Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Fedha Ni Yangu, Na Dhahabu Ni Yangu”

“Fedha Ni Yangu, Na Dhahabu Ni Yangu”

“Fedha Ni Yangu, Na Dhahabu Ni Yangu”

KATIKA karne ya sita K.W.K., Koreshi, mfalme wa Uajemi, aliwaweka huru watu wa Mungu kutoka utekwani huko Babiloni. Maelfu walirudi Yerusalemu ili kujenga upya hekalu la Yehova ambalo lilikuwa magofu. Hali za kiuchumi za wale waliorudi zilikuwa mbaya, na majirani wenye uadui walipinga kazi hiyo ya ujenzi. Hivyo, wajenzi wengine walijiuliza ikiwa kwa kweli wangemaliza mradi huo muhimu sana.

Kupitia nabii Hagai, Yehova aliwahakikishia wajenzi hao kwamba alikuwa pamoja nao. Mungu alisema hivi: “Nitayatikisa mataifa yote, navyo vitu vyenye kutamanika vya mataifa yote vitaingia; nami nitaijaza nyumba hii utukufu.” Kuhusu mahangaiko ya kiuchumi ya wajenzi, Hagai alitoa ujumbe huu: “‘Fedha ni yangu, na dhahabu ni yangu,’ asema Yehova wa majeshi.” (Hagai 2:7-9) Katika muda wa miaka mitano baada ya Hagai kusema maneno hayo yenye kutia moyo, mradi huo ulikamilishwa.—Ezra 6:13-15.

Pia, maneno hayo ya Hagai yamewachochea watumishi wa Mungu katika nyakati za hivi karibuni wanapoanzisha miradi mikubwa inayohusiana na ibada ya Yehova. Katika mwaka wa 1879 mtumwa mwaminifu na mwenye busara alianza kuchapisha gazeti hili, ambalo wakati huo liliitwa Zion’s Watch Tower and Herald of Christ’s Presence. Wakati huo gazeti hili lilikuwa na maneno yafuatayo: “Tunaamini kwamba gazeti ‘Zion’s Watch Tower’ linategemezwa na YEHOVA, na maadamu hivyo ndivyo ilivyo halitawaomba watu wala kuwasihi kamwe walitegemeze. Yule anayesema: ‘Dhahabu yote na fedha ya milimani ni yangu,’ atakaposhindwa kutoa pesa zinazohitajiwa, tutajua kwamba huo ndio wakati wa kusimamisha uchapishaji wa gazeti hili.”

Uchapishaji wa gazeti hilo haujasimamishwa kamwe. Nakala 6,000 za toleo la kwanza zilichapishwa katika Kiingereza tu. Leo, wastani wa kila toleo ni nakala 28,578,000, katika lugha 161. * Wastani wa kila toleo la gazeti la Amkeni! ambalo linatolewa pamoja na Mnara wa Mlinzi, ni nakala 34,267,000, katika lugha 81.

Mashahidi wa Yehova wana miradi mbalimbali ambayo ina kusudi lilelile kama la Mnara wa Mlinzi, yaani, kumtukuza Yehova akiwa Bwana Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu wote na kutangaza habari njema ya Ufalme wake. (Mathayo 24:14; Ufunuo 4:11) Usadikisho ambao Mashahidi wanao leo ni kama ule uliokuwa katika gazeti hili mwaka wa 1879. Wanaamini kwamba Mungu anategemeza kazi yao na kwamba pesa zitaendelea kupatikana kwa ajili ya miradi ambayo anabariki. Hata hivyo, kazi za Mashahidi wa Yehova zinagharimiwa kwa njia gani mbalimbali? Na wana miradi ya aina gani ya kuhubiri habari njema ulimwenguni pote?

Kazi Inagharimiwa kwa Njia Gani?

