Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Neno la Yehova Halikosi Kamwe Kutimia

Neno la Yehova Halikosi Kamwe Kutimia

Neno la Yehova Halikosi Kamwe Kutimia

“Halikukosa kutimia hata neno moja kati ya maneno yote mema ambayo Yehova Mungu wenu amewaambia ninyi. Yote yametimia kwenu.”—YOSHUA 23:14.

1. Yoshua alikuwa nani, na alifanya nini alipokuwa akikaribia mwisho wa maisha yake?

ALIKUWA kiongozi wa jeshi mwenye bidii na asiye na woga, mwanamume mwenye imani na utimilifu. Alitembea pamoja na Musa naye alichaguliwa moja kwa moja na Yehova ili aliongoze taifa la Israeli kutoka katika nyika yenye kutisha na kuingia katika nchi inayotiririka maziwa na asali. Mwanamume huyo mwenye kuheshimiwa sana, Yoshua, aliwatolea wanaume wazee wa Israeli hotuba ya mwisho yenye kugusa moyo alipokuwa akikaribia mwisho wa maisha yake. Bila shaka, hotuba hiyo ilitia nguvu imani ya wale waliomsikiliza. Inaweza kukutia moyo pia.

2, 3. Yoshua alipowahutubia wanaume wazee wa Israeli, Israeli lilikuwa katika hali gani, naye alisema nini?

2 Hebu wazia tukio hilo kama linavyosimuliwa katika Biblia: “Ikawa kwamba baada ya siku nyingi Yehova alipokuwa amekwisha kuwapa Israeli pumziko kutoka kwa adui zao wote kuzunguka pande zote, wakati Yoshua alipokuwa mzee na mwenye siku nyingi, ndipo Yoshua akaita Israeli wote, wanaume wao wazee na wakuu wao na waamuzi wao na maofisa wao, naye akawaambia: ‘Mimi nimekuwa mzee, siku zangu zimekuwa nyingi.’”—Yoshua 23:1, 2.

3 Yoshua aliishi wakati wenye kusisimua zaidi katika historia ya watu wa Mungu, na sasa alikuwa na umri wa miaka 110 hivi. Alikuwa amejionea matendo yenye nguvu ya Mungu, na pia alikuwa ameona ahadi nyingi za Yehova zikitimia. Hivyo, alisema hivi kwa usadikisho kamili kwa sababu ya mambo aliyojionea mwenyewe: “Mnajua vema kwa mioyo yenu yote na kwa nafsi zenu zote kwamba halikukosa kutimia hata neno moja kati ya maneno yote mema ambayo Yehova Mungu wenu amewaambia ninyi. Yote yametimia kwenu. Halikukosa kutimia hata neno moja kati ya hayo.”—Yoshua 23:14.

4. Yehova aliwapa Waisraeli ahadi gani?

4 Ni maneno gani ya Yehova yaliyotimia wakati wa maisha ya Yoshua? Tutazungumzia ahadi tatu ambazo Yehova aliwapa Waisraeli. Kwanza, Mungu aliahidi kuwakomboa kutoka utumwani. Pili, angewalinda. Tatu, angewatunza. Yehova amewapa watu wake wa kisasa ahadi kama hizo, na tumeona ahadi hizo zikitimia katika maisha yetu. Hata hivyo, kabla hatujazungumzia matendo ya Yehova katika nyakati za kisasa, acheni tuzungumzie matendo yake katika siku za Yoshua.

Yehova Anawakomboa Watu Wake

5, 6. Yehova aliwakomboa jinsi gani Waisraeli kutoka Misri, na ukombozi huo ulionyesha nini?

