Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Mathayo

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Mathayo

Neno la Yehova Liko Hai

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Mathayo

MTU wa kwanza kuandika masimulizi yenye kusisimua kuhusu maisha na huduma ya Yesu ni Mathayo, mshirika wa karibu wa Yesu Kristo. Mwanzoni, Mathayo alikuwa mkusanya-kodi. Injili ya Mathayo ambayo kwanza iliandikwa katika Kiebrania kisha ikatafsiriwa katika Kigiriki ilikamilika karibu mwaka wa 41 W.K. na kama daraja, inaunganisha Maandiko ya Kiebrania na Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo.

Inaelekea kwamba Injili ya Mathayo iliandikwa hasa kwa ajili ya Wayahudi. Injili hiyo yenye kuchochea na iliyo muhimu inaonyesha kwamba Yesu ndiye Masihi aliyeahidiwa, Mwana wa Mungu. Kukazia uangalifu ujumbe wa Injili hiyo kutatia nguvu imani yetu katika Mungu wa kweli, Mwana wake, na ahadi Zake.—Ebr. 4:12.

“UFALME WA MBINGUNI UMEKARIBIA”

(Mt. 1:1–20:34)

Kitabu cha Mathayo kinakazia suala la Ufalme na mafundisho ya Yesu, lakini hakifuati tarehe za matukio. Kwa mfano, Mahubiri ya Mlimani yanasimuliwa mwanzoni mwa kitabu hicho, ingawa Yesu aliyatoa karibu katikati ya huduma yake.

Wakati wa huduma yake huko Galilaya, Yesu anafanya miujiza, anawapa wale mitume 12 maagizo kwa ajili ya huduma, anawashutumu Mafarisayo, na anatoa mifano kuhusu Ufalme. Kisha, anaondoka Galilaya na kuja “kwenye mipaka ya Yudea ng’ambo ya Yordani.” (Mt. 19:1) Akiwa njiani, Yesu anawaambia wanafunzi wake hivi: ‘Tunapanda kwenda Yerusalemu, na Mwana wa binadamu atahukumiwa kifo, na siku ya tatu atafufuliwa.’—Mt. 20:18, 19.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

3:16—‘Mbingu zilifunguliwa’ jinsi gani Yesu alipobatizwa? Inaonekana hilo lilimaanisha kwamba Yesu alirudishiwa kumbukumbu ya maisha yake kabla hajawa binadamu.

5:21, 22—Je, kuonyesha ghadhabu ni jambo zito kuliko kuendelea kuwa na ghadhabu? Yesu alionya kwamba mtu anayeendelea kuwa na ghadhabu kuelekea ndugu yake anatenda dhambi nzito. Hata hivyo, kuonyesha ghadhabu kwa kusema jambo la dharau ni kosa zito zaidi, linalomfanya mtu astahili kufikishwa mbele ya mahakama iliyo kuu zaidi kuliko mahakama ya kidunia.

5:48—Je, kweli tunaweza kuwa “wakamilifu, kama Baba [yetu] wa mbinguni alivyo mkamilifu”? Ndiyo, kwa kadiri fulani. Yesu alikuwa akizungumza kuhusu upendo, naye aliwaambia wasikilizaji wake wamwige Mungu na wawe wakamilifu, au kamili katika upendo wao. (Mt. 5:43-47) Jinsi gani? Kwa kupanuka katika upendo wao ili wawapende hata maadui wao.

7:16—Ni “matunda” gani yanayoitambulisha dini ya kweli? Matunda hayo yanatia ndani mengi zaidi ya mwenendo wetu. Yanatia ndani imani yetu, yaani, mafundisho tunayoamini.

10:34-38—Je, ujumbe wa Kimaandiko unapaswa kulaumiwa kuwa ndio unaosababisha migawanyiko katika familia? Sivyo hata kidogo. Badala yake, migawanyiko inasababishwa na msimamo unaochukuliwa na washiriki wa familia ambao si waamini. Wanaweza kuamua kuukataa au kuupinga Ukristo, na hivyo kusababisha migawanyiko katika familia.—Luka 12:51-53.

