Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unaitegemeza Enzi Kuu ya Yehova?

Je, Unaitegemeza Enzi Kuu ya Yehova?

Je, Unaitegemeza Enzi Kuu ya Yehova?

“Semeni kati ya mataifa: ‘Yehova amekuwa mfalme.’” —ZABURI 96:10.

1, 2. (a) Ni tukio gani la pekee lililotukia Oktoba 29 W.K.? (b) Tukio hilo lilikuwa na maana gani kwa Yesu?

TUKIO la pekee sana ambalo halikuwa kamwe limeonekana duniani lilitukia karibu Oktoba (Mwezi wa 10) 29 W.K. Mathayo, mwandikaji wa Injili anasema hivi: “Baada ya kubatizwa Yesu akapanda mara moja kutoka katika maji; na, tazama! mbingu zikafunguliwa, naye [Yohana Mbatizaji] akaona roho ya Mungu ikishuka kama njiwa, ikija juu yake [Yesu]. Tazama! Kulikuwa pia na sauti kutoka mbinguni iliyosema: ‘Huyu ni Mwanangu, mpendwa, ambaye nimemkubali.’” Hilo ni tukio moja kati ya matukio machache ambayo yaliandikwa na waandikaji wote wanne wa Injili.—Mathayo 3:16, 17; Marko 1:9-11; Luka 3:21, 22; Yohana 1:32-34.

2 Yesu alitambulishwa kuwa Mtiwa-Mafuta wakati roho takatifu ilipoonekana ikimwagwa juu yake. Neno Mtiwa-Mafuta linamaanisha Masihi au Kristo. (Yohana 1:33) Mwishowe, ule “uzao” ulioahidiwa ulikuwa umetokea! Yule ambaye Shetani angemtia jeraha kwenye kisigino, na ambaye angemponda kichwa Shetani, adui mkuu wa Yehova na wa enzi Yake kuu alikuwa amesimama mbele za Yohana Mbatizaji. (Mwanzo 3:15) Kuanzia wakati huo na kuendelea, Yesu alitambua kabisa kwamba alipaswa kujitahidi kutimiza kusudi la Yehova kuhusiana na enzi Yake kuu na Ufalme Wake.

3. Yesu alijitayarisha jinsi gani ili kutimiza wajibu wake katika kuitegemeza enzi kuu ya Yehova?

3 Ili ajitayarishe kwa ajili ya kazi iliyokuwa mbele yake, ‘Yesu, akiwa amejaa roho takatifu, alitoka Yordani, naye akaongozwa na roho huku na huku nyikani.’ (Luka 4:1; Marko 1:12) Akiwa nyikani kwa siku 40, Yesu alikuwa na wakati wa kutafakari kwa uzito kuhusu suala la enzi kuu ambalo lilitokezwa na Shetani na kuhusu wajibu ambao angetimiza ili kutegemeza enzi kuu ya Yehova. Suala hilo lilihusisha viumbe wote wenye akili walio mbinguni na duniani. Kwa hiyo, ni vizuri tutafakari kuhusu mwenendo wa uaminifu wa Yesu na kuona mambo ambayo tunapaswa kufanya ili kuonyesha kwamba sisi pia tunataka kuitegemeza enzi kuu ya Yehova.—Ayubu 1:6-12; 2:2-6.

Suala la Enzi Kuu Latokezwa

4. Shetani alichukua hatua gani ambayo ilitokeza waziwazi suala la enzi kuu?

4 Bila shaka, Shetani aliona matukio hayo yote ambayo yametajwa. Bila kukawia, alishambulia sehemu ya msingi ya “uzao” wa “mwanamke” wa Mungu. (Mwanzo 3:15) Shetani alimshawishi Yesu mara tatu, akimpendekezea afanye mambo ambayo alidai yangemletea faida badala ya kufanya mambo ambayo Baba yake alitaka afanye. Kishawishi cha tatu kilitokeza waziwazi suala la enzi kuu. Huku akimwonyesha Yesu “falme zote za ulimwengu na utukufu wazo,” Shetani alimwambia Yesu waziwazi hivi: “Nitakupa mambo yote haya ukianguka chini na kunifanyia tendo la ibada.” Akitambua vizuri kwamba kwa kweli Ibilisi alikuwa na mamlaka juu ya “falme zote za ulimwengu,” Yesu alijibu hivi na hivyo kuonyesha upande ambao alikuwa anaunga mkono kuhusiana na suala la enzi kuu: “Nenda zako, Shetani! Kwa maana imeandikwa, ‘Yehova Mungu wako ndiye unayepaswa kumwabudu, na yeye peke yake ndiye unayepaswa kumtolea utumishi mtakatifu.’”—Mathayo 4:8-10.