5 Waisraeli walipomlilia Mungu kwa sababu ya kuwa watumwa huko Misri, Yehova aliona. (Kutoka 2:23-25) Yehova alimwambia Musa hivi kwenye mti uliokuwa ukiwaka moto: “Ninashuka ili kuwakomboa [watu wangu] kutoka katika mkono wa Wamisri na kuwatoa katika nchi hiyo mpaka kwenye nchi nzuri na kubwa, nchi inayotiririka maziwa na asali.” (Kutoka 3:8) Walisisimka kama nini kuona Yehova akitimiza ahadi hiyo! Farao alipokataa kuwaruhusu Waisraeli waondoke Misri, Musa alimwambia kwamba Mungu angeyageuza maji ya Mto Nile yawe damu. Neno la Yehova halikukosa kutimia. Maji ya Mto Nile yaligeuka na kuwa damu. Samaki wakafa, na watu hawakuweza kunywa maji ya mto huo. (Kutoka 7:14-21) Farao aliendelea kuwa na kichwa kigumu, na Yehova akaleta mapigo mengine tisa. Kabla ya kila pigo, alieleza mambo ambayo yangetukia. (Kutoka, sura ya 8-12) Baada ya pigo la kumi kumuua mzaliwa wa kwanza wa Misri, Farao aliwaamuru Waisraeli waondoke, nao wakaondoka!—Kutoka 12:29-32.

6 Baada ya ukombozi huo, Yehova aliwakubali Waisraeli kuwa taifa lake lililochaguliwa. Ukombozi huo ulimtukuza Yehova kuwa Mtimizaji wa ahadi, yule ambaye neno lake halikosi kamwe kutimia. Ulionyesha kwamba Yehova ni mkuu kuliko miungu ya mataifa. Imani yetu inatiwa nguvu tunaposoma kuhusu ukombozi huo. Wazia jinsi Waisraeli walivyohisi walipokombolewa! Yoshua aliona kwamba bila shaka Yehova ndiye ‘Aliye Juu Zaidi, juu ya dunia yote.’—Zaburi 83:18.

Yehova Anawalinda Watu Wake

7. Yehova aliwalinda jinsi gani Waisraeli kutokana na jeshi la Farao?

7 Namna gani ahadi ya pili, ya kwamba Yehova angewalinda watu wake? Ahadi hiyo ilihusiana na ahadi ya Yehova ya kuwakomboa kutoka Misri na kuwaingiza katika Nchi ya Ahadi. Kumbuka kwamba Farao mwenye hasira aliwafuata Waisraeli akiwa na jeshi lake lenye nguvu, lenye mamia ya magari ya vita. Bila shaka, Farao mwenye kiburi alikuwa na uhakika sana, hasa ilipoonekana kana kwamba Waisraeli walikuwa wamenaswa kati ya milima na bahari! Sasa Mungu akachukua hatua ya kuwalinda watu wake kwa kuweka wingu kati ya kambi hizo mbili. Upande wa Wamisri ulikuwa na giza; na upande wa Waisraeli ulikuwa na nuru. Huku wingu likiwa limewazuia Wamisri kusonga, Musa aliinua fimbo yake na maji ya Bahari Nyekundu yakatengana. Waisraeli wakapata njia ya kuokokea lakini Wamisri wakanaswa. Yehova aliliharibu kabisa jeshi lenye nguvu la Farao na kuwalinda watu Wake walioonekana kana kwamba wangeshindwa.—Kutoka 14:19-28.

8. Waisraeli walilindwa jinsi gani (a) jangwani na (b) walipoingia katika Nchi ya Ahadi?

8 Baada ya kuvuka Bahari Nyekundu, Waisraeli walitangatanga katika nchi inayosemekana kuwa ‘jangwa kubwa na la kutisha, lenye nyoka wenye sumu na nge; nchi kame isiyokuwa na maji.’ (Kumbukumbu la Torati 8:15, Biblia Habari Njema) Yehova aliwalinda watu wake katika jangwa hilo pia. Namna gani walipoingia katika Nchi ya Ahadi? Majeshi yenye nguvu ya Wakanaani yaliwapinga. Lakini, Yehova alimwambia Yoshua hivi: “Simama sasa, vuka huu mto Yordani, wewe na watu hawa wote, mwingie katika nchi ambayo ninawapa wao, wana wa Israeli. Hakuna yeyote atakayesimama imara mbele yako siku zote za maisha yako. Nitakuwa pamoja nawe, kama vile nilivyokuwa pamoja na Musa. Sitakutupa wala kukuacha kabisa.” (Yoshua 1:2, 5) Maneno hayo ya Yehova hayakukosa kutimia. Katika muda wa miaka sita hivi, Yoshua aliwashinda Wafalme 31 na kuchukua sehemu kubwa ya Nchi ya Ahadi. (Yoshua 12:7-24) Hawangeshinda ikiwa Yehova hangewalinda.

