Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Uko Tayari Kwa Ajili ya Siku ya Yehova?

Je, Uko Tayari Kwa Ajili ya Siku ya Yehova?

Je, Uko Tayari Kwa Ajili ya Siku ya Yehova?

“Ile siku kuu ya Yehova iko karibu. Iko karibu, nayo inaharakisha sana.” —SEFANIA 1:14.

1-3. (a) Biblia inasema nini kuhusu siku ya Yehova? (b) Tunakabili ‘siku gani ya Yehova’?

SIKU kuu ya Yehova si kipindi cha saa 24. Ni kipindi kirefu cha kutekeleza hukumu ya Mungu juu ya waovu. Watu wasiomwogopa Mungu wana sababu ya kuogopa siku hiyo ya giza, ghadhabu, hasira yenye kuwaka, taabu, na ukiwa. (Isaya 13:9; Amosi 5:18-20; Sefania 1:15) Unabii wa Yoeli unasema hivi: “Ole wake siku ile; kwa sababu siku ya Yehova iko karibu, nayo itakuja kama mporaji kutoka kwa Mweza-Yote!” (Yoeli 1:15) Hata hivyo, katika siku hiyo kuu, Mungu atakuwa Mwokozi wa wale “walio wanyoofu moyoni.”—Zaburi 7:10.

2 Maneno “siku ya Yehova” yanahusu kutekelezwa kwa hukumu ya Mungu katika nyakati mbalimbali. Kwa mfano, “siku ya Yehova” ilikuja juu ya wakaaji wa Yerusalemu Yehova alipotumia Wababiloni kuharibu jiji hilo mwaka wa 607 K.W.K. (Sefania 1:4-7) Kutekelezwa kwa hukumu ya Mungu kama hiyo kulitukia mwaka wa 70 W.K., Mungu alipotumia Waroma kutekeleza hukumu yake juu ya taifa la Wayahudi ambalo lilimkataa Mwana wake. (Danieli 9:24-27; Yohana 19:15) Pia, Biblia inatabiri kuhusu “siku ya Yehova” wakati atakapopiga ‘vita juu ya mataifa yote.’ (Zekaria 14:1-3) Chini ya mwongozo wa roho ya Mungu, mtume Paulo alihusianisha siku hiyo na kuwapo kwa Kristo, ambako kulianza Yesu alipowekwa kuwa Mfalme mbinguni mwaka wa 1914. (2 Wathesalonike 2:1, 2) Siku ya Yehova inapokaribia sana, andiko la mwaka wa 2007 la Mashahidi wa Yehova limefaa kabisa. Andiko hilo la Sefania 1:14 linasema hivi: “Ile siku kuu ya Yehova iko karibu.”

3 Kwa kuwa siku kuu ya Mungu inakaribia, sasa ndio wakati wa kuwa tayari. Unaweza kujitayarisha jinsi gani kwa ajili ya siku hiyo? Je, unahitaji kuchukua hatua fulani za ziada ili kuwa tayari kwa ajili ya siku ya Yehova?

Uwe Tayari

4. Yesu alijitayarisha kwa ajili ya jaribu gani kali?

4 Katika unabii wake kuhusu mwisho wa mfumo wa mambo, Yesu Kristo aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Iweni tayari.” (Mathayo 24:44) Yesu aliposema maneno hayo, yeye mwenyewe alikuwa tayari kwa ajili ya jaribu kali, yaani, kifo chake akiwa dhabihu ya fidia. (Mathayo 20:28) Tunaweza kujifunza nini kutokana na jinsi Yesu alivyojitayarisha?

5, 6. (a) Kumpenda Mungu na watu kunatusaidia jinsi gani kujitayarisha kwa ajili ya siku ya Yehova? (b) Yesu aliweka mfano gani kuhusu kumpenda jirani?

5 Yesu alimpenda Yehova na viwango Vyake vya uadilifu kwa moyo wake wote. Andiko la Waebrania 1:9 linasema hivi kumhusu Yesu: “Uliupenda uadilifu, nawe ukauchukia uasi-sheria. Ndiyo sababu Mungu, Mungu wako, alikutia mafuta kwa mafuta ya kushangilia kuliko wenzako.” Kwa sababu alimpenda Baba yake wa mbinguni, Yesu alidumisha utimilifu wake kwake. Tukiwa na upendo kama huo kwa Mungu na kuishi kulingana na matakwa yake, atatulinda. (Zaburi 31:23) Upendo na utii kama huo utatusaidia kuwa tayari kwa ajili ya siku kuu ya Yehova.

