Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kazia Uangalifu ‘Ufundi Wako wa Kufundisha’

Kazia Uangalifu ‘Ufundi Wako wa Kufundisha’

Kazia Uangalifu ‘Ufundi Wako wa Kufundisha’

“Lihubiri neno, . . . karipia, kemea, himiza, kwa ustahimilivu wote na ufundi wa kufundisha.”—2 TIM. 4:2.

1. Yesu aliwapa wanafunzi wake amri gani, naye aliweka mfano gani?

HATA ingawa Yesu alifanya kazi nzuri za kuponya katika huduma yake duniani, alijulikana hasa kuwa mwalimu wala si mponyaji au mfanya-miujiza. (Marko 12:19; 13:1) Yesu alitanguliza kazi ya kutangaza habari njema ya Ufalme wa Mungu, na ndivyo wafuasi wake wanavyofanya leo. Wakristo wamepewa mgawo wa kuendeleza kazi ya kufanya wanafunzi kwa kuwafundisha watu kushika mambo yote ambayo Yesu aliamuru.—Mt. 28:19, 20.

2. Tunahitaji kufanya nini ili tutimize mgawo wetu wa kuhubiri?

2 Ili kutimiza mgawo wetu wa kufanya wanafunzi, tunajitahidi daima kuboresha ufundi wetu wa kufundisha. Mtume Paulo alikazia umuhimu wa ufundi huo alipomwandikia Timotheo, mhubiri mwenzake. Alisema hivi: “Jiangalie daima wewe mwenyewe na kufundisha kwako. Kaa katika mambo haya, kwa maana kwa kufanya hivyo utajiokoa wewe mwenyewe na wale wanaokusikiliza pia.” (1 Tim. 4: 16) Kufundisha ambako Paulo alikuwa akizungumzia hakukumaanisha tu kumpa mtu ujuzi. Wahudumu Wakristo wenye matokeo wanafikia mioyo ya watu na kuwachochea wafanye mabadiliko katika maisha yao. Huo ni ufundi. Basi tunaweza kusitawisha jinsi gani “ufundi wa kufundisha” tunapowahubiria wengine habari njema ya Ufalme wa Mungu?—2 Tim. 4:2.

Kusitawisha “Ufundi wa Kufundisha”

3, 4. (a) Tunaweza kusitawisha namna gani “ufundi wa kufundisha”? (b) Shule ya Huduma ya Kitheokrasi inatusaidia jinsi gani kuwa walimu wenye matokeo?

3 Kamusi moja inasema “ufundi” ni “ustadi ambao mtu anapata kwa kujifunza, kutumia yale anayojifunza, au kwa kutazama.” Ili tuwe walimu wa habari njema wenye matokeo tunahitaji kukazia uangalifu mambo hayo matatu. Tunaweza kuelewa kwa usahihi habari tunayofundisha ikiwa tu tutajifunza habari hiyo na kusali. (Soma Zaburi 119:27, 34.) Kuwatazama wahudumu wenye matokeo wakifundisha kunatusaidia kujifunza njia zao na kuwaiga. Na kujitahidi kutumia kwa ukawaida yale tunayojifunza kutatusaidia kuboresha ufundi wetu.—Luka 6:40; 1 Tim. 4:13-15.

4 Yehova ni Mfundishaji wetu Mkuu. Kupitia sehemu inayoonekana ya tengenezo lake, anawapa watumishi wake duniani mwongozo wa jinsi wanavyopaswa kutimiza kazi yao ya kuhubiri. (Isa. 30:20, 21) Kwa kusudi hilo, kila kutaniko linakuwa na Shule ya Huduma ya Kitheokrasi kila juma, ambayo imekusudiwa kuwasaidia wote waliojiandikisha katika shule hiyo kuwa watangazaji wenye matokeo wa Ufalme wa Mungu. Kitabu kikuu cha shule hiyo ni Biblia. Neno la Yehova lililoongozwa na roho linatuambia mambo tunayopaswa kufundisha. Zaidi ya hayo, linaonyesha njia za kufundisha zinazofaa na zenye matokeo. Shule ya Huduma ya Kitheokrasi inatukumbusha kwa ukawaida kwamba tutakuwa walimu wenye ustadi zaidi tukitegemea Neno la Mungu tunapofundisha, tukitumia maswali mazuri, tukifundisha kwa njia rahisi, na kupendezwa kikweli na wengine. Acheni tuchunguze kila moja ya mambo hayo. Kisha, tutazungumzia jinsi tunavyoweza kuufikia moyo wa mwanafunzi.

