Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuchunguza Ndani ya “Mambo Mazito ya Mungu”

Kuchunguza Ndani ya “Mambo Mazito ya Mungu”

Kuchunguza Ndani ya “Mambo Mazito ya Mungu”

“Roho huchunguza ndani ya mambo yote, hata mambo mazito ya Mungu.”—1 WAKORINTHO 2:10.

1. Taja baadhi ya kweli za Biblia ambazo zinaweza kumletea mwanafunzi wa Biblia shangwe kubwa.

WENGI wetu katika kutaniko la Kikristo tunaweza kukumbuka shangwe kubwa tuliyopata tulipojifunza kweli kwa mara ya kwanza. Tulijifunza kwa nini jina la Yehova ni la maana, kwa nini anaruhusu kuteseka, kwa nini watu fulani wanaenda mbinguni, na pia jinsi maisha ya wakati ujao ya wanadamu wengine waaminifu yatakavyokuwa. Huenda tulikuwa tukiisoma Biblia, lakini mambo hayo yalikuwa yamefichwa kwetu kama yalivyo kwa wanadamu wengi. Tulikuwa kama mtu anayeangalia miamba iliyo ndani ya bahari. Bila vifaa, anaweza kuona vitu vichache sana vyenye kuvutia vilivyo ndani ya maji. Lakini akiwa na miwani ya kuogelea au akiwa kwenye mashua yenye sakafu ya kioo, anasisimuka sana kuona kwa mara ya kwanza miamba yenye rangi maridadi, samaki, viumbe wanaofanana na mimea na viumbe wengine wa ajabu. Vivyo hivyo, mtu fulani alipoanza kutusaidia kuelewa Maandiko, tulianza kuchunguza kwa mara ya kwanza “mambo mazito ya Mungu.”—1 Wakorintho 2:8-10.

2. Kwa nini shangwe ya kujifunza Neno la Mungu inaweza kuendelea milele?

2 Je, tutosheke tu na ujuzi wa kijuu-juu wa kweli za Biblia? Maneno “mambo mazito ya Mungu” yanatia ndani kuelewa hekima ya Mungu ambayo Wakristo wanafunuliwa na roho takatifu, lakini ambayo imefichwa kwa wengine. (1 Wakorintho 2:7) Hekima ya Mungu haina mipaka na tunaweza kupata shangwe kubwa kwa kuichunguza! Hatutajua kamwe kila jambo kuhusu hekima ya njia za Mungu. Shangwe tuliyopata tulipojifunza kwa mara ya kwanza mafundisho ya msingi ya Biblia inaweza kuendelea milele ikiwa tutaendelea kuchunguza ndani ya “mambo mazito ya Mungu” bila kuacha.

3. Kwa nini tunahitaji kuelewa kabisa sababu za mambo tunayoamini?

3 Kwa nini tunahitaji kuelewa ‘mambo hayo mazito’? Imani yetu na uhakika wetu unatiwa nguvu tunapoelewa yale tunayoamini na kwa nini tunayaamini, yaani, msingi wa imani yetu. Maandiko yanatuambia tutumie ‘nguvu zetu za kufikiri’ ili ‘tujihakikishie wenyewe mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.’ (Waroma 12:1, 2) Kuelewa kwa nini Yehova anataka tuishi kwa njia fulani kunatia nguvu azimio letu la kumtii. Kwa hiyo, ujuzi wa “mambo mazito” unaweza kutupa nguvu za kushinda kishawishi cha kutenda matendo ya uasi-sheria na unaweza kutuchochea kuwa na “bidii kwa ajili ya kazi njema.”—Tito 2:14.

