Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Simameni Imara Muuone Wokovu wa Yehova”

“Simameni Imara Muuone Wokovu wa Yehova”

“Simameni Imara Muuone Wokovu wa Yehova”

“Yehova yuko upande wangu; sitaogopa. Mtu wa udongo anaweza kunitenda nini?”—ZABURI 118:6.

1. Ni matukio gani muhimu ambayo wanadamu watakabili wakati ujao?

LEO, wanadamu wanakabili matukio makubwa sana ambayo hawajawahi kamwe kukabili. Akitabiri kuhusu siku zetu, Yesu aliwaonya wafuasi wake hivi: ‘Kutakuwa na dhiki kuu ya namna ambayo haijapata kutukia tangu mwanzo wa ulimwengu mpaka sasa, hapana, wala haitatukia tena. Kwa kweli, kama siku hizo hazingefupishwa, hakuna chochote chenye mwili ambacho kingeokolewa; lakini kwa sababu ya wale waliochaguliwa siku hizo zitafupishwa.’—Mathayo 24:21, 22.

2. Ni nini kinachoizuia dhiki kuu isianze?

2 Ingawa wanadamu hawaoni majeshi ya kimbingu, majeshi hayo yanaizuilia hiyo dhiki kuu. Katika ufunuo aliopewa na Yesu, mtume Yohana alipata pendeleo la kuelewa kwa nini dhiki hiyo inazuiliwa. Hivi ndivyo mtume huyo aliyezeeka alivyoeleza kuzuiliwa kwa dhiki hiyo: “Nikaona malaika wanne wamesimama juu ya pembe nne za dunia, wakizishika sana zile pepo nne za dunia . . . Nami nikamwona malaika mwingine akipanda kutoka mashariki, akiwa na muhuri wa Mungu aliye hai; naye akapaaza sauti kubwa kwa wale malaika wanne . . . ‘Msiidhuru dunia au bahari au miti, mpaka baada ya sisi kuwatia muhuri watumwa wa Mungu wetu katika mapaji ya nyuso zao.’”—Ufunuo 7:1-3.

3. Ni nini itakayokuwa sehemu ya kwanza ya ile dhiki kuu?

3 Kutiwa muhuri kwa mara ya mwisho kwa “watumwa wa Mungu,” watiwa-mafuta, kunakaribia kukamilika. Malaika hao wanne wako tayari kuachilia zile pepo za uharibifu. Watakapoziachilia, ni nini kitakachotukia kwanza? Malaika mmoja anajibu swali hilo: “Hivi ndivyo Babiloni lile jiji kubwa litakavyotupwa chini kwa mtupo wa kasi sana, naye hatapatikana tena.” (Ufunuo 18:21) Kutakuwa na shangwe kubwa kama nini mbinguni jambo hilo litakapotukia, wakati milki ya ulimwengu ya dini ya uwongo itakapoharibiwa!—Ufunuo 19:1, 2.

4. Ni matukio gani yanayotarajiwa?

4 Mataifa yote ya dunia yatakuwa yameungana ili kuwapinga watu wa Yehova. Je, mataifa hayo yatafaulu kuwakatilia mbali Wakristo hao waaminifu? Huenda ikaonekana kwamba yatafaulu. Lakini tazama! Majeshi ya kimbingu yanayomfuata Kristo Yesu yataharibu majeshi hayo ya kibinadamu. (Ufunuo 19:19-21) Mwishowe, Ibilisi na malaika wake watatupwa ndani ya abiso, yaani, hali ya kutotenda. Hawataweza tena kuwadanganya wanadamu kwa sababu watafungwa kwa miaka elfu. Lo! Kitakuwa kitulizo kama nini kwa umati mkubwa wa waokokaji!—Ufunuo 7:9, 10, 14; 20:1-3.

5. Wale wanaoendelea kuwa washikamanifu kwa Yehova watapata shangwe gani?

5 Hivi karibuni, tutakabili matukio hayo ya ajabu na yenye kuogopesha. Matukio hayo yote yanahusiana na kutetewa kwa haki ya Yehova ya kutawala, yaani, enzi yake kuu ya ulimwengu wote. Fikiria hili: Tukiendelea kuwa washikamanifu kwa Yehova na kusimama imara upande wa enzi yake kuu, tutapata nafasi ya kushiriki katika kutakaswa kwa jina la Yehova na kutimizwa kwa kusudi lake. Itakuwa shangwe kubwa kama nini!

