Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mfundishe Mtoto Wako Awe Mwenye Kufanya Amani

Mfundishe Mtoto Wako Awe Mwenye Kufanya Amani

Mfundishe Mtoto Wako Awe Mwenye Kufanya Amani

Akiwa amesisimuka sana baada ya familia yao kuhamia sehemu ya mbali, Nicole aliye na umri wa miaka minane aliwasiliana kwa ukawaida na rafiki yake mkubwa, Gabrielle, na kumjulisha kila kitu. Siku moja, kwa ghafula Gabrielle alimwambia Nicole kuwa hajuti kamwe kwamba walihama. Akiwa ameumizwa na kukasirishwa sana, Nicole alimwambia mama yake hivi, “Sitaki kumwona Gabrielle tena!”

KWA kawaida, msaada wa wazazi unahitajiwa ili kutatua matatizo ya watoto kama tatizo lililotokea kati ya Nicole na Gabrielle. Wazazi hawapaswi tu kutuliza hisia za watoto wao bali pia kuwaonyesha jinsi ya kusuluhisha tatizo. Kwa kawaida watoto wadogo wanaonyesha “tabia za mtoto,” na mara nyingi hawajui jinsi maneno na matendo yao yanavyoweza kuumiza. (1 Wakorintho 13:11) Wanahitaji kusaidiwa kusitawisha sifa zinazoweza kuchangia mahusiano yenye amani katika familia na kwingineko.

Wazazi Wakristo wanapendezwa sana kuwazoeza watoto wao ‘watafute amani na kuifuatia.’ (1 Petro 3:11) Kwa kuwa mtu anayefanya amani anapata furaha kubwa, inafaa tujitahidi tuwezavyo kushinda hisia za mashaka, mfadhaiko, na chuki. Ikiwa wewe ni mzazi, unaweza kuwafundisha jinsi gani watoto wako wawe wenye kufanya amani?

Wasaidie Watamani Kumpendeza “Mungu wa Amani”

Yehova anaitwa “Mungu wa amani” na anatambulishwa kuwa yule “anayetoa amani.” (Wafilipi 4:9; Waroma 15:33) Hivyo, wazazi wenye hekima wanatumia kwa ustadi Neno la Mungu, Biblia, ili kusitawisha ndani ya watoto wao tamaa ya kumpendeza Mungu na kuiga sifa zake. Kwa mfano, wasaidie watoto wako wawazie kile ambacho mtume Yohana aliona katika maono, yaani, upinde mkubwa wa mvua wenye rangi yenye kuvutia ya zumaridi ambao unazunguka kiti cha ufalme cha Yehova. * (Ufunuo 4:2, 3) Waeleze kwamba upinde huo wa mvua unafananisha amani na utulivu unaomzunguka Yehova na kwamba wote wanaomtii watapata baraka hiyo.

Pia, Yehova anaandaa mwongozo kupitia Yesu, Mwana wake, ambaye anaitwa “Mkuu wa Amani.” (Isaya 9:6, 7) Hivyo, soma na uzungumze na watoto wako kuhusu masimulizi ya Biblia ambamo Yesu alifundisha masomo muhimu kuhusu kuepuka vita na mabishano. (Mathayo 26:51-56; Marko 9:33-35) Eleza kwa nini Paulo, ambaye mwanzoni alikuwa “mtu mwenye dharau,” alibadili njia zake na akaandika kwamba “mtumwa wa Bwana hahitaji kupigana, bali anahitaji kuwa mpole kwa wote, mwenye sifa za kustahili kufundisha, . . . akiendelea kujizuia chini ya uovu.” (1 Timotheo 1:13; 2 Timotheo 2:24) Mtoto wako anaweza kuitikia kwa njia nzuri kuliko unavyotazamia.

Evan anakumbuka akidhihakiwa katika basi la shule na mvulana fulani alipokuwa na umri wa miaka saba. “Mvulana huyo alinikasirisha sana hivi kwamba nikataka kulipiza kisasi!” anasema. “Kisha nikakumbuka jambo tulilojifunza nyumbani kuhusu wale wanaoanzisha mapigano. Nilijua kwamba Yehova hataki ‘nimlipe yeyote uovu kwa uovu’ bali anataka ‘nifanye amani na watu wote.’” (Waroma 12:17, 18) Hivyo basi, Evan alipata nguvu na ujasiri wa kutatua tatizo hilo kwa upole. Alitaka kumpendeza Mungu wa amani.

Uwe Mzazi Anayefanya Amani

Je, kuna amani nyumbani kwenu? Ikiwa ndivyo, watoto wako wanaweza kujifunza mengi kuhusu amani hata kwa kukutazama tu. Kufanikiwa kwako katika kuwafundisha watoto wako wawe wenye kufanya amani kunategemea sana kadiri unavyoiga njia za amani za Mungu na Kristo.—Waroma 2:21.

