Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Jivikeni Unyenyekevu wa Akili’

‘Jivikeni Unyenyekevu wa Akili’

‘Jivikeni Unyenyekevu wa Akili’

MWANAMUME fulani alilelewa katika jiji maarufu. Alikuwa na cheo cha pekee kwa kuwa alikuwa raia wa Roma kwa kuzaliwa na inaelekea familia yao ilikuwa mashuhuri. Mwanamume huyo ni Sauli. Alikuwa amepata elimu bora zaidi katika karne ya kwanza W.K., alizungumza angalau lugha mbili, naye alikuwa mshiriki wa kikundi cha kidini cha Wayahudi kilichojulikana sana, yaani, Mafarisayo.

Hapana shaka kwamba Sauli alijifunza kuwadharau watu wa hali ya chini na kujivunia uadilifu wake mwenyewe. (Luka 18:11, 12; Matendo 26:5) Mafarisayo wenzake walijiinua juu ya watu wengine nao walipenda umashuhuri na vyeo vilivyofanya wawe maarufu. (Mathayo 23:6, 7; Luka 11:43) Inaelekea kwamba kushirikiana na watu kama hao kulimfanya Sauli awe na kiburi. Tunajua kwamba aliwatesa Wakristo kwa bidii. Miaka kadhaa baadaye, akiwa mtume Paulo, alisema kwamba hapo zamani alikuwa “mkufuru na mtesaji na mtu mwenye dharau.”—1 Timotheo 1:13.

Ndiyo, Sauli alikuja kuwa Mkristo, mtume Paulo, nao utu wake ukabadilika kabisa. Akiwa mtume Mkristo, alisema kwa unyenyekevu kwamba alikuwa “mtu mdogo kuliko aliye mdogo zaidi kati ya watakatifu wote.” (Waefeso 3:8) Alikuwa mweneza-injili mwenye mafanikio, lakini hakujisifu hata kidogo kwa sababu ya mafanikio yake. Badala yake, alimpa Mungu utukufu wote. (1 Wakorintho 3:5-9; 2 Wakorintho 11:7) Paulo ndiye aliyewahimiza hivi Wakristo wenzake: “Jivikeni upendo mwororo wenye huruma, fadhili, unyenyekevu wa akili, upole, na ustahimilivu.”—Wakolosai 3:12.

Je, shauri hilo linafaa katika karne yetu ya 21? Je, kuna faida ya kuwa mnyenyekevu? Je, kwa kweli unyenyekevu unaweza kuwa ishara ya nguvu?

Je, Muumba Mweza-Yote Ni Mnyenyekevu?

Mazungumzo yoyote kuhusu unyenyekevu yanapaswa kutia ndani maoni ya Mungu. Kwa nini? Kwa sababu yeye ndiye Mwenye Enzi Kuu wetu na Muumba wetu. Kinyume naye, sisi tunapaswa kutambua na kukubali mipaka yetu wenyewe. Tunamtegemea yeye. Elihu, mwanamume mwenye hekima aliyeishi zamani, alisema hivi: “Kumhusu Mweza-Yote, sisi hatujamjua; yeye ameinuliwa katika nguvu.” (Ayubu 37:23) Kwa kweli, tunanyenyekezwa tunapofikiria ulimwengu mkubwa unaotuzunguka! “Inueni macho yenu juu, mwone,” nabii Isaya anatoa mwaliko. “Ni nani ameviumba vitu hivi? Ni Yeye anayelileta jeshi lake kulingana na hesabu, ambaye zote anaziita kwa jina. Kutokana na wingi wa nguvu zenye msukumo, yeye pia akiwa hodari katika nguvu, hakuna hata moja kati ya hizo inayokosekana.”—Isaya 40:26.