Tegemea Neno la Mungu Unapofundisha

5. Tunapaswa kutegemea nini tunapofundisha, na kwa nini?

5 Yesu, yule mwalimu mkuu zaidi kati ya walimu wote wa kibinadamu, alitegemea Maandiko alipofundisha. (Mt. 21:13; Yoh. 6:45; 8:17) Hakuzungumza kwa jina lake mwenyewe, bali kwa jina la Yule aliyemtuma. (Yoh. 7:16-18) Tunafuata mfano wake. Kwa hiyo, yale tunayosema iwe tunahubiri nyumba kwa nyumba au tunaongoza mafunzo ya Biblia ya nyumbani, yanapaswa kutegemea mamlaka ya Neno la Mungu. (2 Tim. 3:16, 17) Hata tukitoa hoja za werevu jinsi gani hatuwezi kamwe kuwasaidia watu na kuwachochea kwa nguvu kama Maandiko yaliyoongozwa na roho yanavyoweza kuwachochea. Biblia ina mamlaka. Njia nzuri zaidi ya kumsaidia mwanafunzi aelewe jambo lolote lile ni kumwomba asome yale ambayo Maandiko yanasema kuhusu jambo hilo.—Soma Waebrania 4:12.

6. Mwalimu anaweza kufanya nini ili kuhakikisha kwamba mwanafunzi anaelewa habari ambayo anajifunza?

6 Bila shaka, hilo halimaanishi kwamba mwalimu Mkristo hapaswi kujitayarisha kwa ajili ya funzo la Biblia. Kinyume chake, mwalimu anapaswa kuchagua kimbele na kwa uangalifu maandiko yaliyotajwa ambayo yeye au mwanafunzi atasoma katika Biblia wakati wa funzo. Kwa kawaida, ni vizuri kusoma maandiko ambayo ndiyo msingi wa mafundisho yetu. Ni muhimu pia kumsaidia mwanafunzi aelewe maana ya kila andiko analosoma.—1 Kor. 14:8, 9.

Tumia Maswali kwa Ufundi

7. Kwa nini kutumia maswali ni njia nzuri ya kufundisha?

7 Kutumia maswali kwa ufundi kunachochea fikira na kumsaidia mwalimu kuufikia moyo wa mwanafunzi. Kwa hiyo, badala ya kumfafanulia mwanafunzi wako maandiko, mwombe akufafanulie maandiko hayo. Nyakati nyingine swali la ziada au hata maswali kadhaa yanaweza kumsaidia mwanafunzi aelewe vizuri jambo fulani. Unapotumia maswali kumfundisha mwanafunzi, kwa kweli unamsaidia kuelewa sababu za fundisho hilo na pia unamsaidia yeye mwenyewe asadiki fundisho hilo.—Mt. 17:24-26; Luka 10:36, 37.

8. Tunaweza kutambua jinsi gani mambo yaliyo moyoni mwa mwanafunzi?

8 Njia ya kufundisha inayotumiwa katika vitabu vyetu ni ya maswali na majibu. Hapana shaka kwamba watu wengi unaojifunza nao Biblia wataweza kujibu haraka maswali yaliyo katika kitabu wakitumia habari iliyo katika mafungu. Hata hivyo, mwalimu mwenye utambuzi hatatosheka tu na majibu sahihi. Kwa mfano, mwanafunzi anaweza kueleza kwa usahihi yale ambayo Biblia inasema kuhusu uasherati. (1 Kor. 6:18) Hata hivyo, maswali ya maoni yaliyotungwa kwa ustadi yanaweza kufunua maoni ya mwanafunzi kuhusu yale anayojifunza. Mwalimu anaweza kuuliza hivi: “Kwa nini Biblia inakataza mahusiano ya ngono nje ya ndoa? Una maoni gani kuhusu sheria hiyo ya Mungu? Je, unafikiri kwamba kuna faida yoyote ya kuishi kupatana na viwango vya Mungu vya maadili?” Majibu ya mwanafunzi kwa maswali kama hayo yanaweza kufunua mambo yaliyo moyoni mwake.—Soma Mathayo 16:13-17.

Fundisha kwa Njia Rahisi

9. Tunapaswa kukumbuka nini tunapofundisha habari za Kimaandiko?

9 Kwa kadiri fulani kweli nyingi zilizo katika Neno la Mungu ni rahisi kueleweka. Hata hivyo, huenda watu ambao tunajifunza nao Biblia wamevurugwa na mafundisho ya dini ya uwongo. Daraka letu tukiwa walimu ni kuifanya Biblia ieleweke kwa urahisi. Walimu wazuri wanafundisha kwa njia iliyo rahisi, wazi, na sahihi. Tukifuata mwongozo huo, hatutafanya kweli iwe ngumu kueleweka. Epuka habari zisizo za lazima. Hatuhitaji kuzungumzia kila jambo katika andiko tunalosoma. Kazia tu mambo ya maana yanayofafanua jambo mnalozungumzia. Kadiri mwanafunzi anavyofanya maendeleo, ndivyo atakavyoelewa hatua kwa hatua kweli za ndani za Maandiko.—Ebr. 5:13, 14.

