Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sitawisha Sifa Zinazoweza Kukusaidia Kufanya Wanafunzi

Sitawisha Sifa Zinazoweza Kukusaidia Kufanya Wanafunzi

Sitawisha Sifa Zinazoweza Kukusaidia Kufanya Wanafunzi

“Nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.”—MATHAYO 28:19.

1. Watumishi fulani wa Mungu nyakati za kale walihitaji kusitawisha ustadi na mitazamo gani?

NYAKATI nyingine, ni lazima watumishi wa Yehova wasitawishe ustadi na mitazamo ambayo itawasaidia kufanya mapenzi yake. Kwa mfano, kwa kutii amri ya Mungu, Abrahamu na Sara walitoka jiji la Uru lenye ufanisi na baadaye wakahitaji kusitawisha sifa na uwezo mbalimbali ambao watu walioishi ndani ya mahema walistahili kuwa nao. (Waebrania 11:8, 9, 15) Ili kuwaongoza Waisraeli katika Nchi ya Ahadi, Yoshua alihitaji ujasiri, kumtegemea Yehova, na kujua Sheria yake. (Yoshua 1:7-9) Na ustadi wowote ambao huenda tayari Bezaleli na Oholiabu walikuwa nao, uliboreshwa au kuongezwa na roho ya Mungu ili wanaume hao washiriki na kusimamia kwa mafanikio ujenzi wa maskani na kazi iliyohusiana nayo.—Kutoka 31:1-11.

2. Tutazungumzia maswali gani yanayohusiana na kazi ya kufanya wanafunzi?

2 Karne nyingi baadaye, Yesu Kristo aliwaagiza hivi wafuasi wake: “Nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, . . . na kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi.” (Mathayo 28:19, 20) Kabla ya hapo, watu hawakuwa wamepewa pendeleo la kufanya kazi kubwa kama hiyo. Ni sifa gani zinazohitajiwa katika kazi ya kufanya wanafunzi? Tunaweza jinsi gani kusitawisha sifa hizo?

Onyesha Unampenda Sana Mungu

3. Amri ya kufanya wanafunzi inatupa nafasi gani?

3 Ili kuzungumza na watu na kujitahidi kuwasadikisha wamwabudu Mungu wa kweli, tunahitaji kumpenda sana Yehova. Waisraeli wangeweza kuthibitisha kwamba walimpenda Mungu kwa kutii kwa moyo wote amri zake, kwa kutoa dhabihu zilizokubalika, na kwa kumsifu kwa nyimbo. (Kumbukumbu la Torati 10:12, 13; 30:19, 20; Zaburi 21:13; 96:1, 2; 138:5) Tukiwa wafanya-wanafunzi, sisi pia tunatii amri za Mungu, lakini tunaonyesha pia upendo wetu kwa Yehova kwa kuzungumza na wengine kumhusu yeye na makusudi yake. Tunahitaji kusema kwa usadikisho na kuchagua maneno yanayofaa ili kuonyesha jinsi tunavyohisi kikweli kuhusu tumaini letu tulilopewa na Mungu.—1 Wathesalonike 1:5; 1 Petro 3:15.

4. Kwa nini Yesu alifurahia kuwafundisha watu kumhusu Yehova?

4 Kwa kuwa alimpenda sana Yehova, Yesu alifurahia sana kuzungumza kuhusu makusudi ya Mungu, Ufalme, na ibada ya kweli. (Luka 8:1; Yohana 4:23, 24, 31) Kwa kweli, Yesu alisema: “Chakula changu ni mimi kufanya mapenzi yake aliyenituma na kuimaliza kazi yake.” (Yohana 4:34) Maneno haya ya mtunga-zaburi yanamhusu Yesu: “Ee Mungu wangu, nimependezwa na kufanya mapenzi yako, na sheria yako imo ndani yangu. Nimetangaza habari njema ya uadilifu katika kutaniko kubwa. Tazama! Siizuii midomo yangu. Ee Yehova, wewe mwenyewe unajua hivyo vema.”—Zaburi 40:8, 9; Waebrania 10:7-10.

5, 6. Wafanya-wanafunzi wanahitaji kuwa na sifa gani kuu?

