Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Endelea Kuangalia Huduma Ambayo Uliikubali Katika Bwana”

“Endelea Kuangalia Huduma Ambayo Uliikubali Katika Bwana”

“Endelea Kuangalia Huduma Ambayo Uliikubali Katika Bwana”

“Endelea kuangalia huduma ambayo uliikubali katika Bwana, ili uitimize.”—KOL. 4:17.

1, 2. Wakristo wana wajibu gani kuelekea wanadamu wote?

TUNA wajibu mzito sana kuelekea majirani wetu. Maamuzi ambayo wanafanya sasa yatamaanisha uzima au kifo wakati wa “ile dhiki kuu.” (Ufu. 7:14) Mwandikaji wa kitabu cha Methali alisema hivi kwa mwongozo wa roho: “Wakomboe wale wanaopelekwa kwenye kifo; na uwazuie wale wanaopepesuka wakielekea kuchinjwa.” Ni maneno mazito kama nini! Tunaweza kuwa na hatia ya damu tukikosa kutimiza wajibu wetu wa kuwaonya watu kuhusu uamuzi ulio mbele yao. Kwa kweli, andiko hilo linaendelea kusema hivi: “Ikiwa utasema: ‘Tazama! Hatukujua hili,’ je, yule anayeipima mioyo hatatambua hilo, na yule anayeichunguza nafsi yako mwenyewe hatajua hilo naye hakika hatamlipa mtu wa udongo kulingana na utendaji wake?” Ni wazi kwamba watumishi wa Yehova hawawezi kusema kwamba ‘hawajui’ hatari ambayo watu wanakabili.—Met. 24:11, 12.

2 Yehova anathamini uhai. Anawahimiza watumishi wake wajitahidi kadiri wanavyoweza ili kusaidia kuokoa uhai wa watu wengi iwezekanavyo. Ni lazima kila mhudumu wa Mungu atangaze ujumbe wenye kuokoa uhai ulio katika Neno la Mungu. Kazi yetu ni kama ya mlinzi ambaye anatoa onyo anapoona hatari. Hatutaki damu ya watu wanaokabili hatari ya kuangamia iwe juu ya vichwa vyetu. (Eze. 33:1-7) Kwa hiyo, ni jambo la maana sana tuendelee kujitahidi ‘kulihubiri neno’!—Soma 2 Timotheo 4:1, 2, 5.

3. Funzo hili na makala mbili zinazofuata zitazungumzia mambo gani?

3 Funzo hili litazungumzia jinsi unavyoweza kushinda vipingamizi katika huduma yako ya kuokoa uhai, na pia jinsi unavyoweza kuwasaidia watu wengi zaidi. Funzo linalofuata litazungumzia jinsi unavyoweza kuboresha ufundi wako wa kufundisha kweli zilizo muhimu sana. Makala ya tatu ya funzo itaonyesha matokeo fulani yenye kutia moyo ambayo watangazaji wa Ufalme wanapata ulimwenguni pote. Hata hivyo, kabla ya kuzungumzia habari hizo, ni vizuri tuchunguze tena kwa nini nyakati zetu ni za hatari sana.

Kwa Nini Watu Wengi Hawana Tumaini?

4, 5. Wanadamu wanakumbwa na nini, na watu wengi wanahisi namna gani?

4 Matukio ya ulimwengu yanaonyesha kwamba tunaishi katika “umalizio wa mfumo wa mambo,” na mwisho uko karibu sana. Wanadamu wanakumbwa na matukio na hali ambazo Yesu na wanafunzi wake walisema zingekuwapo katika “siku za mwisho.” “Maumivu ya taabu,” kutia ndani vita, upungufu wa chakula, matetemeko ya nchi, na misiba mingine inawakumba wanadamu. Uasi-sheria, uchoyo, na mitazamo ya kutomwogopa Mungu imeenea sana. Hata watu ambao wanajitahidi kuishi kupatana na viwango vya Biblia wanakabili “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.”—Mt. 24:3, 6-8, 12; 2 Tim. 3:1-5.

5 Hata hivyo, wanadamu wengi hawajui matukio ya ulimwengu yanamaanisha nini. Kwa sababu hiyo, wanahangaikia usalama wao na wa familia zao. Wengi wanafadhaika sana wanapofiwa na wapendwa wao au wanapopata misiba mingine. Watu hao hawana tumaini kwa sababu hawana ujuzi sahihi kuhusu kwa nini mambo kama hayo yanatukia na suluhisho ni nini.—Efe. 2:12.