Zaidi ya kuwa mweza-yote, Yehova Mungu ni mnyenyekevu. Mfalme Daudi alimwambia hivi katika sala: “Utanipa ngao yako ya wokovu, na unyenyekevu wako ndio hunifanya niwe mkuu.” (2 Samweli 22:36) Mungu ni mnyenyekevu katika maana ya kwamba anawajali na kuwaonyesha rehema wanadamu wa hali ya chini wanaojitahidi kumpendeza. Ni kana kwamba Yehova anajishusha kutoka mbinguni ili ashughulike kwa fadhili na wanadamu wanaomwogopa.—Zaburi 113:5-7.

Zaidi ya hilo, Yehova anathamini sana watumishi wake wanapokuwa wanyenyekevu. Mtume Petro aliandika hivi: “Mungu huwapinga wenye majivuno, lakini huwapa wanyenyekevu fadhili zisizostahiliwa.” (1 Petro 5:5)Mwandikaji mmoja wa Biblia alisema hivi juu ya maoni ya Mungu kuhusu kiburi: “Kila mtu mwenye kiburi moyoni ni chukizo kwa Yehova.” (Methali 16:5) Hata hivyo, unyenyekevu unaweza jinsi gani kuwa ishara ya nguvu?

Unyenyekevu Haumaanishi Nini?

Unyenyekevu si sawa na kufedheheshwa. Katika tamaduni fulani za zamani, watu walimwona mtu mnyenyekevu kuwa mtumwa, mtu wa hali ya chini, maskini, na mwenye kusikitikiwa. Kinyume na hilo, Biblia inakazia kwamba unyenyekevu wa akili unamletea mtu heshima. Kwa mfano, mwenye hekima aliandika hivi: “Matokeo ya unyenyekevu na kumwogopa Yehova ni utajiri na utukufu na uzima.” (Methali 22:4) Na tunasoma hivi katika Zaburi 138:6: “Yehova yuko juu, hata hivyo yeye humwona mnyenyekevu; lakini yeye anamjua mwenye kiburi kutoka mbali tu.”

Kuwa mnyenyekevu hakumaanishi kwamba mtu hana uwezo wowote au hajatimiza chochote. Kwa mfano, Yesu Kristo hakuwahi kamwe kukana kwamba yeye ni Mwana mzaliwa pekee wa Yehova, wala hakufanya ionekane kwamba huduma yake hapa duniani haikuwa ya maana. (Marko 14:61, 62; Yohana 6:51) Hata hivyo, Yesu alionyesha unyenyekevu kwa kumpa Baba yake utukufu na kwa kutumia nguvu zake kuwatumikia na kuwasaidia wengine badala ya kuwalemea na kuwakandamiza.

Ni Ishara ya Nguvu

Hapana shaka kwamba watu walioishi siku za Yesu Kristo walimjua “kupitia kazi zenye nguvu.” (Matendo 2:22) Lakini machoni pa watu fulani, Yesu alikuwa “mwanadamu aliye wa hali ya chini zaidi.” (Danieli 4:17) Hakuishi maisha ya kiasi tu bali pia alifundisha tena na tena umuhimu wa unyenyekevu. (Luka 9:48; Yohana 13:2-16) Hata hivyo, unyenyekevu wake haukumfanya awe dhaifu. Hakuwa na woga alipokuwa akilitetea jina la Baba yake na kutimiza huduma yake. (Wafilipi 2:6-8) Katika Biblia, Yesu anafananishwa na simba mwenye ujasiri. (Ufunuo 5:5) Mfano wa Yesu unaonyesha kwamba unyenyekevu ni ishara ya nguvu za kiadili na utu imara.

Tunapojitahidi kusitawisha unyenyekevu wa kweli, tunatambua kwamba jitihada nyingi sana zinahitajiwa ili kufanya unyenyekevu wa akili uwe njia ya maisha. Hilo linahusisha kujinyenyekeza chini ya mapenzi ya Mungu nyakati zote badala ya kufuata njia iliyo rahisi au kufuata tamaa za mwili. Ili tusitawishe unyenyekevu tunapaswa kuwa na nguvu za kiadili, kwa sababu tunahitaji kuweka kando mapendezi yetu ya kibinafsi ili tumtumikie Yehova na kuwajali wengine bila ubinafsi.