Russ na Cindy wanajitahidi sana kuwazoeza wavulana wao wawili, wakiwahimiza watende kwa upendo wanapokasirishwa na wengine. Cindy anasema, “Mtazamo ambao mimi na Russ tunaonyesha kuwaelekea wana wetu na kuwaelekea watu wengine matatizo yanapotokea, una uvutano mkubwa kuhusu jinsi wavulana wetu wanavyoshughulikia hali kama hizo.”

Hata unapokosea—na ni wazazi gani wasiokosea?—bado unaweza kutumia nafasi hiyo kufundisha masomo muhimu. “Kuna nyakati ambazo mimi na mke wangu, Terry, tulikasirika sana na kuwaadhibu watoto wetu watatu bila kupata kwanza habari zote,” anakubali Stephen. “Hilo lilipotukia, tuliomba msamaha.” Terry anaongezea: “Tuliwaambia watoto wetu kwamba sisi pia si wakamilifu na kwamba tunakosea. Tunahisi kwamba kufanya hivyo hakujachangia tu amani katika familia yetu bali pia kumewasaidia watoto wetu kujifunza jinsi ya kufuatia amani.”

Je, watoto wako wanajifunza jinsi ya kuwa wenye kufanya amani wanapotazama jinsi unavyowatendea? Yesu alihimiza hivi: “Mambo yote mnayotaka watu wawatendee ninyi, lazima mwatendee wao pia vivyo hivyo.” (Mathayo 7:12) Ingawa wewe pia unakosea, uwe na hakika kwamba upendo wako kwa watoto wako utakuwa na matokeo mazuri. Watoto wako watatii haraka mwelekezo unaotolewa kwa upendo.

Usiwe Mwepesi wa Kukasirika

Methali 19:11 inasema: “Ufahamu wa mtu hakika hupunguza hasira yake.” Unaweza kuwasaidia jinsi gani watoto wako wawe na ufahamu kama huo? David anaeleza njia ambayo yeye na mke wake, Mariann, wametumia kumsaidia mwana na binti yao. Anasema hivi: “Wanapokasirishwa na mtu anayesema au kutenda jambo lenye kuumiza, tunawasaidia kuonyesha huruma. Tunawauliza maswali rahisi kama vile: ‘Je, mtu huyo amefadhaika? Je, ni mwenye wivu? Je, ameumizwa na mtu mwingine?’” Mariann anaongezea, “Inaelekea kwamba hilo linawatuliza watoto badala ya kuendelea kuumia au kushindana kuhusu ni nani aliyekosea.”

Mazoezi kama hayo yanaweza kuwa na matokeo mazuri sana. Ona jinsi Nicole, aliyetajwa mwanzoni mwa habari hii alivyosaidiwa na mama yake, Michelle, kwa njia ambayo ilitimiza mengi zaidi ya kutatua tu tatizo kati yake na rafiki yake Gabrielle. “Mimi na Nicole tulisoma sura ya 14 ya kitabu Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu,” anasema Michelle. * “Kisha nikaeleza alichomaanisha Yesu aliposema tunapaswa kumsamehe mtu ‘mpaka mara 77.’ Baada ya kumsikiliza Nicole kwa makini akinieleza jinsi alivyohisi, nilimsaidia kuwazia jinsi Gabrielle alivyohuzunika na kufadhaika kwa sababu rafiki yake mkubwa alikuwa amehama.”—Mathayo 18:21, 22.

Ufahamu huo mpya wa Nicole kuhusu jambo ambalo huenda lilimfanya Gabrielle afoke ulimwezesha kuwa na huruma na kumsukuma ampigie simu Gabrielle ili kuomba msamaha. “Tangu hapo,” anasema Michelle, “Nicole anapata furaha kwa kujali hisia za wengine na kuwatendea mema ili kuwafanya wahisi vizuri.”—Wafilipi 2:3, 4.

Wasaidie watoto wako waepuke kukasirishwa na makosa ya wengine na kutoelewana. Huenda ukapata uradhi kuwaona watoto wako wakiwatendea wengine mema na kuwaonyesha upendo wa kweli.—Waroma 12:10; 1 Wakorintho 12:25.

Kazia Kwamba Kusamehe Kunapendeza

Methali 19:11 linasema hivi: ‘Ni jambo lenye kupendeza kupita kosa.’ Yesu alipokuwa na maumivu makali zaidi, alimwiga Baba yake na kuonyesha mtazamo wa kusamehe. (Luka 23:34) Watoto wako wanaweza kujifunza jinsi kusamehe kunavyopendeza wanapopata faraja unapowasamehe.

