Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nilijifunza Kumtegemea Yehova Kabisa

Nilijifunza Kumtegemea Yehova Kabisa

Simulizi la Maisha

Nilijifunza Kumtegemea Yehova Kabisa

Limesimuliwa na Aubrey Baxter

Jumamosi moja jioni (Siku ya Posho) mwaka wa 1940, wanaume wawili walinishambulia, wakanipiga na kuniangusha. Polisi wawili walikuwa wamesimama hapo karibu, lakini badala ya kunisaidia, walinitukana na kuwasifu wanaume waliokuwa wakinipiga. Matukio katika maisha yangu ambayo yalisababisha nifanyiwe tendo hilo la ukatili yalianza miaka mitano hivi mapema nilipokuwa nimeajiriwa kazi katika mgodi wa makaa ya mawe. Acheni nieleze.

NILIKUWA mvulana wa tatu kati ya wavulana wanne, nami nilizaliwa mwaka wa 1913 huko Swansea, mji wa pwani huko New South Wales, Australia. Nilipokuwa na umri wa miaka mitano, familia yetu yote ilishikwa na ugonjwa hatari ulioitwa homa ya Kihispania, ugonjwa ambao uliua mamilioni ya watu ulimwenguni pote. Inafurahisha kwamba sote tulipona. Hata hivyo, mnamo 1933, tulipatwa na msiba Mama alipokufa akiwa na umri wa miaka 47. Alikuwa mcha-Mungu, na alikuwa amepata mabuku mawili ya kitabu Light, ambacho kilikuwa kitabu cha kujifunzia Biblia kilichosambazwa na Mashahidi wa Yehova.

Wakati huo, nilikuwa nikifanya kazi katika mgodi wa makaa ya mawe. Kwa kuwa kazi yangu ilikuwa na vipindi vifupi-vifupi vyenye shughuli nyingi vikifuatwa na vipindi virefu visivyo na shughuli nyingi, nilienda na vitabu hivyo kazini na kuvisoma nikitumia tochi iliyounganishwa na kofia yangu. Muda si muda, niligundua kwamba nimepata kweli. Pia, nilianza kusikiliza hotuba za Biblia zilizotolewa na Mashahidi kwenye redio. Nilipata shangwe zaidi Baba na ndugu zangu walipoanza kupendezwa na kweli ya Biblia.

Mwaka wa 1935 tulipata msiba mwingine wakati Billy, ndugu yangu mdogo aliposhikwa na ugonjwa wa nimonia kisha akafa. Alikuwa na umri wa miaka 16 tu. Hata hivyo, wakati huu familia yetu ilifarijiwa na tumaini la ufufuo. (Matendo 24:15) Baada ya muda, Baba na ndugu zangu wakubwa, Verner na Harold, pamoja na wake zao waliweka maisha yao wakfu kwa Mungu. Kufikia sasa, mimi tu ndiye mshiriki wa familia yetu aliye hai. Hata hivyo, Marjorie, mke wa pili wa Verner, na Elizabeth, mke wa Harold, wangali wanamtumikia Yehova kwa bidii.

Kujifunza Kumtegemea Yehova

Nilizungumza kwa mara ya kwanza na Mashahidi wa Yehova mnamo 1935, mwanamke mmoja kutoka Ukrainia alipokuja nyumbani kwetu kwa baiskeli. Jumapili iliyofuata (Siku ya Yenga), nilihudhuria kwa mara ya kwanza mkutano wa Kikristo, na juma moja baadaye, nikahudhuria mkutano wa utumishi wa shambani. Shahidi aliyeongoza mkutano wa utumishi wa shambani alinipa vijitabu kadhaa, nami nilishangaa sana aliponiambia nihubiri peke yangu! Katika mlango wangu wa kwanza, nilikuwa na wasiwasi mwingi sana hivi kwamba nilitaka dunia ipasuke na kunimeza! Lakini mwenye nyumba alikuwa mzuri na hata alikubali kuchukua vijitabu.

