Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuisikiliza Dhamiri Yako

Kuisikiliza Dhamiri Yako

Kuisikiliza Dhamiri Yako

“Vitu vyote ni safi kwa watu safi. Lakini kwa watu waliotiwa unajisi na wasio na imani hakuna kitu chochote kilicho safi.” —TITO 1:15.

1. Paulo alijihusisha jinsi gani na makutaniko ya Krete?

BAADA ya mtume Paulo kumaliza safari tatu za umishonari, alikamatwa na mwishowe akapelekwa Roma, ambako alifungwa gerezani kwa miaka miwili. Alifanya nini alipowekwa huru? Wakati fulani, Paulo alitembelea kisiwa cha Krete akiwa pamoja na Tito, naye akamwandikia Tito hivi: “Nilikuacha wewe Krete, ili uyarekebishe mambo yaliyokuwa na kasoro na uweke rasmi wanaume wazee.” (Tito 1:5) Mgawo wa Tito ulihusu suala la dhamiri.

2. Tito alipaswa kushughulikia tatizo gani katika kisiwa cha Krete?

2 Paulo alimshauri Tito kuhusu sifa za kustahili za wazee wa kutaniko, kisha akaonyesha kwamba kuna “watu wengi watundu, wanaoongea maneno yasiyo na faida, na wanaodanganya akili za watu.” Watu hao walikuwa ‘wakiharibu nyumba nzima-nzima kwa kufundisha mambo ambayo hawakupaswa kufundisha.’ Tito alipaswa ‘kuendelea kuwakaripia.’ (Tito 1:10-14; 1 Timotheo 4:7) Paulo alisema kwamba akili na dhamiri za watu hao zilikuwa ‘zimetiwa unajisi,’ akitumia maneno hayo katika maana ya kutia doa, kama vile nguo nzuri inavyoweza kutiwa doa na rangi. (Tito 1:15) Huenda wengine kati ya watu hao walikuwa na malezi ya Kiyahudi, kwa kuwa ‘walishikamana na tohara.’ Leo makutaniko hayapotoshwi na watu walio na maoni kama hayo. Hata hivyo, tunaweza kujifunza mengi kuhusu dhamiri kutokana na mashauri ambayo Paulo alimpa Tito.

Wale Walio na Dhamiri Iliyotiwa Unajisi

3. Paulo alimwandikia Tito nini kuhusu dhamiri?

3 Ona ni katika hali gani Paulo alitaja neno dhamiri. “Vitu vyote ni safi kwa watu safi. Lakini kwa watu waliotiwa unajisi na wasio na imani hakuna kitu chochote kilicho safi, bali akili zao na pia dhamiri zao zimetiwa unajisi. Wao hutangaza hadharani kwamba wanamjua Mungu, lakini humkana kwa matendo yao.” Kwa wazi, watu fulani walioishi wakati huo walihitaji kufanya mabadiliko ili “wawe na afya katika imani.” (Tito 1:13, 15, 16) Walikuwa na tatizo la kutofautisha kati ya mambo yaliyokuwa safi na yale ambayo hayakuwa safi, na hilo lilihusisha dhamiri yao.

4, 5. Ni kasoro gani ambazo watu wengine walikuwa nazo katika makutaniko, na hilo lilikuwa na matokeo gani juu yao?

4 Zaidi ya miaka kumi mapema, baraza linaloongoza la Kikristo lilifikia uamuzi wa kwamba waabudu wa kweli hawakuwa tena chini ya takwa la kutahiriwa, na wakayajulisha makutaniko uamuzi huo. (Matendo 15:1, 2, 19-29) Hata hivyo, watu wengine huko Krete walikuwa bado ‘wanashikamana na tohara.’ Walipinga waziwazi maamuzi ya baraza linaloongoza, ‘wakifundisha mambo ambayo hawakupaswa kufundisha.’ (Tito 1:10, 11) Wakiwa na maoni yaliyopotoka, huenda walitetea masharti ya Sheria ya Musa kuhusu vyakula na usafi wa kidesturi. Na huenda hata waliongezea yale ambayo Sheria ilisema, kama walivyofanya watangulizi wao katika siku za Yesu, na pia walitetea hadithi zisizo za kweli za Wayahudi na amri za wanadamu.—Marko 7:2, 3, 5, 15; 1 Timotheo 4:3.