6. Kwa sababu ya mambo yanayokaribia kutukia, tutachunguza nini?

6 Je, tuko tayari kwa ajili ya matukio hayo muhimu? Je, tunaamini nguvu za Yehova za kuokoa? Je, tuna hakika kwamba atatusaidia kwa wakati unaofaa na kwa njia bora zaidi? Ili kujibu maswali hayo ya kibinafsi, tunaweza kufikiria yale ambayo mtume Paulo aliwaambia Wakristo wenzake huko Roma: “Mambo yote yaliyoandikwa zamani yaliandikwa ili kutufundisha sisi, ili kupitia uvumilivu wetu na kupitia faraja kutokana na Maandiko tuwe na tumaini.” (Waroma 15:4) Moja ya mambo yaliyoandikwa ili kutufundisha sisi na kutupa faraja na tumaini, ni simulizi kuhusu wakati Yehova alipowakomboa Waisraeli kutoka katika utumwa wenye kukandamiza wa Wamisri. Kuchunguza kwa makini matukio hayo yenye kusisimua wakati Yehova alipoongoza mambo ili kuwaokoa wana wa Israeli, kunapaswa kututia moyo sana tunapotazamia dhiki kuu inayokaribia haraka.

Yehova Anawaokoa Watu Wake

7. Katika mwaka wa 1513 K.W.K., ni hali gani hatari inayotokea huko Misri?

7 Ni mwaka wa 1513 K.W.K. Tayari Yehova ameleta mapigo tisa juu ya Wamisri. Baada ya pigo la tisa, Farao anamfukuza Musa haraka kwa maneno haya: “Toka mbele yangu! Jiangalie! Usijaribu kuuona uso wangu tena, kwa sababu siku utakayouona uso wangu utakufa.” Musa anajibu: “Kama ambavyo umesema na iwe. Sitajaribu kuuona uso wako tena.”—Kutoka 10:28, 29.

8. Waisraeli wanapewa maagizo gani ya kuwasaidia kuokoka, na kukiwa na matokeo gani?

Sasa Yehova anamfunulia Musa kwamba bado kuna pigo moja zaidi juu ya Farao na Wamisri wote, pigo la mwisho kabisa. Tarehe 14 ya mwezi wa Abibu (Nisani), mzaliwa wa kwanza wa kila Mmisri na wa kila mnyama atakufa. Lakini familia za Waisraeli zinaweza kuhifadhiwa kwa kufuata tu kwa makini maagizo ambayo Mungu anampa Musa. Wanapaswa kupaka damu ya kondoo-dume juu ya miimo miwili ya mlango na sehemu ya juu ya mlango wa nyumba zao na kubaki ndani ya nyumba. Kunatokea nini usiku huo? Acheni Musa mwenyewe atueleze: “Ikawa kwamba katikati ya usiku Yehova akampiga kila mzaliwa wa kwanza katika nchi ya Misri.” Farao anachukua hatua papo hapo. Anawaita Musa na Haruni na kuwaambia: “Simameni, tokeni kati ya watu wangu, . . . na mwende, mkamtumikie Yehova, kama mlivyosema.” Na papo hapo Waisraeli wanaondoka, huenda wakiwa zaidi ya milioni tatu pamoja na “jamii kubwa iliyochangamana” ya watu wasio Waisraeli, ambayo haina hesabu.—Kutoka 12:1-7, 29, 31, 37, 38.

9. Mungu anawapitisha Waisraeli njia gani wanapotoka Misri, na kwa nini?

9 Njia ya karibu zaidi ambayo Waisraeli wanapaswa kupitia ni Bahari ya Mediterania na pia nchi ya Wafilisti. Lakini hilo ni eneo la maadui. Kwa hiyo, inaelekea ili kuwaokoa watu wake wasikabiliane na vita, Yehova anawapitisha njia ya nyika ya Bahari Nyekundu. Ingawa idadi ya wasafiri hao ni mamilioni, umati huo una utaratibu. Masimulizi ya Biblia yanasema hivi: “Wana wa Israeli walitoka nchini Misri wakiwa wamejipanga kivita.”—Kutoka 13:17, 18.