Maandiko kama vile Mhubiri 12:1 na Mathayo 28:19, 20 yalinigusa moyo sana, nami nikataka kuwa painia, yaani, mhudumu wa wakati wote. Baba aliunga mkono uamuzi wangu. Ingawa sikuwa nimebatizwa, niliazimia kuanza upainia Julai 15, 1936 (15/7/1936). Siku hiyo, nilienda kwenye ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova huko Sydney, ambako niliombwa nifanye kazi na kikundi cha mapainia 12 katika kitongoji cha Sydney kinachoitwa Dulwich Hill. Mapainia hao walinifundisha kutumia jiwe la kusagia ngano linalozungushwa kwa mkono, ambalo mapainia walitumia kusagia nafaka na hivyo kupunguza gharama za chakula.

Kufanya Upainia Mashambani

Nilibatizwa baadaye mwaka huo, kisha mimi pamoja na mapainia wengine wawili, Aubrey Wills na Clive Shade, tukatumwa Queensland ya kati. Vifaa vyetu vilitia ndani gari la Aubrey, baiskeli kadhaa, kinanda cha gramafoni cha kuchezea hotuba za Biblia, hema lililokuwa makao yetu kwa miaka mitatu iliyofuata, vitanda vitatu, meza, na sufuria moja. Jioni moja ilipokuwa zamu yangu kupika, niliamua kupika chakula cha “pekee,” chakula cha mboga za majani na ngano yenye maganda. Lakini hakuna yeyote kati yetu aliyeweza kula chakula hicho. Palikuwa na farasi hapo karibu, hivyo nikampa chakula hicho. Alikinusa, akatikisa kichwa chake, kisha akaenda zake! Huo ukawa mwisho wangu wa kufanya majaribio jikoni.

Baada ya muda, tuliamua kuhubiri eneo letu haraka zaidi kwa kuligawanya mara tatu kisha kila mmoja wetu ahubiri eneo lake. Mara nyingi jioni ilipofika, nilikuwa mbali sana na kambi yetu nisiweze kuendesha baiskeli kurudi nyumbani, hivyo nyakati nyingine nililala mashambani nyumbani kwa watu walionikaribisha. Usiku mmoja nililala kwenye kitanda cha fahari katika chumba cha wageni cha shamba fulani la ng’ombe, na usiku uliofuata nikalala kwenye sakafu ya chumba cha mwindaji wa kangaruu huku nikiwa nimezungukwa na marundo ya ngozi zilizokuwa zikinuka. Mara nyingi nililala vichakani. Wakati mmoja, mbwa mwitu walinizunguka kwa mbali na kupiga mayowe mengi gizani. Baada ya kushindwa kulala usiku kucha, niligundua kwamba hawakuwa na haja na mimi bali walitaka ngozi zenye nyama zilizokuwa zimetupwa hapo karibu.

Kuhubiri Tukitumia Gari Lenye Kipaaza-Sauti

Tulitumia vizuri gari lenye kipaaza-sauti kutangaza Ufalme wa Mungu. Katika jiji la Townsville huko Queensland kaskazini, polisi walituruhusu tupige kambi katikati ya jiji. Hata hivyo, hotuba iliyorekodiwa iliwakasirisha washiriki fulani wa Jeshi la Wokovu, nao wakatuambia tuondoke. Tulipokataa, watano kati yao walitikisa gari letu kwa nguvu sana. Wakati huo, nilikuwa ndani ya gari nikishughulikia mfumo wa sauti! Halikuwa jambo la hekima kushikilia haki zetu, hivyo wanaume hao walipoondoka, tulihama eneo hilo.

Katika mji wa Bundaberg mtu fulani anayependezwa alituazima boti ili tuitumie kusambaza ujumbe tukiwa katika Mto Burnett, unaopita mjini. Aubrey na Clive walisafiri kwa boti hiyo wakiwa na mfumo wa sauti nami nikabaki katika jumba tulilokuwa tumekodi. Usiku huo, sauti yenye nguvu iliyorekodiwa ya Joseph F. Rutherford, wa makao makuu ya ulimwengu ya Mashahidi wa Yehova, ilisikika kwa kishindo kotekote mjini Bundaberg ikitangaza ujumbe mzito wa Biblia. Kwa kweli, hizo zilikuwa pindi zenye kusisimua zilizohitaji watu wa Mungu wawe na ujasiri na imani.

