Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Hagai na cha Zekaria

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Hagai na cha Zekaria

Neno la Yehova Liko Hai

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Hagai na cha Zekaria

NI MWAKA wa 520 K.W.K. Miaka 16 imepita tangu Wayahudi waliorudi kutoka uhamishoni Babiloni walipoweka msingi wa hekalu la Yehova huko Yerusalemu. Hata hivyo, hekalu halijakamilika, na kazi ya ujenzi imepigwa marufuku. Yehova anamweka rasmi nabii Hagai, na miezi miwili baadaye anamweka rasmi pia nabii Zekaria ili atangaze neno Lake.

Hagai na Zekaria wana kusudi moja: Kuwachochea watu waanze tena kazi ya kujenga upya hekalu. Jitihada za manabii hao zinafanikiwa, na hekalu linakamilishwa miaka mitano baadaye. Ujumbe ambao Hagai na Zekaria wanatangaza umeandikwa katika vitabu vinavyoitwa kwa majina yao. Kitabu cha Hagai kilikamilishwa mwaka wa 520 K.W.K. na cha Zekaria mwaka wa 518 K.W.K. Kama manabii hao, sisi pia tumepewa kazi na Mungu, ambayo inapaswa kukamilishwa kabla ya mwisho wa mfumo huu wa mambo. Ni kazi ya kutangaza Ufalme na kufanya wanafunzi. Acheni tuone kitia-moyo tunachoweza kupata kutokana na kitabu cha Hagai na cha Zekaria.

“WEKENI MOYO WENU JUU YA NJIA ZENU”

(Hagai 1:1–2:23)

Kwa muda wa siku 112, Hagai anatoa jumbe nne zenye kuchochea. Ujumbe wa kwanza ni: “‘Wekeni moyo wenu juu ya njia zenu. Pandeni mlimani, mkalete miti. Jengeni nyumba hii, nipate kuifurahia na nipate kutukuzwa,’ asema Yehova.” (Hagai 1:7, 8) Watu wanaitikia vizuri. Ujumbe wa pili una ahadi hii: “Nami [Yehova] nitaijaza nyumba hii utukufu.”—Hagai 2:7.

Kulingana na ujumbe wa tatu, kupuuza kwao kazi ya kujenga upya hekalu kumewafanya ‘watu na kazi yote ya mikono yao’ kuwa najisi machoni pa Yehova. Hata hivyo, tangu kazi ya kurekebisha hekalu inapoanza, Yehova ‘anatoa baraka’ juu yao. Kama inavyosemwa katika ujumbe wa nne, Yehova ‘ataangamiza nguvu za falme za mataifa’ na kumweka Gavana Zerubabeli kuwa “pete ya muhuri.”—Hagai 2:14, 19, 22, 23.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

1:6—Maneno “mnakunywa, lakini hamlewi” yanamaanisha nini? Maneno hayo yanaonyesha tu upungufu wa divai. Kwa sababu ya ukosefu wa baraka za Yehova, divai itapungua, yaani, haitatosha kabisa kiasi cha kuweza kulewesha.

2:6, 7, 21, 22—Ni nani au ni nini kinachosababisha kutikiswa, kukiwa na matokeo gani? Yehova ‘anatikisa mataifa yote’ kupitia kazi ya ulimwenguni pote ya kuhubiri ujumbe wa Ufalme. Pia, kazi hiyo inasababisha “vitu vyenye kutamanika vya mataifa yote” viingizwe katika nyumba ya Yehova, na hivyo kuijaza utukufu. Kisha, “Yehova wa majeshi” atatikisa “mbingu na dunia na bahari na nchi kavu,” na kuuharibu kabisa mfumo wote mwovu wa mambo.—Waebrania 12:26, 27.

2:9—Ni katika njia gani ‘utukufu wa nyumba ya baadaye ungekuwa mkubwa kuliko ule wa ile ya zamani’? Angalau katika njia tatu: miaka ambayo hekalu hilo lilidumu, yule ambaye angefundisha katika hekalu hilo, na wale ambao wangemiminika humo ili kumwabudu Yehova. Ingawa utukufu wa hekalu la Sulemani uliendelea kwa miaka 420, tangu mwaka wa 1027 K.W.K. hadi 607 K.W.K., “nyumba hii ya baadaye” ilitumiwa kwa zaidi ya miaka 580, tangu ilipojengwa mwaka wa 515 K.W.K. hadi ilipoharibiwa mwaka wa 70 W.K. Zaidi ya hilo, Masihi, Yesu Kristo, alifundisha katika ‘nyumba hiyo ya baadaye,’ na watu wengi zaidi walikuja katika nyumba hiyo kuliko ile “ya zamani” ili kumwabudu Mungu.—Matendo 2:1-11.

