Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kusonga Kuelekea Ulimwengu Mpya

Kusonga Kuelekea Ulimwengu Mpya

Simulizi la Maisha

Kusonga Kuelekea Ulimwengu Mpya

Limesimuliwa na Jack Pramberg

Nje ya Arboga, mji mdogo wenye kuvutia sana katikati ya Sweden, Mashahidi wa Yehova wana ofisi ya tawi iliyo na wafanyakazi zaidi ya 80 wa kujitolea. Hayo ndiyo makao yetu, ambamo mimi na mke wangu Karin tunaishi na kufanya kazi. Tulifika hapa namna gani?

MWISHONI mwa karne ya 19, msichana mmoja mwenye umri wa miaka 15 alitoka Sweden na kuhamia Marekani. Akiwa katika makao ya wahamiaji huko New York City, alikutana na baharia mmoja kutoka Sweden. Walipendana, wakafunga ndoa, na wakazaa mwana ambaye ni mimi. Nilizaliwa huko Bronx, New York, Marekani, mwaka wa 1916 wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu.

Muda mfupi baadaye, tulihamia Brooklyn, karibu tu na Brooklyn Heights. Baadaye, baba yangu aliniambia kwamba mimi na yeye tulisafiri kwa meli ndogo karibu na Brooklyn Bridge, daraja ambalo linaweza kuonekana kwa urahisi toka makao makuu ya Mashahidi wa Yehova. Wakati huo, sikutambua kwamba kazi iliyokuwa ikifanyika katika makao hayo ingekuwa na uvutano mkubwa katika maisha yangu.

Mwaka wa 1918, Vita vya Kwanza vya Ulimwengu vilikwisha, na kwa muda, mauaji yasiyo na maana yakakoma huko Ulaya. Askari-jeshi walirudi nyumbani ili kukabiliana na matatizo mengine: ukosefu wa kazi na umaskini. Baba alifikiri kwamba ingekuwa vizuri turudi Sweden, na tulirudi huko mwaka wa 1923. Mwishowe, tuliishi huko Erikstad, kijiji kidogo karibu na kituo cha gari-moshi, katika eneo la Dalsland. Tukiwa huko baba alianzisha kazi ya uinjinia, nami nililelewa na kusomea huko.

Mbegu Ilipandwa

Biashara ya baba haikuendelea vizuri. Hivyo mapema katika miaka ya 1930, akawa tena baharia. Tuliachwa pekee yetu, yaani, mama akiwa na mahangaiko mengi na mimi nikijaribu kusimamia kazi ya baba. Siku moja, Mama alimtembelea shemeji yake, Johan. Akiwa na wasiwasi kuhusu hali ya ulimwengu, mama aliuliza: “Johan, je, hali itaendelea tu kuwa hivi?”

“Hapana, Ruth,” akamjibu. Kisha, akamweleza kuhusu ahadi ya Mungu ya kukomesha uovu na kuleta utawala wenye uadilifu duniani kupitia Ufalme ulio mikononi mwa Mfalme Yesu Kristo. (Isaya 9:6, 7; Danieli 2:44) Alieleza kwamba Ufalme ambao Yesu alitufundisha kusali, ni utawala wenye uadilifu, au serikali ambayo itaifanya dunia kuwa paradiso.—Mathayo 6:9, 10; Ufunuo 21:3, 4.

Ahadi hizo za Biblia ziligusa moyo wa Mama moja kwa moja. Alirudi nyumbani huku akimsifu Mungu. Hata hivyo, mimi na Baba hatukufurahi tulipomwona Mama akipendezwa na mambo ya dini. Karibu wakati huo, katikati ya miaka ya 1930, nilihamia Trollhättan, magharibi mwa Sweden, ambako nilipata kazi katika kiwanda kikubwa. Punde si punde, Mama pamoja na Baba, ambaye alikuwa ameacha kazi yake ya ubaharia, walihamia hapo pia. Hivyo familia yetu ikaungana tena.

Ili kutosheleza tamaa yake ya kiroho, Mama aliwatafuta Mashahidi wa Yehova katika eneo hilo. Wakati huo, walikutana katika nyumba za watu binafsi, kama tu walivyofanya Wakristo wa mapema. (Filemoni 1, 2) Siku moja, ilikuwa zamu ya nyumba ya Mama kutumiwa kwa ajili ya mikutano. Akiwa na wasiwasi, alimuuliza Baba ikiwa angeweza kuwaalika marafiki wake. Baba alijibu: “Marafiki wako ni marafiki wangu pia.”

Hivyo, nyumba yetu ilikuwa wazi kwa ajili ya wageni. Watu walipokuwa wakiingia nyumbani, mimi nilitoka. Hata hivyo, baada ya muda, niliamua kukaa walipokuja kwa ajili ya mikutano. Urafiki wa Mashahidi, mtazamo wao mzuri, na mafundisho yao rahisi yaliondoa maoni yote ya ubaguzi akilini mwangu. Mbegu ikaanza kukua moyoni mwangu, yaani, tumaini la wakati ujao.