Vita Vinatokeza Matatizo Zaidi

Punde baada ya Vita vya Pili vya Ulimwengu kuanza Septemba (Mwezi wa 9) 1939, Mnara wa Mlinzi la Novemba (Mwezi wa 11) 1 lilizungumzia msimamo wa Kikiristo wa kutokuwamo kuhusiana na siasa na vita. Baadaye, nilifurahi kwamba nilikuwa nimejifunza habari hiyo kwa wakati unaofaa. Wakati huohuo, baada ya kutumika kwa miaka mitatu pamoja na Aubrey na Clive, tulipokea migawo iliyotutenganisha. Niliwekwa rasmi kuwa mwangalizi anayesafiri huko Queensland kaskazini, mgawo ambao mara nyingi ulijaribu tegemeo langu katika Yehova.

Mnamo Agosti (Mwezi wa 8) 1940, nilitumikia kutaniko la Townsville, ambalo lilikuwa na mapainia wanne—Percy na Ilma Iszlaub * na Norman na Beatrice Bellotti ambao ni mtu na dada yake. Miaka sita baadaye, Beatrice akawa mke wangu. Jumamosi moja jioni baadhi yetu tulipomaliza mahubiri ya barabarani, nilishambuliwa kama nilivyosema mwanzoni. Hata hivyo, tendo hilo lisilo la haki lilinichochea kuendelea kumtumikia Yehova.

Dada wawili mapainia, Una na Merle Kilpatrick, walikuwa wakifanya kazi nzuri huko kaskazini. Nilifurahi kuhubiri pamoja nao siku moja, kisha wakaniomba niwavukishe mto kwa mtumbwi wakatembelee familia moja iliyopendezwa. Hilo lilimaanisha niogelee hadi ng’ambo ya mto nikachukue mtumbwi huo, halafu nipige makasia kurudi ng’ambo ile nyingine, kisha niwavukishe dada hao kwa mtumbwi huo. Hata hivyo, nilipoufikia mtumbwi huo, makasia hayakuwepo! Baadaye tuligundua kwamba mpinzani fulani alikuwa ameyaficha. Lakini mbinu yake haikutuzuia. Kwa miaka kadhaa nilifanya kazi ya kuokoa watu wanaozama wakiogelea na bado nilikuwa mwogeleaji mwenye nguvu. Hivyo nilifungilia kamba ya nanga kwenye kiuno changu na kuuvuta mtumbwi hadi ng’ambo ya mto walipokuwa dada hao, halafu nikawavuta hadi ng’ambo ya pili. Yehova alibariki jitihada zetu, kwa kuwa baada ya muda washiriki wa familia hiyo iliyopendezwa wakawa Mashahidi.

Chini ya Kivuli cha Mkono wa Yehova

Kwa sababu za usalama, jeshi liliweka kizuizi cha barabarani chini tu ya mji wa Innisfail. Kwa kuwa nilikuwa mkaaji wa eneo hilo ningeweza kupata kibali cha kuingia mjini, na hilo lilikuwa jambo lenye thamani sana wakati wawakilishi kutoka ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova walipotutembelea. Ili kuwaingiza mjini kupitia kizuizi hicho, nilikuwa nikiwaficha chini ya kiti cha nyuma cha gari langu.

Wakati huo, watu hawakuruhusiwa kununua mafuta mengi ya gari, na magari mengi yalikuwa na mtambo wa kutokeza gesi. Ili kuendesha injini, mtambo huo ulivuta gesi inayoweza kuunguzwa kutoka katika makaa yenye moto. Ningesafiri usiku nikiwa nimeficha magunia ya makaa juu ya kiti cha nyuma cha gari mahali ambapo ndugu alikuwa amejificha. Niliposimamisha gari katika kizuizi cha barabarani, niliwakengeusha askari kwa kungurumisha gari kwa nguvu na hivyo kufanya chombo cha makaa kiwe na moto kabisa. Usiku mmoja kama huo niliwaambia walinzi kwa sauti: “Nikiizima mota nitavuruga mchanganyiko wa gesi na hewa, na itakuwa vigumu sana kuiwasha tena.” Wakizuiwa na joto, moshi, na masizi, askari hao walikagua gari kijuu-juu tu kisha wakaniruhusu nipite.

Wakati huo, nilipewa mgawo wa kupanga kusanyiko mjini Townsville kwa ajili ya Mashahidi wenyeji. Chakula kilikuwa kikipimwa, na tulihitaji kibali cha hakimu wa eneo hilo ili tupate kiasi tulichohitaji cha chakula. Wakati huo, ndugu zetu Wakristo walikuwa wakifungwa gerezani kwa sababu ya msimamo wao wa kutokuwamo. Hivyo nilipoomba kumwona hakimu nilijiuliza, ‘Je, ninatenda kwa hekima, ama ninamchokoza simbamarara?’ Hata hivyo, nilifanya kama nilivyoagizwa.

