Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Enzi Kuu ya Yehova na Ufalme wa Mungu

Enzi Kuu ya Yehova na Ufalme wa Mungu

Enzi Kuu ya Yehova na Ufalme wa Mungu

“Ee Yehova, ukuu ni wako na nguvu na uzuri na utukufu na heshima . . . Ufalme ni wako, Ee Yehova.”—1 MAMBO YA NYAKATI 29:11.

1. Kwa nini Yehova ana haki ya kuwa Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu wote?

“YEHOVA amekifanya imara kiti chake cha ufalme mbinguni; nao ufalme wake mwenyewe umetawala juu ya kila kitu.” (Zaburi 103:19) Kwa maneno hayo, mtunga-zaburi alitaja kweli ya msingi kuhusu utawala. Yehova Mungu, akiwa Muumba, ana haki ya kuwa Mtawala Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu wote.

2. Danieli alisema nini kuhusu makao ya roho ya Yehova?

2 Bila shaka, ili mtawala awe na enzi ni lazima awe na raia. Kwanza, Yehova alitawala viumbe wa roho ambao aliwaumba, akianza na Mwana wake mzaliwa-pekee na kisha majeshi ya kimalaika. (Wakolosai 1:15-17) Baada ya muda mrefu sana kupita, nabii Danieli alipewa maono ya kimbingu. Alisema hivi: “Nikaendelea kutazama mpaka viti vya ufalme vikawekwa na Mzee wa Siku akaketi. . . . Kulikuwa na maelfu elfu walioendelea kumtumikia, na elfu kumi mara elfu kumi walioendelea kusimama mbele zake.” (Danieli 7:9, 10) Kwa miaka mingi sana Yehova, yule “Mzee wa Siku,” akiwa Mwenye Enzi Kuu aliongoza familia yake kubwa sana ya wana wa roho iliyopangwa vizuri. Wana hao walitumika wakiwa “wahudumu” wanaofanya mapenzi yake.—Zaburi 103:20, 21.

3. Enzi kuu ya Yehova ilipanuka jinsi gani kufikia ulimwengu halisi?

3 Mwishowe, Yehova alipanua utawala wake kwa kuumba ulimwengu halisi ambao ni mkubwa na tata, kutia ndani dunia. (Ayubu 38:4,7) Mtu anayetazama nyota na sayari akiwa duniani anaweza kufikiri kwamba hazihitaji mtu wa kuziongoza au kuzielekeza kwa sababu zinafuata utaratibu wa hali ya juu sana. Hata hivyo, mtunga-zaburi alitangaza hivi: “[Yehova] mwenyewe aliamuru, navyo vikaumbwa. Naye huendelea kuvisimamisha milele, mpaka wakati usio na kipimo. Amelitoa sharti, nalo halitapitilia mbali.” (Zaburi 148:5, 6) Kwa muda wote, Yehova amekuwa akitumia enzi yake kuu kuelekeza na kuongoza utendaji katika makao ya roho na katika ulimwengu halisi.—Nehemia 9:6.

4. Yehova anatawala namna gani akiwa Mwenye Enzi Kuu juu ya wanadamu?

4 Alipoumba wanadamu wawili wa kwanza, Mungu alitumia enzi yake kuu katika njia nyingine. Zaidi ya kuwapa wanadamu kila kitu walichohitaji ili waishi maisha yenye kuridhisha na yaliyo na kusudi, Yehova aliwapa mamlaka ya kutawala viumbe wa hali ya chini duniani. (Mwanzo 1:26-28; 2:8, 9) Basi, ni wazi kwamba Mungu hatawali tu kwa upendo na fadhili, bali pia anawaheshimu na kuwastahi watu ambao anawatawala. Maadamu Adamu na Hawa walijitiisha chini ya enzi kuu ya Yehova, walikuwa na tumaini la kuishi milele katika paradiso duniani.—Mwanzo 2:15-17.

