Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unawaburudisha Wengine?

Je, Unawaburudisha Wengine?

Je, Unawaburudisha Wengine?

KATIKA ncha ya kusini ya Milima ya Anti-Lebanon, kuna Mlima Hermoni ambao una kilele kilichoinuka mita 2,814 juu ya usawa wa bahari. Kilele cha Hermoni kinafunikwa na theluji kwa muda mrefu kila mwaka, na hivyo mvuke wenye joto unaopita juu ya mlima huo wakati wa usiku unaganda na kutokeza umande. Umande huo unashuka juu ya misonobari na miti ya matunda iliyo katika miteremko ya chini na pia unashuka kwenye mashamba ya mizabibu yaliyo chini hata zaidi. Katika majira marefu ya kiangazi katika Israeli la kale, umande kama huo wenye kuburudisha ndio uliokuwa chanzo kikuu cha unyevunyevu kwa ajili ya mimea.

Katika wimbo ulioongozwa na roho, umoja wenye kuburudisha wa waabudu wa Yehova unafananishwa na “umande wa Hermoni unaoshuka kwenye milima ya Sayuni.” (Zaburi 133:1, 3) Kama tu Mlima Hermoni unavyoandalia mimea umande wenye kuburudisha, ndivyo sisi tunavyoweza kuwaburudisha wale tunaokutana nao. Jinsi gani?

Mfano Unaoburudisha wa Yesu

Yesu Kristo alikuwa na uvutano mkubwa juu ya wengine. Iliburudisha sana kuwa naye hata kwa kipindi kifupi tu. Kwa mfano, Marko, mwandikaji wa Injili anasema hivi: “[Yesu] akachukua watoto akawakumbatia na kuanza kuwabariki, akiweka mikono yake juu yao.” (Marko 10:16) Watoto hao waliburudishwa kama nini!

Katika usiku wake wa mwisho duniani akiwa mwanadamu, Yesu aliosha miguu ya wanafunzi wake. Bila shaka, unyenyekevu wake uligusa mioyo yao. Kisha Yesu akawaambia: “Niliweka kielelezo kwa ajili yenu, ili, kama vile nilivyowafanyia ninyi, ninyi pia mfanye hivyo.” (Yohana 13:1-17) Ndiyo, wao pia walihitaji kuwa wanyenyekevu. Ingawa mitume hao hawakupata maana mara moja na baadaye usiku huo walishindana kuhusu ni nani aliye mkubwa, Yesu hakuudhika. Badala yake, alijadiliana nao kwa subira. (Luka 22:24-27) Hata ‘alipotukanwa, Yesu hakujibu kwa matukano.’ Kwa kweli, “alipokuwa akiteseka, hakutoa vitisho, bali aliendelea kujiweka mkononi mwa yule ambaye anahukumu kwa uadilifu.” Mfano wa Yesu wenye kuburudisha unastahili kuigwa.—1 Petro 2:21, 23.

Yesu alisema hivi: “Chukueni nira yangu na mjifunze kutoka kwangu, kwa maana mimi ni mwenye tabia-pole na mnyenyekevu moyoni, nanyi mtapata burudisho kwa ajili ya nafsi zenu.” (Mathayo 11:29) Hebu wazia kufundishwa na Yesu mwenyewe. Baada ya kumsikiliza akifundisha katika sinagogi, watu katika eneo lake la nyumbani walistaajabu na kusema: “Mtu huyu alipata wapi hekima hii na kazi hizi zenye nguvu?” (Mathayo 13:54) Tukisoma masimulizi kuhusu maisha na huduma ya Yesu, tunaweza kujifunza mengi kuhusu jinsi tunavyoweza kuwaburudisha wengine. Acheni tuchunguze jinsi Yesu alivyoweka mfano bora kupitia usemi unaojenga na kuwa na mtazamo wa kuwasaidia wengine.