Mambo Tunayojifunza:

1:2-4. Upinzani kuelekea kazi yetu ya kuhubiri haupaswi kutufanya tuache “kuutafuta kwanza ufalme” na kuanza kutafuta faida zetu.—Mathayo 6:33.

1:5, 7Ni vizuri ‘tuweke moyo wetu juu ya njia zetu’ na kutafakari jinsi uhusiano wetu na Mungu unavyoweza kuathiriwa na njia yetu ya maisha.

1:6, 9-11; 2:14-17. Wayahudi wa siku za Hagai walitafuta kwa bidii faida zao za kibinafsi lakini hawakufurahia matunda ya kazi yao. Walipuuza hekalu, na hivyo hawakubarikiwa na Mungu. Tunapaswa kutanguliza mambo ya kiroho na kumtumikia Mungu kwa nafsi yote, tukikumbuka kwamba hata tukiwa na vitu vingi au vichache, ‘baraka ya Yehova ndiyo hutajirisha.’—Methali 10:22.

2:15, 18. Yehova aliwahimiza Wayahudi kuanzia siku hiyo na kuendelea waweke mioyo yao juu ya kazi ya kujenga upya hekalu, na si juu ya mwelekeo waliokuwa nao wa kupuuza mambo. Vivyo hivyo, tunapaswa kusonga mbele tukikazia fikira ibada yetu kwa Mungu.

‘SI KWA NGUVU, BALI KWA ROHO YANGU’

(Zekaria 1:1–14:21)

Zekaria anaanza kazi yake ya kutoa unabii kwa kuwaomba Wayahudi ‘warudi kwa Yehova.’ (Zekaria 1:3) Maono manane yanayofuata yanatoa uhakikisho wa utegemezo wa Mungu juu ya kazi ya kujenga upya hekalu. (Ona sanduku “Maono Manane ya Mfano ya Zekaria.”) Kazi ya ujenzi itakamilika, “si kwa jeshi, wala kwa nguvu, bali kwa roho [ya Yehova].” (Zekaria 4:6) Mwanamume anayeitwa Chipukizi “atalijenga hekalu la Yehova” na “atakuwa kuhani juu ya kiti chake cha ufalme.”—Zekaria 6:12, 13.

Betheli inatuma wajumbe kuuliza makuhani kuhusu kufunga ili kuadhimisha kuharibiwa kwa Yerusalemu. Yehova anamweleza Zekaria kwamba kuomboleza muda wa mifungo minne ya kukumbuka msiba ambao uliangukia Yerusalemu, kutabadilishwa na kuwa “furaha na kushangilia na majira mema ya sherehe.” (Zekaria 7:2; 8:19) Matangazo mawili yanayofuata yanatia ndani hukumu juu ya mataifa na manabii wa uwongo, unabii wa Kimasihi, na ujumbe wa kurudishwa kwa watu wa Mungu.—Zekaria 9:1; 12:1.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

2:1—Kwa nini mtu fulani alikuwa akipima Yerusalemu kwa kamba? Inaelekea kwamba tendo hilo lilimaanisha kujengwa kwa ukuta wa ulinzi kuzunguka jiji hilo. Malaika anamjulisha mwanamume huyo kwamba Yerusalemu litapanuliwa nalo litalindwa na Yehova.—Zekaria 2:3-5.

6:11-13—Je, kuweka taji juu ya kichwa cha Kuhani Mkuu Yoshua kulimfanya awe mfalme na kuhani? Hapana, Yoshua hakuwa wa ukoo wa kifalme wa Daudi. Hata hivyo, kuvikwa kwake taji kichwani kulikuwa mfano wa kinabii wa kuja kwa Masihi. (Waebrania 6:20) Unabii kuhusu “Chipukizi” umetimizwa na Mfalme na Kuhani wa kimbingu Yesu Kristo. (Yeremia 23:5) Kama vile Yoshua alivyowatumikia Wayahudi waliorudishwa akiwa kuhani mkuu katika hekalu lililojengwa upya, ndivyo Yesu alivyo Kuhani Mkuu wa ibada ya kweli katika hekalu la kiroho la Yehova.