5. Tunaweza kusema nini kuhusu utawala wa Yehova akiwa Mwenye Enzi Kuu?

5 Tunaweza kukata kauli gani kutokana na mambo hayo yote? Kwanza, sikuzote Yehova amekuwa mwenye enzi kuu wa uumbaji wake wote. Pili, Mungu anatawala kwa upendo na heshima. Tatu, tukitii na kuunga mkono utawala wa Mungu tutapata baraka za milele. Si ajabu kwamba Mfalme Daudi wa Israeli la kale alichochewa kusema hivi: “Ee Yehova, ukuu ni wako na nguvu na uzuri na utukufu na heshima; kwa maana kila kitu mbinguni na duniani ni chako. Ufalme ni wako, Ee Yehova, Wewe unayejiinua kuwa kichwa juu ya wote.”—1 Mambo ya Nyakati 29:11.

Kwa Nini Ufalme wa Mungu Unahitajiwa?

6. Kuna uhusiano gani kati ya enzi kuu ya Mungu na Ufalme wake?

6 Kwa kuwa sikuzote Yehova, ambaye ni Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote, amekuwa akitumia nguvu na uwezo wake, kwa nini Ufalme wa Mungu unahitajiwa? Kwa kawaida, mtawala anatawala kupitia wawakilishi fulani ambao amewaweka juu ya raia. Kwa hiyo, Ufalme wa Mungu ni wonyesho au njia ambayo Mungu anatumia kutawala viumbe wake akiwa mwenye enzi kuu ya ulimwengu wote.

7. Kwa nini Yehova alianzisha wonyesho mpya wa enzi yake kuu?

7 Yehova ametumia enzi yake kuu kwa njia tofauti-tofauti nyakati mbalimbali. Alianzisha wonyesho mpya wa enzi yake kuu kwa sababu ya tukio fulani jipya. Huo ni wakati ambapo Shetani, mwana mwasi wa roho wa Mungu aliwashawishi Adamu na Hawa na kuwafanya waasi utawala wa Yehova. Uasi huo ulishambulia enzi kuu ya Mungu. Kwa njia gani? Alipomwambia Hawa kwamba ‘hakika hangekufa’ ikiwa angekula matunda yaliyokatazwa, Shetani alidokeza kwamba Yehova alikuwa mwongo, na hivyo hangeweza kutumainika. Zaidi ya hayo, Shetani alimwambia Hawa hivi: “Mungu anajua kwamba siku ileile mtakapokula matunda yake macho yenu yatafunguliwa, nanyi mtakuwa kama Mungu, mkijua mema na mabaya.” Shetani alikuwa akidokeza kwamba Adamu na Hawa wangekuwa na maisha mazuri ikiwa wangepuuza amri ya Mungu na kuamua kujitegemea. (Mwanzo 3:1-6) Shetani alipinga moja kwa moja haki ya Mungu ya kutawala. Yehova angefanya nini?

8, 9. (a) Mtawala mwanadamu angekabiliana jinsi gani na uasi katika milki yake? (b) Yehova alifanya nini ili kukabiliana na uasi katika Edeni?

8 Tunatazamia mtawala afanye nini kunapokuwa na uasi wa moja kwa moja katika milki yake? Wale ambao wanajua historia wanaweza kukumbuka visa fulani kama hivyo. Badala ya kupuuza jambo hilo, kwa kawaida mwenye enzi, hata akiwa mtawala mwenye fadhili, anawahukumu waasi, na kutangaza kwamba wana hatia ya kosa la usaliti. Kisha, mtawala huyo anaweza kumpa mtu fulani mamlaka ili ayakomeshe majeshi ya waasi na kurudisha amani. Vivyo hivyo, Yehova alionyesha kwamba alidhibiti kabisa uasi alipochukua hatua mara moja na kutangaza hukumu juu ya waasi hao. Alitangaza kwamba Adamu na Hawa hawakustahili zawadi ya uzima wa milele, naye akawafukuza kutoka katika bustani ya Edeni.—Mwanzo 3:16-19, 22-24.