Hakimu huyo aliniomba niketi. Nilipomwambia kwa nini nimemtembelea, aliketi imara na kunikazia macho kwa muda mrefu. Kisha akatulia na kusema, “Unataka chakula kiasi gani?” Nilimpa orodha ya kiasi kidogo zaidi cha chakula tulichohitaji. Aliichunguza na kusema: “Inaonekana kiasi hiki hakitoshi. Afadhali tukiongeze mara mbili.” Niliondoka ofisini mwake nikimshukuru Yehova sana, ambaye alinifundisha tena somo lingine kuhusu kumtegemea.

Mnamo Januari (Mwezi wa 1) 1941, kazi ya Mashahidi wa Yehova ilipigwa marufuku nchini Australia. Watu wengi walitushuku na hata kutushtaki kuwa wapelelezi wa Wajapani! Pindi moja, polisi na wanajeshi waliokuwa kwenye magari mawili walivamia Kingdom Farm, shamba lililokuwa kwenye Uwanda wa Atherton tulilokuwa tumenunua kwa ajili ya kilimo. Walikuwa wakitafuta taa yenye mwanga mkali waliyodai kwamba tuliitumia kuwaelekeza maadui. Pia, tulishtakiwa kwamba tulipanda mahindi kwa mpangilio fulani wenye ujumbe ambao ungeweza kusomwa kutoka angani! Bila shaka, mashtaka yote hayo yalithibitishwa kuwa ya uwongo.

Kwa sababu ya marufuku, ilitubidi kuwa waangalifu na wenye busara tuliposafirisha vichapo. Kwa mfano, kitabu Children kilipotolewa, nilichukua katoni ya vitabu hivyo huko Brisbane, nikasafiri kaskazini kwa gari la moshi, na kuacha vitabu katika vituo ambako kulikuwa na makutaniko. Ili kuwazuia polisi na mainspekta wa jeshi wasifungue katoni hiyo, nilibeba msumeno mkubwa wa mviringo na kuufungilia juu ya katoni hiyo kabla sijashuka. Ingawa ilikuwa mbinu rahisi, haikushindwa kamwe. Watu wa Yehova walifurahi sana kwa sababu marufuku hiyo iliondolewa mnamo Juni (Mwezi wa 6) 1943. Hakimu mmoja alisema kwamba marufuku hiyo “ilitegemea maoni ya mtu mmoja tu, iliwekwa bila kufikiria mambo kwa uzito, na ilikuwa yenye kukandamiza.”

Tunaagizwa Tujiunge na Jeshi

Katika mwaka uliotangulia, mimi, Aubrey Wills, na Norman Bellotti, tuliagizwa tujiunge na jeshi. Aubrey na Norman waliitwa juma moja kabla yangu na wakahukumiwa kifungo cha miezi sita gerezani. Wakati huo, ofisi ya posta ilikuwa ikizuilia magazeti ya Mnara wa Mlinzi yaliyotumwa kwa Mashahidi waliojulikana lakini haikuzuilia magazeti yaliyotumwa kwa watu wengine walioandikisha. Kazi yetu ilikuwa kutafuta mmoja wa watu hao, kutoa nakala za magazeti hayo, kisha kusambaza nakala hizo kwa Mashahidi wenzetu. Kwa njia hiyo, tulipokea chakula cha kiroho kwa ukawaida.

Nilipopokea hukumu niliyotazamia ya kifungo cha miezi sita gerezani, nilikata rufani mara moja kama nilivyoagizwa na ofisi ya tawi huko Sydney. Lengo letu lilikuwa kuchelewesha kifungo hadi Shahidi mwingine awekwe rasmi kusimamia kazi. Nilitumia uhuru wangu kuwatembelea baadhi ya Mashahidi 21 waliokuwa gerezani huko Queensland kaskazini. Wengi wao walikuwa katika gereza moja, na msimamizi wa gereza hilo alituchukia. Nilipomkumbusha kwamba wahudumu wa dini nyingine wangeweza kuwatembelea watu wao, alikasirika sana. “Ikiwa ningeweza,” akapaaza sauti, “Mashahidi wote wa Yehova wangesimamishwa kwenye mstari na kupigwa risasi!” Walinzi walinipeleka nje haraka.