6 Kuwapenda watu kulikuwa sehemu muhimu ya utu wa Yesu. Kwa kweli, ‘aliwasikitikia, kwa sababu walikuwa wamechunwa ngozi na kutupwa huku na huku kama kondoo wasio na mchungaji.’ (Mathayo 9:36) Hivyo, Yesu aliwahubiria watu habari njema, kama vile upendo unavyotuchochea kutangaza ujumbe wa Ufalme kwa majirani wetu. Kumpenda Mungu na jirani kunatusaidia kuendelea kuwa na bidii tukiwa wahudumu Wakristo na hivyo kujitayarisha kwa ajili ya siku kuu ya Yehova.—Mathayo 22:37-39.

7. Kwa nini tunaweza kuwa na shangwe tunapoingojea siku ya Yehova?

7 Yesu alifurahia kufanya mapenzi ya Yehova. (Zaburi 40:8) Tukiwa na mtazamo kama huo, tutapata shangwe katika kumtolea Mungu utumishi mtakatifu. Kama Yesu, tutakuwa watoaji wasio na ubinafsi, na hilo litatuletea furaha ya kweli. (Matendo 20:35) Ndiyo, ‘shangwe ya Yehova ndiyo ngome yetu.’ Tukiwa na shangwe hiyo, tutakuwa tayari zaidi kwa ajili ya siku kuu ya Mungu.—Nehemia 8:10.

8. Kwa nini tunapaswa kuendelea kumkaribia Yehova katika sala?

Sala ya bidii kwa Mungu ilimsaidia Yesu kujitayarisha kwa ajili ya majaribu ya imani. Alikuwa akisali Yohana alipombatiza. Yesu alisali usiku wote kabla ya kuwachagua mitume wake. (Luka 6:12-16) Na ni msomaji gani wa Biblia asiyeguswa moyo na sala za kutoka moyoni ambazo Yesu alitoa usiku wa mwisho wa maisha yake duniani? (Marko 14:32-42; Yohana 17:1-26) Je, unasali mara nyingi kama Yesu alivyofanya? Sali kwa Yehova mara nyingi, usiwe mwenye haraka unaposali, tafuta mwongozo wa roho takatifu, na mwongozo unapotolewa uwe tayari kuukubali. Ni jambo la maana sana kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Baba yetu wa mbinguni wakati huu hatari, wakati ile siku kuu ya Mungu inapokaribia haraka. Hivyo basi, kwa vyovyote vile, endelea kumkaribia Yehova katika sala.—Yakobo 4:8.

9. Kwa nini ni jambo la maana sana kuhangaikia kutakaswa kwa jina la Yehova?

9 Pia, kuhangaikia kutakaswa kwa jina takatifu la Yehova kulimsaidia Yesu kujitayarisha kwa ajili ya majaribu aliyokabili. Kwa kweli, aliwafundisha wafuasi wake kwamba sala zao kwa Mungu zilipaswa kutia ndani ombi hili: “Jina lako na litakaswe.” (Mathayo 6:9) Ikiwa tunatamani sana jina la Yehova litakaswe, au lifanywe kuwa takatifu, tutajitahidi kuepuka kufanya mambo ambayo yataleta suto juu ya jina hilo. Tukifanya hivyo, tutakuwa tayari zaidi kwa ajili ya siku kuu ya Yehova.

Je, Unapaswa Kufanya Mabadiliko Fulani?

10. Kwa nini inafaa tuchunguze maisha yetu?

10 Siku ya Yehova ikija kesho, je, kweli utakuwa tayari kwa ajili yake? Ni vizuri kila mmoja wetu achunguze maisha yake ili aone ikiwa anahitaji kurekebisha matendo au mitazamo fulani. Kwa sababu maisha ni mafupi na hali zinaweza kubadilika wakati wowote, kila mmoja wetu anahitaji kuendelea kuwa macho kiroho kila siku. (Mhubiri 9:11, 12; Yakobo 4:13-15) Hivyo, acheni tuchunguze mambo fulani ambayo huenda yakahitaji uangalifu katika maisha yetu.

