Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ugumu wa Kuwa Mnyenyekevu

Ugumu wa Kuwa Mnyenyekevu

Ugumu wa Kuwa Mnyenyekevu

HUENDA watu wengi wakafikiri kwamba hakuna faida ya kuwa mnyenyekevu katika ulimwengu wa leo. Viongozi wengi wanaoonekana kuwa wenye mafanikio zaidi ni wale wenye kiburi, wale wanaofanya yote wawezayo ili kuwashinda wenzao, na wale wanaosisitiza mambo yafanywe jinsi wanavyotaka. Kwa ujumla, jamii inaonea kijicho mtindo wa maisha wa matajiri na watu mashuhuri, wala si mtindo wa watu wanyenyekevu na wapole. Kwa kawaida, watu walio na mafanikio wanajivuna wakisema kwamba wamefanikiwa kwa sababu ya jitihada zao wenyewe. Badala ya kuwa wanyenyekevu, wanajisifu kwa kiburi kwa sababu ya mafanikio yao.

Mtafiti fulani Mkanada alizungumza kuhusu “kuzuka kwa mtazamo wa ubinafsi na kiburi” nchini Kanada. Wengine wanahisi kwamba tunaishi katika ulimwengu ambamo kuponda raha kunaonwa kuwa muhimu kuliko kutimiza wajibu wetu maishani na kwamba leo watu wengi zaidi na zaidi wanajifikiria wenyewe tu. Katika ulimwengu kama huo, huenda sifa ya unyenyekevu isivutie.

Bila shaka, watu wengi watakubali kwamba unyenyekevu ni sifa inayowafaa wengine, kwa sababu ni rahisi kuishi na watu wanyenyekevu. Hata hivyo, katika ulimwengu wetu ulio na roho ya ushindani, watu fulani wanaogopa kwamba wakiwa wanyenyekevu, wataonekana kuwa dhaifu.

Neno la Mungu, Biblia, lilitabiri kwamba katika wakati wetu watu watakuwa “wenye kujidai, wenye majivuno.” (2 Timotheo 3:1, 2) Je, hukubali kwamba unabii huo unatimizwa leo? Je, unaona faida yoyote ya kuwa mnyenyekevu? Au unafikiri kwamba mtu mnyenyekevu ataonwa kuwa dhaifu, na anayeweza kwa urahisi kutumiwa vibaya na wengine?

Ukweli ni kwamba Biblia inatupa sababu nzuri za kuthamini na kusitawisha sifa ya unyenyekevu. Inatoa maoni yaliyosawazika kuhusu sifa hiyo na inawatia moyo watu waisitawishe, pia, inaonyesha kwamba unyenyekevu wa kweli ni ishara ya nguvu wala si ya udhaifu. Habari inayofuata itazungumzia mambo hayo.

[Picha katika ukurasa wa 3]

Tunapaswa kuhisi namna gani kuhusu mambo tunayotimiza?