9 Alipotangaza hukumu yake juu ya Shetani, Yehova alifunua wonyesho mpya wa enzi yake kuu, njia ambayo atatumia kurudisha amani na utaratibu katika milki yake yote. Mungu alimwambia Shetani hivi: “Nitaweka uadui kati yako na yule mwanamke na kati ya uzao wako na uzao wake. Yeye atakuponda kichwa nawe utamtia jeraha kwenye kisigino.” (Mwanzo 3:15) Hivyo, Yehova alifunua kwamba alikusudia kuupa “uzao” fulani uwezo wa kumponda Shetani na majeshi yake na kuthibitisha kwamba utawala Wake ndio unaofaa.—Zaburi 2:7-9; 110:1, 2.

10. (a) “Uzao” huo ulithibitika kuwa nani? (b) Paulo alisema nini kuhusu kutimizwa kwa unabii wa kwanza?

10 Yesu Kristo pamoja na kikundi cha pekee cha watawala wenzake ndio waliothibitika kuwa “uzao” huo. Ufalme wa Mungu wa Kimasihi unafanyizwa na Yesu na watawala hao. (Danieli 7:13, 14, 27; Mathayo 19:28; Luka 12:32; 22:28-30) Hata hivyo, mambo hayo yote hayakufunuliwa mara moja. Kwa kweli, unabii wa kwanza ulibaki ukiwa “siri takatifu ambayo [ilikuwa] imewekwa katika siri tangu nyakati za zamani za kale.” (Waroma 16:25) Kwa karne nyingi, wanaume wa imani walitamani sana kuona wakati ambapo ‘siri hiyo takatifu’ ingefunuliwa na unabii wa kwanza kutimizwa na hivyo kuitetea enzi kuu ya Yehova.—Waroma 8:19-21.

“Siri Takatifu” Ilifunuliwa Hatua kwa Hatua

11. Yehova alimwambia Abrahamu nini?

11 Kadiri wakati ulivyopita, ndivyo Yehova alivyofunua hatua kwa hatua habari kuhusu “siri takatifu ya ufalme wa Mungu.” (Marko 4:11) Kati ya wale ambao Yehova aliwafunulia siri hiyo ni Abrahamu, ambaye aliitwa “rafiki ya Yehova.” (Yakobo 2:23) Yehova alimwahidi Abrahamu kwamba ‘Angefanya taifa kubwa’ kutokana naye. Baadaye, Mungu alimwambia Abrahamu hivi: “Wafalme watatoka ndani yako,” na “kupitia kwa uzao wako mataifa yote ya dunia hakika yatajibariki.”—Mwanzo 12:2, 3; 17:6; 22:17, 18.

12. Uzao wa Shetani ulijitokeza jinsi gani baada ya Gharika?

12 Kufikia siku za Abrahamu, tayari wanadamu walikuwa wamejaribu kuwatawala wengine. Kwa mfano, Biblia inasema hivi kumhusu Nimrodi, mwana wa mjukuu wa Noa: “Akawa wa kwanza kuwa mwenye nguvu duniani. Akajionyesha kuwa mwindaji mwenye nguvu kwa kumpinga Yehova.” (Mwanzo 10:8, 9) Ni wazi kwamba Nimrodi na watawala wengine waliojichukulia mamlaka walitumiwa na Shetani. Watawala hao pamoja na wale waliowaunga mkono wakawa sehemu ya uzao wa Shetani.—1 Yohana 5:19.

