Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Luka—Mfanyakazi Mwenzi Mpendwa

Luka—Mfanyakazi Mwenzi Mpendwa

Luka—Mfanyakazi Mwenzi Mpendwa

NI MWAKA wa 65 W.K. Mahali penyewe palikuwa Roma. Luka alijua hatari ya kujitambulisha kuwa rafiki ya mtume Paulo, ambaye wakati huo alikuwa ameshtakiwa kwa sababu ya imani yake. Ilionekana kwamba Paulo angehukumiwa kifo. Lakini wakati huo hatari, Luka peke yake ndiye aliyekuwa pamoja na mtume huyo.—2 Timotheo 4:6, 11.

Jina Luka si geni masikioni mwa wasomaji wa Biblia kwa sababu Injili aliyoandika inaitwa kwa jina lake. Luka alifunga safari ndefu pamoja na Paulo. Paulo alimwita Luka “tabibu mpendwa” na ‘mfanyakazi mwenzi.’ (Wakolosai 4:14; Filemoni 24) Maandiko hayasemi mengi kumhusu Luka, nayo yanataja jina lake mara tatu tu. Hata hivyo, ukichunguza habari tuliyo nayo kumhusu Luka, huenda ukavutiwa na Mkristo huyo mwaminifu kama Paulo alivyovutiwa naye.

Mwandikaji na Mmishonari

Injili ya Luka na pia kitabu cha Matendo ya Mitume kimeelekezwa kwa Theofilo, na hilo linaonyesha kwamba vitabu hivyo viwili vilivyoongozwa na roho viliandikwa na Luka. (Luka 1:3; Matendo 1:1) Luka hadai kwamba alijionea mwenyewe huduma ya Yesu Kristo. Badala yake, Luka anasema kwamba alipashwa habari na watu waliokuwa mashahidi wa kujionea, naye ‘alifuata kwa uangalifu mambo yote tangu mwanzo kwa usahihi.’ (Luka 1:1-3) Hivyo, inawezekana kwamba Luka alikuja kuwa mfuasi wa Kristo muda fulani baada ya Pentekoste 33 W.K.

Watu fulani wanadhani Luka alitoka Antiokia ya Siria. Wanasema kwamba kitabu cha Matendo kinataja mambo mengi yaliyotukia katika jiji hilo, na pia kinamtaja waziwazi mmoja wa wale “wanaume saba waliothibitishwa” kuwa “mgeuzwa-imani wa Antiokia,” lakini hakisemi wale wanaume wengine sita walitoka katika majiji gani. Bila shaka, hatuwezi kusema kwa uhakika kwamba hilo linaonyesha Luka alipendezwa sana na Antiokia kwa sababu lilikuwa jiji la nyumbani kwao.—Matendo 6:3-6.

Ingawa Luka hatajwi katika kitabu cha Matendo, anajihusisha katika masimulizi fulani na hivyo anaonyesha kwamba alihusika katika matukio hayo. Luka anapozungumzia matukio katika safari ya Paulo na waandamani wake kupitia Asia Ndogo, anasema hivi: “Wakapita Misia na kushuka mpaka Troa.” Wakiwa Troa Paulo alipata maono ya mwanamume Mmakedonia ambaye alisihi hivi: “Vuka uingie Makedonia utusaidie.” Luka anaongezea: “Basi mara tu alipokuwa amekwisha kuona maono hayo, tukajaribu kuingia Makedonia.” (Matendo 16:8-10) Kwa kuwa mwanzoni alisema “wakapita” na baadaye anasema “tukajaribu,” inaelekea Luka alijiunga na Paulo na wenzake huko Troa. Kisha, Luka anaeleza kuhusu kazi ya kuhubiri huko Filipi kwa njia inayoonyesha kwamba alishiriki kazi hiyo. “Siku ya sabato,” Luka anaandika, “tukatoka nje ya lango kando ya mto, ambapo tulikuwa tukifikiri kwamba palikuwa na mahali pa sala; nasi tukaketi na kuanza kusema na wanawake waliokuwa wamekusanyika.” Matokeo yalikuwa kwamba Lidia na watu wote wa nyumbani mwake walikubali habari njema na kubatizwa.—Matendo 16:11-15.