5 Maoni hayo yalikuwa na matokeo mabaya juu ya maamuzi yao na ufahamu wao wa maadili, yaani, dhamiri yao. Paulo aliandika hivi: “Kwa watu waliotiwa unajisi na wasio na imani hakuna kitu chochote kilicho safi.” Dhamiri zao zilipotoshwa sana hivi kwamba hazingeweza tena kutegemeka katika kuwaongoza kutenda na kuchanganua mambo. Zaidi ya hayo, waliwahukumu Wakristo wenzao katika mambo ya kibinafsi, mambo ambayo Mkristo angeweza kufanya uamuzi unaotofautiana na wa mwingine. Kuhusiana na hilo, Wakrete hao walikuwa wakiona mambo yaliyo safi kuwa najisi. (Waroma 14:17; Wakolosai 2:16) Walidai kwamba wanamjua Mungu, lakini matendo yao yalionyesha kwamba hawakumjua.—Tito 1:16.

“Safi kwa Watu Safi”

6. Paulo alitaja vikundi gani viwili vya watu?

6 Tunaweza kufaidika jinsi gani na yale ambayo Paulo alimwandikia Tito? Ona tofauti iliyopo katika maneno haya: “Vitu vyote ni safi kwa watu safi. Lakini kwa watu waliotiwa unajisi na wasio na imani hakuna kitu chochote kilicho safi, bali akili zao na pia dhamiri zao zimetiwa unajisi.” (Tito 1:15) Bila shaka, Paulo hakuwa akisema kwamba kwa Mkristo aliye safi kiadili, kila kitu ni safi na kinaruhusiwa. Tunaweza kuwa na uhakika kuhusu hilo kwa sababu Paulo alionyesha wazi katika barua nyingine kwamba mtu anayefanya uasherati, kuabudu sanamu, kuwasiliana na pepo, na kadhalika ‘hataurithi ufalme wa Mungu.’ (Wagalatia 5:19-21) Hivyo, tunapaswa kukata kauli kwamba Paulo alikuwa akizungumzia kweli ya ujumla kuhusu vikundi viwili vya watu, wale ambao ni safi kiadili na kiroho na wale ambao si safi.

7. Andiko la Waebrania 13:4 linakataza nini, lakini ni swali gani ambalo huenda likatokea?

7 Hatusemi kwamba mambo ambayo Mkristo mnyoofu anapaswa kuepuka ni yale tu ambayo Biblia inakataza moja kwa moja. Kwa mfano, fikiria maneno haya ya moja kwa moja: “Ndoa na iheshimiwe kati ya wote, na kitanda cha ndoa kiwe bila unajisi, kwa maana Mungu atawahukumu waasherati na wazinzi.” (Waebrania 13:4) Hata watu ambao si Wakristo na wale wasiojua chochote kuhusu Biblia watakata kauli inayofaa kwamba mstari huo unakataza uzinzi. Kutokana na mstari huo na mistari mingine ya Biblia, ni wazi kabisa kwamba Mungu anashutumu ngono kati ya mwanamume au mwanamke aliyefunga ndoa na mtu mwingine ambaye si mume au mke wake halali. Namna gani waseja wawili ambao wanafanya ngono ya kinywa? Matineja wengi wanadai kwamba zoea hilo halina madhara kwa sababu si ngono. Je, Mkristo anaweza kusema kwamba ngono ya kinywa ni zoea safi?

8. Kuhusiana na ngono ya kinywa, Wakristo wanatofautiana jinsi gani na watu wengi ulimwenguni?

8 Andiko la Waebrania 13:4 na la 1 Wakorintho 6:9 linaonyesha kwamba Mungu hakubali uzinzi na uasherati (Kigiriki, por·neiʹa). Uasherati unatia ndani nini? Neno la Kigiriki linatia ndani matumizi ya viungo vya uzazi iwe katika njia ya asili au kwa njia potovu kwa makusudi machafu ya ngono. Neno hilo linatia ndani mahusiano yoyote ya ngono nje ya ndoa inayopatana na Maandiko. Hivyo, por·neiʹa inatia ndani ngono ya kinywa, hata ingawa matineja wengi ulimwenguni wameambiwa au wamekata kauli kwamba ngono ya kinywa inakubalika. Wakristo wa kweli hawaachi maoni na matendo yao yaongozwe na wale “wanaoongea maneno yasiyo na faida, na wanaodanganya akili za watu.” (Tito 1:10) Wanashikamana na viwango vya juu zaidi vya Maandiko Matakatifu. Badala ya kujaribu kutetea ngono ya kinywa, wanaelewa kwamba kulingana na Maandiko ngono ya aina hiyo ni uasherati, por·neiʹa, nao wanazoeza dhamiri yao kukataa zoea hilo. *Matendo 21:25; 1 Wakorintho 6:18; Waefeso 5:3.