11. Una mradi gani wa kusoma Biblia?

11 Jambo moja la maana ni himizo la “mtumwa mwaminifu” la kusoma Biblia kila siku. (Mathayo 24:45) Unaweza kujiwekea mradi wa kusoma na kutafakari Maandiko kila mwaka kuanzia kitabu cha Mwanzo mpaka Ufunuo. Ukisoma sura nne kila siku, unaweza kusoma sura 1,189 za Biblia kwa mwaka mmoja. Kila mfalme wa Israeli alipaswa kusoma Sheria ya Yehova “siku zote za maisha yake.” Inaelekea kwamba Yoshua alifanya jambo kama hilo. (Kumbukumbu la Torati 17:14-20; Yoshua 1:7, 8) Ni jambo la maana kama nini kwa wachungaji wa kiroho kusoma Neno la Mungu kila siku! Kufanya hivyo kunawasaidia kufundisha “fundisho lenye afya.”—Tito 2:1.

12. Kukaribia kwa siku ya Yehova kunapaswa kukuchochea ufanye nini?

12 Kukaribia kwa siku ya Yehova kunapaswa kukuchochea uhudhurie kwa ukawaida mikutano ya Kikristo na kushiriki kikamili iwezekanavyo katika mikutano hiyo. (Waebrania 10:24, 25) Kufanya hivyo kutakusaidia uboreshe ustadi wako ukiwa mhubiri wa Ufalme anayejitahidi kuwatafuta na kuwasaidia wale walio na mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uzima wa milele. (Matendo 13:48) Unaweza kuwa mwenye bidii kutanikoni kwa njia nyingine pia, kama vile kuwasaidia waliozeeka na kuwatia moyo vijana. Jitihada hizo zinaweza kukuletea uradhi kama nini!

Uhusiano Wako Pamoja na Wengine

13. Ni maswali gani tunayoweza kujiuliza kuhusu kuvaa utu mpya?

13 Kwa kuwa siku ya Yehova inakaribia sana, je, unahitaji kutia bidii zaidi ili “kuvaa utu mpya ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu katika uadilifu wa kweli na ushikamanifu”? (Waefeso 4:20-24) Unapositawisha sifa zinazompendeza Mungu, inaelekea wengine wataona kwamba ‘unaendelea kutembea kwa roho ya Mungu’ na kuonyesha matunda yake. (Wagalatia 5:16, 22-25) Je, unaweza kutaja mambo hususa ambayo yanaonyesha kwamba wewe na familia yako mmevaa utu mpya? (Wakolosai 3:9, 10) Kwa mfano, je, unajulikana kwa kuwatendea kwa fadhili waamini wenzako na wengine? (Wagalatia 6:10) Kujifunza Maandiko kwa ukawaida kutakusaidia kusitawisha sifa zinazompendeza Mungu ambazo zitakutayarisha kwa ajili ya siku ya Yehova.

14. Kwa nini mtu anapaswa kusali ili apewe roho takatifu anapojitahidi kusitawisha sifa ya kujizuia?

14 Namna gani ikiwa unakasirika haraka na unatambua kwamba unahitaji kusitawisha zaidi sifa ya kujizuia? Sifa hiyo ni moja ya matunda ambayo roho takatifu ya Mungu inaweza kukuza ndani yako. Kwa hiyo, sali ili upewe roho takatifu, kama Yesu alivyosema: “Endeleeni kuomba, nanyi mtapewa; endeleeni kutafuta, nanyi mtapata; endeleeni kupiga hodi, nanyi mtafunguliwa. . . . Ikiwa ninyi, mjapokuwa waovu, mnajua jinsi ya kuwapa watoto wenu zawadi zilizo njema, je, Baba aliye mbinguni hatawapa hata zaidi roho takatifu wale wanaomwomba!”—Luka 11:9-13.

