Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Hakuna Silaha Itakayofanywa Juu Yako Itakayofanikiwa

Hakuna Silaha Itakayofanywa Juu Yako Itakayofanikiwa

Hakuna Silaha Itakayofanywa Juu Yako Itakayofanikiwa

“Silaha yoyote itakayofanywa juu yako haitafanikiwa.”—ISAYA 54:17.

1, 2. Mambo yaliyowapata Mashahidi wa Yehova wa Albania yanaonyesha jinsi gani ukweli wa Isaya 54:17?

MIAKA mingi iliyopita, katika nchi ndogo yenye milima huko kusini-mashariki mwa Ulaya, kulikuwa na kikundi kisichoogopa cha Wakristo. Serikali moja ya Kikomunisti isiyoamini kuwako kwa Mungu, ilijitahidi juu chini ili kuwakomesha. Hata hivyo, mateso, kambi za kazi ngumu, na propaganda za uwongo hazikuwakomesha. Ni nani hao? Ni Mashahidi wa Yehova wa Albania. Ingawa ilikuwa vigumu sana kukutana pamoja na kuhubiri, uvumilivu wao wa miaka mingi umefanya Ukristo utukuzwe na kuheshimiwa nao umeliletea sifa jina la Yehova. Mwaka jana wakati wa kuwekwa wakfu kwa majengo mapya ya ofisi yao ya tawi, Shahidi mmoja ambaye amekuwa mwaminifu kwa miaka mingi alisema hivi: “Hata Shetani ajitahidi kadiri gani, anaendelea kushindwa naye Yehova anaendelea kushinda!”

2 Mifano yote hiyo inathibitisha ukweli wa ahadi ya Mungu kwa watu wake kwenye Isaya 54:17: “Silaha yoyote itakayofanywa juu yako haitafanikiwa, na ulimi wowote utakaoinuka juu yako katika hukumu wewe utauhukumu.” Historia inathibitisha kwamba hakuna jambo lolote ambalo ulimwengu wa Shetani unaweza kufanya litakalofanikiwa kuzuia ibada ambayo watumishi wa Yehova Mungu waliojiweka wakfu wanamtolea.

Jitihada za Shetani Hazitafanikiwa

3, 4. (a) Silaha za Shetani zinatia ndani nini? (b) Ni katika njia gani silaha za Ibilisi zimeshindwa kufanikiwa?

3 Silaha ambazo zimetumiwa kuwashambulia waabudu wa kweli zimetia ndani marufuku, watu wenye jeuri, magereza, na ‘kutunga matatizo kwa sheria.’ (Zaburi 94:20) Kwa kweli, katika nchi fulani, hata sasa Mashahidi wa Yehova wanapojifunza habari hii, Wakristo hao wa kweli ‘wanajaribiwa’ kuhusiana na utimilifu wao kwa Mungu.—Ufunuo 2:10.

4 Kwa mfano, ofisi moja ya tawi ya Mashahidi wa Yehova iliripoti kwamba katika mwaka mmoja tu, kulikuwa na visa 32 ambavyo watumishi wa Mungu walishambuliwa kimwili walipokuwa wakihubiri. Zaidi ya hilo, kulikuwa na visa 59 vya Mashahidi ambao walikamatwa na polisi walipokuwa wakihubiri hadharani. Mashahidi hao walitia ndani vijana kwa wazee, wanaume kwa wanawake. Wengine walichukuliwa alama za vidole, wakapigwa picha, na kutiwa gerezani kama wahalifu. Wengine walitishwa kwamba wangeumizwa kimwili. Katika nchi nyingine, visa zaidi ya 1,100 vya Mashahidi wa Yehova waliofungwa, kutozwa faini, au kupigwa vimeripotiwa. Zaidi ya visa 200 kati ya hivyo vilitokea siku ambayo Mashahidi walikuwa wamekusanyika ili kuadhimisha kifo cha Yesu! Hata hivyo, roho ya Yehova imewawezesha watu wake waendelee kuishi hata wanapokabili matatizo makubwa, katika nchi hizo na pia katika nchi nyingine. (Zekaria 4:6) Hasira kali ya adui haitawanyamazisha wale wanaomsifu Yehova. Ndiyo, tunaweza kuwa na hakika kwamba hakuna silaha ambayo inaweza kuzuia kusudi la Mungu lisitimizwe.