Upinzani ulitokea huko Filipi, ambako Paulo alimponya kijakazi aliyekuwa akibashiri kwa uwezo wa “roho mwovu wa uaguzi.” Mabwana wake walipoona kwamba chanzo chao cha mapato kimeondolewa, waliwashika Paulo na Sila. Baadaye Paulo na Sila walipigwa na kutupwa gerezani. Inaelekea kwamba Luka hakukamatwa, kwa sababu hajihusishi anapoeleza mambo yaliyowapata wenzake. Walipoachiliwa, ‘Paulo na Sila waliwatia moyo akina ndugu kisha wakaondoka.’ Baadaye Luka anaanza tena kujihusisha katika masimulizi hayo wakati Paulo anaporudi Filipi. (Matendo 16:16-40; 20:5, 6) Huenda Luka alibaki Filipi ili kusimamia kazi katika eneo hilo.

Kukusanya Habari

Luka alipata jinsi gani habari alizoandika katika Injili yake na katika kitabu cha Matendo? Sehemu za kitabu cha Matendo ambazo Luka anajihusisha katika masimulizi, zinaonyesha kwamba Luka alisafiri na Paulo kutoka Filipi kwenda Yerusalemu, ambako mtume huyo alikamatwa tena. Wakiwa njiani, Paulo na wenzake walikaa na Filipo, yule mweneza-injili huko Kaisaria. (Matendo 20:6; 21:1-17) Luka angeweza kupata habari kuhusu kazi ya mapema ya umishonari huko Samaria kutoka kwa Filipo mwenyewe, ambaye aliongoza kazi ya kuhubiri katika eneo hilo. (Matendo 8:4-25) Lakini Luka alipata habari kutoka vyanzo gani vingine?

Huenda miaka miwili ambayo Paulo alikaa kifungoni huko Kaisaria ilimpa Luka nafasi ya kufanya utafiti kuhusu masimulizi yake ya Injili. Hakuwa mbali na Yerusalemu ambako angeweza kuchunguza rekodi za ukoo wa Yesu. Luka aliandika matukio mengi kuhusu maisha na huduma ya Yesu, matukio ambayo hayasimuliwi katika zile Injili nyingine. Msomi mmoja ametaja matukio 82 kama hayo ya pekee.

Inawezekana kwamba Elizabeti mama ya Yohana Mbatizaji, ndiye aliyempasha Luka habari kuhusu kuzaliwa kwa Yohana. Huenda Maria mama ya Yesu, alimjulisha Luka kuhusu kuzaliwa kwa Yesu na maisha yake ya mapema. (Luka 1:5–80) Pengine Petro, Yakobo, au Yohana alimweleza Luka kuhusu muujiza wa kuvua samaki. (Luka 5:4-10) Tunasoma mifano fulani ya Yesu katika Injili ya Luka tu, mifano kama vile, mfano wa Msamaria mwema, wa mlango mwembamba, wa sarafu iliyopotea ya drakma, wa mwana mpotevu, na mfano wa tajiri na Lazaro.—Luka 10:29-37; 13:23, 24; 15:8-32; 16:19-31.

Luka alipendezwa sana na watu. Aliandika kuhusu toleo la kujitakasa la Maria, kuhusu kufufuliwa kwa mwana wa mjane, na kuhusu mwanamke aliyempaka Yesu mafuta miguuni. Luka anawataja wanawake waliomhudumia Kristo na anatueleza kwamba Martha na Maria walimkaribisha Yesu. Injili ya Luka inaeleza kuhusu kuponywa kwa mwanamke aliyepindika mgongo na mwanamume aliyekuwa na ugonjwa unaosababisha mwili kuvimba na pia kuhusu kutakaswa kwa watu kumi wenye ukoma. Luka anatueleza kumhusu Zakayo mfupi, aliyepanda juu ya mti ili amwone Yesu, naye anaandika kuhusu mtazamo wa mtenda-dhambi aliyetubu ambaye alitundikwa kando ya Kristo.—Luka 2:24; 7:11-17, 36-50; 8:2, 3; 10:38-42; 13:10-17; 14:1-6; 17:11-19; 19:1-10; 23:39-43.

Inapendeza kwamba Injili ya Luka inataja jinsi Msamaria mwema katika mfano wa Yesu alivyotibu majeraha. Inaelekea kwamba kwa sababu Luka alikuwa daktari, aliandika maelezo ya Yesu kuhusu msaada uliotolewa kutia ndani kutumia divai ili kuua viini, kutumia mafuta ili kutuliza maumivu, na kufunga majeraha.—Luka 10:30-37.

