Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Nahumu, cha Habakuki, na cha Sefania

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Nahumu, cha Habakuki, na cha Sefania

Neno la Yehova Liko Hai

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Nahumu, cha Habakuki, na cha Sefania

TAYARI serikali kuu ya ulimwengu ya Ashuru imeharibu Samaria, mji mkuu wa ufalme wa Israeli wa makabila kumi. Kwa muda mrefu, Ashuru limekuwa likitisha Yuda. Nabii Nahumu wa Yuda ana ujumbe kuhusu Ninawi, mji mkuu wa Ashuru. Kitabu cha Biblia cha Nahumu ambacho kiliandikwa kabla ya mwaka wa 632 K.W.K., kina ujumbe huo.

Serikali kuu inayoinuka ni Milki ya Babiloni, ambayo nyakati nyingine ilitawaliwa na wafalme Wakaldayo. Kitabu cha Habakuki, ambacho huenda kilikamilishwa mwaka wa 628 K.W.K., kinatabiri jinsi Yehova atakavyotumia serikali hiyo kuu ya ulimwengu kutekeleza hukumu yake na pia kinatabiri yale yatakayoipata Babiloni mwishowe.

Nabii Sefania wa Yuda alikuwa nabii kabla ya Nahumu na Habakuki. Akitoa unabii miaka zaidi ya 40 kabla ya Yerusalemu kuharibiwa mwaka wa 607 K.W.K., anatangaza ujumbe wa uharibifu na wa tumaini kwa Yuda. Pia, kitabu cha Biblia cha Sefania kina matangazo juu ya mataifa mengine.

“OLE WAKE JIJI LA UMWAGAJI WA DAMU”

(Nahumu 1:1–3:19)

“Tangazo juu ya Ninawi” linatoka kwa Yehova Mungu, ambaye “si mwepesi wa hasira naye ni mkuu katika nguvu.” Ingawa Yehova ni “ngome katika siku ya taabu” kwa wale wanaotafuta kimbilio kwake, Ninawi litaharibiwa.—Nahumu 1:1, 3, 7.

“Yehova atakusanya [atarudisha] fahari ya Yakobo.” Hata hivyo, Ashuru limekandamiza taifa la watu wa Mungu kama ‘simba anavyorarua-rarua vipande-vipande.’ Yehova ‘ataliteketeza gari la vita la Ninawi katika moshi. Na upanga utawameza wana-simba wake mwenyewe wenye manyoya shingoni.’ (Nahumu 2:2, 12, 13) “Ole wake jiji la umwagaji wa damu,” yaani, Ninawi. ‘Wote wanaosikia habari juu yake watalipigia makofi’ na kushangilia.—Nahumu 3:1, 19.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

1:9—“Maangamizi kamili” ya Ninawi yatakuwa na matokeo gani juu ya Yuda? Yuda itapata kitulizo cha kudumu kutokana na Ashuru; “taabu haitazuka mara ya pili.” Akizungumza kana kwamba Ninawi halipo tena, Nahumu anaandika hivi: “Tazama! Milimani, miguu ya mtu anayeleta habari njema, anayetangaza amani. Ee Yuda, fanya sherehe zako.”—Nahumu 1:15.

2:6Ni ‘milango gani ya mito’ iliyofunguliwa? Milango hiyo ilimaanisha njia iliyotengenezwa katika kuta za Ninawi na maji ya Mto Tigri. Mwaka wa 632 K.W.K. wakati majeshi ya muungano ya Wababiloni na Wamedi yalipokuja kupigana na Ninawi, jiji hilo halikutishwa hata kidogo. Ninawi lililokuwa limezungukwa na kuta ndefu, lilijiona kuwa jiji lisiloweza kupenywa. Hata hivyo, mvua kubwa ilinyesha na Mto Tigri ukafurika. Kulingana na mwanahistoria anayeitwa Diodorus, mto huo “ulibomoa sehemu ya jiji na kubomoa sehemu fulani ya kuta zake.” Hivyo, milango ya mito ilifunguliwa, na kama ilivyotabiriwa, Ninawi lilishindwa haraka kama moto unavyoteketeza majani makavu.—Nahumu 1:8-10.