10. Ni mambo gani yanayoamua wingi wa habari ambayo mtajifunza wakati wa funzo la Biblia?

10 Tunapaswa kujifunza habari nyingi kadiri gani katika kikao kimoja? Tunahitaji kutumia utambuzi tunapoamua hilo. Uwezo na hali za mwanafunzi na mwalimu zinatofautiana, lakini tunapaswa sikuzote kukumbuka kwamba kusudi letu tukiwa walimu ni kumsaidia mwanafunzi ajenge imani yenye nguvu. Kwa hiyo, tunampa wakati wa kutosha wa kusoma, kuelewa, na kukubali kweli zilizo katika Neno la Mungu. Hatupaswi kuzungumzia habari nyingi kuliko anavyoweza kuelewa. Tunapaswa pia kuhakikisha kwamba funzo linasonga. Mara tu mwanafunzi anapoelewa jambo fulani, tunasonga kwenye jambo linalofuata.—Kol. 2:6, 7.

11. Mfano wa mtume Paulo unatufunza nini kuhusu kufundisha?

11 Mtume Paulo alipozungumza na wapya, alifanya ujumbe wa habari njema ueleweke kwa urahisi. Hata ingawa alikuwa na elimu ya juu, aliepuka kutumia lugha ya wasomi. (Soma 1 Wakorintho 2:1, 2.) Kweli rahisi za Kimaandiko zinawavutia watu wanyoofu na kuwaridhisha. Watu hawahitaji kuwa na elimu ya juu ili waelewe kweli hizo.—Mt. 11:25; Mdo. 4:13; 1 Kor. 1:26, 27.

Wasaidie Wanafunzi Wathamini Mambo Wanayojifunza

12, 13. Ni nini kinachoweza kumchochea mwanafunzi afuate yale anayojifunza? Toa mfano.

12 Ili tuwe na matokeo mazuri, ni lazima mafundisho yetu yaguse moyo wa mwanafunzi. Mwanafunzi anahitaji kuelewa jinsi habari hiyo inavyomhusu yeye binafsi, inavyomletea faida, na jinsi maisha yake yanavyoweza kuwa mazuri zaidi akifuata mwongozo wa Maandiko.—Isa. 48:17, 18.

13 Kwa mfano, huenda tunazungumzia andiko la Waebrania 10:24, 25, ambalo linawatia moyo Wakristo wakusanyike pamoja na waamini wenzao ili watiwe moyo kupitia Maandiko na kufurahia ushirika wenye upendo. Ikiwa mwanafunzi hajaanza kuhudhuria mikutano ya kutaniko, tunaweza kumweleza kwa ufupi jinsi mikutano hiyo inavyofanywa na mambo ambayo yatazungumziwa. Tunaweza kutaja kwamba mikutano ya kutaniko ni sehemu ya ibada yetu na kumwonyesha kwamba inatuletea faida. Kisha tunaweza kumwalika mwanafunzi ahudhurie. Anapaswa kuchochewa kufuata sheria za Kimaandiko kwa sababu anatamani kumtii Yehova, wala si kumpendeza mwalimu wake.—Gal. 6:4, 5.

14, 15. (a) Mwanafunzi wa Biblia anaweza kujifunza nini kumhusu Yehova? (b) Kujua utu wa Mungu kunaweza kumfaidi jinsi gani mwanafunzi wa Biblia?

14 Faida moja ya msingi ambayo wanafunzi wanapata wanapojifunza Biblia na kufuata kanuni zake ni kwamba wanamjua na kumthamini Yehova kibinafsi. (Isa. 42:8) Mbali na kwamba yeye ni Baba mwenye upendo, Muumba, na Mmiliki wa ulimwengu wote, yeye pia anawafunulia utu na uwezo wake wale ambao wanampenda na wanamtumikia. (Soma Kutoka 34:6, 7.) Musa alipokuwa karibu kuongoza taifa la Israeli kutoka utumwani Misri, Yehova alijitambulisha kwa maneno haya: “Nitakuwa kile nitakachokuwa.” (Kut. 3:13-15) Maneno hayo yalimaanisha kwamba Yehova angekuwa chochote kile ambacho angehitaji kuwa ili atimize makusudi yake kuhusiana na watu wake waliochaguliwa. Hivyo, Waisraeli walipata kumjua Yehova akiwa Mwokozi, Shujaa, Mwandalizi, na Mtimizaji wa ahadi na pia walimjua katika njia nyingine nyingi.—Kut. 15:2, 3; 16:2-5; Yos. 23:14.