Wanapohubiri hadharani, ni jambo la kawaida kwa Mashahidi wa Yehova kuulizwa na watu swali hili: “Je, mnalipwa ili kufanya kazi hii?” Jibu ni hapana, hawalipwi. Wanatumia wakati wao bila malipo. Waeneza-injili hao wanatumia saa nyingi kuzungumza na wengine kumhusu Yehova na ahadi za Biblia kwa ajili ya wakati ujao ulio bora zaidi kwa sababu wanachochewa na shukrani. Wanathamini yale ambayo Mungu amewafanyia na jinsi ambavyo ujumbe wa habari njema umeboresha maisha na mtazamo wao. Kwa sababu hiyo, wanataka kushiriki mambo hayo mazuri pamoja na wengine. Kwa kufanya hivyo, wanafuata kanuni hii iliyotolewa na Yesu: “Mlipokea bure, toeni bure.” (Mathayo 10:8) Kwa kweli, tamaa yao ya kuwa mashahidi kwa ajili ya Yehova na Yesu inawachochea kutumia pesa zao wenyewe ili kushiriki na watu imani yao, hata wale wanaoishi mbali sana nao.—Isaya 43:10; Matendo 1:8.

Ukubwa wa kazi hii ya kuhubiri na mambo yanayowasaidia kuitimiza, yaani, uchapishaji, majengo ya ofisi, Majumba ya Kusanyiko, nyumba za wamishonari, na kadhalika, yanahitaji pesa nyingi sana. Pesa hizo zinatoka wapi? Pesa za kugharimia mambo yote hayo zinatoka katika michango ya hiari. Mashahidi wa Yehova hawawaombi washiriki wa kutaniko kutoa pesa ili kutegemeza kazi hizo za tengenezo, wala hawaombi malipo kwa ajili ya vichapo wanavyowapa watu. Yeyote akitaka kutoa mchango ili kutegemeza kazi yao ya elimu, Mashahidi wanafurahi kupokea mchango huo. Acheni tuchunguze yale yanayohusika katika moja tu ya jitihada zinazofanywa ili kuhubiri habari njema ulimwenguni pote, yaani, kutafsiri.

Vichapo Katika Lugha 437

Kwa miaka mingi vichapo vya Mashahidi wa Yehova vimekuwa kati ya vichapo vinavyotafsiriwa zaidi ulimwenguni. Trakti, broshua, magazeti, na vitabu vimetafsiriwa katika lugha 437. Bila shaka, kutafsiri, kama vile utendaji mwingine mbalimbali unaohusika katika kutangaza habari njema, kunahitaji uwezo mkubwa. Utaratibu wa kutafsiri unatia ndani nini?

Wachapishaji wa vichapo vya Mashahidi wa Yehova wanapokamilisha kuandika habari fulani katika Kiingereza, habari hizo zinatumwa kwa njia ya kompyuta kwa vikundi vya watafsiri ambao wamezoezwa katika sehemu mbalimbali za ulimwengu. Kila kikundi cha watafsiri kinashughulikia mojawapo ya lugha ambamo vichapo vinatolewa. Ikitegemea idadi ya vichapo wanavyotafsiri na ugumu wa lugha wanayotafsiri, yaani, lugha lengwa (kama Kiswahili), vikundi hivyo vinaweza kuwa na washiriki kati ya 5 hadi 25.

Habari iliyotafsiriwa inakaguliwa na kusahihishwa. Kusudi moja la kufanya hivyo ni kutafsiri mawazo yaliyo katika lugha ya awali kwa usahihi na waziwazi kadiri iwezekanavyo. Hiyo si kazi rahisi. Wanapotafsiri habari yenye misamiati au maneno ya kitaalamu, watafsiri na wasahihishaji wanahitaji kufanya utafiti mwingi katika lugha zote mbili, yaani, lugha chanzi (Kiingereza, au lugha nyingine kama vile Kifaransa, Kirusi, au Kihispania) na lugha lengwa ili kuhakikisha usahihi wa tafsiri. Kwa mfano, makala katika Amkeni! inapozungumzia habari ya kitaalamu au ya kihistoria, utafiti mwingi sana unahitajiwa.

