Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Sikukuu ya Kipagani Inaweza Kugeuzwa Iwe ya Kikristo?

Je, Sikukuu ya Kipagani Inaweza Kugeuzwa Iwe ya Kikristo?

Je, Sikukuu ya Kipagani Inaweza Kugeuzwa Iwe ya Kikristo?

KATIKA majira ya Krismasi ya mwaka wa 2004, kulikuwa na mjadala mkali nchini Italia. Wakufunzi na walimu fulani waliunga mkono wazo la kupunguza sana au kuondoa kabisa desturi za kidini za Krismasi. Waliunga mkono wazo hilo wakifikiria idadi ya wanafunzi ambao si Wakatoliki au Waprotestanti inayozidi kuongezeka. Hata hivyo, wasomi fulani na wataalamu wengine walisisitiza desturi hizo ziendelee kufuatwa na zidumishwe kabisa.

Hata hivyo, mbali na mawazo hayo yenye kupingana, ni nini hasa chanzo cha desturi nyingi za Krismasi? Mjadala huo ulipokuwa ukifikia upeo wake, gazeti la Vatikani (L’Osservatore Romano) lilisema mambo fulani yenye kupendeza.

Gazeti hilo la Kikatoliki lilisema hivi kuhusu tarehe ya kusherehekea Krismasi: “Kulingana na historia, tarehe yenyewe ambayo Yesu alizaliwa haijulikani kwa sababu historia ya Roma, yaani, rekodi ya hesabu ya watu ya wakati huo na pia utafiti uliofanywa katika karne zilizofuata, hauonyeshi waziwazi tarehe hiyo. . . . Desemba 25, ambayo ni maarufu, ilichaguliwa na Kanisa la Roma katika karne ya nne. Katika Roma iliyojaa ibada ya kipagani, tarehe hiyo iliwekwa wakfu kwa mungu Jua . . . Ijapokuwa Ukristo ulikuwa tayari umekubaliwa katika Milki ya Roma kupitia Amri ya Konstantino, hadithi ya mungu Jua, bado iliaminiwa na watu wengi, hasa askari-jeshi. Sherehe zote zilizotajwa hapo juu, ambazo zilifanywa Desemba 25, zilitokana na desturi zilizofuatwa na watu wengi. Kwa hiyo, Kanisa la Roma likapata wazo la kuipa tarehe hiyo umuhimu wa kidini katika Ukristo kwa kuondoa mungu Jua na kuweka mahali pake, Jua la kweli la Haki, Yesu Kristo, kisha kuichagua tarehe hiyo kuwa siku ya kusherehekea kuzaliwa kwake.”

Namna gani mti wa Krismasi, ambao sasa ni mojawapo ya desturi za Kikatoliki?

Makala hiyo ilionyesha kwamba katika nyakati za kale miti mingi ambayo daima ilikuwa kijani kibichi, kama vile “mholi, butcher’s broom, mlaurusi, na matawi ya msonobari au msindano, yalionwa kuwa yana nguvu za kimzungu au za kimatibabu ambazo zingezuia magonjwa.” Makala hiyo iliendelea kusema hivi: “Katika Desemba 24, mkesha wa Krismasi, Adamu na Hawa walikumbukwa kupitia hadithi zinazopendwa sana za Mti wa Paradiso ya kidunia . . . Mti wenyewe ulipaswa kuwa mtofaa, lakini kwa sababu mtofaa haungefaa wakati wa baridi kali, msindano uliwekwa kwenye jukwaa na matofaa kadhaa yakawekwa kwenye matawi yake, au ili kufananisha kuja kwa Ukombozi, mikate ya ushirika mtakatifu ilitayarishwa kutokana na biskuti zilizopondwa-pondwa katika vyombo vya pekee vilivyokuwa na maumbo yaliyokuwa mfano wa kuwapo kwa Yesu wakati wa Ekaristi, na pia peremende na zawadi kwa ajili ya watoto.” Ni nini kilichotukia baada ya kipindi hicho?

Likitaja kwamba desturi ya kutumia mti wa Krismasi ilianzia Ujerumani katika karne ya 16, gazeti moja (L’Osservatore Romano) linasema hivi: “Italia ilikuwa moja ya nchi za mwisho kuukubali mti wa Krismasi, sababu moja ikiwa uvumi ulioenea sana wa kwamba zoea la kutumia miti ya Krismasi ni la Kiprotestanti na hivyo kitanda kidogo cha mtoto [mandhari ya Kuzaliwa kwa Yesu] ndicho kinachopaswa kutumiwa badala ya mti huo.” Papa Paul wa 6 “alianzisha desturi ya kuweka mti mkubwa wa Krismasi [katika St. Peter’s Square, Roma]” karibu na mandhari ya Kuzaliwa kwa Yesu.

Je, unafikiri inafaa viongozi wa kidini wabadili matukio na mifano inayotokana na ibada ya kale ya kipagani na kuifanya kuwa ya Kikristo? Maandiko yanawahimiza hivi Wakristo wa kweli kuhusu hatua inayofaa kuchukuliwa: “Kuna ushirika gani kati ya uadilifu na uasi-sheria? Au nuru ina ushirika gani na giza?”—2 Wakorintho 6:14-17.

[Picha katika ukurasa wa 8, 9]

Mti wa Krismasi (ukurasa wa 8) na mandhari ya Kuzaliwa kwa Kristo huko Vatikani

[Hisani]

© 2003 BiblePlaces.com

[Picha katika ukurasa wa 9]

Mungu jua

[Hisani]

Museum Wiesbaden