Ndimi za Uwongo Zahukumiwa

5. Ni ndimi gani za uwongo zilizojitokeza kuwapinga watumishi wa Yehova katika karne ya kwanza?

5 Isaya alitabiri kwamba watu wa Mungu wangehukumu ulimi wowote ambao ungejitokeza ili kuwapinga. Katika karne ya kwanza, mara nyingi habari za uwongo zilienezwa juu ya Wakristo, wakidaiwa kuwa watenda-maovu. Maneno ya Matendo 16:20, 21 yanaonyesha shutuma kama hizo: “Watu hawa wanasumbua sana jiji letu, . . . nao wanatangaza desturi ambazo si halali kwetu kuzikubali au kuzitenda, kwa kuwa sisi ni Waroma.” Pindi nyingine, wapinzani wa kidini walijaribu kuwachochea watawala wa jiji wawachukulie hatua wafuasi wa Kristo, wakisema: “Watu hawa ambao wameipindua dunia inayokaliwa wapo hapa pia, . . . wanapingana na maagizo ya Kaisari.” (Matendo 17:6, 7) Mtume Paulo aliitwa “mtu msumbufu” na kiongozi wa madhehebu ambayo yalikuwa yakichochea uasi “katika dunia yote inayokaliwa.”—Matendo 24:2-5.

6, 7. Ni njia gani moja ambayo kupitia hiyo Wakristo wa kweli wanahukumu mashambulizi ya maneno juu yao?

6 Kwa sababu hiyo, haitushangazi kwamba habari nyingi za uwongo zimeenezwa kuhusu Wakristo wa kweli leo, kutia ndani uchongezi mbaya sana, na propaganda za kuwaharibia sifa. Tunahukumu mashambulizi hayo ya maneno kwa njia gani?—Isaya 54:17.

7 Mara nyingi, mwenendo mzuri wa Mashahidi wa Yehova unafunua kwamba shutuma na propaganda hizo ni za uwongo. (1 Petro 2:12) Wakristo wanapojithibitisha kuwa raia wanaotii sheria, wanaofuata maadili, na wanaowahangaikia kikweli wanadamu wenzao, shutuma hizo zinafunuliwa kuwa za uwongo. Mwenendo wetu mzuri unathibitisha kwamba sisi ni wanyoofu. Mara nyingi, watu wanapoona tukiendelea kutenda yaliyo mema, wanachochewa kumtukuza Baba yetu wa mbinguni na kukubali kwamba watumishi wake wana njia bora zaidi ya maisha.—Isaya 60:14; Mathayo 5:14-16.

8. (a) Huenda tukalazimika kufanya nini nyakati nyingine ili kutetea msimamo wetu unaotegemea Maandiko? (b) Kwa kumwiga Kristo, tunahukumu jinsi gani ndimi zinazotupinga?

8 Zaidi ya mwenendo wetu wa Kikristo, huenda nyakati nyingine tukalazimika kutetea kwa ujasiri msimamo wetu unaotegemea Maandiko. Njia moja ni kuomba ulinzi wa serikali na mahakama. (Esta 8:3; Matendo 22:25-29; 25:10-12) Yesu alipokuwa duniani, pindi moja alibishana waziwazi na wapinzani wake, huku akipinga mashtaka yao ya uwongo. (Mathayo 12:34-37; 15:1-11) Tunamwiga Yesu kwa kutumia nafasi tunazopata kuwaeleza wengine waziwazi juu ya usadikisho wetu wa moyoni. (1 Petro 3:15) Tusiruhusu kamwe dhihaka shuleni, kazini, au kutoka kwa watu wa ukoo wasio waamini zituzuie kutangaza kweli ya Neno la Mungu.—2 Petro 3:3, 4.

