Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mwige Mfanya-wanafunzi Mkuu

Mwige Mfanya-wanafunzi Mkuu

Mwige Mfanya-wanafunzi Mkuu

“Kazieni uangalifu jinsi mnavyosikiliza.”—LUKA 8:18.

1, 2. Kwa nini unapaswa kufikiria sana jinsi Yesu alivyoshughulika na watu katika huduma yake?

YESU KRISTO alikuwa akitimiza daraka lake akiwa Mwalimu Mkuu na Mfanya-Wanafunzi Mkuu alipowaambia wafuasi wake hivi: “Kazieni uangalifu jinsi mnavyosikiliza.” (Luka 8:16-18) Kanuni hiyo inatumika katika huduma yako ukiwa Mkristo. Ukisikiliza maagizo ya kiroho, utayatumia na kuwa mtangazaji wa Ufalme mwenye matokeo. Bila shaka, leo huwezi kuisikia sauti ya Yesu, lakini unaweza kusoma yale aliyosema na kufanya, kama yanavyofunuliwa katika Maandiko. Yanafunua nini kuhusu jinsi Yesu alivyowashughulikia watu katika huduma yake?

2 Yesu alikuwa mhubiri bora wa habari njema na mwalimu stadi sana wa kweli za Kimaandiko. (Luka 8:1; Yohana 8:28) Kazi ya kufanya wanafunzi inatia ndani kuhubiri na kufundisha. Hata hivyo, Wakristo fulani ambao ni wahubiri wenye kusifika wanaona ni vigumu kuwafundisha watu vizuri. Ingawa kuhubiri kunatia ndani kutangaza ujumbe, kwa kawaida ili kuwafundisha watu kumhusu Yehova na makusudi yake, ni lazima mwalimu ajenge uhusiano pamoja na mwanafunzi. (Mathayo 28:19, 20) Anaweza kufanya hivyo kwa kumwiga Yesu Kristo, yule Mwalimu Mkuu na Mfanya-Wanafunzi Mkuu.—Yohana 13:13.

3. Jitihada zako za kufanya wanafunzi zitakuwa na matokeo gani ukimwiga Yesu?

3 Ukiiga njia za Yesu za kufundisha, utakuwa ukifuata himizo hili la mtume Paulo: “Endeleeni kutembea kwa hekima kuelekea wale walio nje, mkijinunulia wakati unaofaa. Maneno yenu na yawe yenye neema sikuzote, yenye kukolezwa chumvi, ili mjue jinsi mnavyopaswa kumjibu kila mtu.” (Wakolosai 4:5, 6) Kumwiga Yesu katika kazi ya kufanya wanafunzi kunahitaji jitihada, lakini kufanya hivyo kutakuwezesha kufundisha vizuri kwa sababu kutakusaidia ‘umjibu kila mtu’ kulingana na uhitaji wake.

Yesu Aliwatia Wengine Moyo Wazungumze

4. Kwa nini inaweza kusemwa kwamba Yesu alikuwa msikilizaji mzuri?

4 Tangu akiwa mtoto, Yesu alikuwa na desturi ya kuwasikiliza watu na kuwatia moyo watoe maoni yao. Kwa mfano, alipokuwa na umri wa miaka 12, wazazi wake walimkuta katikati ya walimu hekaluni, “akiwasikiliza na kuwauliza maswali.” (Luka 2:46) Yesu hakwenda hekaluni ili kuwaaibisha walimu kwa ujuzi wake. Alienda huko ili kusikiliza, ingawa pia aliuliza maswali. Mwelekeo wake wa kusikiliza vizuri huenda ni moja ya sifa zilizomfanya apate kibali cha Mungu na wanadamu.—Luka 2:52.

5, 6. Tunajua jinsi gani kwamba Yesu aliwasikiliza wale ambao aliwafundisha?