“Muuone Wokovu wa Yehova”

10. Kwa nini Mungu anawaambia Waisraeli wapige kambi mbele ya Pihahirothi?

10 Kisha, matukio yenye kusisimua yanafuata. Yehova anamwambia Musa: “Sema na wana wa Israeli, kwamba warudi na kupiga kambi mbele ya Pihahirothi katikati ya Migdoli na bahari, kukabili Baal-sefoni.” Umati huo mkubwa unapofuata maagizo hayo, unajikuta umenaswa kati ya milima na Bahari Nyekundu. Inaonekana hakuna njia ya kutokea. Lakini, Yehova anajua kile anachofanya. Anamwambia Musa hivi: “Kwa kweli nitauacha moyo wa Farao uwe mkaidi, naye hakika atawafuatilia wao nami nitajipatia utukufu kupitia kwa Farao na majeshi yake yote; nao Wamisri watajua hakika kwamba mimi ni Yehova.”—Kutoka 14:1-4.

11. (a) Farao anafanya nini, na Waisraeli wanaitikia jinsi gani? (b) Musa anaitikia jinsi gani malalamiko ya Waisraeli?

11 Farao anapoona kwamba amekosea kwa kuwaruhusu Waisraeli waondoke Misri, anawafuatilia mbiombio akiwa na magari 600 ya vita yaliyochaguliwa. Wanapoliona jeshi la Misri, Waisraeli wanaogopa na kumlalamikia Musa hivi: “Je, ni kwa sababu hakuna makaburi yoyote huko Misri ndiyo sababu umetuleta hapa ili tufie nyikani?” Akiwa na uhakika kwamba Yehova atawaokoa, Musa anajibu: “Msiogope. Simameni imara muuone wokovu wa Yehova, atakaowafanyia ninyi leo. . . . Yehova mwenyewe atawapigania ninyi, nanyi wenyewe mtakaa kimya.”—Kutoka 14:5-14.

12. Yehova anawaokoa watu wake jinsi gani?

12 Ili kuthibitisha ukweli wa maneno ya Musa kwamba Yehova mwenyewe atawapigania Waisraeli, majeshi yenye nguvu zinazozidi za wanadamu sasa yanaongoza mambo. Malaika wa Yehova anaipeleka nyuma kimuujiza ile nguzo ya wingu ambayo imekuwa ikiongoza kambi ya Israeli. Nguzo hiyo inawaletea Wamisri giza, lakini inawatolea Waisraeli nuru. (Kutoka 13:21, 22; 14:19, 20) Sasa Musa anatii amri ya Mungu na kunyoosha mkono wake. Simulizi linasema hivi: “Yehova akaanza kuifanya bahari irudi nyuma kwa upepo wenye nguvu wa mashariki usiku kucha . . . Mwishowe wana wa Israeli wakapita katikati ya bahari juu ya nchi kavu, huku maji yakiwa ukuta kwao mkono wao wa kuume na wa kushoto.” Wamisri wanaanza kuwafuatilia, lakini Yehova yuko upande wa watu wake. Anavuruga kambi ya Wamisri, kisha anamwambia Musa: “Unyooshe mkono wako juu ya bahari, ili maji yarudi juu ya Wamisri, magari yao ya vita na askari wao wapanda-farasi.” Jeshi la Farao linaharibiwa kabisa hivi kwamba hakuna hata askari-jeshi mmoja anayebaki hai!—Kutoka 14:21-28; Zaburi 136:15.