Yerusalemu—“Jiwe Lenye Kulemea”

9. Ni Yerusalemu gani linalofananishwa na “jiwe lenye kulemea” linalotajwa kwenye Zekaria 12:3, na ni nani wanaoliwakilisha duniani?

9 Unabii wa Zekaria unafunua kwa nini mataifa yanawapinga Wakristo wa kweli. Ona jinsi andiko la Zekaria 12:3 linavyosema: “Itatukia katika siku hiyo kwamba nitafanya Yerusalemu kuwa jiwe lenye kulemea vikundi vyote vya watu.” Unabii huo unazungumza kuhusu Yerusalemu gani? Unabii wa Zekaria juu ya Yerusalemu unahusu “Yerusalemu la mbinguni,” Ufalme wa mbinguni ambao Wakristo watiwa-mafuta wameitiwa. (Waebrania 12:22) Mabaki wachache wa warithi hao wa Ufalme wa Kimasihi wangali duniani. Pamoja na waandamani wao, “kondoo wengine,” wanawahimiza watu waukubali Ufalme wa Mungu kungali na wakati. (Yohana 10:16; Ufunuo 11:15) Mataifa yameitikia jinsi gani mwaliko huo? Yehova anawapa waabudu wa kweli leo msaada gani? Acheni tuone tunapochunguza kwa undani zaidi maana ya Zekaria sura ya 12. Tukifanya hivyo, tunaweza kuhakikishiwa kwamba ‘hakuna silaha itakayofanikiwa’ juu ya watiwa-mafuta wa Mungu na washiriki wenzao waliojiweka wakfu.

10. (a) Kwa nini watu wa Mungu wanashambuliwa? (b) Ni nini kimewapata wale wanaojaribu kuliinua “jiwe lenye kulemea”?

10 Andiko la Zekaria 12:3 linaonyesha kwamba mataifa yanapata “mikwaruzo mikali.” Hilo linatokea jinsi gani? Mungu ameagiza kwamba lazima habari njema ya Ufalme ihubiriwe. Mashahidi wa Yehova wanachukua kwa uzito wajibu wa kuhubiri. Hata hivyo, kutangazwa kwa Ufalme kuwa tumaini pekee la wanadamu kumekuwa “jiwe lenye kulemea” kwa mataifa. Yanajaribu kuikomesha kabisa kazi hiyo kwa kuwazuia wahubiri wa Ufalme. Kwa kufanya hivyo, mataifa hayo ‘yamejitia mikwaruzo mikali,’ yakijikata-kata yenyewe kila mahali. Hata yamepata aibu yanaposhindwa kwa njia inayofedhehesha. Hayawezi kuwanyamazisha waabudu wa kweli, ambao wanalithamini pendeleo la kuhubiri “habari njema ya milele” ya Ufalme wa Kimasihi wa Mungu kabla ya mwisho wa mfumo huu wa mambo. (Ufunuo 14:6) Alipoona watumishi wa Yehova wakitendewa jeuri, mlinzi mmoja wa gereza katika nchi moja ya Kiafrika alisema hivi: ‘Mnajisumbua bure kuwatesa watu hawa. Hawawezi kamwe kulegeza msimamo wao. Wanazidi tu kuongezeka.’