5. Yesu alihitaji kutimiza kazi gani ngumu?

5 Maisha ya Yesu yalionyesha waziwazi kwamba jambo kuu maishani mwake lilikuwa kuitegemeza enzi kuu ya Yehova. Yesu alijua vizuri kwamba alipaswa kuendelea kuwa mwaminifu mpaka kifo mikononi mwa Shetani ili kuthibitisha kwamba Mungu ana haki ya kuwa mwenye enzi kuu. Kulingana na unabii, Yesu alipokufa ni kana kwamba “uzao” wa mwanamke ulitiwa jeraha kwenye kisigino. (Mathayo 16:21; 17:12) Alihitaji pia kutoa ushahidi kwamba Ufalme wa Mungu ndiyo serikali ambayo Yehova ameipa mamlaka ya kumtiisha yule mwasi, Shetani, na kurudisha amani na utaratibu katika uumbaji wote. (Mathayo 6:9, 10) Yesu alifanya nini ili kutimiza kazi yake ngumu?

“Ufalme wa Mungu Umekaribia”

6. Yesu alionyesha jinsi gani kwamba Mungu atatumia Ufalme ‘kuzivunja kazi za Ibilisi’?

6 Kwanza, “Yesu akaenda Galilaya, akihubiri habari njema ya Mungu na kusema: ‘Wakati uliowekwa umetimizwa, na ufalme wa Mungu umekaribia.’” (Marko 1:14, 15) Kwa kweli, alisema hivi: “Ni lazima nitangaze habari njema ya ufalme wa Mungu kwenye majiji mengine pia, kwa sababu nilitumwa kufanya hivyo.” (Luka 4:18-21, 43) Yesu alisafiri kotekote “akihubiri na kutangaza habari njema ya ufalme wa Mungu.” (Luka 8:1) Yesu alifanya pia kazi nyingi zenye nguvu, kama vile kulisha umati wa watu, kutuliza nguvu za asili, kuwaponya wagonjwa, na kuwafufua wafu. Kupitia miujiza hiyo, Yesu alithibitisha kwamba Mungu anaweza kuondoa madhara na mateso yote ambayo yamesababishwa na uasi katika Edeni na hivyo ‘kuzivunja kazi za Ibilisi.’—1 Yohana 3:8.

7. Yesu aliwaagiza wafuasi wake wafanye nini, na matokeo yalikuwa nini?

7 Ili habari njema ya Ufalme ihubiriwe kwa ukamili iwezekanavyo, Yesu alikusanya kikundi cha wafuasi waaminifu na kuwazoeza kuifanya kazi hiyo. Kwanza, aliwaita mitume 12 na ‘kuwatuma wahubiri ufalme wa Mungu na kuponya.’ (Luka 9:1, 2) Kisha, akawatuma wengine 70 watangaze ujumbe huu: “Ufalme wa Mungu umekuja karibu nanyi.” (Luka 10:1, 8, 9) Wanafunzi hao waliporudi na kumwambia Yesu matokeo ambayo walipata katika kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme, Yesu aliwajibu hivi: “Nilianza kumwona Shetani akiwa tayari ameanguka kama umeme kutoka mbinguni.”—Luka 10:17, 18.

8. Maisha ya Yesu yalionyesha nini waziwazi?

8 Yesu alijitolea kabisa naye hakupoteza nafasi yoyote aliyopata ya kutoa ushahidi kuhusu Ufalme. Alifanya kazi bila kuacha, usiku na mchana, hata alijinyima starehe za kawaida za maisha. Alisema hivi: “Mbweha wana mapango na ndege wa mbinguni wana viota, lakini Mwana wa binadamu hana mahali popote pa kulaza kichwa chake.” (Luka 9:58; Marko 6:31; Yohana 4:31-34) Muda mfupi kabla ya kifo chake, Yesu alisema hivi kwa ujasiri mbele ya Pontio Pilato: “Kwa ajili ya hili nimekuja ulimwenguni, ili nitoe ushahidi juu ya ile kweli.” (Yohana 18:37) Yesu alionyesha katika maisha yake yote kwamba alikuja, si tu kuwa mwalimu mkuu au mfanya-miujiza au hata Mwokozi aliyejidhabihu, bali alikuja kutegemeza mapenzi ya mwenye enzi kuu Yehova na kutoa ushahidi kuhusu uwezo wa Mungu wa kutimiza mapenzi hayo kupitia Ufalme.—Yohana 14:6.