Yehova Anawatunza Watu Wake

9, 10. Yehova aliwatunza namna gani watu wake nyikani?

Sasa fikiria ahadi ya tatu, ya kwamba Yehova angewatunza watu wake. Muda mfupi baada ya kuwakomboa kutoka Misri, Mungu aliwaahidi Waisraeli hivi: “Tazama, nitawanyeshea mkate kutoka mbinguni; nao watu watatoka nje na kuokota kila mtu kiasi chake siku baada ya siku.” Mungu aliwapa “mkate kutoka mbinguni” kama alivyoahidi. ‘Wana wa Israeli walipouona, wakaanza kusemezana: “Ni nini hiki?”’ Ulikuwa mana, mkate ambao Yehova alikuwa amewaahidi.—Kutoka 16:4, 13-15.

10 Kwa miaka 40 ambayo Waisraeli walikuwa nyikani, Yehova aliwatunza kwa kuwapa chakula na maji. Hata alihakikisha kwamba nguo zao hazikuchakaa wala miguu yao kuvimba. (Kumbukumbu la Torati 8:3, 4) Yoshua alijionea yote hayo. Yehova aliwakomboa, aliwalinda, na kuwatunza watu wake, kama vile tu alivyokuwa amewaahidi.

Ukombozi Katika Nyakati za Kisasa

11. Ni nini kilichotukia Brooklyn, New York, mwaka wa 1914, na wakati ulikuwa umefika wa kufanya nini?

11 Namna gani wakati wetu? Ijumaa (Siku ya 5) asubuhi, Oktoba 2, 1914 (2/10/1914), Charles Taze Russell, ambaye aliwaongoza Wanafunzi wa Biblia wakati huo, aliingia ndani ya chumba cha kulia chakula katika Betheli ya Brooklyn, New York. Alisema hivi kwa uchangamfu: “Hamjambo nyote.” Kisha, kabla hajaketi, akatangaza hivi kwa furaha: “Nyakati za Mataifa zimekwisha; siku za wafalme wao zimekwisha.” Kwa mara nyingine tena, wakati ulikuwa umefika wa Yehova, Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu wote, kuchukua hatua ya kuwatetea watu wake. Na alichukua hatua!

12. Ni ukombozi gani uliotukia mwaka wa 1919, na matokeo yalikuwa nini?

12 Miaka mitano tu baadaye, Yehova aliwakomboa watu wake kutoka “Babiloni Mkubwa,” milki yenye nguvu ya dini ya uwongo ulimwenguni. (Ufunuo 18:2) Ni wachache kati yetu ambao walikuwa hai na kushuhudia ukombozi huo wenye kusisimua. Hata hivyo, tunaona wazi matokeo yake. Yehova alianzisha tena ibada safi na kuwaunganisha wale waliotamani kumwabudu. Hilo lilikuwa limetabiriwa kupitia nabii Isaya: “Itatukia katika siku za mwisho kwamba mlima wa nyumba ya Yehova utawekwa imara juu ya kilele cha milima, nao utainuliwa juu ya vilima; na mataifa yote yatamiminika huko.”—Isaya 2:2.