Jifunze Kutokana na Wokovu wa Waisraeli

13. Wana wa Israeli waliitikia jinsi gani walipokombolewa?

13 Ukombozi huo wa kimuujiza ulikuwa na matokeo gani juu ya waokokaji? Kwa ghafula, Musa pamoja na wana wa Israeli wanaanza kuimba, wakimsifu Yehova! Waliimba hivi: “Acheni nimwimbie Yehova, kwa maana ametukuzwa sana. . . . Yehova atatawala akiwa mfalme mpaka wakati usio na kipimo, naam, milele.” (Kutoka 15:1, 18) Ndiyo, jambo la kwanza walilofikiria lilikuwa kumtukuza Mungu. Katika hali hiyo, Yehova alithibitisha enzi yake kuu.

14. (a) Tunaweza kujifunza nini kumhusu Yehova kutokana na mambo ambayo Waisraeli walijionea? (b) Ni andiko gani litakalokuwa andiko la mwaka wa 2008?

14 Tunapata maagizo, faraja, na tumaini gani kutokana na matukio hayo yenye kusisimua? Hapana shaka kwamba Yehova yuko tayari kushughulikia tatizo lolote ambalo watu wake wanakabili. Ana uwezo wa kutatua tatizo lolote ambalo huenda wakakabili. Bahari Nyekundu haikuwa kizuizi kwa Waisraeli Yehova aliposababisha upepo mkubwa wa mashariki uvume. Pia, alifanya hiyo Bahari Nyekundu iwe kaburi la maji la majeshi ya Farao. Tunapotafakari tukio hilo, tunaweza kurudia maneno haya ya mtunga-zaburi aliyesema hivi: “Yehova yuko upande wangu; sitaogopa. Mtu wa udongo anaweza kunitenda nini?” (Zaburi 118:6) Pia, tunaweza kupata faraja kutokana na maneno ya Paulo kwenye Waroma 8:31: “Ikiwa Mungu yuko upande wetu, ni nani atakayekuwa dhidi yetu?” Maneno hayo yaliyoongozwa na roho yanatupa uhakika kama nini! Yanatuliza woga wowote na mashaka ambayo huenda tukawa nayo na yanatupa tumaini. Hivyo basi, andiko letu la mwaka wa 2008 linafaa kabisa: “Simameni imara muuone wokovu wa Yehova”!—Kutoka 14:13.

15. Utii ulikuwa wa maana kadiri gani katika kukombolewa kwa Waisraeli kutoka Misri, na ni wa maana kadiri gani leo?

15 Ni jambo gani lingine ambalo tunaweza kujifunza kutokana na Kutoka kwa Waisraeli Misri? Tunajifunza kwamba tunapaswa kumtii Yehova hata akituomba tufanye nini. Waisraeli walitii na kufanya matayarisho yote yaliyohitajiwa kwa ajili ya Pasaka. Walitii kwa kubaki ndani ya nyumba zao usiku wa Nisani 14. Mwishowe, walipoondoka Misri, walipaswa kwenda “wakiwa wamejipanga kivita.” (Kutoka 13:18) Leo, ni jambo la maana sana kwetu kufuata mwongozo unaotolewa kupitia “mtumwa mwaminifu na mwenye busara”! (Mathayo 24:45) Tunapaswa kusikiliza kwa makini sana neno la Mungu linalotoka nyuma yetu, likisema: “‘Hii ndiyo njia. Tembeeni ndani yake,’ iwe mtakwenda upande wa kuume au iwe mtakwenda upande wa kushoto.” (Isaya 30:21) Tunapokaribia sana mwanzo wa dhiki kuu, huenda tukapokea maagizo fulani yenye mambo mengi. Usalama wetu katika siku hizo zenye misukosuko utategemea kuendelea kushirikiana na watumishi wengine washikamanifu wa Yehova.

16. Tunaweza kujifunza nini kutokana na jinsi Mungu alivyoongoza mambo ili kuwakomboa Waisraeli?

16 Pia, kumbuka kwamba Yehova aliwaelekeza Waisraeli mahali ambapo walionekana kana kwamba wamenaswa kati ya milima na Bahari Nyekundu. Hiyo haikuonekana kuwa njia inayofaa. Lakini Yehova alikuwa akiongoza mambo yote, na yote yalifanikiwa kwa utukufu wake na kwa wokovu wa watu wake. Leo, huenda tusielewe wazi kabisa kwa nini mambo fulani ya kitengenezo yanashughulikiwa kwa njia fulani, lakini tuna sababu nzuri ya kutumaini mwongozo wa Yehova kupitia njia yake yenye kuaminika ya mawasiliano. Nyakati nyingine, huenda ikaonekana kwamba maadui wetu wanafanikiwa. Kwa sababu ya kupungukiwa kwetu, huenda tusielewe mambo yote yanayohusika. Hata hivyo, Yehova ana uwezo wa kuongoza mambo kwa wakati unaofaa, kama tu alivyofanya zamani kwa ajili ya wana wa Israeli.—Methali 3:5.