8:1-23—Matangazo kumi yanayotajwa katika mistari hii yanatimizwa wakati gani? Kila tangazo linafuatwa na maneno “Yehova wa majeshi asema hivi” na ni ahadi ya Mungu ya kuwaletea watu wake amani. Baadhi ya matangazo hayo yalitimia katika karne ya sita K.W.K., lakini yote yametimia kuanzia mwaka wa 1919 W.K. au yanaendelea kutimia sasa. *

8:3—Kwa nini Yerusalemu liliitwa “jiji la ukweli”? Kabla ya kuharibiwa mwaka wa 607 K.W.K., Yerusalemu lilikuwa “jiji lenye kukandamiza,” lililojaa manabii na makuhani wafisadi na watu wasio waaminifu. (Sefania 3:1; Yeremia 6:13; 7:29-34) Hata hivyo, kwa kuwa hekalu lilikuwa limejengwa upya na watu walikuwa wamejitoa kumwabudu Yehova, kweli kuhusu ibada safi zilipaswa kutangazwa huko, na Yerusalemu lingeitwa “jiji la ukweli.”

11:7-14—Ni nini maana ya Zekaria kukata fimbo inayoitwa “Uzuri” na nyingine inayoitwa “Muungano”? Zekaria anaonyeshwa akiwa mjumbe aliyetumwa ‘kulichunga kundi lililokusudiwa kuuawa,’ yaani, watu walio mfano wa kondoo ambao wanakandamizwa na viongozi wao. Katika daraka lake akiwa mchungaji, Zekaria alifananisha kimbele Yesu Kristo, ambaye alitumwa kwa watu waliofanya agano pamoja na Mungu lakini akakataliwa nao. Kukata fimbo iliyoitwa “Uzuri” kulimaanisha kwamba Mungu angekomesha agano la Sheria pamoja na Wayahudi na kuacha kuwatendea mema. Kukata fimbo iliyoitwa “Muungano” kulimaanisha kuharibu ushirikiano wa kindugu kati ya Yuda na Israeli ambao ulitegemea kumwabudu Yehova.

12:11—Ni nini “maombolezo ya Hadadrimoni katika nchi tambarare ya bonde la Megido”? Mfalme Yosia wa Yuda aliuawa akipigana vita na Farao Neko wa Misri katika “nchi tambarare ya bonde la Megido,” na kifo chake kiliombolezwa kwa ‘nyimbo za maombolezo’ kwa miaka mingi. (2 Mambo ya Nyakati 35:25) Kwa hiyo, huenda “maombolezo ya Hadadrimoni” yakarejelea maombolezo ya kifo cha Yosia.

Mambo Tunayojifunza:

1:2-6; 7:11-14. Yehova anapendezwa na anawarudia wale wanaotubu, wanaokubali karipio, na kumrudia ili wamtolee ibada kwa nafsi yao yote. Kwa upande mwingine, hajibu maombi ya kutaka msaada ya wale ‘wanaoendelea kukataa kusikiliza, na kuendelea kugeuza bega kwa ukaidi, wakifanya masikio yao kuwa magumu mno yasiweze kusikia’ ujumbe wake.

4:6, 7Hakuna vizuizi vilivyokuwa vikubwa sana roho ya Yehova isiweze kuvishinda ili kukamilisha kazi ya kujenga upya hekalu. Tunaweza kushinda tatizo lolote ambalo huenda tukakabili katika utumishi wetu kwa Mungu tukiwa na imani katika Yehova.—Mathayo 17:20.

4:10. Wakiongozwa na Yehova, Zerubabeli na watu wake walikamilisha hekalu kulingana na viwango vya juu vya Mungu. Si vigumu sana kwa wanadamu wasio wakamilifu kutimiza matakwa ya Yehova.

