Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wamehesabiwa Kuwa Wanastahili Kuongozwa Kwenye Chemchemi za Maji ya Uzima

Wamehesabiwa Kuwa Wanastahili Kuongozwa Kwenye Chemchemi za Maji ya Uzima

Wamehesabiwa Kuwa Wanastahili Kuongozwa Kwenye Chemchemi za Maji ya Uzima

“Mwana-Kondoo . . . atawachunga, na kuwaongoza kwenye chemchemi za maji ya uzima.”—UFU. 7:17.

1. Neno la Mungu linawatambulisha Wakristo watiwa-mafuta jinsi gani, na Yesu aliwapa daraka gani?

NENO LA MUNGU linawatambulisha Wakristo watiwa-mafuta ambao wanasimamia mambo ya kidunia ya Kristo kuwa “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” Kristo alipomkagua “mtumwa” huyo mwaka wa 1918, aliwakuta watiwa-mafuta hao duniani wakiendelea kwa uaminifu kutoa ‘chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa.’ Hivyo, baada ya hapo, Yesu, yule Bwana, alifurahi kuwaweka rasmi “juu ya mali zake zote.” (Soma Mathayo 24:45-47.) Katika njia hiyo, kabla ya kupokea urithi wao wa kimbingu, watiwa-mafuta wanatumikia waabudu wengine wa Yehova hapa duniani.

2. Mali za Yesu ni nini?

2 Bwana ana mamlaka juu ya mali zake, na anaweza kuzitumia kama anavyopenda. Mali za Yesu Kristo, Mfalme aliyewekwa na Yehova kwenye kiti cha ufalme, zinatia ndani mambo yote yanayohusu Ufalme duniani. Mali hizo zinatia ndani “umati mkubwa” ambao mtume Yohana aliona katika maono. Yohana anasema hivi kuhusu umati huo mkubwa: “Tazama! umati mkubwa, ambao hakuna mtu aliyeweza kuuhesabu, kutoka mataifa yote na makabila na vikundi vya watu na lugha, wamesimama mbele ya kiti cha ufalme na mbele ya Mwana-Kondoo, wamevikwa kanzu nyeupe; na kulikuwa na matawi ya mitende mikononi mwao.”—Ufu. 7:9.

3, 4. Washiriki wa umati mkubwa wana mapendeleo gani makubwa?

3 Washiriki wa umati mkubwa wako kati ya wale ambao Yesu anawaita “kondoo wengine.” (Yoh. 10:16) Tumaini lao ni kuishi milele katika paradiso duniani. Wana hakika kwamba Yesu ‘atawaongoza kwenye chemchemi za maji ya uzima,’ na kwamba Mungu “atafuta kila chozi katika macho yao.” Kwa sababu ya tumaini hilo, “wamefua kanzu zao na kuzifanya nyeupe katika damu ya Mwana-Kondoo.” (Ufu. 7:14, 17) Wana imani katika dhabihu ya Yesu, na hivyo machoni pa Mungu wana ‘kanzu nyeupe.’ Wanatangazwa kuwa waadilifu wakiwa marafiki wa Mungu, kama Abrahamu.

4 Zaidi ya hayo, kwa kuwa washiriki wa umati mkubwa unaoongezeka wa kondoo wengine wanaonwa na Mungu kuwa waadilifu, wanaweza kutumaini kuokoka uharibifu wa mfumo huu wa mambo wakati wa ile dhiki kuu. (Yak. 2:23-26) Wanaweza kumkaribia Yehova, na wakiwa kikundi, wana tumaini zuri ajabu la kuokoka Har–Magedoni. (Yak. 4:8; Ufu. 7:15) Hawajitegemei lakini wanafanya kazi kwa kupenda chini ya mwongozo wa yule Mfalme wa kimbingu na wa ndugu zake watiwa-mafuta walio duniani.

5. Umati mkubwa unawategemeza kwa njia gani ndugu watiwa-mafuta wa Kristo?

5 Wakristo watiwa-mafuta wamekabili na wataendelea kukabili upinzani mkali kutoka kwa ulimwengu wa Shetani. Hata hivyo, wanaweza kutegemea msaada wa waandamani wao wa umati mkubwa. Ingawa sasa hesabu ya Wakristo watiwa-mafuta ni ndogo, umati mkubwa unazidi kuongezeka kwa mamia ya maelfu kila mwaka. Watiwa-mafuta hawawezi kusimamia kibinafsi kila moja ya makutaniko ya Kikristo 100,000 ulimwenguni pote. Hivyo, moja ya njia ambazo kondoo wengine wanawategemeza watiwa-mafuta ni kwamba wanaume wa umati mkubwa walio na sifa za kustahili wanatumika wakiwa wazee wa kutaniko. Wanasaidia kutunza mamilioni ya Wakristo ambao sasa wamekabidhiwa kwa “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.”

6. Msaada ambao kondoo wengine wanawapa Wakristo watiwa-mafuta ulitabiriwa jinsi gani?

6 Msaada ambao kondoo wengine wanawapa kwa kupenda waandamani wao Wakristo watiwa-mafuta, ulitabiriwa na nabii Isaya. Aliandika hivi: “Yehova amesema hivi: ‘Wafanyakazi wa Misri wasiolipwa na wanabiashara wa Ethiopia na Wasabea, watu warefu, watakujia wewe, nao watakuwa wako. Watatembea nyuma yako.’” (Isa. 45:14) Katika maana ya mfano, Wakristo walio na tumaini la kidunia wanatembea nyuma ya jamii iliyotiwa mafuta ya mtumwa na Baraza lake Linaloongoza, nao wanafuata mwongozo wao. Wakiwa ‘wafanyakazi wasiolipwa,’ kondoo wengine wanatumia nguvu na mali zao kwa kupenda na kwa moyo wote ili kutegemeza kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote, kazi ambayo Kristo aliwapa wafuasi wake watiwa-mafuta walio duniani.—Mdo. 1:8; Ufu. 12:17.