11:2-6—Ikiwa baada ya kusikia sauti ya Mungu Yohana alijua kwamba Yesu ndiye Masihi, kwa nini aliuliza ikiwa Yesu ndiye “Yule Anayekuja”? Huenda Yohana aliuliza hilo ili Yesu amhakikishie kibinafsi. Zaidi ya hilo, Yohana alitaka kujua ikiwa kuna “mwingine” ambaye angekuja akiwa na nguvu za Ufalme na kutimiza matumaini yote ya Wayahudi. Jibu la Yesu lilionyesha kwamba hakukuwa na mwingine.

19:28—Ni nani wanaowakilishwa na “makabila kumi na mawili ya Israeli” ambayo yatahukumiwa? Makabila hayo hayawakilishi makabila 12 ya Israeli wa kiroho. (Gal. 6:16; Ufu. 7:4-8) Mitume ambao Yesu alikuwa akizungumzia wangekuwa sehemu ya Israeli wa kiroho, wala si waamuzi wa washiriki wa taifa hilo. Yesu alifanya ‘agano pamoja nao kwa ajili ya ufalme,’ nao wangekuwa ‘ufalme na makuhani kwa Mungu.’ (Luka 22:28-30; Ufu. 5:10) Waisraeli hao wa kiroho “watauhukumu ulimwengu.” (1 Kor. 6:2) Hivyo, ni wazi kwamba “makabila kumi na mawili ya Israeli” ambayo yatahukumiwa na wale wanaoketi katika viti vya ufalme mbinguni, yanafananisha ulimwengu wa wanadamu ambao si sehemu ya ile jamii ya ufalme na makuhani iliyofananishwa na makabila 12 katika Siku ya Upatanisho.—Law., sura ya 16.

Mambo Tunayojifunza:

4:1-10. Simulizi hili linatufundisha kwamba Shetani ni mtu halisi wala si sifa ya uovu. Anatumia “tamaa ya mwili na tamaa ya macho na mtu kujionyesha mali yake maishani” ili kutujaribu. Hata hivyo, kutumia kanuni za Kimaandiko kutatusaidia kuendelea kuwa waaminifu kwa Mungu.—1 Yoh. 2:16.

5:1–7:29. Tambua uhitaji wako wa kiroho. Uwe mwenye kufanya amani. Epuka mawazo yasiyo ya adili. Timiza ahadi zako. Unaposali, tanguliza mambo ya kiroho wala si mambo ya kimwili. Uwe tajiri kwa Mungu. Tafuta kwanza Ufalme na uadilifu wa Mungu. Usiwahukumu wengine. Fanya mapenzi ya Mungu. Mahubiri ya Mlimani yana masomo ya maana kama nini!

9:37, 38. Tunapaswa kutenda kupatana na ombi letu kwa Bwana kwamba “awatume wafanyakazi katika mavuno yake,” kwa kushiriki kwa bidii katika kazi ya kufanya wanafunzi.—Mt. 28:19, 20.

10:32, 33. Hatupaswi kamwe kuogopa kuhubiri kuhusu imani yetu.

13:51, 52. Mtu anayepata maana ya kweli za Ufalme ana wajibu wa kuwafundisha wengine na kuwasaidia kuelewa kweli hizo zenye thamani kubwa.

14:12, 13, 23. Ni jambo la maana kuwa peke yako pindi fulani ili kutafakari vizuri.—Marko 6:46; Luka 6:12.

17:20. Tunahitaji kuwa na imani ili kushinda vipingamizi vilivyo kama milima vinavyotuzuia kufanya maendeleo ya kiroho na hivyo kukabiliana na matatizo. Hatupaswi kupuuza uhitaji wa kujenga na kuimarisha imani yetu katika Yehova na ahadi zake.—Marko 11:23; Luka 17:6.

18:1-4; 20:20-28. Kutokamilika kwa kibinadamu na malezi ya kidini yanayokazia cheo yaliwafanya wanafunzi wa Yesu wahangaikie umashuhuri kupita kiasi. Tunapaswa kusitawisha unyenyekevu huku tukijihadhari na mielekeo yenye dhambi. Pia, tunapaswa kudumisha maoni yanayofaa kuhusu mapendeleo na madaraka.

