Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Mkristo anapaswa kuwa na maoni gani kuhusu kuwinda na kuvua?

Biblia haishutumu uwindaji au uvuvi. (Kumbukumbu la Torati 14:4, 5, 9, 20; Mathayo 17:27; Yohana 21:6) Hata hivyo, Wakristo wanaowinda au kuvua wanapaswa kufikiria kanuni fulani za Kimaandiko.

Mungu alimruhusu Noa na wazao wake waue na kula wanyama, maadamu walimwaga damu ya wanyama hao kabla ya kuwala. (Mwanzo 9:3, 4) Agizo hilo lilikazia kwamba uhai wa wanyama unapaswa kuheshimiwa kwa kuwa umetoka kwa Mungu. Hivyo, Wakristo hawachezi michezo ya kuua wanyama au kuwaua ili kujifurahisha, huku wakitenda bila rehema na kudharau uhai.—Methali 12:10.

Kuna jambo la ziada linalohusu mtazamo wetu. Inaelekea kwamba mitume ambao walikuwa wavuvi walifurahia kuvua samaki wengi. Hata hivyo, hakuna jambo linaloonyesha kwamba walijivunia uwezo wao wa kuvua au kuwinda, au kwamba walivua au kuwinda ili kushindana na wengine, kuonyesha kwamba wao ni wanaume, au kupata msisimko kwa kuwakimbiza wanyama, kupigana nao, au kuwaua.—Zaburi 11:5; Wagalatia 5:26.

Hivyo, huenda tukajiuliza: ‘Je, ninaweka mfano mzuri wa kuheshimu maoni ya Yehova kuhusu uhai? Je, ninafikiri au kuzungumza tu kuhusu kuwinda au kuvua? Je, njia yangu ya maisha inaonyesha kwamba ninapenda sana kuwinda, kushika, na kuua wanyama au samaki, au inanitambulisha kuwa mhudumu wa Mungu? Je, uwindaji au uvuvi unanifanya niwe na uhusiano wa karibu na watu wasio waamini au kunifanya nipuuze familia yangu?’—Luka 6:45

Huenda baadhi ya watu wanaowinda au kuvua ili kupata chakula wakajitetea wanapopuuza mambo ya kiroho katika majira ya kuwinda au kuvua. Hata hivyo, tunaonyesha kwamba tuna imani na tunamtegemea Mungu tunapokataa kuruhusu chochote kiwe muhimu zaidi kuliko mambo ya kiroho. (Mathayo 6:33) Zaidi ya hilo, Wakristo wanatii sheria zote za “Kaisari” kuhusu kuwinda na kuvua, iwe zinatekelezwa au hazitekelezwi na wenye mamlaka.—Mathayo 22:21; Waroma 13:1.

Ili kujipatanisha na maoni ya Yehova juu ya uwindaji na uvuvi, huenda watu fulani wakahitaji kubadili kufikiri kwao kuhusiana na viwango vyake. (Waefeso 4:22-24) Kwa upande mwingine, tunahitaji kuheshimu maamuzi ya wengine yanayotegemea dhamiri. Shauri hili la mtume Paulo linafaa hali hiyo: “Sisi na tusiwe tukihukumiana tena, bali badala yake fanyeni hili kuwa uamuzi wenu, kutokuweka mbele ya ndugu kikwazo.” (Waroma 14:13) Kuonyesha upendo na heshima kama hiyo isiyo na ubinafsi kunaleta amani kutanikoni na kunampendeza Mtengenezaji wetu, aliye Chanzo cha uhai wote.—1 Wakorintho 8:13. *

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 8 Ona pia “Maswali Kutoka kwa Wasomaji” katika toleo la Mnara wa Mlinzi la Mei 15, 1990 (15/5/1990).