3:4Ninawi lilikuwa kama kahaba namna gani? Ninawi lilidanganya mataifa kwa kuahidi kwamba lingefanya urafiki nayo na kuyasaidia, lakini kwa kweli liliyafunga katika nira ya uonevu. Kwa mfano, Ashuru ilimsaidia kwa kiasi fulani Mfalme Ahazi wa Yudea alipokabiliana na njama ya muungano wa Israeli na Siria. Hata hivyo, mwishowe ‘mfalme wa Ashuru akaja kupigana na Ahazi na kumtaabisha.’—2 Mambo ya Nyakati 28:20.

Mambo Tunayojifunza:

1:2-6. Hatua ya Yehova ya kulipiza kisasi juu ya maadui wake, ambao wanakataa kujitoa kikamili kwake, inaonyesha kwamba anawatazamia waabudu wake wajitoe kikamili.—Kutoka 20:5.

1:10. Kuta kubwa zenye mamia ya minara hazikuzuia neno la Yehova juu ya Ninawi lisitimizwe. Maadui wa watu wa Yehova leo hawataweza kuepuka hukumu zake kali.—Methali 2:22; Danieli 2:44.

“MWADILIFU, ATAENDELEA KUISHI”

(Habakuki 1:1–3:19)

Sura mbili za kwanza za kitabu cha Habakuki ni mazungumzo kati ya nabii huyo na Yehova Mungu. Akiwa amehuzunishwa na mambo yanayotukia Yuda, Habakuki anamuuliza Mungu hivi: “Kwa nini unanionyesha jambo lenye kudhuru, nawe unaendelea kutazama taabu tupu?” Yehova anamjibu hivi: “Ninawasimamisha Wakaldayo, taifa lenye uchungu na lenye haraka.” Nabii huyo anashangaa kwamba Mungu ataadhibu Yuda akitumia “wale wanaotenda kwa hila.” (Habakuki 1:3, 6, 13) Habakuki anahakikishiwa kwamba mwadilifu ataendelea kuishi, lakini adui hataepuka adhabu. Zaidi ya hayo, Habakuki anaandika ole tano ambazo zitaletwa juu ya maadui hao Wakaldayo.—Habakuki 2:4.

Katika sala ya kuomba rehema, Habakuki anarudia kutaja katika “nyimbo za huzuni,” matendo ya zamani yaliyoonyesha nguvu za Yehova zenye kutia woga kama yale aliyotenda katika Bahari Nyekundu, nyikani, na huko Yeriko. Nabii huyo anatabiri pia kuhusu wakati ambapo Yehova atasonga mbele akiwa na hasira ili kuangamiza wakati wa Har–Magedoni. Anamalizia sala hiyo kwa maneno haya: “Yehova Bwana Mwenye Enzi Kuu ndiye nguvu zangu; naye ataifanya miguu yangu kama ile ya paa, na mahali pangu pa juu atanitembeza.”—Habakuki 3:1, 19.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

1:5, 6—Kwa nini kuinuka kwa Wakaldayo juu ya Yerusalemu kulionekana kuwa jambo lisiloaminika kwa Wayahudi? Kufikia wakati ambapo Habakuki alianza kutoa unabii, Yuda ilikuwa chini ya uvutano wenye nguvu wa Misri. (2 Wafalme 23:29, 30, 34) Ingawa mamlaka ya Wababiloni ilikuwa ikiongezeka, jeshi lao bado halikuwa limemshinda Farao Neko. (Yeremia 46:2) Zaidi ya hayo, hekalu la Yehova lilikuwa Yerusalemu, na ufalme wa ukoo wa Daudi ulikuwa umetawala bila kukatishwa kutoka katika jiji hilo. Kwa Wayahudi walioishi wakati huo, “utendaji” wa Mungu wa kuruhusu Wakaldayo waharibu Yerusalemu ungeonekana kuwa usiowezekana. Hata hivyo, ingawa hawakuamini maneno ya Habakuki, maono kuhusu Wababiloni wakiharibu Yerusalemu ‘bila shaka yalitimia’ mwaka wa 607 K.W.K.—Habakuki 2:3.