4. Kujifunza Biblia kunatia ndani nini?

4 Ni lazima tujifunze ili tuelewe mambo mazito. Hata hivyo, kujifunza si sawa na kusoma habari fulani kijuu-juu. Kunatia ndani kuchunguza habari kwa makini ili kuona jinsi inavyohusiana na mambo ambayo tayari tunajua. (2 Timotheo 1:13) Kunatia ndani kuelewa sababu za mambo yanayosemwa. Funzo la Biblia linapaswa kutia ndani kutafakari jinsi tunavyoweza kutumia yale tunayojifunza ili kufanya maamuzi yenye hekima na kuwasaidia wengine. Pia, kwa kuwa “Andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu nalo ni lenye faida,” funzo letu linapaswa kutia ndani “kila neno linalotoka katika kinywa cha Yehova.” (2 Timotheo 3:16, 17; Mathayo 4:4) Kujifunza Biblia kunaweza kuwa kazi ngumu! Lakini kunaweza pia kufurahisha, na kuelewa “mambo mazito ya Mungu” si jambo gumu sana.

Yehova Anawasaidia Wanyenyekevu Kuelewa Mambo Mazito

5. Ni nani anayeweza kuelewa “mambo mazito ya Mungu”?

5 Hata ikiwa hukufaulu shuleni na hujazoea kujifunza, usifikiri kwamba huwezi kuelewa “mambo mazito ya Mungu.” Wakati wa huduma ya Yesu duniani, Yehova hakuwafunulia watu wenye hekima na wenye akili kusudi Lake, badala yake aliwafunulia watu wasio na elimu na wa kawaida ambao walikuwa wanyenyekevu sana hivi kwamba wangeweza kufundishwa na mtumishi wa Mungu. Walionekana kama watoto walipolinganishwa na watu waliopata elimu shuleni. (Mathayo 11:25; Matendo 4:13) Kuhusu “mambo ambayo Mungu amewatayarishia wale wanaompenda,” mtume Paulo aliwaandikia hivi waamini wenzake: “Ni kwetu sisi Mungu ameyafunua kupitia roho yake, kwa maana roho huchunguza ndani ya mambo yote, hata mambo mazito ya Mungu.”—1 Wakorintho 2:9, 10.

6. Andiko la 1 Wakorintho 2:10 linamaanisha nini?

6 Roho ya Mungu inachunguza jinsi gani “ndani ya mambo yote, hata mambo mazito ya Mungu?” Badala ya kumfunulia kila Mkristo kweli kibinafsi, Yehova anatumia roho yake kuliongoza tengenezo lake, ambalo linawasaidia watu wa Mungu wenye umoja kuielewa Biblia. (Matendo 20:28; Waefeso 4:3-6) Ulimwenguni pote, makutaniko yote yanafuata programu ileile ya kujifunza Biblia. Kwa miaka mingi, makutaniko yamekuwa yakijifunza kwa undani mafundisho mbalimbali ya Biblia. Roho takatifu inaliongoza kutaniko ili liweze kuwasaidia watu wawe na mtazamo unaofaa ili waelewe “mambo mazito ya Mungu.”—Matendo 5:32.

“Mambo Mazito ya Mungu” Yanatia Ndani Nini?

7. Kwa nini watu wengi hawaelewi “mambo mazito ya Mungu”?

7 Tusifikiri kwamba ni lazima “mambo mazito” yawe mambo magumu. Watu wengi hawajui “mambo mazito ya Mungu” kwa sababu Shetani anawadanganya watu na kuwafanya wakatae msaada ambao Yehova anatoa kupitia tengenezo Lake, wala si kwa sababu ni vigumu sana kupata hekima ya Mungu.—2 Wakorintho 4:3, 4.

8. Paulo alikuwa akizungumzia mambo gani mazito katika sura ya tatu ya barua yake kwa Waefeso?

8 Sura ya tatu ya barua ya Paulo kwa Waefeso inaonyesha kwamba “mambo mazito ya Mungu” yanatia ndani kweli nyingi ambazo watu wengi wa Yehova wanaelewa vizuri sana, kama vile utambulisho wa Uzao ulioahidiwa, kuchaguliwa kwa wanadamu fulani wenye tumaini la kwenda mbinguni, na Ufalme wa Kimasihi. Paulo aliandika hivi: “Katika vizazi vingine siri hii haikujulishwa kwa wana wa binadamu kama vile ambavyo imefunuliwa sasa kwa mitume wake watakatifu na manabii kupitia roho, yaani, kwamba watu wa mataifa wawe warithi wa pamoja na viungo vyenzi vya mwili na washiriki pamoja nasi wa ahadi katika muungano na Kristo Yesu.” Paulo alisema kwamba alikuwa amepewa wajibu wa “kufanya watu waone jinsi siri takatifu inavyosimamiwa ambayo tangu wakati uliopita usio na kipimo imefichwa katika Mungu.”—Waefeso 3:5-9.

