Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Iweni Wenye “Huruma Nyororo”

Iweni Wenye “Huruma Nyororo”

Iweni Wenye “Huruma Nyororo”

HAKUNA wakati mwingine wowote ambapo wanadamu wengi wamehitaji sana kusaidiwa kwa huruma wanapokabili njaa, magonjwa, umaskini, uhalifu, mizozo ya kijamii, na misiba ya asili. Huruma inamaanisha kutambua mateso au taabu ya mtu mwingine, kumsikitikia, na kutamani kumsaidia. Kama miale yenye joto ya jua jangavu inavyofurahisha, huruma inaweza kupunguza maumivu na kumtia moyo mtu aliyevunjika moyo.

Tunaweza kuonyesha huruma kupitia maneno na matendo yetu—kuwajali wengine na kuwa tayari kuwasaidia wanapohitaji msaada. Haifai kuwaonyesha huruma washiriki wa familia yetu tu, marafiki, na watu tunaowafahamu. Tunaweza kuwaonyesha huruma hata watu ambao hatuwajui. “Mkiwapenda wale wanaowapenda ninyi, mna thawabu gani?” aliuliza Yesu Kristo katika Mahubiri ya Mlimani. Mwanamume huyo mwenye huruma alisema hivi pia: “Kwa hiyo, mambo yote mnayotaka watu wawatendee ninyi, lazima mwatendee wao pia vivyo hivyo.”—Mathayo 5:46, 47; 7:12.

Unaweza kusoma maneno hayo katika Maandiko Matakatifu. Wengi wanakubali kwamba Biblia ndiyo inayotoa mwongozo bora kuhusu kuonyesha huruma. Maandiko yanaonyesha tena na tena kwamba tuna wajibu wa kuwasaidia wale wasioweza kujitegemeza kwa sababu yoyote ile. Biblia inaonyesha kwamba Mtungaji wake na Muumba wetu, Yehova Mungu, ndiye mfano bora zaidi wa kuonyesha huruma.

Kwa mfano, tunasoma hivi: “[Mungu] anatetea haki za mayatima na wajane. Anawajali wageni naye huwapa chakula na mavazi.” (Kumbukumbu la Torati 10:18, Contemporary English Version) Yehova Mungu anasemwa kuwa “anayetekeleza hukumu kwa ajili ya waliopunjwa, Yeye anayewapa wenye njaa mkate.” (Zaburi 146:7) Kuhusu wahamiaji walio maskini, Yehova aliagiza hivi: “Yule mkaaji mgeni . . . atakuwa kwenu kama mwenyeji wenu; nawe utampenda kama wewe mwenyewe.”—Mambo ya Walawi 19:34.

Hata hivyo, nyakati nyingine si rahisi kuonyesha huruma. Mtume Paulo aliwaandikia hivi Wakristo huko Kolosai: “Uvueni utu wa zamani pamoja na mazoea yake, na mjivike utu mpya, ambao kupitia ujuzi sahihi unafanywa kuwa mpya kulingana na mfano wa Yule aliyeuumba . . . Kama waliochaguliwa wa Mungu, watakatifu na wapendwa, jivikeni upendo mwororo wenye huruma.”—Wakolosai 3:9, 10, 12.

Hivyo, jitihada zinahitajiwa ili kusitawisha mtazamo wa huruma. Mtazamo huo ni sehemu ya “utu mpya” ambao Wakristo wanapaswa kuvaa. Paulo aliyeishi katika ulimwengu wenye ukatili wa Roma ya kale, aliwatia moyo waamini wenzake wafanye mabadiliko makubwa katika utu wao ili wawe wenye kujali na wenye huruma zaidi.

Nguvu za Huruma

Watu fulani wanawaona wale wenye huruma kuwa dhaifu na wanaoweza kutumiwa vibaya na wengine. Je, maoni hayo ni sahihi?

Sivyo kamwe! Sifa inayomchochea mtu kuonyesha huruma ya kweli ni upendo wenye kina ambao unatokana na Mungu, ambaye ndiye mfano bora zaidi katika kuonyesha upendo mkamilifu. “Mungu ni upendo.” (1 Yohana 4:16) Kwa kufaa, Yehova anaitwa “Baba ya rehema nyororo na Mungu wa faraja yote.” (2 Wakorintho 1:3) Maneno yanayotafsiriwa “rehema nyororo” yanamaanisha hasa “sikitiko, huruma kuelekea wale wanaoteseka.” Kwa kweli, Yehova “ni mwenye fadhili kuwaelekea wasio na shukrani na waovu”!—Luka 6:35.

