Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Toleo Jipya la Funzo la Mnara wa Mlinzi

Toleo Jipya la Funzo la Mnara wa Mlinzi

Toleo Jipya la Funzo la Mnara wa Mlinzi

GAZETI hili unalosoma ndilo toleo la kwanza la funzo la Mnara wa Mlinzi. Tungependa kukueleza mambo fulani kuhusu mpangilio mpya na habari zilizo katika gazeti hili.

Toleo la funzo linachapishwa kwa ajili ya Mashahidi wa Yehova na wanafunzi wa Biblia wanaofanya maendeleo. Litachapishwa mara moja kwa mwezi nalo litakuwa na makala nne au tano za funzo. Tarehe za kujifunza makala hizo za funzo zitachapishwa kwenye jalada la gazeti. Tofauti na toleo la watu wote la Mnara wa Mlinzi, jalada la toleo la funzo halitakuwa na picha tofauti-tofauti, kwa kuwa halitatolewa katika huduma ya shambani.

Kwenye ukurasa wa 2 wa gazeti hili, utapata maelezo mafupi mazuri sana kuhusu kusudi la kila makala ya funzo au mfululizo wa makala za funzo kutia ndani orodha ya makala za ziada. Maelezo hayo yatawasaidia sana viongozi wa Funzo la Mnara wa Mlinzi wanapojitayarisha kuzungumzia habari hizo kwa njia yenye kujenga katika mikutano ya kutaniko.

Utaona kwamba makala za funzo ni fupi kidogo kuliko zilivyokuwa. Kwa sababu hiyo, kutakuwa na wakati zaidi wa kuzungumzia maandiko ya msingi wakati wa Funzo la Mnara wa Mlinzi. Tunakutia moyo usome maandiko yote yaliyotajwa katika makala kila juma. Maandiko fulani yaliyotajwa katika makala yana neno “soma,” nayo yanapaswa kusomwa na kuzungumziwa wakati wa Funzo la Mnara wa Mlinzi. Maandiko mengine yanaweza kusomwa ikiwa kuna wakati. Katika makala fulani, huenda ukapata maandiko yaliyo na neno “linganisha.” Kwa kuwa maandiko kama hayo hayathibitishi moja kwa moja mambo makuu katika fungu, kwa kawaida hayatasomwa katika mkutano wa kutaniko. Lakini, maandiko hayo yana habari za ziada zenye kupendeza, au huenda yanaunga mkono kwa njia isiyo ya moja kwa moja jambo linalozungumziwa. Tunakutia moyo uyachunguze unapojitayarisha kwa ajili ya Funzo la Mnara wa Mlinzi. Huenda ukapata nafasi ya kuyazungumzia unapotoa maelezo.

Ripoti ya kila mwaka haitachapishwa tena katika Mnara wa Mlinzi. Kuanzia mwaka wa 2008, itakuwa ikichapishwa katika nyongeza ya Huduma Yetu ya Ufalme na pia katika Kitabu cha Mwaka. Hata hivyo, kama ilivyotajwa hapo juu, toleo la funzo litakuwa na makala za ziada. Ingawa makala nyingi kati ya hizo hazitazungumziwa katika mikutano ya kutaniko, unatiwa moyo kuzisoma kwa makini. Hizo pia zina chakula cha kiroho kutoka kwa “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.”—Mt. 24:45-47.

Mwishowe, toleo la funzo na toleo la watu wote la Mnara wa Mlinzi si magazeti mawili tofauti. Yote ni Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova. Katika ukurasa wa 2 wa matoleo hayo, kuna fungu lilelile linaloeleza kusudi la Mnara wa Mlinzi. Matoleo yote mawili yatatiwa katika buku la Mnara wa Mlinzi la kila mwaka. Na habari zilizo katika matoleo yote mawili zitapatikana katika makala “Je, Unakumbuka,” ambayo itachapishwa katika toleo la funzo.

Tangu 1879, gazeti la Mnara wa Mlinzi limetangaza kwa uaminifu kweli kuhusu Ufalme wa Mungu. Limefanya hivyo wakati wa vita, matatizo ya kiuchumi, na mateso. Tunasali kwamba kwa msaada wa Yehova, gazeti hili lenye mpangilio mpya litaendelea kufanya hivyo. Na tunamwomba Yehova akubariki unaposoma na kulitumia vizuri toleo jipya la funzo la Mnara wa Mlinzi.