Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Yesu Alikuwa na Biblia?

Je, Yesu Alikuwa na Biblia?

Je, Yesu Alikuwa na Biblia?

HAPANA, Yesu hakuwa na Biblia. Kwa nini? Kwa sababu Biblia nzima kama ile tuliyo nayo leo haikuwapo katika siku za Yesu. Hata hivyo, masinagogi yalikuwa na vitabu vya kukunjwa vyenye maandishi ambayo yamekuja kuwa sehemu ya Biblia tuliyo nayo leo. Yesu alisoma kitabu cha kukunjwa cha Isaya katika sinagogi huko Nazareti. (Luka 4:16, 17) Mtume Paulo alisikiliza ‘kusomwa kwa Sheria na Manabii mbele ya watu wote’ huko Antiokia ya Pisidia. (Matendo 13:14, 15) Na mwanafunzi Yakobo alisema kwamba Musa “husomwa kwa sauti kubwa katika masinagogi kila siku ya sabato.”—Matendo 15:21.

Je, watu mmoja-mmoja katika karne ya kwanza walikuwa na vitabu vyao vya kukunjwa vya Maandiko Matakatifu? Ni wazi kwamba towashi Mwethiopia aliyefanya kazi katika makao ya Malkia Kandake alikuwa na vitabu vyake, kwa kuwa alikuwa “ameketi katika gari lake, akimsoma kwa sauti kubwa nabii Isaya,” mwanafunzi Filipo alipokutana naye katika barabara inayokwenda Gaza. (Matendo 8:26-30) Mtume Paulo alimwomba Timotheo amletee “vile vitabu vya kukunjwa, hasa vile vya ngozi.” (2 Timotheo 4:13) Ingawa Paulo hakusema hivyo vilikuwa vitabu gani, inaelekea sana kwamba vilikuwa visehemu vya Maandiko ya Kiebrania.

Alan Millard, profesa wa lugha za Kiyahudi, anasema inawezekana kwamba miongoni mwa Wayahudi, “wanaume wenye vyeo huko Palestina, watu wote waliodai kuwa na elimu, Mafarisayo fulani, na walimu kama vile Nikodemo,” ndio watu pekee waliokuwa na vitabu vyao wenyewe vya kukunjwa vya Maandiko. Moja ya sababu zilizofanya watu wengi wasiwe na nakala zao, ni bei ghali ya vitabu hivyo. Millard anakadiria kwamba “kitabu cha Isaya kiliuzwa kwa kati ya dinari sita na kumi” na anasema kwamba Biblia nzima ya Kiebrania “ingekuwa na vitabu vya kukunjwa kati ya 15 na 20,” au bei yake ingelingana na mshahara wa nusu mwaka hivi.

Biblia haisemi ikiwa Yesu au wanafunzi wake walikuwa na vitabu vyao wenyewe vya kukunjwa vya Biblia. Hata hivyo, hapana shaka kwamba Yesu aliyajua Maandiko sana, hivi kwamba aliyarejelea au kuyanukuu kutoka moyoni. (Mathayo 4:4, 7, 10; 19:4, 5) Je, hilo halipaswi kutuchochea leo tujitahidi kuijua Biblia vizuri, kwa kuwa inapatikana kwa bei ya chini na kwa urahisi zaidi?