13. Umeona ongezeko gani miongoni mwa watu wa Yehova?

13 Maneno ya Isaya hayakukosa kutimia. Mwaka wa 1919, mabaki watiwa-mafuta walianzisha kwa ujasiri kampeni ya kuhubiri ulimwenguni pote ambayo iliinua ibada ya Mungu wa kweli. Katika miaka ya 1930, ilikuwa wazi kwamba “kondoo wengine” walikuwa wakikusanywa. (Yohana 10:16) Kwanza maelfu walikusanywa, kisha mamia ya maelfu, na sasa mamilioni wanajiunga na ibada safi! Katika maono ambayo mtume Yohana alipata, wanasemwa kuwa “umati mkubwa, ambao hakuna mtu aliyeweza kuuhesabu, kutoka mataifa yote na makabila na vikundi vya watu na lugha.” (Ufunuo 7:9) Umejionea nini maishani mwako? Kulikuwa na Mashahidi wangapi wa Yehova duniani ulipoanza kujifunza kweli? Leo, idadi ya wale wanaomtumikia Yehova ni zaidi ya 6,700,000. Kwa kuwakomboa watu wake kutoka Babiloni Mkubwa, Yehova alifungua njia kwa ajili ya ongezeko linalosisimua ambalo tunaona duniani pote.

14. Ni ukombozi gani unaokaribia?

14 Yehova atafanya tendo lingine la ukombozi hivi karibuni, tendo ambalo litamhusisha kila mtu duniani. Yehova ataonyesha nguvu zake kwa njia ya pekee kwa kuwaangamiza kabisa wote wanaompinga, naye atawakomboa watu wake na kuwaingiza katika ulimwengu mpya ambamo uadilifu utakaa. Tutafurahi kama nini kuona mwisho wa uovu na mwanzo wa enzi yenye utukufu zaidi katika historia yote ya wanadamu!—Ufunuo 21:1-4.

Ulinzi wa Yehova Katika Siku Zetu

15. Kwa nini ulinzi wa Yehova unahitajiwa katika nyakati za kisasa?

15 Kama tulivyoona, Waisraeli wa siku za Yoshua walihitaji ulinzi wa Yehova. Je, watu wa Yehova wa nyakati za kisasa hawahitaji ulinzi? Bila shaka wanahitaji! Yesu aliwaonya hivi wafuasi wake: ‘Watu watawatia ninyi katika dhiki na kuwaua ninyi, nanyi mtachukiwa na mataifa yote kwa sababu ya jina langu.’ (Mathayo 24:9) Kwa miaka mingi, Mashahidi wa Yehova katika nchi nyingi wamevumilia upinzani mkali na mateso ya kikatili. Hata hivyo, Yehova amekuwa akiwategemeza watu wake. (Waroma 8:31) Neno lake linatuhakikishia kwamba hakuna chochote, ndiyo, hakuna ‘silaha yoyote itakayofanywa juu yetu,’ itakayosimamisha kazi yetu ya kuhubiri na kufundisha kuhusu Ufalme.—Isaya 54:17.

16. Umeona ushuhuda gani ambao unaonyesha kwamba Yehova anawalinda watu wake?

16 Watu wa Yehova wameendelea kuongezeka hata ingawa wanachukiwa na ulimwengu. Mashahidi wa Yehova wanasitawi katika nchi 236, na hilo linathibitisha kwa kweli kwamba Yehova anatutegemeza na kutulinda kutokana na wale ambao wanataka kutuangamiza au kutunyamazisha. Je, unaweza kukumbuka majina ya viongozi wa kisiasa au wa kidini wenye nguvu ambao waliwanyanyasa vikali watu wa Mungu? Walipatwa na nini? Wako wapi sasa? Wengi wao wameshindwa kabisa, kama Farao katika siku za Musa na Yoshua. Namna gani watumishi wa Mungu wa nyakati za kisasa ambao wamekufa wakiwa waaminifu? Wanalindwa katika kumbukumbu la Yehova. Wako mahali salama zaidi. Ni wazi kwamba ahadi ya Yehova ya kuwalinda imetimia.