Sauti Mbalimbali, Maamuzi Mbalimbali

9. Ikiwa “vitu vyote ni safi,” kazi ya dhamiri ni nini?

9 Lakini Paulo alimaanisha nini aliposema kwamba “vitu vyote ni safi kwa watu safi”? Paulo alikuwa akizungumza kuhusu Wakristo ambao walikuwa wamepatanisha maoni na ufahamu wao wa kiadili na viwango vya Mungu ambavyo vinapatikana katika Neno lake lililoongozwa na roho. Wakristo kama hao wanatambua kwamba inapohusu mambo mengi yasiyokatazwa moja kwa moja na Mungu, waamini wanaweza kuwa na maamuzi yanayotofautiana. Badala ya kuwahukumu wengine, wanaviona kuwa “safi” vitu ambavyo Mungu hashutumu. Hawatazamii kwamba watu wengine wote watakuwa na maoni kama yao kuhusu mambo fulani maishani ambayo Biblia haitoi mwongozo hususa. Acheni tufikirie mifano fulani.

10. Arusi au mazishi yanaweza jinsi gani kutokeza matatizo?

10 Kuna familia nyingi ambazo zina mwenzi mmoja wa ndoa ambaye ni Mkristo, lakini mwenzi mwingine si Mkristo. (1 Petro 3:1; 4:3) Huenda hilo likatokeza matatizo mbalimbali, kama vile wakati wa arusi au mazishi ya mtu wa ukoo. Fikiria kisa cha mke Mkristo ambaye mume wake ni wa dini tofauti. Mmoja wa watu wa ukoo wa mume anataka kufunga ndoa, na arusi itafanyiwa katika kanisa. (Au mtu wa ukoo, labda mzazi, amekufa, na ibada ya mazishi itafanyiwa kanisani.) Wenzi hao wa ndoa wanaalikwa, na mume anataka mke wake aende pamoja naye. Dhamiri ya mke inasema nini kuhusu kuhudhuria arusi au mazishi hayo? Atafanya nini? Fikiria hali hizi mbili.

11. Eleza jinsi mke mmoja Mkristo anavyoweza kufikiria kuhusu kuhudhuria arusi kanisani, na anafikia uamuzi gani?

11 Loisi anatafakari kwa uzito juu ya amri hii ya Biblia, ‘Tokeni katika Babiloni Mkubwa,’ milki ya ulimwengu ya dini ya uwongo. (Ufunuo 18:2, 4) Zamani alikuwa mshiriki wa kanisa ambako arusi itafanyika na anajua kwamba wakati wa arusi hiyo watu wote wataombwa washiriki matendo ya kidini, kama vile kusali, kuimba, au kufanya ishara za kidini. Ameazimia kutoshiriki katika mambo hayo na hataki hata kuwepo ili asisukumwe kuvunja utimilifu wake. Loisi anamheshimu mume wake ambaye ndiye kichwa chake kulingana na Maandiko, na anataka kushirikiana naye. Hata hivyo, Loisi hataki kulegeza msimamo wake wa kanuni za Maandiko. (Matendo 5:29) Hivyo, kwa busara anamweleza kwamba yeye binafsi hatakwenda huko hata mume wake akiamua kwenda kwenye arusi hiyo. Anaweza kumweleza kwamba akihudhuria na kukataa kushiriki katika mambo fulani, anaweza kumwaibisha mume wake, na kwa hiyo kutohudhuria kwake ni kwa faida ya mume wake. Uamuzi wake unamfanya awe na dhamiri njema.