Watafsiri wengi wanafanya kazi kwa wakati wote au kwa muda kwenye ofisi za tawi za Mashahidi wa Yehova. Wengine wanafanya kazi ya kutafsiri katika eneo ambako lugha lengwa inazungumzwa. Watafsiri hao hawalipwi kwa kazi wanayofanya. Watafsiri wa wakati wote wanapewa tu chumba, chakula, na kiasi kidogo cha pesa kwa ajili ya gharama zao za msingi. Ulimwenguni pote, kuna Mashahidi 2,800 hivi wanaotumika wakiwa watafsiri. Hivi karibuni, ofisi za tawi 98 za Mashahidi wa Yehova zimekuwa na vikundi vya watafsiri au zimesimamia vikundi vilivyo katika maeneo mengine. Kwa mfano, ofisi ya tawi ya Urusi peke yake inasimamia watafsiri zaidi ya 230 wanaofanya kazi kwa wakati wote au kwa muda. Watafsiri hao wanatafsiri katika lugha zaidi ya 30, kutia ndani lugha fulani ambazo hazijulikani sana nje ya eneo hilo, kama vile Kichuvashi, Kioseti, na Kiuighuri.

Kuboresha Tafsiri

Kama anavyojua mtu yeyote ambaye amejaribu kujifunza lugha nyingine, si rahisi kutafsiri kwa usahihi mawazo magumu. Kusudi ni kutafsiri kwa usahihi mambo ya hakika na mawazo ya lugha chanzi na wakati huohuo kufanya tafsiri isomeke kwa njia ya kawaida, kana kwamba iliandikwa kwanza katika lugha lengwa. Ustadi unahitajiwa ili kutimiza hilo. Inachukua miaka mingi kwa watafsiri wapya kupata ustadi huo, na Mashahidi wa Yehova wana programu yenye kuendelea ya kuwaelimisha. Nyakati nyingine walimu wanatembelea vikundi hivyo vya watafsiri ili kuvisaidia kuboresha ustadi wa kutafsiri na kutumia programu za kompyuta.

Mipango hiyo ya mazoezi ina matokeo mazuri. Kwa mfano, ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova ya Nikaragua inaripoti hivi: “Kwa mara ya kwanza, watafsiri wetu wa Miskito walizoezwa na mwalimu kutoka ofisi ya tawi ya Mexico kuhusu utaratibu na mbinu za kutafsiri. Mazoezi hayo yametokeza mabadiliko makubwa katika njia ambayo watafsiri wetu wanafanya kazi yao. Tafsiri imeboreka sana.”

Maneno Yanayogusa Moyo

Biblia na vichapo vya Biblia vinatafsiriwa katika lugha za asili za watu kwa kusudi la kugusa mioyo yao, na hilo hasa ndilo linalotukia. Katika mwaka wa 2006, Mashahidi wa Yehova nchini Bulgaria walisisimka sana wakati Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo ilipotolewa katika Kibulgaria. Ofisi ya tawi ya Bulgaria inaripoti kwamba imepokea barua nyingi za shukrani kuhusu tafsiri hiyo. Washiriki wa kutaniko moja wanasema kwamba “sasa Biblia kwa kweli inagusa mioyo yao, na si akili yao tu.” Mwanamume mmoja mzee kutoka Sofia alieleza hivi: “Nimesoma Biblia kwa miaka mingi, lakini sijawahi kamwe kusoma tafsiri ambayo ni rahisi zaidi kuelewa na inayogusa moyo kama hii.” Vivyo hivyo, huko Albania, baada ya kupokea nakala yake ya Biblia nzima ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya katika Kialbania, Shahidi mmoja mwenyeji alieleza hivi: “Neno la Mungu ni zuri kama nini katika Kialbania! Ni pendeleo kama nini Yehova kuzungumza nasi katika lugha yetu!”

Huenda ikachukua miaka mingi kwa kikundi cha watafsiri kutafsiri Biblia nzima. Lakini je, hukubali kwamba jitihada hizo zinastahili ikiwa zitawezesha mamilioni ya watu kulielewa kwelikweli Neno la Mungu kwa mara ya kwanza?

“Sisi Ni Wafanyakazi Wenzi wa Mungu”

Bila shaka, kutafsiri, ni mojawapo tu ya utendaji mwingi wa lazima ili kuhubiri habari njema kwa matokeo. Kazi ya kuandika, kuchapisha, na kusafirisha vichapo vya Biblia, na kufanya kazi nyingine nyingi za ofisi za tawi, mizunguko, na makutaniko ya Mashahidi wa Yehova, zinahitaji pesa na jitihada kubwa. Hata hivyo, watu wa Mungu ‘wanajitoa kwa hiari’ ili kutimiza kazi hizo. (Zaburi 110:3) Wanaliona kuwa pendeleo kutoa michango na wanaona kuwa heshima kwamba kwa kufanya hivyo, Yehova anawaona kuwa “wafanyakazi wenzi.”—1 Wakorintho 3:5-9.