Kwenda Baharini

Nilirithi tamaa ya kuwa baharia kutoka kwa Baba, kwa kuwa mimi pia nilikuja kuwa baharia. Pia, nilitambua zaidi na zaidi uhitaji wangu wa kiroho. Meli ilipoegeshwa bandarini, nilijitahidi sikuzote kuwatafuta Mashahidi wa Yehova. Huko Amsterdam, Uholanzi, nilienda kwenye ofisi ya posta kuuliza mahali ambapo ningeweza kuwapata. Baada ya mazungumzo mafupi, nilijulishwa mahali ambapo ningewapata. Msichana mwenye umri wa miaka kumi alinikaribisha kwa shauku mlangoni. Nilikuwa mgeni, lakini papo hapo nikawa na urafiki wa karibu sana pamoja naye na familia yao. Ulikuwa mwonjo ulioje wa undugu wa ajabu wa ulimwenguni pote!

Ingawa hatukuzungumza lugha moja, wakati familia hiyo ilipochukua kalenda na programu ya gari-moshi na kuanza kuchora ramani, nilielewa kwamba kusanyiko lingefanywa katika mji wa Haarlem uliokuwa karibu. Nilihudhuria, na ingawa sikuelewa hata neno moja, nilifurahia kusanyiko hilo. Nilipoona Mashahidi wakitoa mialiko kwa ajili ya hotuba ya watu wote ya Jumapili (Siku ya Yenga), nilichochewa kushiriki katika kazi hiyo. Niliokota mialiko ambayo watu walitupa na kuwapa watu wengine.

Pindi moja, meli yetu iliegeshwa kwenye bandari ya Buenos Aires, Argentina, na huko nikapata ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova. Jengo hilo lilikuwa na ofisi moja na chumba kimoja cha kuhifadhia vitu. Mwanamke fulani alikuwa akifuma mezani, na msichana mdogo, ambaye huenda alikuwa binti yake, alikuwa akicheza na mwanasesere. Ilikuwa usiku sana, na mwanamume mmoja alikuwa akichukua vitabu fulani kutoka kwenye rafu, kutia ndani kitabu Creation cha Kiswedi. Nilipoona furaha waliyokuwa nayo na nyuso zao zenye shangwe, nilitaka kuwa mmoja wao.

Tulipokuwa tukirudi nyumbani, meli yetu ilichukua wafanyakazi wa ndege ya jeshi ya Kanada iliyokuwa imeanguka kwenye pwani ya Newfoundland. Siku chache baadaye, tukiwa karibu Scotland, tulikamatwa na wanajeshi wa majini wa Uingereza. Tulipelekwa Kirkwall kwenye Visiwa vya Orkney ili kukaguliwa. Vita vya Pili vya Ulimwengu vilikuwa vimeanza na askari Wanazi wa Hitler walikuwa wamevamia Poland mnamo Septemba (Mwezi wa 9) 1939. Baada ya siku chache, tuliachiliwa huru, na tukarudi Sweden bila shida.

Nilikuwa nyumbani kimwili na kiroho. Sasa nilitaka kwa kweli kuwa mmoja wa watu wa Mungu na sikutaka kuacha kukusanyika pamoja nao. (Waebrania 10:24, 25) Ninafurahi kukumbuka kwamba nikiwa baharia, sikuzote niliwatolea ushahidi mabaharia wengine, na ninajua kwamba mmoja wao alikuja kuwa Shahidi.

Utumishi wa Pekee

Mapema katika mwaka wa 1940, nilitembelea ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova huko Stockholm. Nilikaribishwa na Johan H. Eneroth, ambaye wakati huo alikuwa akisimamia kazi ya kuhubiri nchini Sweden. Nilipomwambia kwamba nilitaka kushiriki katika kazi ya kuhubiri ya wakati wote nikiwa mhudumu painia, alinikazia macho na kuniuliza, “Je, unaamini kwamba hili ni tengenezo la Mungu?”

Nilijibu “ndiyo.” Kisha nikabatizwa Juni 22, 1940, (22/6/1940), na nikaanza kutumika kwenye ofisi ya tawi katika mazingira hayo mazuri pamoja na wafanyakazi wengine wanyoofu. Tulikuwa tukihubiri mwishoni mwa juma. Wakati wa kiangazi, mara nyingi tulisafiri kwa baiskeli ili kuhubiri maeneo ya mbali mwishoni mwa juma, na usiku tukalala katika marundo ya nyasi.