12. Mtu anaweza kufikiria na kutenda jinsi gani kuhusu mwaliko wa kuhudhuria arusi kanisani?

12 Ruthu anakabili tatizo linalofanana na hilo. Anamheshimu mume wake na ameazimia kuwa mshikamanifu kwa Mungu, na hivyo anatii dhamiri yake iliyozoezwa na Biblia. Baada ya kufikiria mambo kama yale ambayo Loisi alifikiria, Ruthu anasali na kuchunguza “Maswali Kutoka kwa Wasomaji” katika gazeti Mnara wa Mlinzi la Mei 15, 2002 (15/5/2002). Anakumbuka kwamba wale Waebrania watatu walitii amri ya kwenda mahali ambapo pangefanyiwa ile ibada ya sanamu. Hata hivyo, walidumisha utimilifu wao kwa kutoshiriki katika tendo la ibada ya sanamu. (Danieli 3:15-18) Anaamua kwenda pamoja na mume wake lakini hatashiriki katika matendo yoyote ya kidini, na hivyo anatenda kulingana na dhamiri yake. Kwa busara lakini waziwazi, anamweleza mume wake mambo ambayo dhamiri yake itamruhusu kufanya na yale ambayo hataweza kufanya. Ruthu anatumaini kwamba mume wake ataona tofauti kati ya ibada ya kweli na ile ya uwongo.—Matendo 24:16.

13. Kwa nini hatupaswi kushangaa Wakristo wawili wanapofanya maamuzi yanayotofautiana?

13 Je, uhakika wa kwamba huenda Wakristo wawili wakafikia maamuzi yanayotofautiana unamaanisha kuwa haidhuru yale ambayo mtu anafanya au kwamba bila shaka mmoja wao ana dhamiri dhaifu? Hapana. Huenda kwa sababu ya mambo aliyojionea wakati uliopita kuhusiana na muziki na vitu vyote vinavyohusiana na sherehe za kanisa, Loisi anatambua kwamba ni hatari kwake kuhudhuria sherehe hizo. Na kushirikiana kwake na mume wake wakati uliopita katika mambo ya kidini huenda kukawa na uvutano juu ya dhamiri yake. Hivyo, anasadiki kabisa kwamba uamuzi ambao amefanya ndio unaomfaa kabisa.

14. Wakristo wanapaswa kukumbuka nini kuhusu masuala ya uamuzi wa kibinafsi?

14 Lakini je, uamuzi wa Ruthu ulikuwa mbaya? Wengine hawana haki ya kumhukumu. Hawapaswi kumhukumu wala kumchambua kwa sababu ya kuamua kuhudhuria sherehe hiyo lakini kutoshiriki katika tendo lolote la kidini. Kumbuka shauri la Paulo juu ya maamuzi ya kibinafsi kuhusu kula au kutokula chakula fulani: “Yeye anayekula asimdharau yeye asiyekula, na yeye asiyekula asimhukumu yeye anayekula . . . Kwa bwana wake mwenyewe yeye husimama au kuanguka. Kwa kweli, atasimamishwa, kwa maana Yehova anaweza kumsimamisha.” (Waroma 14:3, 4) Bila shaka, hakuna Mkristo yeyote mnyoofu ambaye angetaka kumhimiza mtu mwingine apuuze mwongozo wa dhamiri iliyozoezwa, kwa kuwa kufanya hivyo kungekuwa kama kupuuza sauti inayoweza kutoa ujumbe wenye kuokoa uhai.

15. Kwa nini tunapaswa kufikiria kwa uzito dhamiri na hisia za wengine?

15 Tukiendelea kufikiria mfano huo, Wakristo hao wawili wanapaswa kufikiria mambo mengine. Jambo moja ni matokeo ya uamuzi wao juu ya wengine. Paulo alitushauri hivi: “Fanyeni hili kuwa uamuzi wenu, kutokuweka mbele ya ndugu kikwazo au sababu ya kujikwaa.” (Waroma 14:13) Huenda Loisi akajua kwamba hali kama hizo zimesababisha matatizo makubwa kutanikoni au katika familia yake, na labda yale anayofanya yanaweza kuwa na uvutano mkubwa juu ya watoto wake. Tofauti na hilo, huenda Ruthu anajua kwamba maamuzi kama hayo hayajasababisha matatizo katika kutaniko au katika jamii yao. Dada hao wawili, na sisi sote pia, tunapaswa kujua kwamba dhamiri iliyozoezwa vizuri inatambua matokeo ya maamuzi yetu juu ya wengine. Yesu alisema hivi: “Yeyote anayemkwaza mmoja wa hawa wadogo wanaoniamini, ingekuwa afadhali afungiwe shingoni jiwe la kusagia kama lile ambalo huzungushwa na punda na azamishwe katika bahari kuu.” (Mathayo 18:6) Mtu akipuuza uhakika wa kwamba matendo yake yanaweza kuwakwaza wengine, huenda akawa na dhamiri iliyo najisi, kama ya Wakristo fulani huko Krete.