Kuwa na Usemi Unaojenga

Ni rahisi kubomoa jengo kuliko kujenga jengo jipya. Kanuni hiyohiyo ya kubomoa na kujenga inahusu usemi wetu. Tukiwa wanadamu wasio wakamilifu, sisi sote tuna udhaifu na kasoro mbalimbali. Mfalme Sulemani alisema: “Hakuna mwanadamu aliye mwadilifu duniani ambaye huendelea kufanya mema na asifanye dhambi.” (Mhubiri 7:20) Ni rahisi sana kutambua kasoro za mtu mwingine na kumbomoa kwa maneno yenye kuumiza. (Zaburi 64:2-4) Kwa upande mwingine, jitihada na uangalifu unahitajiwa ili kuwa na usemi unaojenga.

Yesu alitumia ulimi wake kuwajenga watu. Aliwaburudisha kiroho kwa kuwatangazia habari njema ya Ufalme. (Luka 8:1) Yesu pia aliwaburudisha wale waliokuja kuwa wanafunzi wake kwa kuwafunulia habari kumhusu Baba yake wa kimbingu. (Mathayo 11:25-27) Si ajabu kwamba watu walivutiwa na Yesu!

Tofauti na hilo, waandishi na Mafarisayo hawakuwajali watu. “Wao hupenda mahali penye kuonekana zaidi kwenye milo ya jioni na viti vya mbele katika masinagogi,” akasema Yesu. (Mathayo 23:6) Kwa kweli, waliwadharau watu wa hali ya chini, wakisema: “Umati huu usiojua Sheria ni watu waliolaaniwa.” (Yohana 7:49) Kwa wazi, mtazamo kama huo haukuwa wenye kuburudisha kwa vyovyote!

Mara nyingi, usemi wetu unafunua jinsi tulivyo kwa ndani na jinsi tunavyowaona wengine. Yesu alisema: “Mtu mwema hutokeza mema katika hazina njema ya moyo wake, lakini mtu mwovu hutokeza maovu katika hazina yake mbovu; kwa maana kutokana na wingi wa moyo kinywa chake husema.” (Luka 6:45) Hivyo basi, tunaweza kufanya nini ili usemi wetu uwajenge na kuwaburudisha wengine?

Jambo moja ni, kutua na kufikiri kabla ya kusema. Methali 15:28 inasema: “Moyo wa mwadilifu hutafakari ili kujibu.” Si lazima tutafakari kwa muda mrefu. Tukifikiri kidogo tu kabla ya kusema, kwa kawaida tunaweza kujua ikiwa watu wataburudishwa na maneno yetu. Tunaweza kujiuliza hivi: ‘Je, jambo ninalotaka kusema ni la upendo? Ni la kweli, au ni porojo tu? Je, ni “neno linalosemwa wakati unaofaa?” Je, litawaburudisha na kuwajenga wale watakaolisikia?’ (Methali 15:23) Tukikata kauli kwamba jambo hilo halijengi au si la wakati unaofaa, na tujitahidi tuwezavyo kulitupilia mbali. Je, haingekuwa bora zaidi kutolisema na badala yake kusema jambo linalojenga na linalofaa? Maneno yanayosemwa bila kufikiri ni kama “upanga unaochoma,” lakini maneno yanayojenga “huponya.”—Methali 12:18.

Msaada mwingine ni kukazia fikira sifa zinazofanya waamini wenzetu wawe wenye thamani machoni pa Mungu. Yesu alisema: “Hakuna mtu anayeweza kuja kwangu isipokuwa Baba, aliyenituma, amvute.” (Yohana 6:44) Yehova anaona sifa nzuri katika kila mmoja wa watumishi wake waaminifu—hata wale ambao huenda tukafikiri kwamba wana utu mgumu. Tukijitahidi kutambua sifa zao nzuri, tutapata sababu ya kusema mambo mema kuwahusu.