9. Kwa nini ni pendeleo kuelewa “mambo mazito ya Mungu”?

9 Pia, Paulo alieleza ni mapenzi ya Mungu kwamba ‘katika mahali pa kimbingu ijulishwe kupitia kutaniko hekima ya Mungu ya namna nyingi sana.’ (Waefeso 3:10) Malaika wanafaidika kwa kuchunguza na kuelewa hekima ya shughuli za Yehova pamoja na kutaniko la Kikristo. Tuna pendeleo kubwa kama nini kuelewa mambo ambayo yanawapendeza hata malaika! (1 Petro 1:10-12) Kisha, Paulo anasema kwamba tunapaswa kujitahidi “kufahamu kabisa akilini pamoja na watakatifu wote, upana na urefu na kimo na kina,” cha imani ya Kikristo. (Waefeso 3:11, 18) Acheni sasa tuzungumzie mifano fulani ya mambo mazito ambayo yanaweza kupanua ufahamu wetu.

Mifano ya Mambo Mazito

10, 11. Kulingana na Maandiko, Yesu alipata kuwa sehemu ya msingi ya “uzao” wa “mwanamke” wa kimbingu wa Mungu wakati gani?

10 Tunajua kwamba Yesu ndiye sehemu ya msingi ya “uzao” wa “mwanamke” wa kimbingu wa Mungu anayetajwa katika Mwanzo 3:15. Ili kuelewa zaidi jambo hilo, tunaweza kuuliza hivi: ‘Yesu alipata kuwa Uzao ulioahidiwa wakati gani? Je, ni katika maisha yake ya kabla ya kuwa mwanadamu, alipozaliwa kama mwanadamu, wakati alipobatizwa, au ni wakati alipofufuliwa?’

11 Mungu alikuwa ameahidi kwamba sehemu ya kimbingu ya tengenezo lake, linalotajwa katika unabii kuwa “mwanamke” wake, ingetokeza uzao ambao ungemponda nyoka kichwa. Lakini maelfu ya miaka ilipita, na mwanamke wa Mungu hakuwa ametokeza uzao ambao ungeweza kumharibu Shetani na kazi zake. Kwa hiyo, unabii wa Isaya unasema kwamba mwanamke huyo ni “tasa” na mwenye “kuumizwa katika roho.” (Isaya 54:1, 5, 6) Mwishowe, Yesu alizaliwa huko Bethlehemu. Lakini ni baada tu ya Yesu kubatizwa na kuzaliwa kwa roho ili kuwa mwana wa kiroho wa Mungu, ndipo Yehova alipotangaza hivi: “Huyu ni Mwanangu.” (Mathayo 3:17; Yohana 3:3) Hatimaye, sehemu ya msingi ya “uzao” wa mwanamke ilikuwa imejitokeza. Baadaye, wafuasi wa Yesu walitiwa mafuta pia na kuzaliwa kwa roho takatifu. “Mwanamke” wa Yehova ambaye kwa muda mrefu alihisi kama ‘mwanamke ambaye hakuzaa,’ angeweza mwishowe ‘kupiga vigelegele kwa shangwe.’—Isaya 54:1; Wagalatia 3:29.

12, 13. Ni maandiko gani yanayoonyesha kwamba Wakristo wote watiwa-mafuta walio duniani ndio “mtumwa mwaminifu na mwenye busara”?