5 Baada ya kubatizwa na kutiwa mafuta awe Masihi, Yesu aliendelea kuwasikiliza watu. Hakuwa mwenye shughuli nyingi sana za kuwafundisha watu hivi kwamba akawasahau wale waliokuja kumsikiliza. Mara nyingi, alitua kidogo, aliwauliza maoni yao, na kusikiliza majibu yao. (Mathayo 16:13-15) Kwa mfano, baada ya kifo cha Lazaro, ndugu ya Martha, Yesu alimwambia Martha hivi: “Kila mtu aliye hai na ananiamini hatakufa kamwe.” Kisha akamuuliza Martha: “Je, unaamini hilo?” Na bila shaka Yesu alisikiliza Martha alipomjibu hivi: “Ndiyo, Bwana; nimeamini kwamba wewe ndiye Kristo Mwana wa Mungu.” (Yohana 11:26, 27) Ilipendeza kama nini kumsikia Martha akieleza imani yake kwa njia hiyo!

6 Wanafunzi wengi walipomwacha Yesu, yeye alitaka kujua maoni ya mitume wake. Hivyo aliuliza hivi: “Je, ninyi pia mnataka kwenda?” Simoni Petro akamjibu: “Bwana, tutaenda kwa nani? Wewe una maneno ya uzima wa milele; na sisi tumeamini na tumejua kwamba wewe ndiye Mtakatifu wa Mungu.” (Yohana 6:66-69) Maneno hayo yalimfurahisha Yesu kama nini! Bila shaka, maneno kama hayo ya imani kutoka kwa mwanafunzi wa Biblia yatakufurahisha wewe pia.

Yesu Alisikiliza kwa Heshima

7. Kwa nini Wasamaria wengi walimwamini Yesu?

Sababu nyingine iliyomfanya Yesu awe na matokeo mazuri katika kazi ya kufanya wanafunzi ni kwamba aliwajali watu na kuwasikiliza kwa heshima. Kwa mfano, pindi moja Yesu alimhubiria mwanamke Msamaria karibu na chemchemi ya Yakobo huko Sikari. Wakati wa mazungumzo hayo, Yesu hakuzungumza tu; alimsikiliza mwanamke huyo. Alipokuwa akimsikiliza, Yesu alitambua kwamba alipendezwa na ibada na akamwambia kwamba Mungu alikuwa akitafuta watu ambao wangemwabudu kwa roho na kweli. Yesu alimheshimu na kumhangaikia mwanamke huyo, na hivyo mwanamke huyo akawaambia wengine kumhusu Yesu, na “wengi wa Wasamaria kutoka jiji hilo walimwamini kwa sababu ya neno la yule mwanamke.”—Yohana 4:5-29, 39-42.

8. Mwelekeo wa watu wa kutaka kutoa maoni yao unaweza kukusaidia jinsi gani kuanzisha mazungumzo katika huduma?

8 Kwa kawaida, watu wanafurahia kutoa maoni yao. Kwa mfano, wakaaji wa kale wa Athene walifurahia kutoa maoni yao na kusikiliza mambo mapya. Hilo lilimwongoza mtume Paulo kutoa hotuba iliyokuwa na matokeo mazuri kwenye Areopago katika jiji hilo. (Matendo 17:18-34) Unapoanza mazungumzo pamoja na mwenye nyumba katika huduma yako leo, unaweza kusema, “Ninakutembelea kwa sababu ningependa kujua maoni yako kuhusu [habari fulani].” Sikiliza maoni ya mtu huyo, na useme jambo fulani kuhusu maoni yake, au uliza swali kuhusu maoni hayo. Kisha, kwa fadhili mwonyeshe yale ambayo Biblia inasema juu ya habari hiyo.

