Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Watu Wanaunganishwa Ulimwenguni—Jinsi Gani?

Watu Wanaunganishwa Ulimwenguni—Jinsi Gani?

Watu Wanaunganishwa Ulimwenguni—Jinsi Gani?

“UMOJA” ni nini? Watu fulani wanafikiri kwamba neno hilo linamaanisha tu kutokuwepo kwa uadui au mapambano. Kwa mfano, ikiwa mataifa mawili au zaidi yanatia sahihi mkataba na yanakubaliana kudumisha amani, inaweza kusemwa kwamba yana umoja. Lakini je, hivyo ndivyo ilivyo? Si lazima iwe hivyo.

Fikiria hili: Katika historia yote, watu wamefanya na kuvunja maelfu ya mikataba ya amani. Kwa nini? Mara nyingi, ni kwa sababu viongozi wa ulimwengu wanahangaikia zaidi mamlaka yao kuliko kuhangaikia amani au umoja. Pia, mataifa mengine yanaogopa kile ambacho kinaweza kutukia ikiwa hayatakuwa na uwezo wa kijeshi kama mataifa mengine.

Hivyo, uhakika wa kwamba mataifa mawili hayako vitani haumaanishi kwamba yana umoja na amani. Je, kweli inaweza kusemwa kwamba wanaume wawili ambao wanaelekezeana bastola wana amani eti kwa sababu tu hawafyatuliani risasi? Wazo hilo halipatani na akili hata kidogo! Hata hivyo, mataifa mengi leo yamo katika hali hiyo. Kwa sababu ya kutoaminiana ambako kunazidi kuongezeka kuna hofu kwamba siku moja silaha zitatumiwa. Ni jitihada gani ambazo zimefanywa ili kuzuia msiba kama huo?

Woga wa Silaha za Nyuklia Unatisha Umoja

Watu wengi wanatumaini Mkataba wa Kuzuia Kuenea kwa Silaha za Nyuklia. Mkataba huo ulioidhinishwa mwaka wa 1968, unakataza nchi ambazo hazina silaha za nyuklia zisitengeneze silaha hizo na unazuia nchi zenye silaha hizo zisiziongeze. Kusudi la Mkataba huo, ambao umekubaliwa na zaidi ya mataifa 180, ni kumaliza kabisa silaha.

Hata kusudi hilo likisikika kuwa zuri kadiri gani, wachambuzi wengine wana maoni kwamba Mkataba huo unajaribu tu kuzuia nchi fulani zisiingie katika kikundi cha “nchi zilizo na silaha za nyuklia,” yaani, unazuia mataifa ambayo hayana silaha hizo yasizitengeneze. Hivyo, watu wanaogopa kwamba mataifa fulani ambayo yalitia sahihi mkataba huo huenda yakafikiria upya msimamo wao. Kwa kweli, mataifa fulani yanaona kwamba si haki hata kidogo yazuiwe kutengeneza silaha ambazo kulingana na maoni yao zitawawezesha kujilinda.

Kile kinachofanya jambo hilo liwe gumu hata zaidi, na labda hata liwe hatari zaidi, ni uhakika wa kwamba hakuna taifa ambalo linakatazwa kuzalisha nguvu za umeme kutokana na nyuklia. Hilo limefanya wengine waogope kwamba huenda mataifa yanayotumia nguvu za nyuklia kwa makusudi ya amani yakatengeneza silaha za nyuklia kisiri.

Hata mataifa ambayo tayari yana silaha za nyuklia huenda yakapuuza Mkataba huo. Wachambuzi wanasema kwamba lingekuwa jambo la upumbavu kutazamia mataifa yenye silaha nyingi yaharibu au hata yapunguze rundo lao la silaha. Kulingana na uchunguzi fulani, ‘ili kutimiza hilo ni lazima mataifa yanayozozana yawe na uhusiano mzuri na yaaminiane na ni vigumu kuamini kwamba hilo linaweza kutukia.’

Jitihada za wanadamu za kupata umoja, hata ziwe za unyoofu kadiri gani, zimeshindwa. Hilo haliwashangazi wanafunzi wa Biblia, kwa kuwa Neno la Mungu linasema: “Mwanadamu anayetembea hana uwezo wa kuongoza hatua yake.” (Yeremia 10:23) Pia, Biblia inasema waziwazi hivi: “Kuna njia ambayo imenyooka mbele ya mwanadamu, lakini njia za kifo ndizo mwisho wake baadaye.” (Methali 16:25) Jitihada za serikali za wanadamu za kupata umoja zina mipaka. Hata hivyo, tuna tumaini.