Mwandamani wa Mfungwa

Luka alimhangaikia mtume Paulo. Paulo alipokuwa kizuizini huko Kaisaria, mtawala Mroma aliyeitwa Feliksi aliamuru kwamba ‘yeyote kati ya watu wa Paulo,’ asikatazwe “kumhudumia.” (Matendo 24:23) Inaelekea kwamba Luka alikuwa mmoja wa wahudumu hao. Kwa kuwa nyakati nyingine Paulo hakuwa na afya njema, huenda kumhudumia kulitia ndani kutunzwa na huyo “tabibu mpendwa.”—Wakolosai 4:14; Wagalatia 4:13.

Paulo alipokata rufani kwa Kaisari, Festo mtawala Mroma alimtuma mtume huyo huko Roma. Luka aliandamana kwa ushikamanifu na mfungwa huyo aliposafirishwa kwa meli hadi Italia, naye aliandika simulizi lililo wazi kuhusu kuvunjika kwa meli yao. (Matendo 24:27; 25:9-12; 27:1, 9-44) Akiwa katika kifungo cha nyumbani huko Roma, Paulo aliandika barua kadhaa zilizoongozwa na roho, naye anamtaja Luka katika barua mbili. (Matendo 28:30; Wakolosai 4:14; Filemoni 24) Inaelekea kwamba Luka aliandika kitabu cha Matendo katika kipindi hicho cha miaka miwili.

Hapana shaka kwamba kulikuwa na shughuli nyingi za kiroho katika nyumba ya Paulo huko Roma. Akiwa hapo, Luka angeweza kukutana na wafanyakazi wengine wenzi wa Paulo, kama vile Tikiko, Aristarko, Marko, Yusto, Epafra, na Onesimo.—Wakolosai 4:7-14.

Paulo alipofungwa mara ya pili, wakati alipohisi kwamba kifo chake kilikuwa kimekaribia, Luka mwenye ushikamanifu na ujasiri alikuwa pamoja naye hata ingawa watu wengine walikuwa wamemwacha mtume huyo. Huenda Luka alihatarisha uhuru wake mwenyewe kwa kubaki na Paulo. Labda akitenda kama mwandishi, huenda Luka aliandika maneno haya ya Paulo: “Luka peke yake ndiye yupo pamoja nami.” Kulingana na mapokeo, Paulo aliuawa kwa kukatwa kichwa muda mfupi baadaye.—2 Timotheo 4:6-8, 11, 16.

Luka alikuwa mwenye kujidhabihu na mwenye kiasi. Hakujivunia masomo yake wala kujaribu kuwavutia watu. Ndiyo, kazi yake kuu maishani ingekuwa utabibu, lakini aliamua kuendeleza kazi ya Ufalme. Kama Luka, na tutangaze habari njema bila ubinafsi na kutumikia kwa unyenyekevu ili kumletea Yehova utukufu.—Luka 12:31.

[Sanduku katika ukurasa wa 19]

THEOFILO ALIKUWA NANI?

Luka anaelekeza Injili yake na pia kitabu cha Matendo ya Mitume kwa Theofilo. Katika Injili ya Luka, mwanamume huyo anaitwa “mtukufu Theofilo.” (Luka 1:3) “Mtukufu” lilikuwa jina la cheo la kumrejelea mtu mashuhuri aliyekuwa na mali nyingi sana au ofisa wa cheo cha juu katika serikali ya Roma. Mtume Paulo alimwita Festo mtawala Mroma wa jimbo la Yudea, kwa jina hilohilo la cheo.—Matendo 26:25.

Kwa wazi, Theofilo alikuwa amesikia ujumbe kumhusu Yesu na alipendezwa nao. Luka alitumaini kwamba masimulizi yake ya Injili yangemwezesha Theofilo ‘kujua kabisa uhakika wa mambo ambayo alikuwa amefundishwa kwa mdomo.’—Luka 1:4.

Kulingana na msomi Mgiriki Richard Lenski, inawezekana kwamba Theofilo hakuwa mwamini Luka alipomwita “mtukufu,” kwa kuwa “katika maandishi yote ya Kikristo, . . . hakuna ndugu Mkristo anayeheshimiwa kwa kuitwa kwa jina kama hilo la cheo.” Baadaye Luka alipoandika kitabu cha Matendo, hakutumia jina hilo la cheo, yaani, “mtukufu,” bali alisema: “Ee Theofilo.” (Matendo 1:1) Lenski anakata kauli hii: “Luka alipomwandikia Theofilo Injili yake, mtu huyo mashuhuri hakuwa Mkristo, hata hivyo, alipendezwa sana na mambo ya Ukristo; lakini Luka alipomwandikia kitabu cha Matendo, Theofilo alikuwa mwamini.”