Yesu Alijua Jinsi ya Kuanzisha Mazungumzo

9. Yesu alifanya nini kabla ya ‘kuwafungulia Maandiko’ Kleopa na msafiri mwenzake?

9 Yesu hakukosa kamwe jambo la kusema. Zaidi ya kuwa msikilizaji mzuri, mara nyingi Yesu alijua yale ambayo watu walikuwa wakifikiri, na alijua ni nini hasa alipaswa kusema. (Mathayo 9:4; 12:22-30; Luka 9:46, 47) Kwa mfano: Muda mfupi baada ya ufufuo wa Yesu, wanafunzi wawili walikuwa wakisafiri kwa miguu kutoka Yerusalemu kwenda Emau. Simulizi la Injili linasema hivi: “Walipokuwa wakiongea na kujadiliana, Yesu akakaribia, akaanza kutembea pamoja nao; lakini macho yao yalizuiwa wasiweze kumtambua. Akawaambia: ‘Ni mambo gani haya ambayo mnajadiliana kati yenu wenyewe mnapotembea?’ Nao wakasimama tuli wakiwa na nyuso zenye huzuni. Yule aliyeitwa Kleopa akajibu, akamwambia: ‘Je, wewe unakaa peke yako kama mgeni katika Yerusalemu na kwa hiyo huyajui mambo ambayo yametukia humo siku hizi?’ Naye akawaambia: ‘Mambo gani?’” Mwalimu Mkuu aliwasikiliza walipokuwa wakieleza kwamba Yesu Mnazareti aliwafundisha watu, alifanya miujiza, na aliuawa. Sasa watu wengine walikuwa wakisema kwamba alifufuliwa kutoka kwa wafu. Yesu alimwacha Kleopa na msafiri mwenzake wajieleze. Kisha, akawaeleza mambo waliyohitaji kujua, ‘akawafungulia Maandiko.’—Luka 24:13-27, 32.

10. Unaweza kujua jinsi gani maoni ya kidini ya mtu unayekutana naye katika huduma yako?

10 Huenda usijue jambo lolote kuhusu maoni ya kidini ya mwenye nyumba fulani. Ili kujua maoni yake, labda unaweza kusema kwamba ungependa kusikia yale ambayo watu wanafikiri kuhusu sala. Kisha unaweza kuuliza, “Je, unafikiri kweli kuna yeyote anayesikiliza sala?” Huenda jibu utakalopewa litafunua mengi kuhusu maoni ya mtu huyo na malezi yake ya kidini. Ikiwa anapendezwa na mambo ya kidini, huenda ukajua mengi zaidi kuhusu maoni yake kwa kuuliza, “Je, unafikiri Mungu anasikiliza sala zote, au huenda kuna sala nyingine ambazo hasikilizi?” Maswali kama hayo yanaweza kuongoza kwenye mazungumzo mazuri. Ikiwa inafaa kumwonyesha yale ambayo Biblia inasema kuhusu jambo hilo, utahitaji kufanya hivyo kwa busara, lakini hupaswi kushambulia imani ya mtu huyo. Ikiwa anafurahia kukusikiliza, huenda akataka umrudie. Lakini namna gani akiuliza swali ambalo huwezi kujibu? Unaweza kufanya utafiti fulani na kurudi ukiwa tayari kumtolea ‘sababu ya tumaini lililo ndani yako, lakini ukifanya hivyo kwa tabia-pole na heshima kubwa.’—1 Petro 3:15.

Yesu Alifundisha Wale Waliostahili

11. Ni nini kitakachokusaidia kuwapata watu wanaostahili kufundishwa?

11 Yesu, yule mtu mkamilifu, alikuwa na utambuzi ambao ulimwezesha kujua watu waliostahili kufundishwa. Si jambo rahisi kwetu kuwapata wale ‘walio na mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uzima wa milele.’ (Matendo 13:48) Ilikuwa hivyo pia kwa mitume ambao Yesu aliwaambia hivi: “Katika jiji lolote lile au kijiji chochote kile mtakapoingia, tafuteni ni nani humo anayestahili.” (Mathayo 10:11) Kama mitume wa Yesu, unapaswa pia kuwatafuta watu walio tayari kusikiliza na kufundishwa kweli za Kimaandiko. Unaweza kuwapata watu wanaostahili kwa kusikiliza kwa makini mtu mmoja baada ya mwingine, na kufikiria mtazamo wa kila mtu.