6. Kwa nini “Babiloni Mkubwa” ameshindwa kuwasaidia wafuasi wake?

6 “Babiloni Mkubwa,” milki ya ulimwengu ya dini ya uwongo, haijawafariji wanadamu. Badala yake, kupitia “divai ya uasherati wake” imefanya watu wengi wayumbe-yumbe na kuvurugika kiroho. Zaidi ya hayo, kama kahaba, dini ya uwongo imewashawishi na kuwaongoza “wafalme wa dunia.” Inatumia mafundisho ya uwongo na mazoea ya kuwasiliana na pepo kuwafanya wanadamu wengi wajitiishe kabisa kwa viongozi wao wa kisiasa. Kwa hiyo, dini ya uwongo imekuwa na nguvu na uvutano, hata hivyo, imekataa kabisa kweli ya kidini.—Ufu. 17:1, 2, 5; 18:23.

7. Wanadamu wengi watapatwa na nini, lakini baadhi yao wanaweza kusaidiwa jinsi gani?

7 Yesu alifundisha kwamba wanadamu wengi wanatembea katika barabara pana ambayo inaongoza kwenye uharibifu. (Mt. 7:13, 14) Watu fulani wako kwenye barabara hiyo pana kwa sababu wameamua kukataa kimakusudi mafundisho ya Biblia, lakini wengine wengi wako kwenye barabara hiyo kwa sababu wamedanganywa, au wako gizani kwa sababu hawajafundishwa na viongozi wao wa kidini mambo ambayo kwa kweli Yehova anataka wafanye. Labda wengine wangebadili maisha yao ikiwa wangeonyeshwa waziwazi sababu za Kimaandiko za kufanya hivyo. Lakini wale ambao wanabaki ndani ya Babiloni Mkubwa na kuendelea kukataa viwango vya Biblia hawataokolewa wakati wa “ile dhiki kuu.”—Ufu. 7:14.

Endelea Kuhubiri “Bila Kuacha”

8, 9. Wakristo wa karne ya kwanza walifanya nini walipokabili upinzani, na kwa nini?

8 Yesu alisema kwamba wanafunzi wake wangehubiri habari njema ya Ufalme na kufanya wanafunzi. (Mt. 28:19, 20) Kwa hiyo, Wakristo wa kweli sikuzote wameona kushiriki katika kazi ya kuhubiri kuwa uthibitisho wa ushikamanifu wao kwa Mungu na takwa la msingi la imani yao. Hivyo, wafuasi wa mapema wa Yesu waliendelea kuhubiri hata walipokabili upinzani. Walimtegemea Yehova ili awape nguvu, huku wakimwomba awawezeshe kuendelea “kusema neno [lake] kwa ujasiri wote.” Kwa hiyo, Yehova aliwajaza roho takatifu, nao wakasema neno la Mungu kwa ujasiri.—Mdo. 4:18, 29, 31.

9 Wafuasi wa Yesu walipopingwa kwa jeuri, je, waliyumbayumba katika azimio lao na kuacha kuhubiri? Hawakuacha kamwe. Kazi ya kuhubiri ya mitume iliwaudhi viongozi wa dini ya Kiyahudi, wakawakamata mitume, wakawatisha, na kuwapiga viboko. Hata hivyo, mitume ‘waliendelea bila kuacha kufundisha na kutangaza habari njema juu ya Kristo, Yesu.’ Walielewa waziwazi kwamba walipaswa ‘kumtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.’—Mdo. 5:28, 29, 40-42.

10. Wakristo wanakabili majaribu gani leo, lakini mwenendo wao mzuri unaweza kuwa na matokeo gani?

10 Watumishi wengi wa Mungu leo hawajawahi kupigwa viboko wala kutiwa gerezani kwa sababu ya kuhubiri. Hata hivyo, Wakristo wote wa kweli wanakabili majaribu na matatizo mbalimbali. Kwa mfano, dhamiri yako iliyozoezwa na Biblia inaweza kukuchochea ujiendeshe kwa njia isiyopendwa na watu wengi au inayokufanya uonekane kuwa tofauti. Wafanyakazi na wanashule wenzako, au majirani wanaweza kukuona kuwa mtu wa ajabu kwa sababu maamuzi yako yanategemea kanuni za Biblia. Hata hivyo, maoni yao mabaya hayapaswi kukuvunja moyo. Ulimwengu uko katika giza la kiroho, lakini Wakristo wanapaswa ‘kuangaza kama mianga.’ (Flp. 2:15) Huenda watu fulani wenye mioyo minyoofu wataona na kuvutiwa na matendo yako mazuri na kumpa Yehova utukufu.—Soma Mathayo 5:16.

11. (a) Huenda watu fulani wakaitikia jinsi gani kazi ya kuhubiri? (b) Paulo alikabili upinzani wa aina gani, naye alifanya nini?