5 Wakichochewa na upendo kwa Mungu, nyakati nyingine wapya ambao wamejifunza kweli za Biblia hivi karibuni wanasema kwa usadikisho mwingi kumhusu Yehova na Ufalme wake hivi kwamba wanakuwa na matokeo sana katika kuwasadikisha wengine wayachunguze Maandiko. (Yohana 1:41) Kumpenda Mungu ni sifa kuu ambayo inatuchochea katika kazi ya kufanya wanafunzi. Hivyo basi, tuendelee kudumisha upendo huo kwa kusoma na kutafakari Neno lake kwa ukawaida.—1 Timotheo 4:6, 15; Ufunuo 2:4.

6 Bila shaka, kumpenda Yehova kulimsaidia Yesu Kristo kuwa mwalimu mwenye bidii. Lakini hiyo haikuwa sababu pekee iliyomfanya awe mhubiri wa Ufalme mwenye matokeo. Hivyo basi, ni sifa gani nyingine iliyomfanya Yesu apate mafanikio katika kazi ya kufanya wanafunzi?

Wahangaikie Watu kwa Upendo

7, 8. Yesu alikuwa na maoni gani kuhusu watu?

7 Yesu aliwahangaikia watu na alipendezwa sana nao. Hata kabla ya kuwa mwanadamu na akiwa “stadi wa kazi” wa Mungu, Yesu alipendezwa na vitu vilivyohusiana na wanadamu. (Methali 8:30, 31) Akiwa mwanadamu duniani, Yesu aliwahurumia watu, na akawaburudisha wale waliokuja kwake. (Mathayo 11:28-30) Yesu alionyesha upendo na huruma ya Yehova, na jambo hilo liliwavuta watu kwenye ibada ya Mungu wa pekee wa kweli. Watu wa namna zote walimsikiliza Yesu kwa sababu aliwahangaikia kwa upendo na kufikiria hali zao.—Luka 7:36-50; 18:15-17; 19:1-10.

8 Mwanamume fulani alipomuuliza Yesu kile ambacho alihitaji kufanya ili aurithi uzima wa milele, ‘Yesu alimtazama na kumpenda.’ (Marko 10:17-21) Kuhusu watu fulani ambao walifundishwa na Yesu huko Bethania, tunasoma hivi: “Yesu alimpenda Martha na dada yake na Lazaro.” (Yohana 11:1, 5) Yesu aliwajali sana watu hivi kwamba badala ya kupumzika, aliamua kuwafundisha. (Marko 6:30-34) Kuwahangaikia sana wanadamu wenzake kwa upendo kulimfanya Yesu awe na matokeo zaidi kuliko mtu mwingine yeyote yule katika kuwavuta watu kwenye ibada ya kweli.

9. Paulo alikuwa na mtazamo gani akiwa mfanya-wanafunzi?

9 Pia, mtume Paulo alipendezwa sana na watu aliowahubiria. Kwa mfano, aliwaambia hivi wale ambao waligeuka na kuwa Wakristo huko Thesalonike: “Tukiwa na upendo mwororo kwa ajili yenu, tulipendezwa vema kuwapa ninyi, si habari njema ya Mungu tu, bali pia nafsi zetu wenyewe, kwa sababu ninyi mlikuwa wapendwa kwetu.” Kwa sababu ya jitihada zenye upendo za Paulo, watu fulani huko Thesalonike ‘walitoka kwenye ibada ya sanamu ili kumtumikia Mungu aliye hai.’ (1 Wathesalonike 1:9; 2:8) Tukiwahangaikia watu kikweli kama walivyofanya Yesu na Paulo, huenda sisi pia tukafurahia kuona habari njema ikifikia mioyo ya wale ambao ‘wana mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uzima wa milele.’—Matendo 13:48.

Onyesha Roho ya Kujidhabihu

10, 11. Kwa nini roho ya kujidhabihu inahitajiwa tunapojaribu kufanya wanafunzi?