Hata hivyo, mara nyingi tulihubiri nyumba kwa nyumba katika mji wa Stockholm na maeneo ya kandokando. Siku moja, nilimkuta mwanamume fulani katika chumba cha chini, akitengeneza haraka-haraka na kwa wasiwasi mtambo wake wa kuchemsha maji. Basi nikakunja mikono ya shati langu na kumsaidia. Mtambo huo ulipoacha kuvuja, mwanamume huyo alinitazama na kunishukuru huku akisema: “Ninafikiri kwamba umekuja kwa sababu nyingine pia. Basi acha tupande juu, tunawe mikono na kisha tunywe kikombe cha kahawa.” Tulienda juu, na tulipokuwa tukinywa kikombe hicho cha kahawa, nilimtolea ushahidi. Mwishowe, mtu huyo alikuja kuwa Mkristo mwenzangu.

Ingawa Sweden ilitangaza kwamba haitashiriki katika vita hivyo, viliwaumiza sana watu wa Sweden. Wanaume wengi waliagizwa wajiunge na jeshi, kutia ndani mimi. Nilipokataa kupata mazoezi ya kijeshi, nilifungwa gerezani kwa vipindi vifupi. Baadaye, nilihukumiwa kifungo cha gereza. Mara nyingi, vijana Mashahidi walipelekwa mahakamani, na tuliweza kutoa ushahidi kuhusu Ufalme wa Mungu. Hilo lilitimiza unabii huu wa Yesu: “Mtakokotwa na kupelekwa mbele ya magavana na wafalme kwa ajili yangu, ili kuwa ushahidi kwao na kwa mataifa.”—Mathayo 10:18.

Maisha Yangu Yanabadilika

Vita vilimalizika Ulaya mwaka wa 1945. Baadaye mwaka huo, Nathan H. Knorr, ambaye alikuwa akisimamia kazi ulimwenguni pote, alitutembelea kutoka Brooklyn, akiwa pamoja na mwandishi wake, Milton Henschel. Ziara yao ilikuwa muhimu sana katika kupanga upya kazi ya kuhubiri nchini Sweden, na hasa kwangu binafsi. Niliposikia kuhusu uwezekano wa kuhudhuria Shule ya Gileadi (Watchtower Bible School of Gilead) nilijaza fomu papo hapo.

Mwaka uliofuata, nilihudhuria shule hiyo, ambayo wakati huo ilikuwa ikifanyiwa karibu na South Lansing, New York. Kwa muda wa miezi mitano ya elimu, nilipokea mazoezi ambayo yalinisaidia kuithamini zaidi Biblia na tengenezo la Mungu. Niligundua kwamba wale ambao waliongoza kazi ya kuhubiri ulimwenguni walikuwa wenye urafiki na wenye fadhili. Walifanya kazi kwa bidii pamoja nasi. (Mathayo 24:14) Sikushangazwa na jambo hilo, hata hivyo nilifurahi kulishuhudia.

Kisha, wakati wa kuhitimu kwa darasa la nane la Shule ya Gileadi ukafika Februari 9, 1947 (9/2/1947). Ndugu Knorr alitangaza nchi ambako wanafunzi wangetumwa. Zamu yangu ilipofika, alisema hivi: “Ndugu Pramberg anarudi Sweden kutumikia ndugu zake huko.” Kwa kweli sikufurahia kurudi nyumbani.

Kutimiza Mgawo Mgumu

Niliporudi Sweden, nilijifunza kazi mpya iliyokuwa ikianzishwa katika nchi nyingi ulimwenguni pote, yaani, kazi ya wilaya. Niliwekwa rasmi kutumikia nikiwa mwangalizi wa wilaya wa kwanza nchini Sweden, na nilizunguka nchi nzima. Nilipanga na kusimamia yale ambayo yaliitwa baadaye makusanyiko ya mzunguko, ambayo yalifanywa katika majiji na miji kotekote nchini Sweden. Kwa kuwa mpango huo ulikuwa mpya kabisa, nilipokea maagizo machache sana. Mimi na Ndugu Eneroth tuliketi chini na kutayarisha programu nzuri iwezekanavyo. Niliogopa nilipopokea mgawo huo, nami nilisali mara nyingi, nyingi sana kwa Yehova. Kwa miaka 15, nilikuwa na pendeleo la kutumika katika kazi ya wilaya.

Siku hizo, ilikuwa vigumu kupata mahali pazuri pa kufanyia mikutano. Tulitumia kumbi za kuchezea dansi na mahali pengine kama hapo, ambapo mara nyingi palikuwa na baridi na hapakutunzwa vizuri. Mfano mmoja ni kusanyiko tulilofanya huko Rökiö, Finland. Tulitumia jumba la zamani la jumuiya ambalo kwa muda fulani halikuwa likitumiwa. Kulikuwa na dhoruba ya theluji, na kulikuwa na baridi kali sana. Hivyo, tuliwasha majiko mawili makubwa yaliyotengenezwa kwa mapipa ya mafuta. Hata hivyo, hatukujua kwamba ndege walikuwa wamejenga viota vyao ndani ya bomba la moshi. Moshi ulitufunika! Hata hivyo, huku tukiwa tumejifunika makoti na macho yakiwasha, kila mtu aliendelea kuketi. Tukio hilo lilifanya kusanyiko hilo likumbukwe sana.