13. Yehova alitabiri nini kupitia Yakobo?

13 Hata ingawa Shetani amejitahidi sana kutokeza watawala wa kibinadamu, kusudi la Yehova linasonga mbele. Kupitia Yakobo, mjukuu wa Abrahamu, Yehova alifunua hivi: “Fimbo ya enzi haitageuka kando kutoka kwa Yuda, wala fimbo ya kiongozi kutoka katikati ya miguu yake, mpaka Shilo aje; na vikundi vya watu vitamtii yeye.” (Mwanzo 49:10) Neno “Shilo” linamaanisha “Yeye Ambaye Ni Yake; Yeye Ambaye Ni Mali Yake.” Hivyo, maneno hayo ya kinabii yalionyesha kwamba yule aliye na haki ya kisheria ya kupokea “fimbo ya enzi” au utawala, na “fimbo ya kiongozi” juu ya “vikundi vya watu” au wanadamu wote, angetokea. Huyo angekuwa nani?

“Mpaka Shilo Aje”

14. Yehova alifanya agano gani pamoja na Daudi?

14 Kati ya wazao wa Yuda, mtu wa kwanza kuchaguliwa na Yehova kuwa mfalme juu ya watu wake alikuwa mchungaji Daudi, mwana wa Yese. * (1 Samweli 16:1-13) Hata ingawa alitenda dhambi na makosa, Daudi alipata kibali machoni pa Yehova kwa sababu alikuwa mshikamanifu kwa enzi kuu ya Yehova. Akifunua mengi zaidi kuhusu unabii uliotolewa katika Edeni, Yehova alifanya agano pamoja na Daudi, aliposema hivi: ‘Nitainua uzao wako baada yako, ambao utatoka ndani ya viuno vyako; nami kwa kweli nitaufanya imara ufalme wake.’ Hilo lingehusisha wengine mbali na Sulemani, mwana wa Daudi ambaye alitawala baada yake, kwa kuwa agano hilo lilisema hivi: “Nami hakika nitakifanya imara kiti cha ufalme wake mpaka wakati usio na kipimo.” Agano hilo la Daudi lilionyesha wazi kwamba “uzao” ulioahidiwa wa Ufalme ungetokea katika ukoo wa Daudi.—2 Samweli 7:12, 13.

15. Kwa nini ufalme wa Yuda ungeweza kuonwa kuwa wonyesho wa kimbele wa Ufalme wa Mungu?

15 Daudi ndiye aliyekuwa mfalme wa kwanza katika ukoo wa wafalme ambao walitiwa mafuta matakatifu na kuhani mkuu. Hivyo, wafalme hao wangeweza kuitwa watiwa-mafuta, au masihi. (1 Samweli 16:13; 2 Samweli 2:4; 5:3; 1 Wafalme 1:39) Ilisemekana kwamba waliketi kwenye kiti cha ufalme cha Yehova na kutawala wakiwa wafalme kwa ajili ya Yehova huko Yerusalemu. (2 Mambo ya Nyakati 9:8) Ndiyo sababu ufalme wa Yuda uliwakilisha Ufalme wa Mungu, wonyesho wa enzi kuu ya Yehova.

16. Utawala wa wafalme wa Yudea ulikuwa na matokeo gani?

16 Mfalme na watu walipojitiisha chini ya enzi kuu ya Yehova, aliwalinda na kuwabariki. Kulikuwa na amani na ufanisi usio na kifani wakati wa utawala wa Sulemani. Hali hizo zilionyesha kinabii jinsi hali zitakavyokuwa chini ya utawala wa Ufalme wa Mungu wakati ambapo uvutano wa Shetani utakuwa umeondolewa kabisa na enzi kuu ya Yehova kutetewa. (1 Wafalme 4:20, 25) Inahuzunisha kwamba wafalme wengi wa ukoo wa Daudi walishindwa kufuata matakwa ya Yehova, na watu wakatumbukia katika ibada ya sanamu na upotovu wa maadili. Mwishowe, Yehova aliruhusu ufalme huo uharibiwe na Wababiloni mwaka wa 607 K.W.K. Ilionekana kana kwamba Shetani alikuwa amefanikiwa katika jitihada zake za kuonyesha kwamba enzi kuu ya Yehova si nzuri.