15 Huenda Yehova asiwasaidie wanafunzi wetu kimuujiza kama alivyomsaidia Musa. Hata hivyo, kadiri wanafunzi wanavyoendelea kukua katika imani na kuthamini zaidi yale wanayojifunza na kuanza kuyatumia, bila shaka, wataona uhitaji wa kumtegemea Yehova ili awape ujasiri, hekima, na mwongozo. Wanapofanya hivyo, wao pia watapata kumjua Yehova akiwa Mshauri mwenye hekima na mwenye kutegemeka, Mlinzi, na Mwandalizi mkarimu wa vitu vyote wanavyohitaji.—Zab. 55:22; 63:7; Met. 3:5, 6.

Pendezwa Kikweli na Mwanafunzi

16. Kwa nini uwezo wa kiasili wa kufundisha si muhimu zaidi ili kuwa mwalimu mwenye matokeo?

16 Ikiwa unahisi kwamba wewe si mwalimu stadi, jipe moyo. Yehova na Yesu wanasimamia programu ya elimu inayoendeshwa ulimwenguni pote leo. (Mdo. 1:7, 8; Ufu. 14:6) Wanaweza kubariki jitihada zetu hivi kwamba maneno yetu yanaweza kuwachochea watu wenye mioyo minyoofu. (Yoh. 6:44) Hata ikiwa mwalimu hana uwezo wa kiasili wa kufundisha, upendo wake wa kutoka moyoni unaweza kuwa na matokeo mazuri sana kwa mwanafunzi. Mtume Paulo alionyesha kwamba alielewa umuhimu wa kuwapenda wanafunzi.—Soma 1 Wathesalonike 2:7, 8.

17. Tunaweza kuonyesha kwa njia gani kwamba tunapendezwa kikweli na kila mwanafunzi wa Biblia?

17 Vivyo hivyo, tunaweza kupendezwa kikweli na kila mwanafunzi wa Biblia tukitumia wakati ili kumfahamu. Tunapozungumzia kanuni za Maandiko pamoja naye, inaelekea kwamba tutaelewa hali zake. Huenda tukaona kwamba tayari anaishi kupatana na mambo fulani ambayo amejifunza katika Biblia. Lakini labda anahitaji kufanya marekebisho fulani katika mambo mengine. Tukimsaidia mwanafunzi kuona kwamba habari tunayozungumzia katika funzo la Biblia inamhusu yeye binafsi, tunaweza kumsaidia kwa upendo awe mwanafunzi wa kweli wa Kristo.

18. Kwa nini ni jambo la maana kusali pamoja na mwanafunzi wetu na kusali kwa ajili yake?

18 Jambo la maana hata zaidi ni kwamba tunaweza kusali pamoja na mwanafunzi wetu na kusali kwa ajili yake. Anapaswa kuona wazi kwamba kusudi letu ni kumsaidia amjue Muumba wake vizuri zaidi, amkaribie zaidi, na kufaidika kwa kufuata mwongozo wa Mungu. (Soma Zaburi 25:4, 5.) Tunaposali ili Yehova abariki jitihada za mwanafunzi za kutumia yale anayojifunza, mwanafunzi ataona umuhimu wa kuwa ‘mtendaji wa neno.’ (Yak. 1:22) Mwanafunzi anaposikiliza sala zetu za kutoka moyoni, yeye pia atajifunza kusali. Ni shangwe kama nini kuwasaidia wanafunzi wa Biblia wasitawishe uhusiano wao pamoja na Yehova!

19. Habari inayofuata itazungumzia jambo gani?

19 Inatia moyo kujua kwamba Mashahidi zaidi ya milioni sita na nusu ulimwenguni pote wanajitahidi sana kusitawisha “ufundi wa kufundisha,” wakiwa na kusudi la kuwasaidia watu wenye mioyo minyoofu washike mambo yote ambayo Yesu aliamuru. Kazi yetu ya kuhubiri ina matokeo gani? Swali hilo litajibiwa katika habari inayofuata.

Je, Unakumbuka?

• Kwa nini Wakristo wanahitaji kusitawisha “ufundi wa kufundisha”?

• Ili tufanikiwe tunapofundisha tunahitaji kutumia njia gani?

• Ni nini kinachoweza kutusaidia kupata matokeo mazuri ikiwa hatuna uwezo wa kiasili wa kufundisha?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 9]

Je, umejiandikisha katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi?

[Picha katika ukurasa wa 10]

Kwa nini ni muhimu kumwomba mwanafunzi asome andiko katika Biblia?

[Picha katika ukurasa wa 12]

Sali pamoja na mwanafunzi wako na kwa ajili yake