Ni kweli kwamba yule anayesema “fedha ni yangu, na dhahabu ni yangu” hategemei misaada yetu ya kifedha ili kutimiza kazi yake. Hata hivyo, Yehova amewatukuza watumishi wake kwa kuwapa pendeleo la pekee la kushiriki katika kutakaswa kwa jina lake kupitia michango wanayotoa ili kuhubiri “kwa mataifa yote” kweli zinazookoa uhai. (Mathayo 24:14; 28:19, 20) Je, huchochewi kufanya yote uwezayo ili kutegemeza kazi hii ambayo haitafanywa tena?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Kuhusu orodha ya lugha, ona ukurasa wa 2 wa gazeti hili.

[Sanduku katika ukurasa wa 18]

“YANATUFANYA TUFIKIRI KWA UZITO”

Msichana mmoja mwenye umri wa miaka 14 aliiandikia hivi ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova ya Kamerun: “Baada ya kununua vifaa vyangu vya shule vya mwaka mzima, niliweza kuuza vitabu viwili vya mwaka uliopita kwa faranga 2,500 [dola 5 za Marekani]. Ninachanga pesa hizo na ninaongeza faranga 910 [dola 1.82 za Marekani] kutoka katika akiba yangu. Ningependa kuwatia moyo mwendelee na kazi nzuri mnayofanya. Asanteni kwa ajili ya magazeti Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Yanatufanya tufikiri kwa uzito.”

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 18]

MCHANGO WA PEKEE

Ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova ya Mexico ilipokea barua ifuatayo kutoka kwa Manuel, mwenye umri wa miaka 6, anayeishi katika Jimbo la Chiapas. Kwa kuwa hajajua kuandika, aliomba rafiki yake amwandikie. Manuel anasema hivi: “Nyanya yangu alinipa nguruwe jike. Nguruwe huyo alipozaa, nilichagua kitoto bora zaidi na ndugu wakanisaidia kukitunza. Kwa upendo mwingi, ninatuma mchango niliopata kwa kumuuza nguruwe huyo. Alikuwa na uzito wa kilo 100, na nilimuuza pesos 1,250 [dola 110 za Marekani]. Tafadhali tumieni pesa hizo kwa ajili ya Yehova.”

[Sanduku katika ukurasa wa 19]

‘TUMIENI PESA HIZO KUTAFSIRI BIBLIA’

Katika makusanyiko ya wilaya ya Mashahidi wa Yehova ya mwaka wa 2005 huko Ukrainia, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo ilitolewa katika lugha ya Ukrainia. Siku iliyofuata,  ujumbe huu ulipatikana ndani ya sanduku la michango: “Nina umri wa miaka tisa. Asanteni sana kwa Maandiko ya Kigiriki. Mama yetu alinipa mimi na ndugu yangu pesa hizi ili tupande basi kwenda shule. Lakini wakati hakukuwa na mvua, tulitembea kwa miguu hadi shuleni na tukahifadhi hryvnia 50 hizi [dola 10 za Marekani]. Mimi na ndugu yangu tungependa mtumie pesa hizo kutafsiri Biblia nzima katika lugha ya Ukrainia.”

[Sanduku katika ukurasa wa 20, 21]

JINSI AMBAVYO WENGINE HUTOA MICHANGO

MICHANGO KWA AJILI YA KAZI YA ULIMWENGUNI POTE

Wengi hutenga kiasi fulani cha pesa ambacho wao hutia katika masanduku ya michango yaliyoandikwa, “Michango kwa Ajili ya Kazi ya Ulimwenguni Pote—Mathayo 24:14.”

Kila mwezi, makutaniko hutuma pesa hizo kwenye ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova inayohudumia nchi yao. Pia, michango ya hiari ya pesa inaweza kutumwa moja kwa moja kwa Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania, Attention Treasurer’s Office, 25 Columbia Heights, Brooklyn, New York 11201-2483, au kwenye ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova inayohudumia nchi yenu. Hundi za benki zinapaswa kuonyesha kwamba zitalipwa kwa shirika la “Watch Tower.” Vito au vitu vingine vyenye thamani vinaweza kuchangwa pia. Barua fupi inayoonyesha kwamba vitu hivyo ni zawadi inayotolewa bila masharti inapaswa kuambatanishwa na michango hiyo.