11. Mungu ametimiza jinsi gani ahadi aliyotoa katika Zekaria 12:4?

11 Soma Zekaria 12:4. Yehova anaahidi kwamba kwa njia ya mfano atawapofusha na kuwatia “wazimu” wale wanaowapinga wajumbe wake wa Ufalme wenye ujasiri. Ametimiza neno lake. Kwa mfano, katika nchi moja ambako ibada ya kweli ilikuwa imepigwa marufuku, wapinzani walishindwa kuwazuia watu wa Mungu wasipate chakula cha kiroho. Hata gazeti moja lilidai kwamba Mashahidi wa Yehova walikuwa wakitumia baluni (ballons) ili kuingiza vichapo vya Biblia nchini. Ahadi ya Mungu kwa watumishi wake washikamanifu imethibitika kuwa ya kweli: “Nitafungua macho yangu . . . nami nitampofusha kila farasi wa vikundi vya watu.” Wakiwa wamepofushwa na hasira, maadui wa Ufalme hawajui waelekee wapi. Hata hivyo, tuna hakika kwamba Yehova atawalinda na kuwatunza watu wake wakiwa kikundi.—2 Wafalme 6:15-19.

12. (a) Yesu aliwasha moto alipokuwa duniani katika maana gani? (b) Mabaki ya watiwa-mafuta wamewasha jinsi gani moto kwa njia ya kiroho, na matokeo yamekuwa nini?

12 Soma Zekaria 12:5, 6“Mashehe wa Yuda” wanafananisha waangalizi kati ya watu wa Mungu. Yehova anawachochea waangalizi hao watiwa mafuta kuwa na bidii nyingi ya kutetea mambo yanayohusu Ufalme wake duniani. Pindi moja, Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Nilikuja kuwasha moto juu ya dunia.” (Luka 12:49) Kwa kweli, aliwasha moto. Kwa kuhubiri kwa bidii, Yesu alifanya watu watambue kwamba Ufalme wa Mungu ndilo jambo kuu zaidi. Hilo lilitokeza ubishi mkali katika taifa hilo la Wayahudi. (Mathayo 4:17, 25; 10:5-7, 17-20) Vivyo hivyo, “kama chombo cha moto kati ya miti na kama mwenge wenye moto katika fungu la nafaka iliyokatwa hivi karibuni,” leo wale wanaofuata hatua za Kristo wanawasha moto kwa njia ya kiroho. Kitabu The Finished Mystery * kilichochapishwa mwaka wa 1917, kilifunua waziwazi unafiki wa dini zinazodai kuwa za Kikristo. Hilo liliwakasirisha sana makasisi. Hivi karibuni, trakti Habari za Ufalme Na. 37, yenye kichwa “Mwisho wa Dini ya Uwongo Unakaribia!” imewachochea wengi wachukue hatua ya kusimama upande wa Ufalme wa Mungu au waupinge.

“Mahema ya Yuda” Yanaokolewa

13. Maneno “mahema ya Yuda” yanaonyesha nini, na kwa nini Yehova anawaokoa wale wanaoshambuliwa?

13 Soma Zekaria 12:7, 8. Katika Israeli la kale, mahema yalikuwa ya kawaida sana nchini, kwa kuwa yalitumiwa mara kwa mara na wachungaji na wakulima. Watu hao wangekuwa wa kwanza kushambuliwa na wangehitaji ulinzi ikiwa maadui wa taifa lingine wangeshambulia jiji la Yerusalemu. Maneno “mahema ya Yuda” yanaonyesha kwamba, katika maana ya mfano, mabaki ya watiwa-mafuta wakati wetu wako katika eneo lililo wazi na lisilo na ulinzi, wala si katika majiji yenye ngome. Wakiwa katika eneo hilo wanatetea bila woga mambo yanayohusu Ufalme wa Kimasihi. Yehova wa majeshi atayaokoa “mahema ya Yuda kwanza” kwa sababu mahema hayo ndiyo shabaha ya shambulizi la Shetani.

14. Yehova anawalinda jinsi gani wale walio katika “mahema ya Yuda” na kuwazuia wasijikwae?

14 Kwa kweli, historia inathibitisha kwamba Yehova anawalinda mabalozi hao watiwa-mafuta wa Ufalme wakiwa katika “mahema” yao yaliyo katika eneo lililo wazi. * Anawazuia ‘wasijikwae’ katika maana ya kwamba anawatia nguvu na kuwafanya wawe jasiri kama Daudi, mfalme shujaa wa vita.