Wakati ulipofika wa kusikilizwa kwa kesi yangu ya rufani, nilipewa wakili kama ilivyotakiwa na sheria. Hata hivyo, kwa kweli, niliendesha kesi yangu mimi mwenyewe, na hilo lilimaanisha kumtegemea sana Yehova. Naye Yehova hakunikatisha tamaa. (Luka 12:11, 12; Wafilipi 4:6, 7) Kwa kushangaza, nilishinda kesi hiyo kwa kuwa iligunduliwa kwamba karani wa mahakama alikuwa amekosea alipokuwa akijaza hati ya mashtaka!

Mwaka wa 1944, nilipewa mgawo wa kutumikia mzunguko mkubwa katika eneo lote la South Australia, Victoria kaskazini, na jiji la Sydney huko New South Wales. Mwaka uliofuata, kampeni ya ulimwenguni pote ya kutoa hotuba za watu wote ilianzishwa, na kila msemaji alipaswa kutayarisha hotuba yake mwenyewe, akitumia muhtasari wa ukurasa mmoja ulioandaliwa na tengenezo. Haikuwa rahisi kutoa hotuba za saa nzima, lakini tulijitahidi huku tukimtegemea Yehova kabisa, naye alibariki jitihada zetu.

Ndoa na Wajibu Mpya

Mnamo Julai 1946, mimi na Beatrice Bellotti tulifunga ndoa, nasi tukatumika pamoja tukiwa mapainia. Nyumba yetu ilikuwa gari la kukokotwa ambalo lilijengwa kwa mbao. Jannyce (Jann), binti yetu ambaye ndiye mtoto wetu wa pekee, alizaliwa mnamo Desemba 1950. Tulifanya upainia katika sehemu mbalimbali, kutia ndani mji wa Kempsey, huko New South Wales. Eneo hilo halikuwa na Mashahidi wengine. Kila Jumapili tulienda katika jumba la jumuiya la eneo hilo nikiwa tayari kutoa hotuba ya watu wote ambayo tulikuwa tumetangaza kupitia mialiko. Kwa miezi michache, Beatrice na mtoto wetu Jann ndio tu waliohudhuria. Hata hivyo, muda si muda, watu wengine walianza kuhudhuria. Leo kuna makutaniko mawili ambayo yamesitawi mjini Kempsey.

Jann alipokuwa na miaka miwili, tuliamua kuishi Brisbane. Halafu alipomaliza shule, tukafanya upainia tukiwa familia kwa miaka minne mjini Cessnock huko New South Wales, na mwishowe tukarudi Brisbane kumsaidia mama ya Beatrice ambaye alikuwa mgonjwa. Kwa sasa, nina pendeleo la kutumika nikiwa mzee katika Kutaniko la Chermside.

Mimi na Beatrice tunamshukuru Yehova kwa baraka tele ambazo ametupa, kutia ndani pendeleo la kuwasaidia watu 32 wamjue. Mimi binafsi ninamshukuru Yehova kwa sababu ya mke wangu mpendwa, ambaye ingawa ni mwenye fadhili na mpole, amekuwa akitetea kweli za Biblia bila woga. Upendo na tegemeo lake kwa Mungu, na jicho ‘lake rahisi’ limemfanya awe mke na mama mwenye uwezo kwelikweli. (Mathayo 6:22, 23; Methali 12:4) Mimi na mke wangu tunaweza kusema hivi kwa moyo wetu wote: “Amebarikiwa yule mtu hodari anayemtegemea Yehova.”—Yeremia 17:7.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 19 Simulizi la maisha la Percy Iszlaub lilichapishwa katika toleo la Kiingereza la Mei 15, 1981 (15/5/1981), la gazeti hili.

[Picha katika ukurasa wa 9]

Tulitumia gari hili lenye kipaaza-sauti huko Queensland kaskazini

[Picha katika ukurasa wa 10]

Kuwasaidia Una na Merle Kilpatrick kuvukisha gari lao katika majira ya mvua huko Queensland kaskazini

[Picha katika ukurasa wa 12]

Siku yetu ya arusi