10 Wale wanaopata matokeo katika kazi ya kufanya wanafunzi wana roho ya kujidhabihu. Bila shaka, hawaoni kupata mali kuwa jambo la maana zaidi. Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Jinsi itakavyokuwa vigumu kwa wale wenye pesa kuingia katika ufalme wa Mungu!” Wanafunzi walishangaa waliposikia maneno hayo, lakini Yesu aliongeza hivi: “Wanangu, jinsi ilivyo vigumu kuingia katika ufalme wa Mungu! Ni rahisi zaidi ngamia kupita katika tundu la sindano kuliko tajiri kuingia katika ufalme wa Mungu.” (Marko 10:23-25) Yesu aliwapendekezea wafuasi wake waishi maisha rahisi ili wakazie fikira kazi ya kufanya wanafunzi. (Mathayo 6:22-24, 33) Kwa nini roho ya kujidhabihu inatusaidia katika kazi ya kufanya wanafunzi?

11 Jitihada nyingi zinahitajiwa ili kufundisha mambo yote ambayo Yesu aliamuru. Kwa kawaida, Mkristo anayetaka kufanya wanafunzi anajitahidi kujifunza Biblia kila juma na mtu anayependezwa. Ili kupata nafasi zaidi za kuwatafuta watu wanyoofu, wahubiri fulani wa Ufalme wameacha kazi ya wakati wote na kutafuta kazi ya muda. Maelfu ya Wakristo wamejifunza lugha nyingine ili kuwahubiria watu wa makabila fulani katika eneo lao. Wakristo wengine wanaoshiriki katika kazi ya kufanya wanafunzi wamehama makwao na kwenda katika eneo au nchi nyingine ili kushiriki kwa ukamili zaidi katika mavuno. (Mathayo 9:37, 38) Yote hayo yanahitaji roho ya kujidhabihu. Lakini mengi zaidi yanahitajiwa ili kuwa na matokeo katika kazi ya kufanya wanafunzi.

Uwe Mwenye Subira Lakini Usipoteze Wakati

12, 13. Kwa nini subira ni ya maana sana katika kufanya wanafunzi?

12 Subira ni sifa nyingine ambayo inatusaidia kufanya wanafunzi. Watu wanahitaji kuchukua hatua ya haraka wanaposikia ujumbe wetu wa Kikristo, lakini mara nyingi kufanya wanafunzi kunachukua wakati mrefu na kunahitaji subira. (1 Wakorintho 7:29) Yesu alikuwa mwenye subira kumwelekea ndugu yake wa kambo, Yakobo. Ingawa inaelekea Yakobo alijua vizuri kazi ya Yesu ya kuhubiri, kwa muda fulani alisitasita kuwa mwanafunzi wake. (Yohana 7:5) Hata hivyo, katika kipindi kifupi kati ya kifo cha Kristo na Pentekoste 33 W.K., inaonekana kwamba Yakobo alikuja kuwa mwanafunzi, kwa kuwa Maandiko yanadokeza kwamba alikusanyika kwa ajili ya sala pamoja na mama yake, ndugu zake, na mitume. (Matendo 1:13, 14) Yakobo alifanya maendeleo mazuri ya kiroho, na baadaye akawa na madaraka mazito katika kutaniko la Kikristo.—Matendo 15:13; 1 Wakorintho 15:7.

13 Kama wakulima, Wakristo wanakuza sifa ambazo mara nyingi zinakua polepole, yaani, uelewaji wa Neno la Mungu, upendo kwa Yehova, na roho kama ya Kristo. Subira inahitajiwa ili kukuza sifa hizo. Yakobo aliandika hivi: “Onyesheni subira, akina ndugu, mpaka kuwapo kwa Bwana. Tazama! Mkulima huendelea kungojea matunda yenye thamani ya nchi, anayasubiri mpaka apate mvua ya mapema na mvua ya baadaye. Ninyi pia onyesheni subira; fanyeni mioyo yenu kuwa imara, kwa sababu kuwapo kwa Bwana kumekaribia.” (Yakobo 5:7, 8) Yakobo alikuwa akiwahimiza waamini wenzake ‘waonyeshe subira mpaka kuwapo kwa Bwana.’ Ikiwa wanafunzi hawakuelewa jambo fulani, kwa subira Yesu alieleza au kutoa mfano ili kuwasaidia. (Mathayo 13:10-23; Luka 19:11; 21:7; Matendo 1:6-8) Kwa kuwa sasa Bwana yupo, sisi pia tunahitaji kuwa wenye subira tunapojitahidi kufanya wanafunzi. Wale ambao wanakuwa wafuasi wa Yesu katika siku zetu wanahitaji kufundishwa kwa subira.—Yohana 14:9.