“Imetimizwa!”

9. Mwishowe Shetani alifaulu jinsi gani kuutia jeraha “uzao” wa mwanamke wa Mungu?

9 Mambo yote ambayo Yesu alifanya kuhusiana na Ufalme hayakumfurahisha yule Adui, Shetani Ibilisi. Shetani alijaribu tena na tena kuua “uzao” wa mwanamke wa Mungu akitumia sehemu ya kidunia ya “uzao” wake, yaani, sehemu ya kisiasa na ya kidini. Tangu alipozaliwa na mpaka mwisho wa maisha yake duniani, Yesu alikuwa shabaha ya Shetani na wale wanaomuunga mkono. Mwishowe, katika mwaka wa 33 W.K., wakati ulifika wa Mwana wa binadamu kuwekwa mikononi mwa yule Adui ili amtie jeraha kwenye kisigino. (Mathayo 20:18, 19; Luka 18:31-33) Masimulizi ya Injili yanaonyesha wazi jinsi watu kama vile Yuda Iskariote, makuhani wakuu, waandishi, Mafarisayo, na Waroma walivyoongozwa na Shetani kumshutumu na kumuua Yesu kwa maumivu makali kwenye mti wa mateso.—Matendo 2:22, 23.

10. Yesu alipokufa kwenye mti wa mateso alitimiza nini hasa?

10 Unawazia nini unapomfikiria Yesu akiwa kwenye mti wa mateso akiteseka na kufa kifo cha polepole chenye maumivu makali sana? Labda unakumbuka dhabihu ya fidia ambayo Yesu alitoa bila ubinafsi kwa ajili ya wanadamu wenye dhambi. (Mathayo 20:28; Yohana 15:13) Huenda ukastaajabu kujua upendo mkubwa sana ambao Yehova alionyesha alipotoa dhabihu hiyo. (Yohana 3:16) Labda unahisi kama yule ofisa-jeshi Mroma ambaye alichochewa kusema hivi: “Hakika huyu alikuwa Mwana wa Mungu.” (Mathayo 27:54) Bila shaka ni sawa kuhisi hivyo. Kwa upande mwingine, kumbuka neno hili la mwisho ambalo Yesu alisema akiwa kwenye mti wa mateso: “Imetimizwa!” (Yohana 19:30) Ni nini kilichokuwa kimetimizwa? Ingawa Yesu alitimiza mambo mengi wakati wa maisha na kifo chake, je, sababu kuu iliyomfanya Yesu aje duniani haikuwa kujibu suala la enzi kuu ya Yehova? Na je, haikuwa imetabiriwa kwamba akiwa ule “uzao,” angejaribiwa vikali na Shetani ili aondoe kabisa suto juu ya jina la Yehova? (Isaya 53:3-7) Hayo yalikuwa madaraka mazito sana, lakini Yesu aliyatimiza kikamili kabisa. Alitimiza mambo muhimu kama nini!

11. Yesu atafanya nini ili atimize kikamili unabii uliotolewa katika Edeni?

11 Kwa sababu ya uaminifu na ushikamanifu wake, Yesu hakufufuliwa akiwa mwanadamu, bali akiwa “roho inayotoa uhai.” (1 Wakorintho 15:45; 1 Petro 3:18) Yehova alimwambia hivi Mwana wake aliyetukuzwa: “Keti kwenye mkono wangu wa kuume mpaka niwaweke adui zako kuwa kiti cha miguu yako.” (Zaburi 110:1) “Adui” hao wanatia ndani adui mkuu, Shetani, pamoja na wote ambao ni sehemu ya “uzao” wake. Akiwa Mfalme wa Ufalme wa Kimasihi wa Yehova, Yesu Kristo ataongoza katika kuwaangamiza waasi wote duniani na katika makao ya roho. (Ufunuo 12:7-9; 19:11-16; 20:1-3, 10) Kisha unabii wa Mwanzo 3:15 utatimizwa kikamili na pia sala hii ambayo Yesu aliwafundisha wafuasi wake: “Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.”—Mathayo 6:10; Wafilipi 2:8-11.

Kielelezo cha Kufuata

12, 13. (a) Watu wanaitikia jinsi gani habari njema ya Ufalme leo? (b) Tunapaswa kufikiria nini ikiwa tunataka kufuata hatua za Kristo?