2:5—“Mwanamume” huyo ni nani, na kwa nini “hatafikia mradi wake”? Wakiwa kikundi, Wababiloni waliotumia nguvu zao za kijeshi kuyashinda mataifa, walifananishwa na “mwanamume.” Ushindi ulimfanya awe kama mtu aliyelewa divai. Hata hivyo, hangefanikiwa kujikusanyia mataifa yote, kwa sababu Yehova angetumia Wamedi na Waajemi kumwangusha. Leo, “mwanamume” huyo anafananisha mamlaka za kisiasa. Mwanamume huyo pia amelewa kiburi na majivuno naye ana tamaa isiyoweza kutoshelezwa ya kupanua milki yake. Lakini hafikii mradi wake wa “kujikusanyia kwake mataifa yote.” Ufalme wa Mungu tu ndio utakaowaunganisha wanadamu.—Mathayo 6:9, 10.

Mambo Tunayojifunza:

1:1-4; 1:12–2:1. Habakuki aliuliza maswali manyoofu, na Yehova akamjibu. Mungu wa kweli anasikiliza sala za watumishi wake waaminifu.

2:1. Kama Habakuki, tunapaswa kuendelea kuwa macho kiroho na kuwa watendaji. Tunapaswa pia kuwa tayari kubadili mawazo yetu ili yapatane na ‘karipio’ au nidhamu yoyote ambayo huenda tukapokea.

2:3; 3:16. Tunapongojea kwa imani kuja kwa siku ya Yehova, tusipoteze kamwe mtazamo wetu wa uharaka.

2:4. Ili kuokoka siku ya hukumu ya Yehova inayokuja, ni lazima tuvumilie kwa uaminifu.—Waebrania 10:36-38.

2:6, 7, 9, 12, 15, 19. Bila shaka, ole itampata mtu mwenye pupa ya kupata pato lisilo la haki, anayependa jeuri, aliye na mwenendo mpotovu kingono, au anayeabudu sanamu. Ni lazima tujilinde ili tuepuke sifa na mazoea hayo.

2:11. Tusipofunua uovu wa ulimwengu huu, “jiwe litalia kwa huzuni.” Ni muhimu tuendelee kuhubiri kwa ujasiri ujumbe wa Ufalme!

3:6. Hakuna kitu kitakachomzuia Yehova kutekeleza hukumu yake, hata mashirika ya wanadamu ambayo yanaonekana kuwa ya kudumu kama milima na vilima hayatamzuia.

3:13. Tumehakikishiwa kwamba Har–Magedoni haitawaharibu watu wote. Yehova atawaokoa watumishi wake waaminifu.

3:17-19. Hata ingawa huenda tutakabili matatizo kabla na wakati wa Har–Magedoni, tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova atatupa “nguvu” tunapoendelea kumtumikia kwa shangwe.

“ILE SIKU YA YEHOVA IKO KARIBU”

(Sefania 1:1–3:20)

Ibada ya Baali imeenea sana katika Yuda. Yehova anasema hivi kupitia nabii wake Sefania: “Nitaunyoosha mkono wangu juu ya Yuda na wakaaji wote wa Yerusalemu.” Sefania anaonya hivi: “Ile siku ya Yehova iko karibu.” (Sefania 1:4, 7, 14) Wale tu wanaotimiza matakwa ya Mungu ndio ‘watakaofichwa’ katika siku hiyo.—Sefania 2:3.

“Ole . . . jiji lenye kukandamiza”—Yerusalemu! “‘Endeleeni kunitarajia,’ asema Yehova, ‘mpaka siku nitakaposimama kwenda kuteka nyara, kwa maana uamuzi wangu wa hukumu ni kukusanya mataifa . . . ili [niyamwagie] shutuma yangu.’ “ Lakini Mungu anaahidi hivi: “Nitawafanya ninyi kuwa jina na sifa kati ya vikundi vyote vya watu wa dunia, ninapowakusanya ili kuwarudisha mateka wenu mbele ya macho yenu.”—Sefania 3:1, 8, 20.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

2:13, 14—Ni ‘sauti ya nani itakuwa inaimba’ katika jiji la Ninawi lililobaki ukiwa kabisa? Kwa kuwa Ninawi lilipaswa kuwa mahali pa wanyama-mwitu na ndege, sauti ambayo ingekuwa inaimba ni sauti ya ndege wanaoimba na labda sauti ya upepo ukivuma kupitia madirisha ya nyumba zilizobaki ukiwa.