Moja ya maagizo ya kupanga makusanyiko ya mzunguko ya siku tatu lilikuwa kuwapikia wajumbe chakula. Mwanzoni, hatukuwa na vyombo na uzoefu wa kufanya kazi hiyo. Lakini tulikuwa na ndugu na dada wazuri ambao walikubali kwa furaha kufanya kazi hiyo ngumu. Siku iliyotangulia kusanyiko, ungewaona wakiinama juu ya pipa, wakimenya viazi huku wakisimulia kwa shangwe mambo yaliyoonwa. Urafiki wa miaka mingi kati ya ndugu na dada ulianza katika pindi kama hizo walipokuwa wakifanya kazi pamoja kwa bidii.

Wakati huo, kazi yetu ilitia ndani kutembea na mabango ili kutangaza makusanyiko hayo ya mzunguko. Tulitembea kwa msafara mjini au kijijini, tukiwaalika watu kwenye hotuba ya watu wote. Kwa ujumla, mara nyingi watu walikuwa wenye fadhili na heshima. Siku moja katika mji wa Finspång, barabara ilikuwa imejaa wafanyakazi waliokuwa wakitoka kiwandani. Kwa ghafula, mmoja wao alipaaza sauti hivi: “Tazameni, watu ambao walimshinda Hitler!”

Tukio Kubwa Katika Maisha Yangu

Muda si muda, maisha yangu nikiwa mhudumu anayesafiri yangebadilika baada ya kukutana na Karin, mwanamke mwenye kuvutia sana. Sote wawili tulialikwa kuhudhuria kusanyiko la kimataifa huko Yankee Stadium, New York City, mnamo Julai (Mwezi wa 7) 1953. Katika pindi hiyo, Jumatatu (Siku ya Kwanza) tarehe 20, wakati wa mapumziko, Milton Henschel alitoa hotuba ya arusi yetu. Lilikuwa tukio lisilo la kawaida katika uwanja huo wa kimataifa wa besiboli. Baada ya kutumika pamoja katika kazi ya kusafiri hadi mwaka wa 1962, mimi na Karin tulialikwa kujiunga na familia ya Betheli ya Sweden. Kwanza, nilifanya kazi katika Idara ya Magazeti. Kisha, kwa sababu ya uzoefu wangu nikiwa fundi wa magari, nilipewa mgawo wa kusimamia mashini za kuchapishia na mashini nyingine kwenye ofisi ya tawi. Karin alitumika kwa miaka mingi katika idara ya kufua nguo. Na kwa miaka mingi sasa, amekuwa akitumika katika Idara ya Usahihishaji.

Kwa miaka zaidi ya 54 ambayo tumekuwa tukimtumikia Yehova tukiwa wenzi wa ndoa, maisha yetu yenye furaha na kusudi yamekuwa na matukio mengi muhimu na yenye kusisimua! Kwa kweli, Yehova amelibariki tengenezo lake lenye watumishi wenye bidii na upendo. Nilipoanza kutumika kwenye ofisi ya tawi mwaka wa 1940, kulikuwa na Mashahidi 1,500 tu nchini Sweden. Lakini sasa wako zaidi ya 22,000. Ukuzi umekuwa mkubwa hata zaidi katika sehemu nyingine ulimwenguni, hivi kwamba sasa kuna Mashahidi zaidi ya milioni sita na nusu duniani pote.

Roho ya Yehova inategemeza kazi yetu, ikitusaidia daima kusonga mbele. Kwa macho ya imani, tunaona ng’ambo ya bahari ya wanadamu yenye mchafuko, lakini hatuogopi. Huku tukisonga mbele, tunaona waziwazi ulimwengu mpya wa Mungu. Mimi na Karin tunamshukuru Mungu kwa wema wake wote na tunasali kila siku ili tupate nguvu za kudumisha utimilifu wetu na mwishowe tufikie mradi wetu, yaani, kupata kibali cha Mungu na uzima wa milele!—Mathayo 24:13.

[Picha katika ukurasa wa 12]

Nikiwa nimebebwa na mama yangu

[Picha katika ukurasa wa 13]

Nilikosafiri baharini na Baba kwa meli ndogo mapema miaka ya 1920

[Picha katika ukurasa wa 15]

Nikiwa na Herman Henschel (baba ya Milton) katika Gileadi, 1946

[Picha katika ukurasa wa 16]

Tulifunga ndoa huko Yankee Stadium mnamo Julai 20, 1953