15. Unapaswa kufanya nini ikiwa uhusiano kati yako na mwamini mwenzako si mzuri?

15 Tuseme kwamba uhusiano kati yako na mwamini mwenzako si mzuri. Unapaswa kujitahidi juu chini ili kuboresha uhusiano wenu, na hivyo kuendeleza amani na umoja wa kutaniko. (Zaburi 133:1-3) Tumia shauri la Yesu kwenye Mathayo 5:23, 24 au Mathayo 18:15-17. Ikiwa umekuwa ukiacha jua litue ukiwa bado katika hali ya kuchokozeka, rekebisha mambo haraka. Mara nyingi jambo linalohitajiwa tu ni kuwa tayari kusamehe. Paulo aliandika hivi: “Iweni wenye fadhili ninyi kwa ninyi, wenye huruma nyororo, mkisameheana kwa hiari kama vile Mungu pia kupitia Kristo alivyowasamehe ninyi kwa hiari.”—Waefeso 4:25, 26, 32.

16. Kwa nini huruma inahitajiwa katika ndoa?

16 Wenzi wa ndoa wanapaswa kuwa na huruma nyororo na nyakati nyingine, kusameheana. Ikiwa unahitaji kuwa mwenye upendo na mwenye huruma zaidi kumwelekea mwenzi wako, jitahidi sana kufikia mradi huo kwa msaada wa Mungu na Neno lake. Je, unahitaji kusitawisha sifa fulani ili uishi kupatana na andiko la 1 Wakorintho 7:1-5 na hivyo kupunguza shida na kuepuka ukosefu wa uaminifu? Hapana shaka kwamba katika maisha ya ndoa mume na mke wanahitaji kuwa “wenye huruma nyororo.”

17. Mtu anapaswa kuchukua hatua gani ikiwa ametenda dhambi nzito?

17 Namna gani ikiwa umetenda dhambi fulani nzito? Chukua hatua za kurekebisha hali haraka iwezekanavyo. Kwa vyovyote vile, tafuta msaada wa wazee Wakristo. Sala na mashauri yao yatakusaidia kuwa tena na afya nzuri ya kiroho. (Yakobo 5:13-16) Sali kwa Yehova ukiwa na mtazamo wa kutubu. Usipofanya hivyo utajihisi ukiwa mwenye hatia na utasumbuliwa na dhamiri. Daudi alihisi hivyo, lakini alipata kitulizo kama nini baada ya kutubu kwa Yehova! Daudi aliandika hivi: “Mwenye furaha ni mtu ambaye amesamehewa maasi yake, ambaye dhambi yake imefunikwa. Mwenye furaha ni mtu ambaye Yehova hamhesabii kosa, na ambaye katika roho yake hamna udanganyifu.” (Zaburi 32:1-5) Yehova anawasamehe wale wanaotenda dhambi lakini ambao wanatubu kikweli.—Zaburi 103:8-14; Methali 28:13.

Dumisha Msimamo wa Kutokuwa Sehemu ya Ulimwengu

18. Unapaswa kuwa na maoni gani kuhusu ulimwengu?

18 Bila shaka, unatazamia ulimwengu mpya mzuri ajabu ambao umeahidiwa na Baba yetu wa mbinguni. Ikiwa ndivyo, una maoni gani kuhusu ulimwengu wa jamii ya wanadamu wasio waadilifu waliotengwa mbali na Mungu? Shetani “mtawala wa ulimwengu,” hakuwa na uwezo juu ya Yesu Kristo. (Yohana 12:31; 14:30) Bila shaka, hutaki Ibilisi na ulimwengu wake uwe na uwezo juu yako. Hivyo, tii maneno haya ya mtume Yohana: “Msiwe mkiupenda ulimwengu au vitu vilivyo katika ulimwengu.” Hiyo ndiyo njia ya hekima, kwa kuwa “ulimwengu unapitilia mbali na pia tamaa yake, lakini yeye anayefanya mapenzi ya Mungu anadumu milele.”—1 Yohana 2:15-17.