15. Kwa nini Yehova ‘anatafuta kuyaangamiza mataifa yote,’ na atafanya hilo wakati gani?

15 Soma Zekaria 12:9. Kwa nini Yehova ‘anatafuta kuyaangamiza mataifa yote’? Kwa sababu yanaendelea kuupinga Ufalme wa Kimasihi. Mataifa hayo yanahukumiwa kwa sababu yanawanyanyasa na kuwatesa watu wa Mungu. Hivi karibuni, wawakilishi wa Shetani duniani watawashambulia kwa mara ya mwisho waabudu wa kweli wa Mungu, jambo ambalo litaongoza kwenye hali ya ulimwengu ambayo Biblia inaita Har–Magedoni. (Ufunuo 16:13-16) Akijibu shambulio hilo, Mwamuzi Mkuu Kuliko Wote atawalinda watumishi wake na kulitakasa jina lake kati ya mataifa.—Ezekieli 38:14-18, 22, 23.

16, 17. (a) Ni nini “fungu la urithi la watumishi wa Yehova”? (b) Uvumilivu wetu tunaposhambuliwa na Shetani unathibitisha nini?

16 Shetani hana silaha ambayo inaweza kudhoofisha imani au kuzima bidii ya watu wa Mungu ulimwenguni pote. Amani yetu ya kiroho, ambayo inatokana na kujua kwamba Yehova ana nguvu za kuokoa, ndilo “fungu la urithi la watumishi wa Yehova.” (Isaya 54:17) Hakuna mtu anayeweza kutunyang’anya amani na ufanisi wetu wa kiroho. (Zaburi 118:6) Shetani ataendelea kuchochea upinzani na kujaribu kutokeza mateso. Uvumilivu wetu mshikamanifu tunaposhutumiwa unathibitisha kwamba roho ya Mungu iko juu yetu. (1 Petro 4:14) Habari njema ya kusimamishwa kwa Ufalme wa Yehova inahubiriwa ulimwenguni pote. Kama silaha zinazomgonga mtu na kumpumbaza, ndivyo watu wa Mungu wamerushiwa ‘mawe mengi ya kombeo’ ya mfano ya upinzani. Hata hivyo, kwa uwezo wa Yehova watumishi wake wanashinda upinzani huo ulio kama mawe na kuufanya usiwe na matokeo. (Zekaria 9:15) Mabaki watiwa-mafuta na waandamani wao washikamanifu hawatanyamazishwa!

17 Tunatazamia kukombolewa kabisa kutokana na mashambulizi ya Ibilisi. Tunafarijiwa kama nini tunapohakikishiwa kwamba ‘silaha yoyote itakayofanywa juu yetu haitafanikiwa, na ulimi wowote utakaoinuka juu yetu katika hukumu sisi tutauhukumu’!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 12 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova lakini hakichapishwi tena.

^ fu. 14 Kwa habari zaidi, ona kitabu Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu, ukurasa wa 675-676, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

Ungetoa Jibu Gani?

• Ni nini kinachoonyesha kwamba silaha za Shetani hazijafanikiwa?

• Yerusalemu la mbinguni limekuwa “jiwe lenye kulemea” jinsi gani?

• Yehova anaokoa “mahema ya Yuda” jinsi gani?

• Tunapokaribia Har–Magedoni, unaweza kuwa na uhakika gani?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 21]

Watu wa Yehova huko Albania waliendelea kuwa waaminifu ingawa walishambuliwa na Shetani

[Picha katika ukurasa wa 23]

Yesu alipinga mashtaka ya uwongo

[Picha katika ukurasa wa 24]

Hakuna silaha itakayofanywa juu ya wale wanaotangaza habari njema itakayofanikiwa