Muumba wetu anataka sisi pia tuonyeshe sifa zenye fadhili, kama vile huruma. Tunasoma hivi katika Mika 6:8: “Ee mtu wa udongo, yeye amekuambia yaliyo mema. Na Yehova anataka nini kutoka kwako ila kutenda haki na kupenda fadhili na kuwa na kiasi katika kutembea na Mungu wako?” Katika Methali 19:22, tunasoma hivi: “Kinachotamanika katika mtu wa udongo ni fadhili zake zenye upendo.” Vilevile, Mwana wa Mungu, Yesu Kristo, ambaye aliiga kikamilifu utu wa Baba yake, aliwahimiza hivi wanafunzi wake: “Endeleeni kuwa wenye rehema, kama vile Baba yenu alivyo mwenye rehema.” (Luka 6:36) Biblia ya Union Version inasema hivi: “Basi iweni wenye huruma, kama baba yenu alivyo mwenye huruma.”

Kuna sababu nzuri za kuwa wenye huruma, kwa kuwa huruma ina nguvu ya kuleta thawabu kubwa. Mara nyingi tunaona ukweli wa maneno ya Methali 11:17: “Mwanamume mwenye fadhili zenye upendo anaitendea kwa kuipa thawabu nafsi yake mwenyewe.” Tunapomwonyesha huruma mtu aliye na uhitaji, Mungu anaona hilo kuwa tendo la fadhili kumwelekea Yeye. Anajitwika wajibu wa kuwalipa kwa fadhili waabudu wake kwa sababu ya huruma yoyote wanayoonyesha. Akiongozwa na roho, Mfalme Sulemani alisema hivi: “Anayemwonyesha kibali mtu wa hali ya chini anamkopesha Yehova, na Yeye atamlipa matendo yake.” (Methali 19:17) Naye Paulo aliandika hivi: “Mnajua kwamba wema wowote ambao huenda kila mmoja akafanya, Yehova atamlipa huo.”—Waefeso 6:8.

Huruma ina nguvu za kudumisha upatano na inasaidia kutatua migogoro na kutoelewana. Inasaidia kutatua matatizo ya kutoelewana, nayo inafungua njia ya kusamehe. Kutoelewana kunaweza kutokea kwa sababu nyakati nyingine hatuelezi maoni au hisia zetu kwa njia ambayo tungependa, au matendo yetu yanaeleweka vibaya. Inapokuwa hivyo, huruma inasaidia kutatua matatizo na kudumisha amani. Ni rahisi kumsamehe mtu ambaye anajulikana kuwa mwenye huruma. Huruma inatusaidia kutii shauri hili ambalo mtume Paulo aliwapa Wakristo: “Endeleeni kuvumiliana na kusameheana kwa hiari ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika juu ya mwingine.”—Wakolosai 3:13.

Huruma Inaonyeshwa kwa Matendo ya Kuwajali Wengine

Zaidi ya hayo, huruma ina nguvu za kupunguza mateso. Kama tulivyoona, huruma inaonyesha kwamba tunawajali wale walio na taabu, nayo inatufanya tuteseke pamoja na wale wanaoteseka. Huruma inatia ndani kuwa na hisia nyororo kuwaelekea wale walio katika taabu na kuchukua hatua inayofaa ili kuwasaidia.

Wakristo wanamwiga Yesu wanapowajali wengine. Yesu hakuwa na shughuli nyingi asiwasaidie wengine katika njia ya kimwili na ya kiroho. Alipotambua kwamba wengine wana uhitaji, aliwahurumia na kuwasaidia.