3:9—“Lugha safi” ni nini, na inazungumzwa jinsi gani? Lugha safi ni kweli ya Mungu iliyo katika Neno lake, Biblia. Inatia ndani mafundisho yote ya Biblia. Tunaizungumza tunapoamini kweli, tunapowafundisha wengine kwa njia inayofaa, na tunapoishi kupatana na mapenzi ya Mungu.

Mambo Tunayojifunza:

1:8. Inaonekana watu fulani katika siku za Sefania ‘walivaa mavazi ya kigeni’ ili wayapendeze mataifa yaliyowazunguka. Lingekuwa jambo la upumbavu kama nini kwa waabudu wa Yehova leo kujaribu kujipatanisha na ulimwengu kwa njia hiyo!

1:12; 3:5, 16. Yehova aliendelea kuwatuma manabii wake ili wawaonye watu wake kuhusu maamuzi yake ya hukumu. Alifanya hivyo hata ingawa Wayahudi wengi walikuwa kama machicha yaliyo ndani ya pipa la divai wakifuata njia zao kwa ushupavu na kupuuza ujumbe wake. Siku ya Yehova inapokaribia, badala ya kuruhusu mtazamo wa kutojali wa watu ufanye ‘mikono yetu ilegee,’ tunahitaji kuendelea kutangaza ujumbe wa Ufalme bila kuchoka.

2:3. Yehova peke yake ndiye anayeweza kutuokoa katika siku ya hasira yake. Ili tuendelee kuwa na kibali chake, tunahitaji ‘kumtafuta Yehova’ kwa kujifunza kwa uangalifu Neno lake, Biblia; kwa kusali ili tupate mwongozo wake; na kwa kumkaribia. Ni lazima ‘tutafute uadilifu’ kwa kuishi maisha safi kiadili. Na tunahitaji ‘kutafuta upole’ kwa kusitawisha mtazamo wa unyenyekevu na wa kujitiisha.

2:4-15; 3:1-5. Katika siku ambayo hukumu ya Yehova itatekelezwa, dini zinazodai kuwa za Kikristo na pia mataifa yote, ambayo yamewaonea watu wa Mungu, yataharibiwa kama Yerusalemu la kale na mataifa yaliyolizunguka. (Ufunuo 16:14, 16; 18:4-8) Tunapaswa kuendelea kutangaza hukumu za Mungu bila woga.

3:8, 9Tunapoingojea siku ya Yehova, tunajitayarisha kuokoka kwa kujifunza kuongea “lugha safi” na ‘kuliitia jina la Mungu’ kwa kujiweka wakfu kwake kibinafsi. Pia, tunamtumikia Yehova “bega kwa bega” tukishirikiana na watu wake na kumtolea “dhabihu ya sifa” kama zawadi.—Waebrania 13:15.

“Inaharakisha Sana”

Mtunga-zaburi aliimba hivi: “Bado muda kidogo tu, na mtu mwovu hatakuwako tena; nawe hakika utapaangalia mahali pake, naye hatakuwapo.” (Zaburi 37:10) Tunapotafakari mambo yaliyotabiriwa kuhusu Ninawi katika kitabu cha Nahumu, na kuhusu Babiloni na ufalme wa Yuda ulioasi imani katika kitabu cha Habakuki, hatuna shaka kwamba maneno ya mtunga-zaburi yatatimia. Hata hivyo, tunahitaji kungoja kwa muda gani zaidi?

Andiko la Sefania 1:14 linasema: “Ile siku kuu ya Yehova iko karibu.” (Sefania 1:14) “Iko karibu, nayo inaharakisha sana.” Kitabu cha Sefania pia kinatuonyesha jinsi tunavyoweza kufichwa katika siku hiyo na mambo ambayo ni lazima tufanye sasa ili tuokolewe. Kwa kweli, “neno la Mungu liko hai nalo lina nguvu.”—Waebrania 4:12.

[Picha katika ukurasa wa 8]

Kuta kubwa za Ninawi hazikuzuia unabii wa Nahumu usitimie

[Hisani]

Randy Olson/National Geographic Image Collection