Yesu aliwaambia hivi: “Ninyi hamjasikia sauti yake wakati wowote wala kuona umbo lake; nanyi hamna neno lake likikaa ndani yenu.” (Yohana 5:37, 38) Hatujawahi kusikia sauti halisi ya Mungu. Hata hivyo, tunaweza kujua jinsi anavyofikiri kwa kusoma neno lake na hivyo kuwa kama yeye na kuhisi kama anavyohisi.

16. Simulizi kumhusu Yosefu linaonyesha nini kuhusu kuizoeza na kuifuata dhamiri yetu?

16 Simulizi kumhusu Yosefu akiwa katika nyumba ya Potifa linaonyesha jambo hilo. Mke wa Potifa alijaribu kumtongoza Yosefu. Ingawa aliishi wakati ambapo vitabu vya Biblia havikuwa vimeandikwa na Amri Kumi hazikuwa zimetolewa, Yosefu alisema hivi: “Ninawezaje kufanya ubaya huu mkubwa na kwa kweli nimtendee Mungu dhambi?” (Mwanzo 39:9) Watu wa familia yake waliishi mbali naye, kwa hiyo hakusema hivyo ili awafurahishe. Alitaka hasa kumpendeza Mungu. Yosefu alijua kiwango cha Mungu kuhusu ndoa, yaani, mwanamume mmoja kwa mwanamke mmoja, wote wawili wakiwa “mwili mmoja.” Na inaelekea alipata habari kuhusu jinsi Abimeleki alivyohisi alipojua kwamba Rebeka alikuwa ameolewa, yaani, ingekuwa vibaya kumchukua na hivyo kuleta hatia juu ya watu wake. Ndiyo, Yehova alibariki matokeo ya kisa hicho, na hivyo akaonyesha maoni yake kuhusu uzinzi. Inaelekea kwamba kujua matukio yote hayo ya wakati uliopita kuliitia nguvu dhamiri ya Yosefu, na kumchochea kukataa upotovu wa maadili katika ngono.—Mwanzo 2:24; 12:17-19; 20:1-18; 26:7-14.

17. Inapohusu kuwa kama Baba yetu, kwa nini tuko katika hali nzuri zaidi kuliko Yosefu?

17 Bila shaka, leo tuko katika hali nzuri zaidi kuliko Yosefu. Tuna Biblia nzima ambamo tunaweza kujifunza mawazo na hisia za Baba yetu, kutia ndani mambo anayokubali na yale anayokataza. Kadiri tunavyojua Maandiko, ndivyo tutakavyomkaribia zaidi Mungu na kuwa kama yeye. Tukifanya hivyo, inaelekea sihi za dhamiri yetu zitapatana hata zaidi na mawazo ya Baba yetu. Sihi hizo zitapatana hata zaidi na mapenzi ya Baba yetu.—Waefeso 5:1-5.

18. Ingawa huenda tulifinyangwa kwa njia mbalimbali wakati uliopita, tunaweza kufanya nini ili dhamiri yetu iwe yenye kutegemeka?

18 Namna gani kuhusu dhamiri yetu kufinyangwa na mazingira? Huenda tumefinyangwa na maoni na matendo ya watu wetu wa ukoo na pia mazingira ambamo tulilelewa. Hivyo, huenda dhamiri yetu imenyamazishwa au kupotoshwa. Au huenda dhamiri yetu ilifuata maoni ya wengine. Ni kweli kwamba hatuwezi kubadili mambo tuliyofanya zamani. Hata hivyo, tunaweza kuazimia kuchagua marafiki na mazingira ambayo yatakuwa na uvutano mzuri juu ya dhamiri yetu. Hatua muhimu ni kushirikiana kwa ukawaida na Wakristo wenye kujitoa ambao wamejitahidi kwa muda mrefu kuwa kama Baba yao. Mikutano ya kutaniko, kutia ndani kushirikiana na wengine kabla na baada ya mikutano hiyo, kunatupa nafasi nzuri sana za kufanya hivyo. Tunaweza kuona jinsi Wakristo wenzetu wanavyofikiri na kutenda kupatana na Biblia, na pia utayari wao wa kuisikiliza dhamiri yao inapoonyesha maoni na njia za Mungu. Baada ya muda, hilo linaweza kutusaidia kuipatanisha dhamiri yetu na kanuni za Biblia, na hivyo kutufanya tumwige Mungu zaidi na zaidi. Tunapoipatanisha sauti yetu ya ndani na kanuni za Baba yetu na kufuata mfano mzuri wa Wakristo wenzetu, dhamiri yetu itakuwa yenye kutegemeka zaidi na tutakuwa na mwelekeo zaidi wa kusikiliza yale inayosema.—Isaya 30:21.

19. Ni mambo gani yanayohusu dhamiri ambayo yanastahili uangalifu?

19 Hata hivyo, wengine wanapambana kila siku ili watende kulingana na dhamiri yao. Habari inayofuata itachunguza hali fulani ambazo Wakristo wamepambana nazo. Kwa kuchunguza hali kama hizo, huenda tukaelewa zaidi kazi ya dhamiri, kwa nini dhamiri zinaweza kutofautiana, na jinsi tunavyoweza kuisikiliza zaidi sauti ya dhamiri yetu.—Waebrania 6:11, 12.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Vivyo hivyo, Owen Gingerich, profesa wa utafiti wa elimu ya nyota kwenye Chuo Kikuu cha Harvard, aliandika hivi: “Kwa kweli, huenda kuwajali wengine kukatokeza swali ambalo . . . haliwezi kujibiwa kisayansi kutokana na uchunguzi wa wanyama. Huenda ikawa kwamba jibu linalosadikisha zaidi linatokana na chanzo kingine na linahusiana na sifa za ubinadamu ambazo tumepewa na Mungu, zinazotia ndani dhamiri.”

Umejifunza Nini?

• Kwa nini uwezo wa kutambua yaliyo sawa na yasiyo sawa, au dhamiri, unapatikana katika tamaduni zote?

• Kwa nini tunahitaji kuwa waangalifu kuhusu kuiacha tu dhamiri yetu ituongoze?

• Taja njia fulani zinazoweza kutusaidia kuboresha sauti tunayosikia kutoka ndani yetu.

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 23]

Daudi alisumbuliwa na dhamiri . . .

lakini Sauli wa Tarso hakusumbuliwa

[Picha katika ukurasa wa 24]

Tunaweza kuizoeza dhamiri yetu