Chanzo cha Umoja wa Kweli

Biblia ina ahadi ya Mungu ya kwamba ulimwengu utaunganishwa lakini si kwa jitihada za wanadamu. Muumba ambaye alikusudia wanadamu waishi kwa amani ulimwenguni pote ndiye atakayetimiza kile ambacho wanadamu hawawezi. Huenda wengine wakaona vigumu kuamini hilo. Hata hivyo, tangu mwanzo Mungu alikusudia wanadamu waishi kwa amani na upatano. * Maandiko mengi katika Biblia yanathibitisha kwamba bado Mungu anakusudia wanadamu waishi kwa umoja. Fikiria tu mifano michache:

• “Njooni, tazameni matendo ya Yehova, jinsi ambavyo ameweka matukio ya kushangaza duniani. Anakomesha vita mpaka kwenye mwisho wa dunia. Upinde anauvunja na kuukata mkuki vipande-vipande; magari ya kukokotwa anayateketeza motoni.”—ZABURI 46:8, 9.

• “Hawatasababisha madhara yoyote wala kusababisha uharibifu wowote katika mlima wangu wote mtakatifu; kwa maana dunia hakika itajawa na kumjua Yehova kama vile maji yanavyoifunika bahari.”—ISAYA 11:9.

• “Yeye kwa kweli atameza kifo milele, na Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova hakika atafuta machozi katika nyuso zote. Na shutuma ya watu wake ataiondoa katika dunia yote, kwa maana Yehova mwenyewe amesema hayo.”—ISAYA 25:8.

• “Kulingana na ahadi yake tunangojea mbingu mpya na dunia mpya, na humo uadilifu utakaa.”—2 PETRO 3:13.

• “[Mungu] atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.”—UFUNUO 21:4.

Ahadi hizo zinategemeka. Kwa nini? Kwa sababu akiwa Muumba, Yehova Mungu ana nguvu na uwezo wa kuwaunganisha wanadamu. (Luka 18:27) Pia, anatamani kufanya hivyo. Kwa kweli, Biblia inaita tamaa hiyo ‘upendezi wake mwema, yaani, kukusanya tena pamoja vitu vyote katika Kristo, vitu vilivyo mbinguni na vitu vilivyo duniani.’—Waefeso 1:8-10.

Ahadi ya Mungu ya “dunia mpya” ambamo “uadilifu utakaa” si ndoto tu. (2 Petro 3:13) Kuhusu ahadi yake, Yehova Mungu anasema hivi: “Halitarudi kwangu bila matokeo, bali hakika litatenda yale ambayo yamenipendeza, na hakika litafanikiwa katika yale ambayo nimelituma.”—Isaya 55:11.

Wanaunganishwa na Neno la Mungu

Kama ilivyotajwa katika habari iliyotangulia, mara nyingi dini imewatenganisha watu badala ya kuwaunganisha. Hilo ni jambo linalostahili kuchunguzwa kwa uzito, kwa kuwa ikiwa tunakubali kwamba kuna Muumba, je, si jambo linalopatana na akili kutazamia kwamba wale wanaomwabudu wawe na amani na umoja kati yao? Bila shaka!

Migawanyiko kati ya wanadamu ambayo inasababishwa na dini haiungwi mkono na Yehova Mungu na Neno lake. Badala yake, inafunua dini ambazo zinaunga mkono mipango ya wanadamu badala ya kutegemeza kusudi la Mungu. Yesu aliwaita viongozi wa kidini wa wakati wake “wanafiki” na aliwaambia hivi: “Isaya kwa kufaa alitoa unabii juu yenu, aliposema, ‘Watu hawa huniheshimu kwa midomo yao, bali moyo wao umepelekwa mbali nami. Wao huniabudu bure, kwa sababu wao hufundisha amri za wanadamu kuwa mafundisho.’”—Mathayo 15:7-9.