“MWANA WA BINADAMU ATATOLEWA”

(Mt. 21:1–28:20)

Akiwa “amepanda juu ya punda,” Yesu anakuja Yerusalemu mnamo Nisani 9, 33 W.K. (Mt. 21:5) Kesho yake, anakuja hekaluni na kulisafisha. Katika Nisani 11, anafundisha hekaluni, anawashutumu waandishi na Mafarisayo, kisha anawapa wanafunzi wake “ishara ya kuwapo [kwake] na ya umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mt. 24:3) Siku inayofuata, anawaambia hivi: “Mnajua kwamba siku mbili tangu sasa kutakuwa na pasaka, naye Mwana wa binadamu atatolewa ili atundikwe mtini.”—Mt. 26:1, 2.

Ni Nisani 14. Baada ya kuanzisha Ukumbusho wa kifo chake, Yesu anasalitiwa, anakamatwa, anahukumiwa, na kutundikwa. Siku ya tatu, anafufuliwa kutoka kwa wafu. Kabla hajapanda kwenda mbinguni, Yesu aliyefufuliwa anawaamuru wafuasi wake hivi: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.”—Mt. 28:19.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

22:3, 4, 9—Mialiko mitatu ya karamu ya ndoa inatolewa wakati gani? Mwaliko wa kwanza wa kukusanya jamii ya bibi arusi ulitolewa Yesu na wanafunzi wake walipoanza kuhubiri mwaka wa 29 W.K., na uliendelea mpaka 33 W.K. Mwaliko wa pili ulianza kutolewa roho takatifu ilipomwagwa katika Pentekoste ya 33 W.K. mpaka 36 W.K. Mialiko hiyo miwili ilielekezwa tu kwa Wayahudi, Wayahudi waliogeuzwa imani, na Wasamaria. Hata hivyo, mwaliko wa tatu ulitolewa kwa watu waliokuwa kwenye barabara zinazotoka jijini, yaani, Watu wa Mataifa ambao hawajatahiriwa, kuanzia kugeuzwa kwa ofisa Mroma Kornelio katika 36 W.K. na unaendelea mpaka siku zetu.

23:15—Kwa nini mtu aliyegeuzwa imani na Mafarisayo ‘alistahili Gehena mara mbili zaidi kuliko’ Mafarisayo wenyewe? Baadhi ya watu waliogeuzwa imani na Mafarisayo huenda zamani walikuwa watu waliozoea kutenda dhambi nzito. Hata hivyo, kwa kugeuzwa imani na kuanza kushika msimamo mkali wa Mafarisayo, watu hao walichukua hatua mbaya zaidi, na huenda walikuwa wabaya kuliko walimu wao walioshutumiwa. Hivyo, wakilinganishwa na Mafarisayo Wayahudi, watu hao ‘walistahili Gehena’ mara mbili zaidi.

27:3-5—Yudasi alijuta kwa sababu gani? Hakuna jambo linaloonyesha kwamba Yudasi alijuta kwa sababu alitubu kikweli. Badala ya kumwomba Mungu amsamehe, alikiri kosa lake kwa kuhani mkuu na wanaume wazee. Baada ya kutenda “dhambi inayoleta kifo,” kwa kufaa Yudasi alilemewa na hisia za hatia na kukata tamaa. (1 Yoh. 5:16) Alijuta kwa sababu hakuwa na tumaini lolote.

Mambo Tunayojifunza:

21:28-31. Yehova anathamini hasa tunapofanya mapenzi yake. Kwa mfano, tunapaswa kuwa wenye bidii katika kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme na kufanya wanafunzi.—Mt. 24:14; 28:19, 20.

22:37-39. Amri mbili zilizo kuu zaidi zinaeleza kwa ufupi sana yale ambayo Mungu anataka waabudu wake wafanye!

[Picha katika ukurasa wa 31]

Je, unashiriki kwa bidii katika kazi ya kuvuna?

[Hisani]

© 2003 BiblePlaces.com

[Picha katika ukurasa wa 31]

Mathayo anakazia suala la Ufalme