Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Malaki

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Malaki

Neno la Yehova Liko Hai

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Malaki

HEKALU la Yerusalemu lililojengwa upya limekuwapo kwa miaka zaidi ya 70. Hata hivyo, hali ya kiroho ya Wayahudi imezidi kuzorota kadiri miaka inavyopita. Hata makuhani wamekuwa wafisadi. Ni nani atakayewajulisha jinsi hali yao ilivyo na kujaribu kuwaamsha kiroho? Yehova anampa nabii Malaki kazi hiyo.

Malaki ameandika ujumbe mzito sana katika kitabu cha mwisho cha Maandiko ya Kiebrania. Kitabu hicho kina unabii ulioongozwa na Mungu. Kukazia uangalifu neno la kinabii la Malaki kunaweza kutusaidia kujitayarisha kwa ajili ya “ile siku ya Yehova iliyo kuu na yenye kuogopesha,” wakati mfumo huu mbovu wa mambo utakapofikia mwisho wake.—Malaki 4:5.

MAKUHANI ‘WAMESABABISHA WENGI WAJIKWAE’

(Malaki 1:1–2:17)

Yehova anaonyesha hisia zake kuelekea Israeli kwa kusema hivi: “Nimewapenda ninyi.” Lakini makuhani wamelidharau jina la Mungu. Kwa njia gani? “Kwa kutoa juu ya madhabahu [yake] mkate uliotiwa unajisi,” na kwa kutoa “mnyama kilema au mgonjwa” kwa ajili ya dhabihu.—Malaki 1:2, 6-8.

Makuhani ‘wamesababisha wengi wajikwae katika sheria.’ Watu ‘wanatendeana kwa hila.’ Wengine wamechukua wake wa kigeni. Na wengine wao wamewatendea hila ‘wake wa ujana wao.’—Malaki 2:8, 10, 11, 14-16.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

2:2—Yehova ‘alizilaani baraka’ za makuhani waasi kwa njia gani? Mungu alizilaani katika maana ya kwamba baraka ambazo makuhani wao waliomba ziligeuka na kuwa laana.

2:3—Makuhani ‘wangepakwa mavi juu ya nyuso zao’ katika maana gani? Kulingana na Sheria, mavi ya mnyama wa dhabihu yalipaswa kupelekwa nje ya kambi na kuteketezwa. (Mambo ya Walawi 16:27) Kupaka mavi juu ya nyuso za makuhani kulimaanisha kwamba Yehova alikataa dhabihu hizo na kwamba wale waliozitoa walimchukiza.

2:13—Madhabahu ya Yehova yalikuwa yamefunikwa kwa machozi ya nani? Yalikuwa machozi ya wake ambao walikuja katika patakatifu pa hekalu na kumimina mioyo yao mbele za Yehova. Ni nini kilichosababisha huzuni yao? Waume wao Wayahudi walikuwa wamewataliki kwa misingi isiyo halali ili waoe wanawake vijana wa kigeni.

Mambo Tunayojifunza:

1:10. Yehova hakufurahia matoleo ya makuhani wenye pupa, ambao walidai malipo hata kwa utumishi mdogo kama vile kufunga milango au kuwasha moto katika madhabahu. Ni jambo la maana kama nini tushiriki katika matendo ya ibada na katika huduma ya Kikristo kwa sababu tunampenda Mungu na jirani bila ubinafsi, wala si kwa sababu tunataka faida ya kifedha!—Mathayo 22:37-39; 2 Wakorintho 11:7.

1:14; 2:17. Yehova havumilii unafiki.

2:7-9. Wale ambao wamepewa pendeleo la kufundisha kutanikoni wanapaswa kuhakikisha kwamba yale wanayofundisha yanapatana na Neno la Mungu, yaani, Maandiko Matakatifu, na pia yanapatana na vichapo vya “msimamizi-nyumba mwaminifu.”—Luka 12:42; Yakobo 3:11.

2:10, 11. Yehova anatarajia waabudu wake wachukue kwa uzito shauri la kuoa “katika Bwana tu.”—1 Wakorintho 7:39.

2:15, 16. Waabudu wa kweli wanapaswa kuheshimu agano la ndoa walilofanya na mke wa ujana wao.

