Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unatumia Kila Nafasi Kuzungumza Kuhusu Imani Yako?

Je, Unatumia Kila Nafasi Kuzungumza Kuhusu Imani Yako?

Je, Unatumia Kila Nafasi Kuzungumza Kuhusu Imani Yako?

“JE, KWELI kamili inaweza kupatikana?” Hicho ndicho kilikuwa kichwa cha mashindano ya kitaifa ya kuandika insha huko Poland. Maagizo kuhusu mashindano hayo yalisema hivi: “Hatuhitaji kweli kamili. Hakuna mtu anayehitaji kweli hiyo. Kwa vyovyote vile, hakuna kweli kamili.” Agata, mwanafunzi mwenye umri wa miaka 15 na ambaye ni Shahidi wa Yehova, aliamua kutumia nafasi hiyo kuzungumza na wengine kuhusu imani yake ya kidini.

Ili kujitayarisha kwa ajili ya mashindano hayo, Agata alisali na kuomba mwongozo wa Yehova, kisha akaanza kukusanya habari kuhusu kichwa hicho. Alipata habari inayohusiana na kichwa hicho katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Julai 1, 1995. Alinukuu swali hili linalokumbukwa sana ambalo Pontio Pilato alimuuliza Yesu: “Kweli ni nini?” (Yohana 18:38) Agata aliandika kwamba swali hilo lilionyesha mashaka, kana kwamba Pilato alikuwa akiuliza: ‘Kweli? Ni nini hiyo? Hakuna kitu kama hicho!’ Agata aliandika hivi: “Swali la Pilato linanikumbusha maagizo ya kuandika insha hii.”

Kisha, akazungumza kuhusu kusitawi kwa imani ya kwamba kweli inategemea maoni ya mtu binafsi, yaani, wazo la kwamba jambo linaloonekana kuwa la kweli kwa mtu fulani huenda lisiwe la kweli kwa yule mwingine na kwamba mawazo hayo mawili huenda yakawa “sawa.” Agata aliuliza maswali kama, “Ni nani kati yetu angethubutu kupanda ndege ikiwa hatuamini kwamba sheria za mwendo wa angani ni za kweli kabisa?” Kisha, akaelekeza kwenye Biblia, na kusema: “Kulitegemea Neno la Mungu ni jambo ambalo limethibitishwa kabisa na mambo ya hakika.” Alionyesha tumaini lake kwamba wale wanaotafuta kwa unyoofu kweli kamili watakuwa na subira inayohitajiwa ili kuipata.

Agata alishinda cheti cha pekee naye akapata nafasi ya kutoa hotuba mbele ya darasa lote. Baadhi ya wanafunzi wenzake walikubali pendekezo lake la kujifunza Biblia pamoja nao. Agata anashukuru kwamba alitumia nafasi hiyo kuzungumza na watu wengi kuhusu imani yake. Ndiyo, kuwa makini kutumia kila nafasi kuzungumza kuhusu imani yetu kunaweza kuzaa matunda. Unaweza kutumia nafasi gani kuzungumza kuhusu imani yako?