14. Ingawa sisi ni wenye subira, tunaweza jinsi gani kutumia kwa hekima wakati wetu tukiwa wafanya-wanafunzi?

14 Hata ingawa sisi ni wenye subira, neno halizai matunda ndani ya mioyo ya watu wengi ambao tumeanza kujifunza nao Biblia. (Mathayo 13:18-23) Kwa hiyo, baada ya kufanya jitihada za kutosha ili kuwasaidia, kwa hekima tunapaswa kuacha kutumia wakati wetu pamoja na watu kama hao na kujaribu kutafuta wale ambao huenda watathamini zaidi kweli ya Biblia. (Mhubiri 3:1, 6) Bila shaka, huenda hata watu ambao wanaithamini kweli ya Biblia wakahitaji kusaidiwa zaidi ili wabadili maoni yao, mitazamo yao, na mambo wanayotanguliza maishani. Hivyo, tunakuwa wenye subira kama Yesu alivyokuwa mwenye subira kuelekea wanafunzi wake ambao walikuwa na tatizo la kusitawisha mtazamo unaofaa.—Marko 9:33-37; 10:35-45.

Sitawisha Ufundi wa Kufundisha

15, 16. Kwa nini kueleza mambo kwa njia rahisi na kujitayarisha vizuri ni muhimu tunapofanya wanafunzi?

15 Kumpenda Mungu, kuwahangaikia watu, roho ya kujidhabihu, na subira ni mambo ya maana ili kufanikiwa katika kazi ya kufanya wanafunzi. Pia, ustadi wa kufundisha unahitaji kusitawishwa, kwa kuwa unatuwezesha kueleza mambo waziwazi na kwa njia rahisi. Kwa mfano, maneno mengi ya Mwalimu Mkuu, Yesu Kristo, yalikuwa yenye matokeo hasa kwa sababu yalikuwa rahisi. Inaelekea unakumbuka maneno kama haya ya Yesu: “Jiwekeeni hazina mbinguni.” “Msiwape mbwa kitu kitakatifu.” “Hekima huonyeshwa kuwa yenye uadilifu kwa matendo yake.” “Mlipeni Kaisari vitu vya Kaisari, lakini Mungu vitu vya Mungu.” (Mathayo 6:20; 7:6; 11:19; 22:21) Bila shaka, Yesu hakutumia tu semi fupifupi. Alifundisha kwa njia iliyokuwa wazi na akaeleza mambo kwa wakati uliofaa. Unaweza kuiga jinsi gani njia ya Yesu ya kufundisha?

16 Kujitayarisha kwa uangalifu ni jambo la maana ili kufundisha kwa njia rahisi na iliyo wazi. Mhudumu ambaye hakujitayarisha ana mwelekeo wa kuzungumza kupita kiasi. Huenda asiweke wazi mambo makuu kwa sababu anazungumza sana, akisema kila jambo ambalo anajua kuhusu habari hiyo. Tofauti na hilo, mhudumu ambaye amejitayarisha vizuri anamfikiria mwanafunzi, anatafakari kuhusu habari, na anaeleza waziwazi mambo yanayohitajiwa tu. (Methali 15:28; 1 Wakorintho 2:1, 2) Anafikiria habari ambazo tayari mwanafunzi anajua na mambo yanayopaswa kukaziwa wakati wa funzo. Huenda mhudumu akajua mambo mengi yenye kupendeza kuhusu habari hiyo, lakini ili habari iwe wazi ni lazima aepuke habari ambazo si za lazima.

17. Tunaweza kuwasaidia jinsi gani watu wafikiri kwa kutumia Maandiko?

17 Pia, Yesu aliwasaidia watu kufikiri, badala ya kuwapa habari tu. Kwa mfano, katika pindi moja, aliuliza hivi: “Unaonaje, Simoni? Wafalme wa dunia hupokea ushuru au kodi ya kichwa kutoka kwa nani? Kutoka kwa wana wao au kutoka kwa wageni?” (Mathayo 17:25) Huenda tukafurahia sana kuifafanua Biblia hivi kwamba tunahitaji kujizuia ili kumruhusu mwanafunzi ajieleze au aeleze jambo mnalozungumzia katika funzo la Biblia la nyumbani. Kwa kawaida, hatupaswi kuwauliza watu maswali mengi. Badala yake, tukitoa mifano mizuri kwa busara na tukiuliza maswali yaliyofikiriwa vizuri, tunaweza kuwasaidia waelewe mawazo ya Biblia yaliyo katika vichapo vyetu vya Biblia.

