Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Waliboresha Maisha Yao—Je, Unaweza Kuwaiga?

Waliboresha Maisha Yao—Je, Unaweza Kuwaiga?

Waliboresha Maisha Yao—Je, Unaweza Kuwaiga?

MARC, ndugu fulani nchini Kanada, aliajiriwa kazi na kampuni fulani ya kutengeneza roboti za hali ya juu zinazotumiwa na mashirika ya anga za juu. Alikuwa akifanya kazi ya muda na pia alikuwa painia wa kawaida. Kisha, msimamizi fulani akampa Marc nafasi ya kupandishwa cheo—kazi ya siku nzima na mshahara mkubwa. Marc alifanya nini?

Amy, dada fulani huko Filipino, alifanya upainia wa kawaida huku akimalizia masomo yake. Baada ya kuhitimu, alipewa kazi ya wakati wote yenye mshahara mnono lakini ambayo ingechukua wakati wake mwingi. Amy alifanya uamuzi gani?

Marc na Amy walifanya maamuzi yanayotofautiana, na matokeo ya maamuzi yao yanaonyesha hekima ya mashauri ambayo Wakristo walipewa katika Korintho la kale. Mtume Paulo aliandika hivi: “Wale wanaoutumia ulimwengu wawe kama wale wasioutumia kwa ukamili.”—1 Kor. 7:29-31.

Utumie Ulimwengu Lakini Si kwa Ukamili

Kabla ya kuchunguza yale yaliyowapata Marc na Amy, acheni kwanza tuzungumzie kwa ufupi maana ya neno “ulimwengu” (au, koʹsmos katika Kigiriki) ambalo Paulo alitumia katika barua yake kwa Wakorintho. Katika mstari huo wa Biblia, neno koʹsmos linamaanisha mfumo wa ulimwengu ambamo tunaishi, jamii nzima ya kibinadamu, nao unatia ndani vitu vya kawaida vilivyo sehemu ya maisha ya kila siku kama vile nyumba, chakula, na mavazi. * Ili kupata vitu hivyo vya lazima vya kila siku, wengi wetu wanalazimika kufanya kazi. Kwa kweli, tunalazimika kuutumia ulimwengu ili kutimiza wajibu wetu wa Kimaandiko wa kutosheleza mahitaji yetu na ya familia zetu. (1 Tim. 5:8) Hata hivyo, tunatambua pia kwamba “ulimwengu unapitilia mbali.” (1 Yoh. 2:17) Hivyo, tunautumia ulimwengu kwa kiasi tu wala si “kwa ukamili.”—1 Kor. 7:31.

Wakichochewa na mashauri ya Biblia kuhusu kuutumia ulimwengu kwa kadiri ndogo iwezekanavyo, ndugu na dada wengi wamechanganua upya hali zao, wamepunguza wakati wanaotumia kazini, na kurahisisha mtindo wao wa maisha. Baada ya kufanya hivyo, wamegundua kwamba maisha yao yameboreka kwa kuwa wamepata wakati zaidi wa kutumia pamoja na familia zao katika utumishi wa Yehova. Zaidi ya hilo, maisha yao rahisi yamewawezesha kuacha kuutegemea sana ulimwengu na badala yake kumtegemea Yehova zaidi. Je, unaweza kuwaiga, yaani, kurahisisha maisha yako ili uendeleze kazi ya Ufalme wa Mungu?—Mt. 6:19-24, 33.

“Tunajihisi Tukiwa Karibu Zaidi na Yehova Kuliko Zamani”

Marc, aliyetajwa mwanzoni, alitii shauri la Biblia kuhusu kutotumia ulimwengu kwa ukamili. Alikataa cheo kikubwa alichopewa kazini. Siku chache baadaye, msimamizi wake alimwahidi mshahara mnono hata zaidi ili kumshawishi akubali cheo hicho. “Hilo lilikuwa jaribu,” anasema Marc, “lakini nilikataa tena.” Anaeleza kwa nini alikataa: “Mimi na mke wangu Paula, tulitaka utumishi kwa Yehova uwe jambo kuu iwezekanavyo maishani mwetu. Hivyo, tuliazimia kurahisisha maisha yetu. Tulimwomba Yehova atupe hekima ili tufikie mradi wetu na tukaweka tarehe hususa tuliyotaka kuanza kumtumikia Yehova kwa kadiri kubwa zaidi.”

Paula anasema hivi: “Nilifanya kazi siku tatu kwa juma nikiwa mwandishi katika hospitali fulani nami nilipokea mshahara mzuri. Pia nilikuwa painia wa kawaida. Hata hivyo, kama Marc, mimi pia nilitaka kumtumikia Yehova mahali popote penye uhitaji mkubwa zaidi wa watangazaji wa Ufalme. Lakini, nilipopeleka ombi langu la kujiuzulu, msimamizi wangu alisema ninastahili kuwa katibu mkuu, nafasi iliyokuwa tu imetokea. Hicho kilikuwa cheo chenye mshahara mkubwa zaidi cha katibu katika hospitali hiyo, lakini nilishikamana na uamuzi wangu wa kujiuzulu. Nilipomweleza msimamizi huyo kwa nini ninakataa cheo hicho, alinipongeza kwa sababu ya imani yangu.”