Kwa mfano, Willy, aliye na umri wa miaka mitano, anapenda kupaka picha rangi pamoja na nyanya yake. Pindi moja, Nyanya aliacha ghafula kupaka picha rangi, akamkemea Willy kwa ukali, kisha akaenda zake. Willy alifadhaika. Baba yake, Sam, alisema hivi: “Nyanya ya Willy ana ugonjwa wa Alzheimer. Hivyo, tulimweleza Willy jambo hilo kwa njia ambayo angeelewa.” Baada ya kumkumbusha Willy kwamba alikuwa amesamehewa mara nyingi na kwamba anapaswa kuwasamehe wengine, Sam alishangaa kuona itikio la Willy. “Unaweza kuwazia jinsi mimi na mke wangu tulivyohisi,” anasema Sam, “tulipomwona mwana wetu mdogo akimwendea nyanya yake mwenye umri wa miaka 80, akizungumza naye na kumwomba msamaha, kisha akimshika mkono na kumrudisha mezani!”

Kwa kweli inapendeza watoto wanapojifunza ‘kuendelea kuvumilia’ udhaifu na makosa ya wengine na kuwasamehe. (Wakolosai 3:13) Hata watu wanapomuudhi mtoto wako kimakusudi, mhakikishie kwamba kutenda kwa njia ya amani kunaweza kuwa na matokeo makubwa, kwa kuwa “Yehova anapofurahia njia za mtu, huwafanya hata adui zake wawe na amani naye.”—Methali 16:7.

Endelea Kumsaidia Mtoto Wako Awe Mwenye Kufanya Amani

Wazazi wanapotumia Neno la Mungu kuwafundisha watoto wao “chini ya hali zenye amani,” wanakuwa chanzo cha baraka ya kweli kwa watoto wao. (Yakobo 3:18) Wazazi kama hao wanawapa watoto wao mazoezi wanayohitaji ili kutatua matatizo na kuwa wenye kufanya amani. Hilo litawasaidia sana wawe na furaha na uradhi katika maisha yao yote.

Dan na Kathy wana vijana watatu ambao wanaendelea vizuri kiroho. “Ijapokuwa haikuwa rahisi kuwazoeza walipokuwa wachanga,” anasema Dan, “tunafurahi sana kwamba watoto wetu wameendelea vizuri kiroho. Sasa wanapatana na wengine, na wanawasamehe wengine kwa kupenda wakati jambo fulani linapotishia kuvuruga amani.” Kathy anasema, “Hilo hasa linatutia moyo, kwa kuwa amani ni sehemu ya matunda ya roho ya Mungu.”—Wagalatia 5:22, 23.

Hivyo, mkiwa wazazi Wakristo mna sababu nzuri ya ‘kutokufa moyo’ au ‘kutochoka kabisa’ kuwafundisha watoto wenu wawe wenye kufanya amani, hata kama mwanzoni watoto hawafanyi maendeleo haraka. Mnapofanya hivyo, mwe na hakika kwamba “Mungu wa upendo na wa amani atakuwa pamoja nanyi.”—Wagalatia 6:9; 2 Wakorintho 13:11.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Ona picha kwenye ukurasa wa 75 wa kitabu Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu! kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 16 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 20]

JE, NI UVUTANO MZURI?

Mtungo au insha yenye kichwa “Jeuri katika Burudani za Vyombo vya Habari” ambayo ilichapishwa na mtandao fulani (Media Awareness Network), inasema hivi: “Wazo la kwamba jeuri ni njia ya kutatua matatizo limekaziwa na vipindi ambamo wahusika wote, wazuri kwa wabaya wanatenda jeuri mara nyingi.” Karibu asilimia 10 tu ya vipindi vya televisheni, sinema, na video za muziki zilizochunguzwa ndizo zilizoonyesha matokeo mabaya ya jeuri. Badala yake, insha hiyo inasema, “jeuri ilionyeshwa tu kuwa tendo la haki, la kiasili, na lisiloepukika—njia rahisi zaidi ya kutatua tatizo.”

Je, unaona uhitaji wa kufanya marekebisho kuhusu utazamaji wa televisheni nyumbani mwako? Usiruhusu burudani za vyombo vya habari zidhoofishe jitihada zako za kuwafundisha watoto wako wawe wenye kufanya amani.

[Picha katika ukurasa wa 17]

Sitawisha ndani ya watoto wako tamaa ya kumpendeza “Mungu wa amani”

[Picha katika ukurasa wa 18]

Tumia wakati kurekebisha usemi na matendo yenye kuumiza

[Picha katika ukurasa wa 19]

Watoto wako wanapaswa kujifunza kuomba msamaha na kusamehe