18. Ni nini kinachohusika katika kusitawisha “ufundi wa kufundisha”?

18 Maandiko yanasema kuhusu “ufundi wa kufundisha.” (2 Timotheo 4:2; Tito 1:9) Uwezo huo wa kufundisha unatia ndani mengi zaidi ya kumsaidia mtu aweke akilini mambo hakika. Tunapaswa kujaribu kumsaidia mwanafunzi wa Biblia aelewe tofauti kati ya kweli na uwongo, lililo zuri na lililo baya, hekima na upumbavu. Tunapofanya hivyo na kujitahidi kumsaidia mtu ampende Yehova kutoka moyoni, huenda akaona kwa nini anapaswa kumtii Yehova.

Shiriki kwa Bidii Katika Kazi ya Kufanya Wanafunzi

19. Wakristo wote wanaweza kusaidia jinsi gani katika kufanya wanafunzi?

19 Kutaniko la Kikristo ni tengenezo la kufanya wanafunzi. Mtu mpya anapokuwa mwanafunzi, wengine wanashangilia kutia ndani Shahidi wa Yehova aliyempata na kumsaidia kujifunza yale ambayo Biblia inafundisha. Kikundi cha watu kinapokuwa katika shughuli za kumtafuta mtoto aliyepotea, huenda mtu mmoja tu katika kikundi hicho ndiye atakayempata mtoto huyo. Lakini mtoto huyo anapoungana tena na wazazi wake, kila mtu aliyehusika katika shughuli hiyo ya kumtafuta anashangilia. (Luka 15:6, 7) Vivyo hivyo, kutaniko lote linahusika katika kazi ya kufanya wanafunzi. Wakristo wote wanashiriki katika kuwatafuta wale ambao huenda wakawa wanafunzi wa Yesu. Na mtu mpya anapoanza kuhudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme, kila Mkristo katika Jumba la Ufalme anamsaidia mtu huyo kuithamini zaidi ibada ya kweli. (1 Wakorintho 14:24, 25) Hivyo, Wakristo wote wanaweza kushangilia kwamba mamia ya maelfu ya wanafunzi wapya wanafanywa kila mwaka.

20. Unapaswa kufanya nini ikiwa unataka kuwafundisha wengine kweli ya Biblia?

20 Wakristo wengi waaminifu wangefurahi kumfundisha mtu fulani kumhusu Yehova na ibada ya kweli. Hata hivyo, huenda wasiweze kufanya hivyo hata wakijitahidi kadiri gani. Ikiwa hiyo ndiyo hali yako, endelea kuimarisha upendo wako kwa Yehova, wahangaikie watu, jidhabihu, uwe mwenye subira, na ujitahidi kuboresha ustadi wako wa kufundisha. Zaidi ya yote, sali kuhusu tamaa yako ya kufundisha kweli. (Mhubiri 11:1) Pata faraja kwa kujua kwamba kila jambo unalofanya katika utumishi wa Yehova linasaidia katika kazi ya kufanya wanafunzi ambayo inamtukuza Mungu.

Je, Unaweza Kueleza?

• Kwa nini kazi ya kufanya wanafunzi inajaribu upendo wetu kwa Mungu?

• Ni sifa gani zinazohitajiwa na wafanya-wanafunzi?

• “Ufundi wa kufundisha” unatia ndani nini?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 21]

Kwa kufanya wanafunzi, Wakristo wanaonyesha wanampenda sana Mungu

[Picha katika ukurasa wa 23]

Kwa nini Wakristo wanaofanya wanafunzi wanapaswa kupendezwa na wengine?

[Picha katika ukurasa wa 24]

Ni baadhi ya sifa gani ambazo wafanya-wanafunzi wanahitaji?

[Picha katika ukurasa wa 25]

Wakristo wote wanasisimka wanapoona matokeo mazuri ya kazi ya kufanya wanafunzi