Kinyume na hilo, ibada ya kweli inawaunganisha watu. Nabii Isaya alitabiri hivi: “Itatukia katika siku za mwisho kwamba mlima wa nyumba ya Yehova utawekwa imara juu ya kilele cha milima, nao utainuliwa juu ya vilima; na mataifa yote yatamiminika huko. Naye hakika atafanya hukumu kati ya mataifa na kunyoosha mambo kuhusu vikundi vingi vya watu. Nao watafua panga zao ziwe majembe na mikuki yao iwe miundu. Taifa halitainua upanga juu ya taifa, wala hawatajifunza vita tena.”—Isaya 2:2, 4.

Leo katika nchi zaidi ya 230, Mashahidi wa Yehova wanafuata mafundisho yanayotolewa na Yehova Mungu kuhusu njia za kupata umoja. Ni nini msingi wa umoja wao? Mtume Paulo aliandika hivi: “Jivikeni upendo, kwa maana huo ni kifungo kikamilifu cha muungano.” (Wakolosai 3:14) Neno la awali ambalo Paulo alitumia linalotafsiriwa “kifungo” linaweza kurejelea misuli ya mwili wa mwanadamu. Misuli hiyo ni yenye nguvu kama kamba, na inatimiza kazi mbili muhimu. Inashikilia viungo vya mwili, na inaunganisha mifupa.

Ndivyo ulivyo upendo. Sifa hiyo inatimiza mengi zaidi kuliko tu kuwazuia watu wasiuane. Upendo kama wa Kristo unawafanya watu wa malezi mbalimbali washirikiane kwa amani. Kwa mfano, unawawezesha watu kuishi kulingana na ile kanuni ya Yesu inayojulikana sana kwenye Mathayo 7:12. Yesu Kristo alisema hivi: “Kwa hiyo, mambo yote mnayotaka watu wawatendee ninyi, lazima mwatendee wao pia vivyo hivyo.” Kufuata mwongozo huo kumewasaidia watu wengi washinde ubaguzi.

“Upendo Kati Yenu Wenyewe”

Mashahidi wa Yehova wameazimia kujithibitisha kuwa wanafunzi wa Kristo kwa kufuata yale ambayo Yesu alisema: “Wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo kati yenu wenyewe.” (Yohana 13:35) Upendo huo umeonyeshwa kwa njia kubwa wakati wa misukosuko ya kikabila na kisiasa. Kwa mfano, wakati wa maangamizi ya jamii nzima-nzima ya mwaka 1994 nchini Rwanda, Mashahidi wa Yehova walionyeshana upendo. Mashahidi Wahutu walihatarisha uhai wao ili kulinda ndugu zao Watutsi!

Bila shaka, si jambo la akili kutazamia mataifa ya ulimwengu yakuze upendo wa jirani kwa kadiri itakayoleta umoja ulimwenguni. Kulingana na Biblia, Mungu atatimiza jambo hilo kwa wakati wake. Lakini, hata sasa, watu wanaweza kujivika upendo na hivyo kuishi kwa umoja.

Mwaka uliopita, Mashahidi wa Yehova walitumia saa zaidi ya bilioni moja wakiwatembelea watu na kuzungumza nao kuhusu Biblia na umuhimu wake katika maisha ya leo. Ujuzi sahihi wa Neno la Mungu umeunganisha mamilioni ya watu, ambao wengine wao walichukiana hapo zamani. Watu hao wanatia ndani Waarabu na Wayahudi, Waarmenia na Waturuki, Wajerumani na Warusi, na wengineo.

Je, ungependa kujifunza zaidi kuhusu jinsi Neno la Mungu, Biblia, linavyowaunganisha watu? Ikiwa ndivyo, tafadhali wasiliana na Mashahidi wa Yehova wa eneo lenu, au tumia anwani inayofaa kati ya zile zilizoorodheshwa kwenye ukurasa wa 2.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 12 Kwa habari zaidi kuhusu kusudi la Mungu kwa ajili ya wanadamu, ona sura ya 3 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Blabu katika ukurasa wa 4]

Maelfu ya mikataba ya amani imefanywa na kuvunjwa

[Blabu katika ukurasa wa 7]

Kutumia kanuni za Biblia kumetimiza yale ambayo serikali za wanadamu haziwezi kutimiza

[Picha katika ukurasa wa 5]

Neno la Mungu linaonyesha Chanzo cha umoja wa kweli

[Picha katika ukurasa wa 7]

Mashahidi wa Yehova Wahutu na Watutsi wanashirikiana kujenga mahali pa ibada