Faida za Unyenyekevu

Mtu mnyenyekevu hana kiburi au majivuno. Maandiko yanatumia maneno “unyenyekevu wa akili” ili kufafanua sifa hiyo. (Waefeso 4:2) Tunaweza kuwa na unyenyekevu wa akili tukijichanganua inavyofaa, yaani, tukichanganua nguvu na udhaifu wetu, mafanikio na makosa yetu. Paulo alitoa shauri zuri kuhusu jambo hilo alipoandika hivi: “Kila mtu hapo kati yenu asijifikirie mwenyewe zaidi kuliko ilivyo lazima kufikiri; bali kufikiri ili awe na akili timamu.” (Waroma 12:3) Wowote wanaofuata shauri hilo ni wanyenyekevu.

Pia, tunaonyesha unyenyekevu tunapotanguliza kwa unyoofu mapendezi ya wengine badala ya kutanguliza mapendezi yetu. Akiongozwa na roho, Paulo aliwahimiza hivi Wakristo: “[Msifanye] jambo lolote kwa ugomvi au kwa kujisifu, bali kwa unyenyekevu wa akili mkiwaona wengine kuwa ni bora kuliko ninyi.” (Wafilipi 2:3) Hilo lilipatana na amri ambayo Yesu aliwapa wafuasi wake: “Aliye mkubwa zaidi katikati yenu lazima awe mhudumu wenu. Yeyote yule anayejiinua atanyenyekezwa, na yeyote yule anayejinyenyekeza atainuliwa.”—Mathayo 23:11, 12.

Ndiyo, unyenyekevu wa akili unamfanya mtu ainuliwe machoni pa Mungu. Mwanafunzi Yakobo alikazia jambo hilo alipoandika hivi: “Jinyenyekezeni machoni pa Yehova, naye atawainua ninyi.” (Yakobo 4:10) Ni nani ambaye hangependa Mungu amwinue?

Kukosa unyenyekevu kumesababisha mvurugo na fujo nyingi kati ya watu na kati ya vikundi vya watu. Kwa upande mwingine, kuwa mnyenyekevu kunaleta faida. Tunaweza kupata shangwe ya kuwa na kibali cha Mungu. (Mika 6:8) Tunaweza kuwa na amani ya akili kwa sababu pana uwezekano mkubwa kwa mtu mnyenyekevu kupata furaha na uradhi kuliko mtu mwenye kiburi. (Zaburi 101:5) Mahusiano yetu na familia, marafiki, wafanyakazi wenzetu, na watu wengine yatakuwa mazuri zaidi na yenye kupendeza zaidi. Watu wanyenyekevu wanaepuka kuwaudhi wengine na kuwa wenye kudai mno, kwa kuwa kufanya hivyo kunaweza kwa urahisi kuwakasirisha watu, kuharibu mahusiano, na kusababisha kinyongo na uchungu.—Yakobo 3:14-16.

Ndiyo, kusitawisha unyenyekevu wa akili ni njia nzuri ya kudumisha mahusiano mazuri na wengine. Unaweza kutusaidia kushinda matatizo ya ulimwengu wenye roho ya ubinafsi na mashindano. Kwa msaada wa Mungu, mtume Paulo alifaulu kushinda majivuno na kiburi alichokuwa nacho hapo mwanzoni. Vivyo hivyo leo, tunapaswa kuzuia mwelekeo wowote wa kiburi au wa kufikiri kwamba sisi ni bora kuliko wengine. Biblia inaonya hivi: “Kiburi hutangulia kuanguka, na roho ya majivuno hutangulia kujikwaa.” (Methali 16:18) Tukifuata mfano na shauri la Paulo, tutaona faida ya ‘kujivika unyenyekevu wa akili.’—Wakolosai 3:12.

[Picha katika ukurasa wa 4]

Paulo alifaulu kushinda majivuno na kiburi

[Picha katika ukurasa wa 7]

Kuwa na unyenyekevu wa akili kunatusaidia kudumisha mahusiano mazuri na wengine

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 5]

Anglo-Australian Observatory/David Malin Images