11 Tunahitaji ujasiri ili kuendelea kuhubiri ujumbe wa Ufalme. Huenda watu fulani, hata watu wa ukoo, wakakudhihaki au kujaribu kukuvunja moyo kwa njia nyingine. (Mt. 10:36) Mtume Paulo alipigwa kihalisi mara nyingi kwa sababu alitimiza huduma yake kwa uaminifu. Ona jinsi alivyosema kuhusu upinzani huo: “Baada ya sisi kuwa tumeteseka kwanza na kutendewa kwa dharau,” akaandika, “tulijipa ujasiri kwa njia ya Mungu wetu ili kuwaambia ninyi habari njema ya Mungu kwa kupambana sana.” (1 The. 2:2) Bila shaka, haikuwa rahisi kwa Paulo kuendelea kuhubiri habari njema baada ya kukamatwa, kuvuliwa nguo, kupigwa kwa fimbo, na kutupwa gerezani. (Mdo. 16:19-24) Alipata jinsi gani ujasiri wa kuendelea? Tamaa yake kubwa ilikuwa kutimiza kazi ya kuhubiri aliyopewa na Mungu.—1 Kor. 9:16.

12, 13. Watu wengine wana matatizo gani, nao wanajitahidi kukabiliana nayo jinsi gani?

12 Inaweza pia kuwa vigumu kudumisha bidii yetu katika maeneo ambako watu hawapatikani nyumbani kwa urahisi au ambako wengi hawapendezwi na ujumbe wa Ufalme. Tunaweza kufanya nini katika hali kama hizo? Huenda tukahitaji kujipa ujasiri zaidi na kuwahubiria watu kwa njia isiyo rasmi. Tunaweza pia kubadili wakati wetu wa kuhubiri au kuhubiri hasa katika maeneo ambako tunaweza kupata watu wengi.—Linganisha Yoh. 4:7-15; Mdo. 16:13; 17:17.

13 Watu wengi wanakabili matatizo mengine kama vile uzee na magonjwa, ambayo yanaweza kuwazuia kushiriki kwa ukamili zaidi katika kazi ya kuhubiri. Ikiwa unapatwa na matatizo hayo, usivunjike moyo. Yehova anajua udhaifu wako na anathamini yale unayoweza kufanya. (Soma 2 Wakorintho 8:12.) Hata ikiwa unakabili matatizo ya aina gani, iwe ni upinzani, kutopendezwa kwa watu, au magonjwa, wahubirie wengine habari njema kadiri hali zako zinavyokuruhusu.—Met. 3:27; linganisha Marko 12:41-44.

“Endelea Kuangalia Huduma” Yako

14. Mtume Paulo aliwawekea Wakristo wenzake mfano gani, naye alitoa shauri gani?

14 Mtume Paulo aliitimiza huduma yake kwa bidii sana, naye aliwatia moyo waamini wenzake wafanye hivyo. (Mdo. 20:20, 21; 1 Kor. 11:1) Mtu mmoja ambaye Paulo alimtia moyo sana ni Arkipo, Mkristo aliyeishi katika karne ya kwanza. Paulo aliandika hivi katika barua yake kwa Wakolosai: “Mwambieni Arkipo hivi: ‘Endelea kuangalia huduma ambayo uliikubali katika Bwana, ili uitimize.’” (Kol. 4:17) Hatujui Arkipo alikuwa nani au alikabili hali gani, lakini tunajua kwamba aliikubali huduma. Ikiwa wewe ni Mkristo aliyejiweka wakfu, wewe pia umeikubali huduma. Je, unaendelea kuiangalia huduma hiyo ili uitimize?

15. Wakfu wa Mkristo unahusisha nini, na ni maswali gani yanayotokea?

15 Kabla ya kubatizwa, tulisali kutoka moyoni na kuweka wakfu maisha yetu kwa Yehova. Hivyo, tuliazimia kufanya mapenzi yake. Kwa hiyo basi, tunapaswa kujiuliza hivi: ‘Je, kweli kufanya mapenzi ya Mungu ndilo jambo la maana zaidi maishani mwangu?’ Huenda tukawa na wajibu mbalimbali ambao Yehova anatutazamia tutimize, kama vile kuandaa mahitaji ya familia yetu. (1 Tim. 5:8) Lakini tunatumia namna gani nguvu na wakati wetu unaobaki? Tunatanguliza nini maishani?—Soma 2 Wakorintho 5:14, 15.

16, 17. Vijana Wakristo au wale ambao hawana madaraka mengi wanaweza kufikiria mapendeleo gani?