Wasaidie Wengine

Yesu alielewa kabisa hali ya watu waliokandamizwa. Kwa kweli, “alipouona umati akawasikitikia, kwa sababu walikuwa wamechunwa ngozi na kutupwa huku na huku kama kondoo wasio na mchungaji.” (Mathayo 9:36) Lakini Yesu hakuona tu hali yao yenye kusikitisha; alichukua hatua ya kuwasaidia. Alitoa mwaliko huu: “Njooni kwangu, nyote mnaotaabika na kulemewa na mizigo, nami nitawaburudisha ninyi.” Pia alitoa uhakikisho huu: “Nira yangu ni laini na mzigo wangu ni mwepesi.”—Mathayo 11:28, 30.

Leo, tunaishi katika “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1) Watu wengi wanahisi wamelemewa na “mahangaiko ya mfumo huu wa mambo.” (Mathayo 13:22) Wengine wanalemewa na hali za kibinafsi zenye kuhuzunisha. (1 Wathesalonike 5:14) Tunaweza kuwaburudisha jinsi gani wale walio na uhitaji? Kama Kristo, tunaweza kuwasaidia kwa kufanya mzigo wao uwe mwepesi.

Ili kujaribu kuondoa mambo yanayowalemea, watu fulani wanawajulisha wengine matatizo yao. Watu walioshuka moyo wakija kwetu ili kupata msaada, je, tunatumia wakati kuwasikiliza kwa makini? Mtu anahitaji kujitia nidhamu ili awe msikilizaji mwenye huruma. Kusikiliza kwa huruma kunahusisha kukazia fikira mambo yanayosemwa na mtu mwingine, badala ya kufikiria jinsi utakavyojibu au utakavyotatua tatizo lake. Kwa kumsikiliza mtu kwa makini, kumtazama, na kutabasamu inapofaa, tunaonyesha kwamba tunamjali.

Katika kutaniko la Kikristo, kuna nafasi nyingi za kuwatia moyo waamini wenzetu. Kwa mfano, tunapohudhuria mikutano katika Jumba la Ufalme, tunaweza kuwatafuta wale ambao wana matatizo ya afya. Nyakati nyingine, kinachohitajiwa tu ni kutenga dakika chache kabla au baada ya mikutano ili kuwaambia jambo lenye kutia moyo. Tunaweza pia kuweka akilini orodha ya wale wanaokosekana katika Funzo la Kitabu la Kutaniko tunalohudhuria. Labda tunaweza kuwapigia simu ili kuwajulia hali au kujitolea kuwasaidia.—Wafilipi 2:4.

Wazee Wakristo wana majukumu mazito kutanikoni. Tunaweza kuwasaidia sana kurahisisha mzigo wao kwa kushirikiana nao na kutimiza kwa unyenyekevu migawo yoyote tunayopewa. Neno la Mungu linatuhimiza hivi: “Watiini wale wanaoongoza katikati yenu na mnyenyekee, kwa maana wanaendelea kuzilinda nafsi zenu kama wale watakaotoa hesabu; ili wafanye hivyo kwa shangwe na si kwa kuugua, kwa maana kufanya hivyo kungewadhuru ninyi.” (Waebrania 13:17) Tukijitoa kwa kupenda, tunaweza kuwaburudisha wale “wanaosimamia kwa njia nzuri.”—1 Timotheo 5:17.

Zidi Kujenga kwa Usemi na Kusaidia kwa Matendo

Umande unaoburudisha unatokana na maelfu ya matone madogo ya maji yanayoanguka taratibu, kana kwamba bila kutazamiwa. Vivyo hivyo, hatuwaburudishi wengine kwa kuwatendea tendo moja tu lenye kusifika bali kwa kuonyesha sifa kama za Kristo nyakati zote.

“Katika upendo wa kindugu iweni na upendo mwororo kwa mtu na mwenzake,” akaandika mtume Paulo. “Katika kuonyeshana heshima iweni wa kwanza.” (Waroma 12:10) Acheni tufuate shauri la Paulo. Na tuwaburudishe wengine kikweli kupitia usemi na matendo yetu.

[Picha katika ukurasa wa 16]

Umande wa Mlima Hermoni —chanzo chenye kuburudisha cha unyevunyevu kwa ajili ya mimea

[Picha katika ukurasa wa 17]

Mtu anayesikiliza kwa huruma anawaburudisha wengine