“BWANA WA KWELI ATAKUJA KWENYE HEKALU LAKE”

(Malaki 3:1–4:6)

“Kwa ghafula Bwana wa kweli [Yehova Mungu] atakuja kwenye hekalu Lake,” na “mjumbe wa agano [Yesu Kristo].” Mungu ‘atawakaribia watu wake ili kuwahukumu,’ naye atakuwa shahidi wa haraka juu ya watenda mabaya wote. Zaidi ya hayo, “kitabu cha kumbukumbu” kitaandikwa kwa ajili ya wale wanaomwogopa Yehova.—Malaki 3:1, 3, 5, 16.

Siku ambayo “inawaka kama tanuru” itakuja na kuwateketeza waovu wote. Kabla ya siku hiyo kuja, nabii atatumwa ili ‘kugeuza mioyo ya akina baba irudi kwa wana, na mioyo ya wana irudi kwa akina baba.’—Malaki 4:1, 5, 6.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

3:1-3—“Bwana wa kweli” na “mjumbe wa agano” walikuja kwenye hekalu wakati gani, na ni nani aliyetumwa mbele yao? Yehova alikuja kwenye hekalu lake kupitia mwakilishi wake na kulisafisha mnamo Nisani 10, 33 W.K. Wakati huo, Yesu aliingia katika hekalu na kuwafukuza wale waliokuwa wakinunua na kuuza. (Marko 11:15) Yesu alifanya hivyo miaka mitatu na nusu baada ya kutiwa mafuta na kuwa Mfalme Aliyechaguliwa. Vivyo hivyo, inaonekana kwamba miaka mitatu na nusu baada ya kuwekwa kuwa Mfalme mbinguni, Yesu alienda pamoja na Yehova katika hekalu la kiroho na kupata kwamba watu wa Mungu walihitaji kusafishwa. Katika karne ya kwanza, Yohana Mbatizaji alitumwa ili kuwatayarisha Wayahudi kwa ajili ya kuja kwa Yesu Kristo. Katika nyakati za kisasa, mjumbe alitumwa ili amtayarishie Yehova njia ya kuja kwenye hekalu lake la kiroho. Mapema katika miaka ya 1880, kikundi cha wanafunzi wa Biblia kilianza kufanya kazi ya kutoa elimu ya Biblia na kuwafundisha watu wanyoofu kweli nyingi za msingi za Biblia.

3:10—Je, kuleta “sehemu zote za kumi,” au kutoa zaka, kunamaanisha kwamba tumetoa vitu vyetu vyote kwa Yehova? Sheria ya Musa ilifutiliwa mbali kwa msingi wa kifo cha Yesu, kwa hiyo kutoa pesa si takwa la kumwabudu Mungu leo. Hata hivyo, kutoa sehemu ya kumi kuna maana ya mfano. (Waefeso 2:15) Hakumaanishi tutoe vitu vyetu vyote. Sehemu ya kumi ililetwa kila mwaka, lakini sisi tunamtolea Yehova vitu vyetu vyote mara moja tu, tunapojiweka wakfu kwake na kuonyesha wakfu huo kwa kubatizwa katika maji. Kuanzia wakati huo na kuendelea, kila kitu tulicho nacho kinakuwa cha Yehova. Hata hivyo, bado anaturuhusu tutumie katika utumishi wake sehemu ya vitu tulivyo navyo, yaani, zaka ya mfano. Zaka hiyo ni chochote ambacho moyo wetu unatuchochea kufanya kulingana na hali zetu. Matoleo tunayomtolea Yehova yanatia ndani wakati, nguvu, na mali nyingine zinazotumiwa katika kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme na kufanya wanafunzi. Pia, yanatia ndani kuhudhuria mikutano ya Kikristo, kuwatembelea waamini wenzetu walio wagonjwa na waliozeeka, na kutegemeza ibada ya kweli kwa pesa.

4:3—Waabudu wa Yehova ‘watawakanyagia chini waovu’ jinsi gani? Watu wa Mungu duniani ‘hawatawakanyagia chini waovu’ kihalisi, yaani, hawatashiriki katika kutekeleza hukumu yake juu yao. Badala yake, jambo hilo linadokeza kwamba watumishi wa Yehova walio duniani watafanya hivyo kwa kushiriki kwa moyo wote katika sherehe ya ushindi baada ya ulimwengu wa Shetani kuharibiwa.—Zaburi 145:20; Ufunuo 20:1-3.