16 Je, wewe ni Mkristo kijana aliyejiweka wakfu ambaye amemaliza au anakaribia kumaliza masomo? Inaelekea kwamba kwa sasa huna madaraka mazito ya familia. Basi, unapanga kutumia maisha yako jinsi gani? Ni maamuzi gani ambayo yatakusaidia zaidi kutimiza ahadi yako ya kufanya mapenzi ya Yehova? Vijana wengi wamepanga mambo yao ili wafanye upainia, na wamepata uradhi na shangwe kubwa sana.—Zab. 110:3; Mhu. 12:1.

17 Labda wewe ni kijana. Umeajiriwa kazi ya wakati wote lakini huna madaraka mengi isipokuwa kutimiza mahitaji yako. Bila shaka, unafurahi kushiriki katika utendaji wa kutaniko kadiri hali zako zinavyokuruhusu. Je, unaweza kupata shangwe zaidi? Je, umefikiria kupanua huduma yako? (Zab. 34:8; Met. 10:22) Katika maeneo fulani, bado kuna kazi nyingi ya kumtangazia kila mtu ujumbe wa kweli unaoleta uzima. Je, unaweza kufanya mabadiliko fulani katika maisha yako ili utumike katika eneo lenye uhitaji mkubwa zaidi wa wahubiri wa Ufalme?—Soma 1 Timotheo 6:6-8.

18. Wenzi fulani wa ndoa ambao ni vijana walifanya mabadiliko gani, na matokeo yalikuwa nini?

18 Kwa mfano, mfikirie Kevin na Elena, kutoka Marekani. * Walitaka sana kununua nyumba kama wenzi wengi wa ndoa wanavyofanya katika eneo lao baada ya kufunga ndoa. Wote wawili walifanya kazi ya wakati wote na waliishi maisha ya starehe. Lakini, hawakuwa na wakati wa kutosha wa kushiriki katika utumishi wa shambani kwa sababu ya kazi zao za kuajiriwa na kazi nyingine za nyumbani. Walitambua kwamba walikuwa wakitumia wakati na nguvu nyingi kutunza mali yao. Hata hivyo, Kevin na Elena walipoona maisha rahisi na yenye furaha ya wenzi fulani wa ndoa mapainia, waliamua kubadili mambo wanayotanguliza maishani. Baada ya kutafuta mwongozo wa Yehova kupitia sala, waliuza nyumba yao na kuhamia kwenye nyumba ya kupanga. Elena aliamua kufanya kazi kwa saa chache na akawa painia. Kevin alichochewa na matokeo mazuri ambayo mke wake alikuwa akipata katika huduma, akaacha kazi yake ya wakati wote na akawa painia. Punde si punde, walihamia nchi moja ya Amerika Kusini ili watumike katika eneo lenye uhitaji mkubwa wa wahubiri wa Ufalme. Kevin anasema hivi: “Ndoa yetu ilikuwa yenye furaha sikuzote, lakini tulipojitahidi kufikia miradi ya kiroho, furaha yetu iliongezeka zaidi.”—Soma Mathayo 6:19-22.

19, 20. Kwa nini kuhubiri habari njema ndiyo kazi ya maana zaidi leo?

19 Kuhubiri habari njema ndiyo kazi ya maana zaidi inayofanywa duniani leo. (Ufu. 14:6, 7) Inachangia kutakaswa kwa jina la Yehova. (Mt. 6:9) Ujumbe wa Biblia unaboresha maisha ya maelfu ya watu ambao wanaukubali kila mwaka, na hilo linaweza kuwaongoza kwenye wokovu. Hata hivyo, “watasikiaje bila mtu wa kuhubiri?” akauliza mtume Paulo. (Rom. 10:14, 15) Kwa kweli watasikiaje tusipohubiri? Kwa nini usiazimie kufanya yote unayoweza ili utimize huduma yako?

20 Njia nyingine ya kuwasaidia watu waelewe umuhimu wa nyakati hizi zenye hatari na matokeo ya maamuzi yao ni kuboresha uwezo wako wa kufundisha. Habari inayofuata itazungumzia jinsi unavyoweza kufanya hivyo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 18 Majina yamebadilishwa.

Ungetoa Jibu Gani?

• Wakristo wana wajibu gani kuelekea wanadamu wote?

• Tunapaswa kukabiliana jinsi gani na vipingamizi katika kazi yetu ya kuhubiri?

• Tunaweza kutimiza namna gani huduma ambayo tumekubali?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 5]

Ujasiri unahitajiwa ili kuhubiri kunapokuwa na upinzani

[Picha katika ukurasa wa 7]

Unaweza kufanya nini ikiwa unahubiri katika maeneo ambako watu hawapatikani nyumbani kwa urahisi?