16. Kadiri wakati unavyopita, tunaweza kutazamia Mkristo afanye mabadiliko gani?

16 Mkristo anapaswa kuendelea kukua kiroho, na hilo linahusu pia kufanya maendeleo katika kusikia na kusikiliza dhamiri yake. Acheni tufikirie mfano wa Marko, aliyebatizwa hivi karibuni. Dhamiri yake inamwambia akatae mazoea yake ya zamani ambayo hayakupatana na Maandiko. Labda yanatia ndani ibada ya sanamu au matumizi ya damu. (Matendo 21:25) Kwa kweli, kwa sasa anaepuka kabisa hata vitu ambavyo vinafanana kidogo sana na mambo ambayo Mungu anakataza. Kwa upande mwingine, anashangaa kwa nini wengine wanakataa vitu fulani ambavyo yeye anaona kuwa vinakubalika, kama vile vipindi fulani vya televisheni.

17. Toa mfano ambao unaonyesha jinsi wakati na maendeleo ya kiroho yanavyoweza kuwa na matokeo juu ya dhamiri na maamuzi ya Mkristo.

17 Kadiri wakati unavyopita, ujuzi wa Marko unaongezeka naye anamkaribia Mungu zaidi. (Wakolosai 1:9, 10) Kunakuwa na matokeo gani? Sauti yake ya ndani inazoezwa kwa kadiri kubwa zaidi. Sasa Marko ana mwelekeo wa kusikiliza zaidi dhamiri yake na kufikiria kwa uzito kanuni za Kimaandiko. Kwa kweli, anatambua kwamba baadhi ya vitu “vinavyofanana kidogo” na vile alivyokuwa akikataa havipingani na maoni ya Mungu. Zaidi ya hayo, kwa kuwa amejipatanisha zaidi na kanuni za Biblia na yuko tayari kusikiliza dhamiri yake iliyozoezwa vizuri, sasa Marko anachochewa na dhamiri yake kuepuka vipindi ambavyo hapo zamani alifikiri kwamba vinakubalika. Ndiyo, dhamiri yake imesafishwa.—Zaburi 37:31.

18. Tuna sababu gani ya kushangilia?

18 Katika makutaniko mengi, kuna watu ambao wamefikia hatua mbalimbali za ukomavu wa Kikristo. Wengine wao ni wapya katika imani. Labda dhamiri yao haisemi sana juu ya mambo fulani, lakini inasema kwa sauti kubwa kuhusu mambo mengine. Huenda watu kama hao wanahitaji wakati na msaada ili kujipatanisha na mwongozo wa Yehova na kusikiliza dhamiri yao iliyozoezwa. (Waefeso 4:14, 15) Hata hivyo, inaelekea kwamba katika makutaniko hayohayo, kuna wengi walio na ujuzi mwingi, uzoefu wa kutumia kanuni za Biblia, na dhamiri inayopatana sana na maoni ya Mungu. Ni shangwe kama nini kuwa kati ya “watu safi” kama hao ambao wanaviona kuwa “safi” kiadili na kiroho vitu ambavyo vinakubalika machoni pa Bwana! (Waefeso 5:10) Basi sote na tujiwekee mradi wa kufikia ukomavu huo na kudumisha dhamiri kama hiyo kupatana na ujuzi sahihi wa ile kweli na ujitoaji-kimungu.—Tito 1:1.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 8 Gazeti la Mnara wa Mlinzi la Januari 1, 1984 (1/1/1984), ukurasa wa 7-8, linatoa maelezo kwa ajili ya wale waliofunga ndoa.

Ungetoa Jibu Gani?

• Kwa nini Wakristo fulani wa Krete walikuwa na dhamiri zilizotiwa unajisi?

• Wakristo wawili walio na dhamiri zilizozoezwa vizuri wanaweza kufanya maamuzi yanayotofautiana kwa sababu gani?

• Kadiri wakati unavyopita, dhamiri yetu inapaswa iwe katika hali gani?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 26]

 

Sisili

UGIRIKI

Krete

ASIA NDOGO

Saiprasi

BAHARI YA MEDITERANIA

[Picha katika ukurasa wa 28]

Huenda Wakristo wawili wanaokabili hali ileile wakafanya maamuzi yanayotofautiana