12 Leo, habari njema ya Ufalme inahubiriwa katika nchi nyingi, kama Yesu alivyotabiri. (Mathayo 24:14) Matokeo ni kwamba mamilioni ya watu wameweka maisha yao wakfu kwa Mungu. Wanasisimuka kwa sababu ya baraka ambazo Ufalme huo utaleta. Wanatazamia kuishi milele kwa amani na usalama katika paradiso duniani, na kwa shangwe wanawaambia wengine kuhusu tumaini lao. (Zaburi 37:11; 2 Petro 3:13) Je, wewe ni mmoja wa watangazaji hao wa Ufalme? Ikiwa ndivyo, unastahili pongezi. Hata hivyo, kuna jambo lingine ambalo kila mmoja wetu anapaswa kufikiria.

13 Mtume Petro aliandika hivi: “Kristo aliteseka kwa ajili yenu, akiwaachia ninyi kielelezo ili mfuate hatua zake kwa ukaribu.” (1 Petro 2:21) Ona kwamba katika andiko hilo, Petro hakutaja bidii ya Yesu ya kuhubiri au ustadi wake wa kufundisha, alitaja mateso yake. Petro alijionea hayo, kwa hivyo alijua vizuri jinsi Yesu alivyokuwa tayari kuteseka ili ajitiishe chini ya enzi kuu ya Yehova na kuthibitisha kwamba Shetani ni mwongo. Basi, tunaweza kufuata hatua za Yesu jinsi gani? Tunapaswa kujiuliza: ‘Niko tayari kuteseka kadiri gani ili niitegemeze na kuiletea heshima enzi kuu ya Yehova? Je, maisha na huduma yangu inaonyesha kwamba ninahangaikia hasa kuitegemeza enzi kuu ya Yehova?’—Wakolosai 3:17.

14, 15. (a) Yesu alifanya nini alipopewa mapendekezo yenye kupotosha, na kwa nini alifanya hivyo? (b) Tunapaswa sikuzote kukazia akilini suala gani? (Tia ndani maelezo kutoka katika sanduku lenye kichwa “Simama Upande wa Yehova.”)

14 Kila siku, tunakabili majaribu na maamuzi, makubwa na madogo. Tunapaswa kufikiria nini tunapoyashughulikia? Kwa mfano, tunaposhawishiwa moja kwa moja tufanye jambo fulani ambalo litahatarisha msimamo wetu wa Kikristo, tunatenda jinsi gani? Petro alipomwambia Yesu ajitendee kwa fadhili, Yesu alisema nini? Alisema hivi kwa uthabiti: ‘Nenda nyuma yangu, Shetani! Unafikiri, si fikira za Mungu, bali za wanadamu.’ (Mathayo 16:21-23) Au tunapopewa nafasi za kupata pesa zaidi au kupandishwa cheo na kuhatarisha hali yetu ya kiroho, je, tunafanya kama Yesu alivyofanya? Yesu alipotambua kwamba wale walioona miujiza yake “walikuwa karibu kuja kumkamata wamfanye kuwa mfalme,” aliondoka haraka na kwenda zake.—Yohana 6:15.

15 Kwa nini Yesu alichukua hatua imara katika pindi hizo na pindi nyingine? Kwa sababu aliona wazi kwamba mambo mengine yalihusika zaidi ya usalama wake au faida yake ya kibinafsi. Alitaka kufanya mapenzi ya Baba yake na kuitegemeza enzi kuu ya Yehova chini ya hali zozote. (Mathayo 26:50-54) Hivyo, ikiwa hatukazii akilini nyakati zote suala linalohusika la enzi kuu, kama Yesu alivyofanya, tutakabili daima hatari ya kulegeza msimamo wetu au tutashindwa kufanya yaliyo sawa. Kwa nini? Kwa sababu tunaweza kudanganywa kwa urahisi na mbinu zenye hila za Shetani, ambaye ni fundi katika kufanya mambo yasiyofaa yapendeze, kama alivyofanya alipokuwa akimshawishi Hawa.—2 Wakorintho 11:14; 1 Timotheo 2:14.