12 Jambo la pili kati ya mambo mazito ambayo tumefunuliwa linahusu kusudi la Mungu la kuwachagua watu 144,000 kutoka miongoni mwa wanadamu. (Ufunuo 14:1, 4) Tunakubali fundisho la kwamba watiwa-mafuta wote wanaoishi duniani katika kipindi chochote kile wanakuwa “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” ambaye Yesu alisema kwamba angewaandalia watumishi wa nyumbani mwake “chakula” kwa wakati unaofaa. (Mathayo 24:45) Ni maandiko gani ya Biblia yanayothibitisha kwamba uelewaji huo ni sahihi? Je, inawezekana kwamba Yesu alikuwa akizungumza kwa ujumla kuhusu Mkristo yeyote ambaye anawajenga ndugu zake kwa kuwapa chakula cha kiroho?

13 Mungu aliliambia hivi taifa la Israeli: “Ninyi ni mashahidi wangu . . . mtumishi wangu ambaye nimemchagua.” (Isaya 43:10) Lakini Nisani 11 ya mwaka wa 33 W.K., Yesu aliwaambia viongozi wa Israeli kwamba Mungu alikuwa amelikataa taifa lao lisiwe mtumishi Wake. Alisema hivi: “Ufalme wa Mungu utachukuliwa kutoka kwenu na kupewa taifa lenye kuzaa matunda yake.” Yesu aliuambia hivi umati: “Tazama! Nyumba yenu mmeachiwa hali ya ukiwa.” (Mathayo 21:43; 23:38) Nyumba ya Israeli ilikuwa mtumwa wa Yehova lakini haikuwa na uaminifu wala busara. (Isaya 29:13, 14) Baadaye, siku hiyohiyo, Yesu alipouliza: “Ni nani kwa kweli mtumwa mwaminifu na mwenye busara?” ni kana kwamba alikuwa akiuliza, ‘Ni taifa gani lenye busara litakalochukua mahali pa Israeli na kuwa mtumwa mwaminifu wa Mungu?’ Mtume Petro alijibu swali hilo alipoliambia hivi kutaniko la Wakristo watiwa-mafuta: “Ninyi ni . . . ‘taifa takatifu, watu wa kuwa mali ya pekee.’” (1 Petro 1:4; 2:9) Taifa hilo la kiroho, “Israeli wa Mungu,” likawa mtumwa mpya wa Yehova. (Wagalatia 6:16) Kama vile washiriki wote wa Israeli la kale walivyokuwa “mtumwa” mmoja, ndivyo Wakristo wote watiwa-mafuta walio duniani katika kipindi chochote kile wanavyokuwa ‘mtumwa mmoja mwaminifu na mwenye busara.’ Tuna pendeleo kubwa sana la kupokea “chakula” kupitia mtumwa wa Mungu.

Unaweza Kufurahia Funzo la Kibinafsi

14. Kwa nini kujifunza Biblia badala ya kuisoma tu kunaleta shangwe zaidi?

14 Tunapopata uelewaji mpya kuhusu Maandiko, je, hatufurahi kwa sababu ya jinsi unavyotia nguvu imani yetu? Ndiyo sababu kujifunza Biblia, badala ya kuisoma tu kunaweza kuleta shangwe zaidi. Kwa hiyo, unaposoma vichapo vya Kikristo, jiulize hivi: ‘Maelezo haya yanalingana jinsi gani na ujuzi wangu kuhusu habari hii? Ninakumbuka maandiko gani mengine ya Biblia au sababu gani nyingine ambazo zinaunga mkono hoja zinazotolewa katika habari hii?’ Ikiwa unahitaji kufanya utafiti zaidi, andika swali ambalo ungependa kupata jibu, na ulifanyie utafiti katika funzo lako wakati ujao.