Muda mfupi baadaye, Marc na Paula walipokea mgawo wa kutumika wakiwa mapainia wa pekee katika kutaniko dogo katika eneo la mbali huko Kanada. Walipata matokeo gani kwa kuhamia eneo hilo? Marc anasema: “Nilikuwa na wasiwasi baada ya kuacha kazi yenye kutegemeka ambayo nilikuwa nimefanya karibu nusu ya maisha yangu, lakini Yehova alibariki huduma yetu. Tuna shangwe kubwa sana inayotokana na kuwapa wengine zawadi za kiroho. Pia, utumishi wa wakati wote umeboresha ndoa yetu. Mazungumzo yetu yanahusu mambo yaliyo ya maana kikweli, mambo ya kiroho. Tunajihisi tukiwa karibu zaidi na Yehova kuliko zamani.” (Mdo. 20:35) Paula anaongezea: “Unapoacha kazi yako na starehe za nyumbani, unalazimika kumtegemea Yehova kabisa. Tulifanya hivyo, na Yehova akatubariki. Ndugu na dada wapendwa katika kutaniko letu jipya wanatufanya tuhisi tunapendwa na kuhitajiwa. Sasa ninatumia nguvu nilizokuwa nikitumia kazini kuwasaidia watu kiroho. Ninashangilia sana kutumika katika mgawo huu.”

‘Nilifanikiwa, Lakini Sikuwa na Furaha’

Amy, aliyetajwa mwanzoni, alichagua njia tofauti. Alikubali kazi ya wakati wote yenye mshahara mnono. Amy anasema: “Mwaka wa kwanza, nilikuwa mwenye bidii katika huduma, lakini pole kwa pole niliacha kukazia fikira kazi ya Ufalme na badala yake nikaanza kufikiria kuwa na cheo kikubwa kazini. Nilipata nafasi za kupandishwa cheo nami nikaanza kutumia nguvu zangu ili kupanda ngazi kazini. Kadiri madaraka yangu yalivyoongezeka kazini, ndivyo nilivyotumia wakati mchache zaidi na zaidi katika huduma. Mwishowe, niliacha kabisa kuhubiri.”

Akitazama nyuma, Amy anasema: “Nilifanikiwa kiuchumi. Nilisafiri sana nami nilifurahia umashuhuri niliopata kutokana na cheo changu kazini. Lakini sikuwa na furaha. Ingawa nilikuwa na pesa, nilikuwa na matatizo mengi. Nilijiuliza nina shida gani. Mwishowe, nilitambua kwamba kwa kufuatia cheo katika ulimwengu huu, nilikuwa karibu ‘kupotoshwa kutoka kwenye imani.’ Matokeo yalikuwa sawa na yale yanayosemwa na Neno la Mungu, nilikuwa nikijichoma kwa ‘maumivu mengi.’”—1 Tim. 6:10.

Amy alichukua hatua gani? Anasema: “Niliwaomba wazee wanisaidie kuwa tena na afya nzuri kiroho na nikaanza kuhudhuria mikutano. Wimbo fulani ulipokuwa ukiimbwa, nilianza kulia. Nilikumbuka furaha niliyokuwa nayo miaka mitano niliyoshiriki katika kazi ya mavuno nikiwa painia, ingawa nilikuwa maskini. Nilijua ninapaswa kuacha kupoteza wakati wangu kutafuta pesa na kuanza kutanguliza kazi ya Ufalme. Niliamua kushuka cheo kazini, na hivyo kupoteza nusu ya mshahara wangu, nami nikaanza tena kushiriki katika kazi ya kuhubiri.” Amy anasema hivi kwa furaha: “Nilipata shangwe ya kuwa painia kwa miaka michache. Sasa ninahisi nimetimiza jambo fulani, hisia ambayo sikuwahi kuwa nayo nilipotumia wakati mwingi kuutumikia ulimwengu.”

Je, unaweza kurekebisha hali zako na kurahisisha mtindo wako wa maisha? Ukitumia wakati utakaopata kuendeleza kazi ya Ufalme, wewe pia utaboresha maisha yako.—Met. 10:22.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Ona Insight on the Scriptures, Buku la 2, ukurasa wa 1207-1208 au Étude perspicace des Écritures, Buku la 2, ukurasa wa 318-319.

[Blabu katika ukurasa wa 19]

Je, unaweza kurekebisha hali zako na kurahisisha mtindo wako wa maisha?

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 19]

“Tayari Ninaufurahia!”

David, mzee Mkristo huko Marekani, alitamani kujiunga na mke na watoto wake katika utumishi wa wakati wote. Alipanga ili afanye kazi ya muda katika kampuni iliyokuwa imemwajiri kazi, naye akawa painia wa kawaida. Je, badiliko hilo liliboresha maisha yake? Miezi kadhaa baadaye, David alimwandikia hivi rafiki yake: “Hakuna jambo linalomridhisha mtu kuliko kumtumikia Yehova kikamili pamoja na familia yake. Kwa kweli, nilifikiri ingechukua wakati fulani kuzoea upainia, lakini tayari ninaufurahia! Unaburudisha sana.”

[Picha katika ukurasa wa 18]

Marc na Paula katika huduma