Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Uishi kwa Ajili ya Leo Tu?

Je, Uishi kwa Ajili ya Leo Tu?

Je, Uishi kwa Ajili ya Leo Tu?

“SIFIKIRII kamwe wakati ujao. Unafika haraka sana.” Inasemekana kwamba mwanasayansi maarufu Albert Einstein ndiye aliyesema maneno hayo yanayonukuliwa mara nyingi. Watu wengi wana maoni kama hayo. Huenda wakauliza: “Kwa nini uhangaikie wakati ujao?” Au labda umewasikia watu wakisema mambo kama vile: “Endelea na maisha yako.” “Ishi kwa ajili ya leo.” “Sahau ya kesho.”

Bila shaka, mtazamo huo ambao ni wa kawaida, si mpya. “Ule, unywe, na ujifurahishe. Mambo mengine yote hayana maana.” Huo ndio uliokuwa mwito wa Waepikurea wa kale. Watu fulani walioishi katika siku za mtume Paulo walikuwa na maoni kama hayo. Walionelea hivi: “Na tule na tunywe, kwa maana kesho tutakufa.” (1 Wakorintho 15:32) Waliamini kwamba maisha haya mafupi ndiyo maisha pekee tuliyo nayo, kwa hiyo, wakaeneza wazo la kwamba tunapaswa kufurahia kabisa maisha haya.

Kwa mamilioni ya watu duniani, bila shaka kufurahia kabisa maisha haya hakumaanishi kuponda raha. Hali ngumu za leo zinafanya maisha ya wengi yawe magumu sana, nao wanajitahidi kufa na kupona ili waendelee kuishi. Kwa nini wafikirie ya “kesho” au ya wakati ujao ambao mara nyingi unaonekana kuwa wenye giza na usio na tumaini lolote?

Je, Tufanye Mipango kwa Ajili ya Kesho?

Hata watu walio katika hali ambazo si ngumu sana mara nyingi hawaoni faida ya kufanya mipango kwa ajili ya kesho. Huenda wakauliza, “Kwa nini tujisumbue?” Wengine wanaweza kudai kwamba wale wanaofanya mipango mwishowe wanavunjika moyo na kukata tamaa. Hata Ayubu, mzee wa ukoo wa nyakati za kale alikata tamaa sana alipoona mipango yake ‘ikivunjika,’ na hivyo akapoteza vitu ambavyo vingemletea yeye na familia yake wakati ujao wenye furaha.—Ayubu 17:11; Mhubiri 9:11.

Robert Burns, mtungaji wa mashairi Mskoti, alilinganisha hali yetu na hali ya panya mdogo wa shambani. Bila kutazamia, Burns aliharibu nyumba ya panya huyo kwa jembe la kukokotwa. Panya huyo alikimbia ili kujiokoa wakati makao yake yalipoharibiwa. Mtungaji huyo wa mashairi alifikiri hivi: ‘Ndiyo, mara nyingi tunajikuta tukiwa hoi kabisa tunapokabili hali zinazopita uwezo wetu hivi kwamba hata mipango mizuri sana mara nyingi haifanikiwi kamwe.’

Basi je, ni ubatili kufanya mipango kwa ajili ya wakati ujao? Ukweli ni kwamba kukosa kufanya mipango ya kutosha kunaweza kusababisha hasara kubwa sana wakati vimbunga au misiba mingine ya asili inapotokea. Ni kweli kwamba hakuna mtu ambaye angeweza kuzuia Kimbunga Katrina. Lakini je, utambuzi na mipango mizuri ya mapema haingepunguza sana hasara ambayo kimbunga hicho kilisababisha katika jiji na kwa wakaaji wake?

Una maoni gani? Je, kweli ni jambo linalopatana na akili kuishi kwa ajili ya leo tu na kupuuza ya kesho? Chunguza yale ambayo habari inayofuata inasema kuhusu jambo hilo.

[Picha katika ukurasa wa 3]

“Ule, unywe, na ujifurahishe. Mambo mengine yote hayana maana”

[Picha katika ukurasa wa 4]

Je, utambuzi na mipango haingepunguza hasara iliyosababishwa na Kimbunga Katrina?

[Hisani]

U.S. Coast Guard Digital