Yehova Anawatunza Watu Wake Leo

17. Yehova alitoa uhakikisho gani kuhusu chakula cha kiroho?

17 Yehova aliwatunza watu wake nyikani, naye anawatunza leo. “Mtumwa mwaminifu na mwenye busara” anatulisha kiroho. (Mathayo 24:45) Tunapokea ujuzi wa kweli za kiroho ambazo zilikuwa siri kwa karne nyingi. Malaika alimwambia Danieli hivi: “Yafanye siri maneno hayo na kukifunga kitabu kwa muhuri, mpaka wakati wa mwisho. Wengi watakwenda huku na huku, na ujuzi wa kweli utakuwa mwingi.”—Danieli 12:4.

18. Kwa nini tunaweza kusema kwamba ujuzi wa kweli ni mwingi leo?

18 Leo tunaishi katika wakati wa mwisho, na kwa hakika ujuzi wa kweli ni mwingi sana. Ulimwenguni pote, roho takatifu imewaongoza wale wanaopenda kweli kupata ujuzi sahihi juu ya Mungu wa kweli na makusudi yake. Biblia zimejaa duniani leo, na kuna vichapo vingi vya kuwasaidia watu kuelewa kweli zenye thamani zilizo katika Biblia. Kwa mfano, angalia ukurasa wa yaliyomo katika kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? * Kina sura kama vile: “Ukweli Kumhusu Mungu,” “Wafu Wako Wapi?,” “Ufalme wa Mungu Ni Nini?,” na “Kwa Nini Mungu Anawaacha Watu Wateseke?” Wanadamu wamefikiria maswali hayo kwa maelfu ya miaka. Sasa majibu ya maswali hayo yanapatikana kwa urahisi. Hata ingawa watu hawakuwa na ujuzi wa Biblia na ingawa dini zinazodai kuwa za Kikristo zilifundisha mafundisho ya uasi-imani kwa karne nyingi, bado Neno la Mungu linadumu na kuwaongoza wote wanaotamani kumtumikia Yehova.

19. Umeona ahadi gani zikitimia, na umekata kauli gani?

19 Bila shaka, kutokana na yale ambayo tumejionea wenyewe, tunaweza kusema hivi: “Halikukosa kutimia hata neno moja kati ya maneno yote mema ambayo Yehova Mungu wenu amewaambia ninyi. Yote yametimia kwenu. Halikukosa kutimia hata neno moja kati ya hayo.” (Yoshua 23:14) Yehova anawakomboa, anawalinda, na kuwatunza watumishi wake. Je, unaweza kutaja ahadi yake yoyote ambayo imekosa kutimia kwa wakati alioweka? Haiwezekani. Kwa hekima, tunaliamini Neno la Mungu lenye kutegemeka.

20. Kwa nini tunaweza kutazamia wakati ujao tukiwa na uhakika?

20 Namna gani wakati ujao? Yehova ametuambia kwamba wengi wetu tunaweza kuwa na tumaini la kuishi katika dunia iliyogeuzwa kuwa paradiso yenye kupendeza. Wachache kati yetu wana tumaini la kutawala pamoja na Kristo mbinguni. Hata tuwe na tumaini gani, tuna sababu nzuri za kuendelea kuwa waaminifu kama Yoshua. Siku moja tumaini letu litatimia. Kisha tutafikiria ahadi zote ambazo Yehova alitoa, na sisi pia tutasema: ‘Zote zimetimia.’

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 18 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

Je, Unaweza Kueleza?

• Yoshua aliona ahadi gani za Yehova zikitimia?

• Umeona ahadi gani za Yehova zikitimia?

• Tunaweza kuwa na uhakika gani kuhusu Neno la Mungu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 23]

Yehova aliingilia kati ili kuwakomboa watu wake

[Picha katika ukurasa wa 23]

Yehova aliwalinda jinsi gani watu wake katika Bahari Nyekundu?

[Picha katika ukurasa wa 24]

Yehova aliwatunza namna gani watu wake nyikani?

[Picha katika ukurasa wa 25]

Yehova anawatunza watu wake leo