Fikiria jinsi Yesu alivyofanya alipouona umati wa watu waliokuwa wamepuuzwa kiroho: “Alipouona umati akawasikitikia, kwa sababu walikuwa wamechunwa ngozi na kutupwa huku na huku kama kondoo wasio na mchungaji.” (Mathayo 9:36) Msomi mmoja wa Biblia anasema kwamba neno linalotafsiriwa hapo kuwa “akawasikitikia” linamaanisha “hisia ya ndani kabisa inayomchochea mtu.” Kwa kweli, inasemekana kuwa neno hilo ndilo neno lenye nguvu zaidi la Kigiriki la kuonyesha hisia za huruma.

Vivyo hivyo, Wakristo wenye huruma hawakawii kuwasaidia wengine kimwili na kiroho. Mtume Petro aliandika hivi: “Ninyi nyote iweni na akili zinazopatana, mkionyesha hisia-mwenzi, mkiwa na upendo wa kindugu, wenye huruma nyororo.” (1 Petro 3:8) Kwa mfano, familia moja ya Kikristo iliyo maskini ilipolazimika kuhamia eneo lingine kwa sababu za kiafya, waamini wenzao katika eneo hilo waliwaruhusu waishi katika nyumba fulani bila kulipa kodi ya nyumba kwa miezi sita. Mume alisema hivi: “Kila siku walikuja kutujulia hali, na maneno yao yenye kutia moyo yalitustarehesha.”

Wakristo wa kweli wanahangaikia mahitaji ya wageni pia. Kwa shangwe wanatumia wakati, nguvu, na mali zao ili kuwatumikia watu wasiowafahamu. Wafanyakazi wa kujitolea waliotajwa katika habari iliyotangulia ambao waliwasaidia watu wasiowafahamu ni Mashahidi wa Yehova.

Mazingira yenye huruma na fadhili zenye upendo yameenea katika kutaniko lote la Kikristo. Wakichochewa na upendo, washiriki wa kutaniko hilo wanapata nguvu za kutumikia. Huenda mayatima na wajane katika kutaniko wakahitaji uwahangaikie na kuwajali kwa sababu ya matatizo mbalimbali ya kibinafsi. Je, unaweza kuwasaidia watu kama hao wapambane na umaskini, ukosefu wa matibabu yanayofaa, ukosefu wa makao, na matatizo mengine ya kibinafsi?

Wafikirie wenzi fulani wa ndoa huko Ugiriki. Mume alipopatwa na ugonjwa wa kiharusi, alipelekwa katika hospitali iliyokuwa mamia ya kilomita kutoka kwao na mke wake alienda pamoja naye. Wenzi hao wangepata mapato yao madogo ikiwa tu shamba lao la machungwa lingevunwa. Lakini kwa kuwa walikuwa hospitalini, ni nani angefanya kazi hiyo? Kutaniko la kwao lilichukua hatua. Washiriki wa kutaniko hilo walivuna na kuuza machungwa hayo, na hivyo kuwaandalia mapato mume na mke huyo na kuwawezesha kuwa na amani ya akili.

Huruma inaweza kuonyeshwa kwa njia nyingi. Kwa mfano, Wakristo wenye huruma wanatambua kwamba nyakati nyingine baadhi ya wale wanaoteseka wanahitaji hasa kutembelewa na kuonyeshwa fadhili na watu watakaowasikiliza kwa huruma, watakaowajali, na kuwafariji kupitia Maandiko.—Waroma 12:15.

Furahia Mazingira Yenye Huruma

Kutaniko la Kikristo la ulimwenguni pote limethibitika kuwa makao ya amani na faraja ambamo huruma na fadhili zinaonyeshwa. Wakristo wa kweli wanatambua kwamba huruma inawavutia watu, lakini ukatili unachukiza. Hivyo, wanapojaribu kumwiga Baba yao wa mbinguni, wanajitahidi kuonyesha “huruma nyororo” katika njia zinazofaa.

Mashahidi wa Yehova wanakukaribisha kwa uchangamfu katika jamii yao ya Kikristo ili ufurahie mazingira yenye huruma na upendo ambamo watu wanawajali wengine. Wana hakika kwamba utavutiwa na kupendezwa na mazingira hayo.—Waroma 15:7.

[Picha katika ukurasa wa 5]

Paulo aliwahimiza Wakristo Wakolosai wajivike upendo mwororo wenye huruma

[Picha katika ukurasa wa 7]

Yesu alipotambua kwamba wengine wana uhitaji, aliwahurumia na kuwasaidia