16. Tunapaswa kuwa na kusudi gani kuu tunapowasaidia wengine?

16 Katika huduma yetu, tunajitahidi kuzungumza na watu kuhusu mahangaiko yao na kuwaonyesha majibu ya Biblia. Hiyo ni njia nzuri ya kuwafanya wapendezwe na funzo la Biblia. Hata hivyo, kusudi letu kuu si kuwasaidia tu wajue yale ambayo Biblia inasema au baraka ambazo Ufalme wa Mungu utaleta. Ni lazima tuwasaidie kuelewa kabisa suala la enzi kuu ya Yehova. Je, wako tayari kuwa Wakristo wa kweli na kuuchukua ‘mti wao wa mateso’ na kuteseka kwa ajili ya Ufalme? (Marko 8:34) Je, wako tayari kujiunga na wale ambao wako upande wa enzi kuu ya Yehova na hivyo kuthibitisha kwamba Shetani ni mwongo na mchongezi? (Methali 27:11) Tuna pendeleo la kujitahidi kuunga mkono enzi kuu ya Yehova na kuwasaidia wengine wafanye hivyo.—1 Timotheo 4:16.

Mungu Atakapokuwa “Vitu Vyote kwa Kila Mtu”

17, 18. Tunaweza kutazamia wakati gani wenye utukufu ikiwa tutaonyesha kwamba tunaitegemeza enzi kuu ya Yehova?

17 Tunapofanya yote tunayoweza ili kuonyesha kwa mwenendo na huduma yetu kwamba tunaitegemeza enzi kuu ya Yehova, tunaweza kutazamia wakati Yesu Kristo “atakapomkabidhi ufalme Mungu wake ambaye pia ni Baba yake.” Ni wakati gani huo? Mtume Paulo anaeleza hivi: “Wakati atakapokuwa ameangamiza serikali yote na mamlaka yote na nguvu zote. Kwa maana ni lazima atawale akiwa mfalme mpaka Mungu awe ameweka adui zote chini ya miguu yake. . . . Ndipo Mwana mwenyewe atakapojitiisha pia kwa Yeye aliyevitiisha vitu vyote kwake, ili Mungu awe vitu vyote kwa kila mtu.”—1 Wakorintho 15:24, 25, 28.

18 Wakati Mungu atakapokuwa “vitu vyote kwa kila mtu,” utakuwa wakati wenye utukufu kama nini! Ufalme utakuwa umetimiza kusudi lake. Wapinzani wote wa enzi kuu ya Yehova watakuwa wameondolewa kabisa. Amani na utaratibu utakuwa umerudishwa katika ulimwengu wote. Viumbe wote wataimba kama alivyoimba mtunga-zaburi: “Mhesabieni Yehova utukufu wa jina lake . . . Semeni kati ya mataifa: ‘Yehova amekuwa mfalme.’”—Zaburi 96:8, 10.

Je, Unaweza Kujibu?

• Yesu alitanguliza jinsi gani suala la enzi kuu ya Mungu?

• Yesu alitimiza nini hasa kupitia huduma na kifo chake?

• Tunaweza kufuata mfano wa Yesu katika njia gani na hivyo kuonyesha kwamba tunaunga mkono enzi kuu ya Yehova?

[Maswali ya Funzo]

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 29]

SIMAMA UPANDE WA YEHOVA

Kama ndugu wengi wa Korea na wa nchi nyinginezo wanavyojua, Wakristo wanapokabili majaribu makali, kuna faida ya kuelewa vizuri kabisa kwa nini wanapata majaribu hayo.

Shahidi mmoja wa Yehova aliyefungwa gerezani wakati wa utawala wa Sovieti alisema hivi: “Niliweza kuvumilia kwa sababu nilielewa vizuri kabisa suala lililotokezwa katika bustani ya Edeni, suala la haki ya Mungu ya kutawala. . . . Tulijua kwamba tulikuwa na nafasi ya kuutegemeza utawala wa Yehova. . . . Hilo lilitutia nguvu na kutuwezesha kushika utimilifu wetu.”

Shahidi mwingine alieleza kilichomsaidia na kuwasaidia Mashahidi wenzake katika kambi ya kazi ngumu. Alisema hivi: “Yehova alitutegemeza. Hata ingawa tulikuwa katika hali ngumu, tulikuwa macho kiroho. Sikuzote tulitiana moyo kwa kukumbushana kwamba tulikuwa tunasimama upande wa Yehova wa suala la enzi kuu ya ulimwengu wote.”

[Picha katika ukurasa wa 26]

Yesu alitegemeza jinsi gani enzi kuu ya Yehova aliposhawishiwa na Shetani?

[Picha katika ukurasa wa 28]

Kifo cha Yesu kilitimiza nini?