12. Unaweza kuendelea kumsaidia jinsi gani mtu anayependezwa?

12 Baada ya kuachana na mtu aliyependezwa kwa kadiri fulani na ujumbe wa Ufalme, ingefaa uendelee kufikiria mahitaji yake ya kiroho. Ukiandika mambo ambayo umejifunza baada ya kuzungumza na mtu fulani kuhusu habari njema, hilo litakusaidia kuendelea kumsaidia kiroho. Unapofanya ziara ya kurudia, unahitaji kusikiliza kwa makini ikiwa unataka kujifunza mengi zaidi kuhusu imani ya kidini, mtazamo, au hali za mtu huyo.

13. Ni nini kinachoweza kukusaidia kutambua maoni ya mtu kuhusu Biblia?

13 Unaweza jinsi gani kuwatia watu moyo wakueleze maoni yao kuhusu Neno la Mungu? Katika maeneo fulani, swali hili linafaa, “Je, unaona ni vigumu kuielewa Biblia?” Mara nyingi, jibu la swali hilo linafunua mtazamo wa mtu kuelekea mambo ya kiroho. Njia nyingine ni kusoma andiko na kuuliza, “Una maoni gani kuhusu hilo?” Kama Yesu, unaweza kutimiza mengi katika huduma yako kwa kutumia maswali vizuri. Hata hivyo, ni vizuri kuwa mwangalifu.

Yesu Alitumia Maswali Vizuri

14. Unaweza kuonyesha jinsi gani kwamba unapendezwa na maoni ya watu bila kuwahoji?

14 Pendezwa na maoni ya wengine bila kuwaaibisha. Iga njia za Yesu. Hakuuliza maswali bila busara, lakini aliuliza maswali ambayo yalichochea fikira. Pia, Yesu alikuwa msikilizaji mwenye fadhili ambaye aliwaburudisha watu wanyoofu na kuwafanya wastarehe. (Mathayo 11:28) Watu wa aina zote walijihisi huru kuzungumza naye kuhusu matatizo yao. (Marko 1:40; 5:35, 36; 10:13, 17, 46, 47) Ukitaka watu wajisikie huru kukueleza maoni yao kuhusu Biblia na mafundisho yake, unapaswa kuepuka kuwahoji.

15, 16. Unaweza kuanzisha jinsi gani mazungumzo na watu kuhusu mambo ya kidini?

15 Zaidi ya kutumia maswali vizuri, unaweza kumtia mtu moyo azungumze kwa kusema jambo fulani lenye kupendeza na kisha kusikiliza itikio lake. Kwa mfano, Yesu alimwambia Nikodemo hivi: “Mtu asipozaliwa tena, hawezi kuuona ufalme wa Mungu.” (Yohana 3:3) Maneno hayo yalikuwa yenye kuvutia sana hivi kwamba Nikodemo hangejizuia kuitikia na kumsikiliza Yesu. (Yohana 3:4-20) Wewe pia unaweza kuanzisha mazungumzo na watu kwa njia kama hiyo.

16 Leo, kutokea kwa dini nyingi mpya ni habari inayowavutia watu wengi barani Afrika, Ulaya Mashariki, na Amerika ya Latini. Katika maeneo kama hayo, mara nyingi unaweza kuanzisha mazungumzo kwa kusema hivi: “Sielewi kwa nini kuna dini nyingi mno. Lakini ninatumaini kuona hivi karibuni watu kutoka katika mataifa yote wakiunganishwa katika ibada ya kweli. Je, ungependa kuona jambo hilo likitukia?” Kwa kusema jambo fulani lenye kushangaza kuhusu tumaini lako, unaweza kuwachochea watu watoe maoni yao. Ni rahisi watu kujibu maswali wanapopewa nafasi ya kuchagua kati ya majibu mawili. (Mathayo 17:25) Baada ya mwenye nyumba kujibu swali lako, jibu swali hilo kwa kutumia andiko moja au mawili. (Isaya 11:9; Sefania 3:9) Ukimsikiliza kwa makini na kufikiria jibu lake, unaweza kujua yale mtakayozungumzia utakaporudi.