7:8-10; 8:16, 17. Ili kupata kibali cha Yehova, ni lazima tutende haki, tuonyeshe fadhili zenye upendo, tutende kwa rehema, na tuseme kweli mtu na mwenzake.

8:9-13. Yehova anatubariki ‘mikono yetu inapokuwa yenye nguvu’ katika kutimiza kazi tuliyopewa. Baraka hizo zinatia ndani amani, usalama, na maendeleo ya kiroho.

12:6. Wale ambao ni waangalizi kati ya watu wa Yehova wanapaswa kuwa “kama mwenge wenye moto,” yaani, wanapaswa kuwa wenye bidii sana.

13:3. Tunapaswa kuwa washikamanifu kwa Mungu wa kweli na kwa tengenezo lake kuliko kwa mwanadamu yeyote, hata kama tuna uhusiano wa karibu sana naye.

13:8, 9Waasi-imani ambao Yehova alikataa walikuwa wengi sana, walikuwa sehemu mbili ya watu wote wa nchi. Ni sehemu moja ya tatu tu ya watu hao iliyosafishwa kana kwamba kupitia moto. Katika siku zetu, dini zinazodai kuwa za Kikristo zinafanyiza sehemu kubwa ya wale ambao wanadai kuwa Wakristo, lakini zimekataliwa na Yehova. Ni sehemu ndogo tu, yaani, Wakristo watiwa-mafuta, ambao ‘wameliitia jina la Yehova’ na kukubali kusafishwa. Wao na waamini wenzao wanathibitisha wazi kwamba wao si Mashahidi wa Yehova kwa jina tu.

Tunachochewa Kutenda kwa Bidii

Ujumbe ambao Hagai na Zekaria walitangaza unatuhusu jinsi gani leo? Tunapotafakari jinsi ujumbe wao ulivyowachochea Wayahudi kukazia uangalifu kazi ya ujenzi wa hekalu, je, hatuchochewi kushiriki kwa bidii katika kazi ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi?

Zekaria alitabiri kwamba Masihi angekuja akiwa “amepanda juu ya punda,” kwamba angesalitiwa kwa “vipande 30 vya fedha,” angepigwa, na kwamba “wale wa kundi [wangetawanyika].” (Zekaria 9:9; 11:12; 13:7) Kutafakari juu ya utimizo wa unabii huo mbalimbali wa Zekaria kuhusu Masihi kutajenga imani yetu kama nini! (Mathayo 21:1-9; 26:31, 56; 27:3-10) Uhakika wetu katika Neno la Yehova na katika maandalizi yake ya kutuokoa unatiwa nguvu.—Waebrania 4:12.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 25 Ona gazeti la Mnara wa Mlinzi la Januari 1, 1996, ukurasa wa 9-22.

[Sanduku katika ukurasa wa 11]

MAONO MANANE YA MFANO YA ZEKARIA

1:8-17: Yanatoa uhakikisho wa kwamba hekalu litakamilishwa na yanaonyesha kuwa Yerusalemu na majiji mengine katika Yuda yatabarikiwa.

1:18-21: Yanaahidi mwisho wa ‘pembe nne ambazo zilitawanya Yuda,’ yaani, serikali zote zilizopinga ibada ya Yehova.

2:1-13: Yanaonyesha kwamba Yerusalemu litapanuka na kwamba Yehova atakuwa kwake “ukuta wa moto kuzunguka pande zote,” yaani, atalilinda.

3:1-10: Yanaonyesha kwamba Shetani anahusika katika kupinga kazi ya hekalu na kwamba Kuhani Mkuu Yoshua anaokolewa na kusafishwa.

4:1-14: Yanatoa uhakikisho wa kwamba vizuizi vilivyo kama mlima vitalainishwa na kwamba Gavana Zerubabeli atakamilisha ujenzi wa hekalu.

5:1-4: Yanatangaza hukumu ya laana kwa watenda-maovu ambao hawajaadhibiwa.

5:5-11: Yanatabiri mwisho wa uovu.

6:1-8: Yanaahidi usimamizi na ulinzi wa malaika.

[Picha katika ukurasa wa 8]

Ujumbe wa Hagai na Zekaria ulikuwa na kusudi gani?

[Picha katika ukurasa wa 10]

Wale ambao ni waangalizi ni “kama mwenge wenye moto” jinsi gani?