17. Ni nini kinachoonyesha kwamba bado Yehova alikuwa na mamlaka kamili hata ingawa ufalme wa ukoo wa Daudi ulipinduliwa?

17 Kupinduliwa kwa ufalme wa ukoo wa Daudi, na kupinduliwa mapema kwa ufalme wa kaskazini wa Israeli, kulithibitisha matokeo mabaya ya uvutano wa Shetani na uamuzi wa wanadamu wa kutomtegemea Mungu. Lakini hilo halikumaanisha kwamba enzi kuu ya Yehova ina kasoro au imepungukiwa. (Methali 16:25; Yeremia 10:23) Ili kuonyesha kwamba bado alikuwa mwenye enzi kuu, Yehova alitangaza hivi kupitia nabii Ezekieli: “Kiondoe kilemba, na kulivua taji. . . . Nitaliharibu, nitaliharibu, nitaliharibu. Nalo hili pia, hakika hili halitakuwa la mtu yeyote mpaka atakapokuja yule aliye na haki ya kisheria, nami nitampa yeye.” (Ezekieli 21:26, 27) Maneno hayo yanaonyesha kwamba “uzao” ulioahidiwa, Yule “ambaye [alikuwa] na haki ya kisheria,” hakuwa amekuja.

18. Malaika Gabrieli alimtangazia Maria nini?

18 Acheni tusonge mbele karibu mwaka wa 2 K.W.K. Malaika Gabrieli alitumwa kwa Maria, msichana bikira huko Nazareti, katika mji wa Galilaya, kaskazini mwa Palestina. Alitangaza hivi: “Tazama! utachukua mimba katika tumbo lako la uzazi na kuzaa mwana, nawe utamwita jina lake Yesu. Huyo atakuwa mkuu naye ataitwa Mwana wa Aliye Juu Zaidi; na Yehova Mungu atampa kiti cha ufalme cha Daudi baba yake, naye atatawala akiwa mfalme juu ya nyumba ya Yakobo milele, na ufalme wake hautakuwa na mwisho.”—Luka 1:31-33.

19. Wakati ulikuwa umekaribia wa matukio gani yenye kusisimua?

19 Mwishowe, wakati ulikuwa umekaribia wa ile “siri takatifu” kufunuliwa. Yule aliyekuwa sehemu ya msingi ya ule “uzao” ulioahidiwa alikuwa karibu kutokea. (Wagalatia 4:4; 1 Timotheo 3:16) Shetani angemtia jeraha kwenye kisigino. Lakini “uzao” huo ungemponda kichwa Shetani na kumharibu kabisa pamoja na wafuasi wake wote. Pia, Yesu angetoa ushahidi kwamba kupitia Ufalme wa Mungu, madhara yote ambayo yamesababishwa na Shetani yataondolewa na enzi kuu ya Yehova itatetewa. (Waebrania 2:14; 1 Yohana 3:8) Yesu angetimiza hilo jinsi gani? Alituwekea mfano gani wa kuiga? Maswali hayo yatajibiwa katika habari inayofuata.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 14 Sauli, ambaye alichaguliwa kwanza na Mungu awe mtawala wa Israeli, alikuwa wa kabila la Benyamini.—1 Samweli 9:15, 16; 10:1.

Je, Unaweza Kueleza?

• Kwa nini Yehova ana haki ya kuwa Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu wote?

• Kwa nini Yehova alikusudia kuanzisha Ufalme?

• Yehova alifunua jinsi gani ile “siri takatifu” hatua kwa hatua?

• Ni nini kinachoonyesha kwamba Yehova alikuwa na mamlaka kamili hata ingawa ufalme wa ukoo wa Daudi ulipinduliwa?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 23]

Yehova alionyesha nini kimbele kupitia Abrahamu?

[Picha katika ukurasa wa 25]

Kwa nini kupinduliwa kwa ufalme wa ukoo wa Daudi hakukuthibitisha kwamba enzi kuu ya Yehova ilikuwa na kasoro?