19. Vijana Wakristo wanahimizwa kuwa na miradi ya aina gani?

19 Je, unawasaidia watoto wako ‘waendelee kujitunza bila doa kutokana na ulimwengu’? (Yakobo 1:27) Shetani angependa kuwanasa watoto wako kama vile mtu anavyonasa samaki. Vikundi mbalimbali na matengenezo mengine yanakusudiwa kuwafanya vijana wawe sehemu ya ulimwengu wa Shetani. Lakini tayari watumishi wa Yehova ni sehemu ya tengenezo pekee ambalo litaokoka mwisho wa mfumo huu mbovu wa mambo. Hivyo, vijana Wakristo wanapaswa kutiwa moyo wawe na “mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana.” (1 Wakorintho 15:58) Wazazi ambao wanamwogopa Mungu wanahitaji kuwasaidia watoto wao wajiwekee miradi itakayowaletea maisha yenye furaha na yenye kuthawabisha, ambayo yanamletea Mungu heshima na kuwasaidia kuwa tayari kwa ajili ya siku ya Yehova.

Fikiria Maisha Baada ya Siku Kuu ya Yehova

20. Kwa nini tunapaswa kuendelea kuutazamia uzima wa milele?

20 Utaweza kuingojea siku ya Yehova kwa moyo mtulivu ikiwa utaendelea kuutazamia uzima wa milele. (Yuda 20, 21) Unatazamia uzima wa milele katika Paradiso, na hivyo una tumaini la kupata tena nguvu za ujana na wakati usio na kipimo wa kufuatia miradi mizuri na kujifunza mengi zaidi kumhusu Yehova. Kwa kweli, unaweza kuendelea kujifunza milele kumhusu Mungu kwa sababu kwa sasa wanadamu wanajua tu “kingo za njia zake.” (Ayubu 26:14) Ni matarajio yenye kusisimua kama nini!

21, 22. Huenda wewe na watu watakaofufuliwa mtazungumzia mambo gani?

21 Katika Paradiso, wale watakaofufuliwa watatusaidia kujua mambo fulani ya wakati uliopita. Enoko atakuwepo na atatueleza jinsi alivyokuwa na ujasiri uliohitajiwa ili kutangaza ujumbe wa Yehova kwa watu wasiomwogopa Mungu. (Yuda 14, 15) Bila shaka, Noa ataeleza jinsi kazi ya kujenga safina ilivyokuwa. Abrahamu na Sara watatufunulia jinsi walivyohisi wakati walipoacha maisha ya starehe ya Uru na kuishi katika mahema. Fikiria Esta akieleza jinsi alivyowatetea watu wake na kuzuia njama ya Hamani ya kuwaangamiza. (Esta 7:1-6) Fikiria Yona akieleza kuhusu siku zake tatu katika tumbo la samaki mkubwa au Yohana Mbatizaji akieleza jinsi alivyohisi wakati alipombatiza Yesu. (Luka 3:21, 22; 7:28) Itapendeza kama nini kujifunza mambo hayo yote!

22 Wakati wa Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo, huenda ukawa na pendeleo la kuwasaidia watu watakaofufuliwa wapate “kumjua Mungu.” (Methali 2:1-6) Leo, inafurahisha kama nini kuona watu wakijifunza kumhusu Yehova Mungu na kutenda kulingana na mambo wanayojifunza! Lakini fikiria shangwe utakayopata wakati ujao Yehova atakapobariki jitihada zako za kuwafundisha watu walioishi zamani za kale na kuona wakiitikia kwa mioyo yenye shukrani!

23. Tunapaswa kuazimia kufanya nini?

23 Kwa kuwa sisi si wakamilifu hatuwezi kuhesabu au kupima faida tunazopata sasa tukiwa watu wa Yehova. (Zaburi 40:5) Tunamshukuru Mungu hasa kwa maandalizi yake ya kiroho. (Isaya 48:17, 18) Hata hali zetu ziwe namna gani, acheni tutoe utumishi mtakatifu kwa moyo wetu wote huku tukingojea ile siku kuu ya Yehova.

Ungetoa Jibu Gani?

• “Siku ya Yehova” ni nini?

• Unaweza kujitayarisha jinsi gani kwa ajili ya siku ya Yehova?

• Siku kuu ya Mungu inapokaribia sana, huenda tukahitaji kufanya mabadiliko gani?

• Unatazamia nini baada ya siku ya Yehova?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 12]

Yesu alijitayarisha kwa ajili ya majaribu

[Picha katika ukurasa wa 15]

Litakuwa pendeleo kama nini kuwasaidia wale watakaofufuliwa wajifunze kumhusu Yehova!