MPANGO WA MICHANGO YENYE MASHARTI

Pesa zinaweza kuwekwa amana kwa Watch Tower ili zitumiwe kwa kazi ya ulimwenguni pote. Hata hivyo, zinaweza kurudishwa iwapo zitaitishwa. Kwa habari zaidi, tafadhali wasiliana na Ofisi ya Mweka-Hazina ukitumia anwani iliyoonyeshwa juu.

UTOAJI ULIOPANGWA

Mbali na zawadi za kifedha zinazotolewa bila masharti, kuna njia nyinginezo za kutoa kwa ajili ya kazi ya Ufalme ulimwenguni pote. Zinatia ndani:

Bima: Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania linaweza kuandikishwa kuwa shirika ambalo litafaidika kutokana na bima ya maisha, malipo ya kustaafu, au ya uzeeni.

Akiba za Benki: Akaunti za benki, hati za amana, au akiba za pesa za kustaafu za mtu mmoja-mmoja zinaweza kuwekwa amana, au kulipwa wakati wa kifo, kwa Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania, kulingana na matakwa ya benki za kwenu.

Hisa na Dhamana: Hisa na dhamana zinaweza kuchangwa kwa Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania zikiwa zawadi isiyo na masharti.

Ardhi na Nyumba: Ardhi au nyumba zinazoweza kuuzwa zinaweza kutolewa zikiwa zawadi isiyo na masharti au iliyo na masharti, yaani, mtoaji anaweza kuendelea kuishi humo hadi kifo chake. Wasiliana na ofisi ya tawi katika nchi yenu kabla ya kutoa ardhi au nyumba kama mchango.

Malipo-Mwaka: Huo ni mpango wa kutoa pesa, hisa na amana, ziwe mali za mojawapo ya mashirika yanayotumiwa na Mashahidi wa Yehova. Yule anayetoa mchango huo, au mtu fulani aliyechaguliwa na mtoaji, hupata kiasi fulani cha pesa kila mwaka maishani mwake. Mtoaji hupunguziwa kodi ya serikali mwaka ule ambao mpango huo unaanzishwa.

Wasia na Amana: Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania linaweza kuachiwa urithi wa mali au pesa kwa njia ya wasia halali, au linaweza kuandikishwa kuwa shirika ambalo litafaidika katika mkataba wa amana. Kuwa na amana inayofaidi shirika la kidini kunaweza kupunguza kwa kiasi fulani kiwango cha kodi.

Kama vile usemi “utoaji uliopangwa” unavyodokeza, ili mtu atoe michango ya aina hii anapaswa kufanya mipango hususa. Broshua yenye kichwa Charitable Planning to Benefit Kingdom Service Worldwide imetayarishwa katika Kiingereza na Kihispania ili kuwasaidia watu wanaotamani kuendeleza kazi inayofanywa na Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote kwa njia ya utoaji uliopangwa. Broshua hiyo ilichapishwa ili kuonyesha njia mbalimbali za kutoa zawadi sasa au kupitia wasia mtu anapokufa. Baada ya kusoma broshua hiyo na kushauriana na washauri wao wa mambo ya sheria au kodi, wengi wameweza kuunga mkono kazi ya kidini na ya kutoa misaada ya Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote, na kupunguziwa kodi wanapofanya hivyo. Unaweza kuomba broshua hiyo moja kwa moja kutoka kwenye Charitable Planning Office.

Ukitaka habari zaidi, unaweza kuwasiliana na Charitable Planning Office, ama kwa kuandika ama kwa kupiga simu, kwenye anwani iliyoonyeshwa chini, au unaweza kuwasiliana na ofisi ya tawi inayohudumia nchi yenu.

Charitable Planning Office

Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania

100 Watchtower Drive

Patterson, New York 12563-9204

Telephone: (845) 306-0707

[Picha katika ukurasa wa 19]

Watafsiri wa lugha ya Miskito, ofisi ya tawi ya Nikaragua