4:4—Kwa nini tunapaswa ‘kuikumbuka sheria ya Musa’? Wakristo hawako chini ya Sheria hiyo, hata hivyo, ilikuwa “kivuli cha mambo mema yatakayokuja.” (Waebrania 10:1) Hivyo, kuikazia uangalifu Sheria ya Musa kunaweza kutusaidia kuona jinsi mambo yaliyoandikwa humo yanavyotimia. (Luka 24:44, 45) Kwa kuongezea, Sheria hiyo inataja “mifano ya uhalisi wa vitu vilivyo mbinguni.” Ni lazima tujifunze Biblia ikiwa tunataka kuelewa mafundisho na mwenendo wa Kikristo.—Waebrania 9:23.

4:5, 6—“Nabii Eliya” anafananisha nani? Ilitabiriwa kwamba “Eliya” angefanya kazi ya kurudisha, yaani, kuitayarisha mioyo ya watu. Katika karne ya kwanza W.K., Yesu Kristo alimtambulisha Yohana Mbatizaji kuwa “Eliya.” (Mathayo 11:12-14; Marko 9:11-13) Eliya wa siku hizi anatumwa “kabla ya kuja kwa ile siku ya Yehova iliyo kuu na yenye kuogopesha.” Eliya wa leo si mwingine ila “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mathayo 24:45) Jamii hiyo ya Wakristo watiwa-mafuta imekuwa ikiwasaidia kwa bidii watu wawe na uhusiano mzuri pamoja na Mungu.

Mambo Tunayojifunza:

3:10. Kutompa Yehova matoleo yetu yaliyo bora ni kujinyima baraka zake.

3:14, 15. Kwa sababu ya mfano mbaya wa makuhani, Wayahudi walianza kupuuza utumishi wa Mungu. Wale walio na mapendeleo katika kutaniko la Kikristo wanapaswa kuwa vielelezo vizuri.—1 Petro 5:1-3.

3:16. Yehova anaweka rekodi ya wale wanaomwogopa na walio waaminifu kwake. Anawakumbuka na atawahifadhi atakapoharibu ulimwengu mbovu wa Shetani. Kwa hiyo, tusiruhusu kamwe azimio letu la kuendelea kuwa watimilifu kwa Mungu lidhoofike.—Ayubu 27:5.

4:1. Katika siku ya kutoa hesabu kwa Yehova, “tawi” litapata mambo yatakayoupata “mzizi,” yaani, watoto wachanga watapokea hukumu ileile kama ya wazazi wao. Wazazi wana daraka zito kama nini kuelekea watoto wao wachanga! Ni lazima baba na mama Wakristo wajitahidi sana kupata kibali cha Mungu na kuendelea kuwa na msimamo mzuri mbele zake.—1 Wakorintho 7:14.

“Mwogope Mungu wa Kweli”

Ni nani atakayeokoka “siku ya Yehova iliyo kuu na yenye kuogopesha”? (Malaki 4:5) “Kwenu ninyi mnaoliogopa jina langu,” asema Yehova, “jua la uadilifu litaangaza, likiwa na kiponyaji katika mabawa yake; nanyi mtatoka nje na kuukanyaga udongo kama ndama waliononeshwa.”—Malaki 4:2.

“Jua la uadilifu,” Yesu Kristo, anawaangazia wale wanaoliogopa na kuliheshimu jina la Mungu, nao wanapata kibali cha Yehova. (Yohana 8:12) Wanapata “kiponyaji katika mabawa yake.” Wanaponywa kiroho sasa na wataponywa kabisa kimwili, kiakili, na kihisia katika ulimwengu mpya wa Mungu. (Ufunuo 22:1, 2) Wanasisimuka na kufurahi “kama ndama waliononeshwa.” Tunapongojea baraka hizo, acheni tutii himizo hili la Mfalme Sulemani: “Mwogope Mungu wa kweli na kushika amri zake. Kwa maana huo ndio wajibu wote wa mwanadamu.”—Mhubiri 12:13.

[Picha katika ukurasa wa 26]

Nabii Malaki, alikuwa mtumishi mwenye bidii na mwenye kujitoa kwa Mungu

[Picha katika ukurasa wa 29]

Mambo tunayofundisha yanapaswa kupatana na Biblia

[Picha katika ukurasa wa 29]

Watumishi wa Yehova wanaheshimu agano lao la ndoa