15. Ni miradi gani ya kujifunza unayoweza kujiwekea, na inaweza kukuletea jinsi gani faida ya kudumu?

15 Ni miradi gani ya kujifunza itakayokusaidia kuelewa mambo mapya? Kwa mfano, mradi wa kuchunguza kwa undani maagano mbalimbali ambayo Mungu amefanya kwa faida ya wanadamu utaongeza ujuzi wetu. Unaweza kuitia nguvu imani yako kwa kujifunza unabii mbalimbali kumhusu Yesu Kristo au kuchunguza mojawapo ya vitabu vya kinabii vya Biblia mstari kwa mstari. Imani yako itatiwa nguvu pia ukipitia historia ya kisasa ya Mashahidi wa Yehova kwa kutumia kitabu Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu, ikiwa kinapatikana katika lugha yenu. * Na bila shaka, kupitia “Maswali Kutoka kwa Wasomaji” ya wakati uliopita ambayo yalichapishwa katika Mnara wa Mlinzi kutakusaidia kuelewa vizuri zaidi maandiko fulani. Angalia kwa uangalifu sababu za Kimaandiko zinazotumiwa kufikia kauli fulani zinazotolewa. Kufanya hivyo kutakusaidia kuzoeza ‘nguvu zako za ufahamu’ na kusitawisha utambuzi. (Waebrania 5:14) Unapojifunza, andika habari katika Biblia yako au kwenye karatasi ili wewe na wale unaoweza kuwasaidia mpate faida ya kudumu.

Wasaidie Vijana Wafurahie Funzo la Biblia

16. Unaweza kuwasaidia jinsi gani vijana wafurahie funzo la Biblia?

16 Wazazi wanaweza kuwasaidia sana watoto wao kusitawisha hamu ya mambo ya kiroho. Usiwadharau vijana na kufikiri kwamba hawawezi kuelewa mambo mazito. Wape jambo fulani la kufanyia utafiti kwa ajili ya funzo la Biblia la familia, kisha uwaulize mambo ambayo wamejifunza. Funzo la familia linaweza pia kutia ndani vipindi vya kuwazoeza vijana kuitetea imani yao na kuthibitisha kwamba yale ambayo wamefundishwa ni ya kweli. Kwa kuongezea, unaweza kutumia broshua ‘Ona Nchi Nzuri’ * kuwafundisha kuhusu nchi zinazotajwa katika Biblia na kueleza habari mnayosoma katika usomaji wenu wa Biblia wa kila juma.

17. Kwa nini tunahitaji kuwa na usawaziko katika miradi yetu ya kujifunza Biblia kibinafsi?

17 Miradi ya kujifunza Biblia kibinafsi inaweza kusisimua sana na kuitia nguvu imani, lakini uwe mwangalifu usiruhusu miradi hiyo ikuzuie kutayarisha mikutano ya kutaniko. Mikutano ni njia nyingine ambayo Yehova anatufundisha kupitia “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” Hata hivyo, utafiti zaidi unaweza kukusaidia kutoa maelezo yenye maana mikutanoni, kwa mfano, kwenye Funzo la Kitabu la Kutaniko au wakati wa mambo makuu ya usomaji wa Biblia wa kila juma katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi.

18. Kwa nini ni muhimu kujitahidi kujifunza “mambo mazito ya Mungu”?

18 Kujifunza kwa undani Neno la Mungu kunaweza kukusaidia umkaribie Yehova. Ili kuonyesha umuhimu wa funzo kama hilo, Biblia inasema hivi: “Hekima ni ulinzi, kama vile pesa ni ulinzi; lakini faida ya ujuzi ni kwamba hekima huwahifadhi hai waliyo nayo.” (Mhubiri 7:12) Kwa hiyo, ni muhimu kujitahidi kuelewa kwa undani mambo ya kiroho. Biblia inawaahidi hivi wale wanaoendelea kutafuta: ‘Utapata kumjua Mungu.’—Methali 2:4, 5.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 15 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 16 Iliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

Je, Unaweza Kueleza?

• “Mambo mazito ya Mungu” ni mambo gani?

• Kwa nini hatupaswi kuacha kamwe kujifunza mambo mazito?

• Kwa nini Wakristo wote wanaweza kupata shangwe ya kuelewa “mambo mazito ya Mungu”?

• Unaweza kufaidika kabisa jinsi gani kwa kujua “mambo mazito ya Mungu”?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 28]

Yesu alipata kuwa Uzao ulioahidiwa wakati gani?

[Picha katika ukurasa wa 31]

Wazazi wanaweza kuwapa watoto wao habari ya kufanyia utafiti kwa ajili ya funzo la familia