Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Una Mshauri wa Mambo ya Kiroho?

Je, Una Mshauri wa Mambo ya Kiroho?

Je, Una Mshauri wa Mambo ya Kiroho?

AKIWA na umri wa miaka 16 tu, Uzia aliwekwa kuwa mfalme wa ufalme wa kusini wa Yuda. Alitawala kwa miaka zaidi ya 50, kuanzia mwishoni mwa karne ya tisa mpaka mwanzoni mwa karne ya nane K.W.K. Tangu akiwa na umri mdogo, Uzia ‘aliendelea kufanya yaliyokuwa sawa machoni pa Yehova.’ Ni nini kilichomchochea kuishi maisha ya uadilifu? Masimulizi ya historia yanasema hivi: “[Uzia] akaendelea kuwa na mwelekeo wa kumtafuta Mungu katika siku za Zekaria, aliyekuwa akiwafundisha watu kumwogopa Mungu wa kweli; na katika zile siku alizokuwa akimtafuta Yehova, Mungu wa kweli alimfanikisha.”—2 Mambo ya Nyakati 26:1, 4, 5.

Mbali na masimulizi hayo ya Biblia, hatuna habari zaidi kumhusu Zekaria, aliyekuwa mshauri wa mfalme Uzia. Hata hivyo, ingawa ‘alikuwa akiwafundisha watu kumwogopa Mungu wa kweli,’ Zekaria alikuwa na uvutano mzuri juu ya mtawala huyo kijana na alimchochea kufanya yaliyo sawa. Kitabu kimoja (The Expositor’s Bible) kinasema kwamba bila shaka Zekaria “alikuwa mtu aliyejua mafundisho ya kiroho, mwenye uzoefu mkubwa sana wa kiroho, na aliyeweza kuwapa wengine ujuzi aliokuwa nao.” Msomi mmoja wa Biblia alikata kauli hii kumhusu Zekaria: “Alijua sana unabii, naye . . . alikuwa mtu mwenye akili, mtu mwema aliyejitoa kwa Mungu; na inaonekana kwamba alimchochea sana Uzia.”

Uaminifu wa Uzia ulimletea baraka nyingi, na “alionyesha nguvu kwa kiwango kisicho cha kawaida” kwa sababu ‘Mungu wa kweli aliendelea kumsaidia.’ Ndiyo, mafanikio yake katika mambo ya kimwili yalitegemea mafanikio ya kiroho aliyopata “katika siku za Zekaria.” (2 Mambo ya Nyakati 26:6-8) Baada ya Uzia kufanikiwa, aliacha mafundisho ya Zekaria, mshauri wake. ‘Moyo wa Uzia ukawa na majivuno hata kufikia hatua ya kusababisha uharibifu, hivi kwamba akatenda kwa ukosefu wa uaminifu kwa Yehova.’ Kwa sababu ya kutenda jambo fulani lisilo la heshima, alipigwa na ugonjwa wa ngozi wenye kuchukiza, ambao ulimlemaza, hivi kwamba hangeweza kuendelea kutimiza wajibu wake wote wa kifalme.—2 Mambo ya Nyakati 26:16-21.

Je, una mtu fulani ambaye anaweza kuitwa mwalimu au mshauri anayekuchochea ‘umtafute Yehova’? Unaweza kuwa na mshauri iwe wewe ni kijana au umepita siku za ujana, iwe wewe ni mwanaume au mwanamke. Mthamini mshauri wako kwa kuwa mashauri yake yanaweza kukusaidia uendelee kufanya yaliyo sawa machoni pa Yehova. Msikilize Mkristo huyo mkomavu na uchukue mashauri yake kwa uzito. Usiache kamwe maneno yenye hekima ya mshauri huyo ‘anayekufundisha kumwogopa Mungu wa kweli.’—Methali 1:5; 12:15; 19:20.