Yesu Aliwasikiliza Watoto

17. Ni nini kinachoonyesha kwamba Yesu alipendezwa na watoto?

17 Yesu hakupendezwa tu na watu wazima, bali pia na watoto. Alijua michezo ya watoto na mambo waliyozungumzia. Nyakati nyingine aliwaita watoto waje kwake. (Luka 7:31, 32; 18:15-17) Watoto wengi walikuwa kati ya umati wa watu waliomsikiliza Yesu. Wavulana walipopiga kelele wakimsifu Masihi, Yesu alitambua jambo hilo na kuonyesha kwamba Maandiko yalikuwa yamelitabiri. (Mathayo 14:21; 15:38; 21:15, 16) Leo, watoto wengi wanakuwa wanafunzi wa Yesu. Unaweza kuwasaidia jinsi gani?

18, 19. Unaweza jinsi gani kumsaidia kiroho mtoto wako?

18 Ili kumsaidia kiroho mtoto wako, unapaswa kumsikiliza. Unahitaji kuelewa mawazo yake ambayo huenda hayapatani na maoni ya Yehova. Hata mtoto wako akisema nini, ni jambo la hekima kumpongeza kwanza. Kisha unaweza kutumia maandiko kumsaidia mtoto wako kuelewa maoni ya Yehova kuhusu mambo.

19 Maswali yanaweza kukusaidia kutambua maoni ya watoto. Lakini watoto hawapendi hata kidogo kuulizwa-ulizwa maswali. Badala ya kumuuliza mtoto wako maswali magumu, kwa nini usiseme mambo machache yanayokuhusu wewe mwenyewe? Ikitegemea jambo mnalozungumzia, unaweza kumweleza jinsi ulivyokuwa ukihisi na kwa nini ulihisi hivyo. Kisha unaweza kumuuliza, “Je, wewe pia unahisi hivyo?” Jibu la mtoto wako linaweza kuongoza kwenye mazungumzo mazuri ya Kimaandiko yenye kujenga.

Endelea Kumwiga Mfanya-Wanafunzi Mkuu

20, 21. Kwa nini unapaswa kuwa msikilizaji mzuri katika kazi yako ya kufanya wanafunzi?

20 Iwe unazungumzia jambo fulani na mtoto wako au na mtu mwingine yeyote, ni lazima usikilize kwa makini. Kwa kweli, kufanya hivyo ni uthibitisho wa upendo. Kwa kusikiliza, unatenda kwa njia ya unyenyekevu, na hivyo unamheshimu na kumhangaikia kwa upendo msikilizaji wako. Bila shaka, kusikiliza kunamaanisha kukazia uangalifu yale ambayo mtu huyo anasema.

21 Unaposhiriki katika huduma ya Kikristo, endelea kuwasikiliza wenye nyumba kwa makini. Ikiwa unasikiliza kwa makini sana yale wanayosema, inaelekea utatambua ni kweli gani za Biblia zitakazowavutia. Kisha, jitahidi kuwasaidia kwa kutumia njia mbalimbali za kufundisha ambazo Yesu alitumia. Ukifanya hivyo, utathawabishwa kwa kuwa mwenye shangwe na uradhi kwa sababu unamwiga Mfanya-Wanafunzi Mkuu.

Ungetoa Jibu Gani?

• Yesu aliwatia wengine moyo jinsi gani watoe maoni yao?

• Kwa nini Yesu aliwasikiliza wale ambao alifundisha?

• Unaweza kutumia maswali kwa njia gani katika huduma yako?

• Unaweza kufanya nini ili kuwasaidia watoto kiroho?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 28]

Unapohubiri, sikiliza kwa makini

[Picha katika ukurasa wa 30]

Tunamwiga Yesu tunapowasaidia kiroho watoto