Uwe na Uhakika Katika Yehova

17. Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kamili katika mwongozo wa Mungu?

17 Je, unaweza kufikiria uhakika ambao Waisraeli walikuwa nao walipokumbuka ile nguzo ya wingu iliyowaongoza mchana na nguzo ya moto usiku? Ilikuwa wazi kwamba “malaika wa Mungu wa kweli” alikuwa akiwaongoza katika safari yao. (Kutoka 13:21, 22; 14:19) Leo, tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova yuko pamoja na watu wake ili kuwaongoza, kuwalinda, na kuwakomboa. Tunaweza kuitumaini kabisa ahadi hii: “[Yehova] hatawaacha washikamanifu wake. Hakika watalindwa mpaka wakati usio na kipimo.” (Zaburi 37:28) Na tusiyasahau kamwe majeshi ya kimalaika yenye nguvu ambayo yanawasaidia watumishi wa Mungu leo. Kwa msaada wao, tunaweza ‘kusimama imara na kuuona wokovu wa Yehova.’—Kutoka 14:13.

18. Kwa nini tunahitaji ‘kuvaa mavazi kamili ya silaha kutoka kwa Mungu’?

18 Ni nini kitakachotuwezesha sote ‘tusimame imara’ katika njia ya kweli? Ni kuvaa silaha za kiroho zinazoelezwa na Paulo katika barua yake kwa Waefeso. Ona kwamba mtume huyo anatuhimiza ‘tuvae mavazi kamili ya silaha kutoka kwa Mungu.’ Je, tunavaa sehemu zote za silaha hizo za kiroho? Mwaka ujao, kila mmoja wetu anapaswa kujichunguza ili ahakikishe kwamba amevaa vizuri kabisa kila sehemu ya silaha hizo. Adui wetu, Shetani Ibilisi, anajua udhaifu wetu, na anajaribu kutunasa au kutushambulia kupitia udhaifu huo. Tuna “kushindana mweleka” na roho waovu. Hata hivyo, tunaweza kushinda kwa nguvu za Yehova!—Waefeso 6:11-18; Methali 27:11.

19. Tukivumilia, huenda tukapata pendeleo gani?

19 Yesu aliwaambia wafuasi wake hivi: “Nanyi kwa kuvumilia mtajipatia nafsi zenu.” (Luka 21:19) Acheni basi tuwe kati ya wale ambao wanavumilia kwa uaminifu matatizo yoyote ambayo huenda wakakabili na hivyo kwa fadhili zisizostahiliwa za Mungu kupata pendeleo la ‘kusimama imara na kuuona wokovu wa Yehova.’

Ungetoa Jibu Gani?

• Ni matukio gani yenye kusisimua yatakayotukia hivi karibuni?

• Katika mwaka wa 1513 K.W.K., Yehova alithibitisha jinsi gani kwamba ana uwezo wa kuokoa?

• Umeazimia kufanya nini wakati ujao?

[Maswali ya Funzo]

[Blabu katika ukurasa wa 20]

Andiko la mwaka wa 2008 litakuwa: “Simameni imara muuone wokovu wa Yehova.”—Kutoka 14:13.

[Picha katika ukurasa wa 17]

“Mambo yote yaliyoandikwa zamani yaliandikwa ili kutufundisha sisi”

[Picha katika ukurasa wa 18]

Ukaidi wa Farao ulileta msiba juu ya Misri

[Picha katika ukurasa wa 19]

Waisraeli waliokoka walipofanya mambo yote ambayo Yehova aliwaamuru