Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kushangilia “Ushindi Pamoja na Mwana-Kondoo”

Kushangilia “Ushindi Pamoja na Mwana-Kondoo”

Kushangilia “Ushindi Pamoja na Mwana-Kondoo”

KATIKA barua aliyoandika mwaka wa 1971, Carey W. Barber alizungumzia miaka yake 50 ya kumtumikia Mungu wa kweli: “Miaka ambayo nimemtumikia Yehova imekuwa mizuri sana. Kushirikiana na watu wake; kulindwa kutokana na watenda-maovu wa ulimwengu wa Shetani; tarajio la kupata ushindi pamoja na Mwana-Kondoo, Yesu Kristo; na uthibitisho wa upendo wa Yehova, ni mambo yanayoleta amani yenye kupendeza sana na uradhi wa ndani ambao unalinda moyo na kumpa mtu tumaini hakika la ushindi wa mwisho.”

Miaka sita baadaye, Ndugu Barber, ambaye ni Mkristo mtiwa-mafuta, akawa mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova. Katika miaka 30 iliyofuata, akiwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza, aliendelea kutazamia “ushindi pamoja na Mwana-Kondoo.” Alipata ushindi huo kwa kuendelea kuwa mwaminifu mpaka alipokufa akiwa na umri wa miaka 101 mnamo Jumapili (Siku ya Yenga), Aprili 8, 2007.—1 Wakorintho 15:57.

Carey Barber alizaliwa nchini Uingereza mwaka wa 1905, naye akabatizwa huko Winnipeg, Kanada, mnamo 1921. Miaka miwili baadaye, yeye pamoja na Norman, ndugu yake pacha, walihamia Brooklyn New York ili kusaidia katika mradi fulani mpya. Wakati huo, watu wa Yehova walikuwa karibu kuanza kuchapisha vitabu vyao wenyewe vya kueneza habari njema ya Ufalme “katika dunia yote inayokaliwa.” (Mathayo 24:14) Moja ya migawo ya kwanza kabisa ya Ndugu Barber ulikuwa kuendesha mashini ndogo ya kuchapishia. Vitu vilivyochapishwa vilitia ndani taarifa fupi za kisheria za kesi zilizokuwa zikipelekwa katika Mahakama Kuu ya Marekani. Baada ya muda, Ndugu Barber alifanya kazi katika Idara ya Utumishi, akishughulikia masuala ya makutaniko na kazi ya kuhubiri nchini kote.

Akiwa na uzoefu huo, Ndugu Barber alikuwa na sifa za kustahili alipowekwa kuwa mwangalizi anayesafiri mnamo 1948, ili kuyatembelea makusanyiko na makutaniko kotekote katika eneo la magharibi la Marekani. Alisema kwamba alifurahia hasa kuwa nje kwenye hewa safi katika huduma ya shambani. Mgawo huo uliwawezesha ndugu na dada wengi kufahamiana na Ndugu Barber. Akili yake makini na bidii yake katika huduma ilifaa sana baadaye alipohudhuria darasa la 26 la Shule ya Gileadi (Watchtower Bible School of Gilead). Akiwa katika shule hiyo, alifahamiana na Sydney Lee Brewer, mwanafunzi kutoka Kanada. Baada ya kuhitimu walioana, na fungate yao ilikuwa safari fupi waliyofunga kwenda kuyatembelea makutaniko katika eneo la Chicago, Illinois. Dada Barber alithibitika kuwa mwandamani mwenye thamani sana na alimtegemeza sana mume wake katika makumi mawili ya miaka katika huduma ya kusafiri.

Wale waliopata nafasi ya kukutana na Ndugu Barber na waliomfahamu katika makumi ya miaka aliyotumikia akiwa mwangalizi wa wilaya na wa mzunguko, na katika miaka 30 aliyotumia akifanya kazi na kusafiri akiwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza, wataendelea kukumbuka hotuba zake na maelezo yake machangamfu. Tuna sababu nyingi za kushangilia ‘ushindi wake pamoja na Mwana-Kondoo.’