7. Umati mkubwa unazoezwa kwa ajili ya mapendeleo gani?

7 Wanapowategemeza ndugu zao watiwa-mafuta, washiriki wa umati mkubwa wanazoezwa wakiwa msingi wa jamii mpya ya wanadamu, ambayo itaendelea kuishi duniani baada ya Har–Magedoni. Ni lazima msingi huo uwe thabiti na imara, na ni lazima washiriki wake wafuate kwa kupenda mwongozo wa Bwana. Kila Mkristo anapewa nafasi ya kuonyesha kwamba anaweza kutumiwa na Mfalme, Kristo Yesu. Kwa kuwa na imani na kuonyesha ushikamanifu sasa, Mkristo huyo anaonyesha kwamba atafuata bila kusita miongozo ambayo huyo Mfalme atampa katika ulimwengu mpya.

Umati Mkubwa Unathibitisha Imani Yao

8, 9. Washiriki wa umati mkubwa wanathibitisha imani yao kwa njia gani?

8 Kondoo wengine ambao ni waandamani wa kutaniko la Wakristo watiwa-mafuta wanathibitisha imani yao katika njia mbalimbali. Kwanza, wanawategemeza watiwa-mafuta katika kutangaza habari njema ya Ufalme wa Mungu. (Mt. 24:14; 28:19, 20) Pili, wanafuata kwa kupenda mwongozo unaotolewa na Baraza Linaloongoza.—Ebr. 13:17; soma Zekaria 8:23.

9 Tatu, washiriki wa umati mkubwa wanawategemeza ndugu zao watiwa-mafuta kwa kuishi kulingana na kanuni za uadilifu za Yehova. Wanajitahidi kusitawisha “upendo, shangwe, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujizuia.” (Gal. 5:22, 23) Leo, huenda wengi wakafurahia “matendo ya mwili,” kuliko kuonyesha sifa hizo. Hata hivyo, washiriki wa umati mkubwa wameazimia kuepuka “uasherati, uchafu, mwenendo mpotovu, ibada ya sanamu, mazoea ya kuwasiliana na pepo, uadui, mizozo, wivu, milipuko ya hasira, magomvi, migawanyiko, madhehebu, husuda, vipindi vya kulewa, karamu za kupindukia, na mambo kama hayo.”—Gal. 5:19-21.

10. Washiriki wa umati mkubwa wameazimia kufanya nini?

10 Kwa kuwa sisi si wakamilifu, inaweza kuwa vigumu kusitawisha matunda ya roho, kuepuka matendo ya mwili, na kushinda uvutano wa ulimwengu wa Shetani. Hata hivyo, tumeazimia kutoruhusu kuvunjika moyo kwa sababu ya udhaifu wetu, makosa yetu, au kupungukiwa kimwili kudhoofishe imani yetu au kupunguze upendo wetu kwa Yehova. Tunajua kwamba Yehova atatimiza ahadi yake ya kuulinda hai umati mkubwa na kuuokoa kutoka katika ile dhiki kuu.

11. Ni mbinu gani ambazo Shetani ametumia katika jitihada zake za kudhoofisha imani ya Wakristo?

11 Hata hivyo, tunajihadhari sikuzote kwa sababu tunajua kwamba adui yetu hasa ni Ibilisi, na hashindwi kwa urahisi. (Soma 1  Petro 5:8.) Amejaribu kutumia waasi-imani na watu wengine kutusadikisha kwamba mafundisho tunayofuata ni ya uwongo. Lakini kwa kawaida mbinu hiyo imeshindwa. Vivyo hivyo, ingawa nyakati nyingine mateso yamezuia kazi ya kuhubiri kwa kadiri fulani, mara nyingi yamesaidia tu kutia nguvu imani ya wale wanaoteswa. Hivyo, Shetani anazidi kutumia mbinu ambayo inaelekea anaamini itafaulu zaidi kudhoofisha imani yetu. Shetani anatumia hisia za kuvunjika moyo. Wakristo wa karne ya kwanza walionywa kuhusu hatari hiyo walipoambiwa hivi: “Mfikirieni sana [Kristo] yeye ambaye amevumilia maneno ya aina hii yenye kupinga yanayotolewa na watenda-dhambi kinyume cha faida zao wenyewe.” Kwa nini? “Ili ninyi msichoke na kuzimia katika nafsi zenu.”—Ebr. 12:3.

12. Mashauri ya Biblia yanawatia nguvu jinsi gani wale wanaovunjika moyo?

12 Je, umewahi kufikiria kuacha kumtumikia Yehova? Je, nyakati nyingine unahisi kwamba umeshindwa? Ikiwa ndivyo, usimruhusu Shetani atumie hisia hizo kukuzuia usimtumikie Yehova. Kujifunza Biblia kwa undani, kusali kwa bidii, na kuhudhuria mikutano kwa ukawaida na kushirikiana na Wakristo wenzako, kutakutia nguvu na kukulinda ‘usizimie katika nafsi yako.’ Yehova ameahidi kuwapa nguvu mpya wale wanaomtumikia, na ahadi yake ni hakika. (Soma Isaya 40:30, 31.) Kazia macho yako kwenye utumishi wa Ufalme. Epuka vikengeusha-fikira vinavyochukua wakati mwingi, na ujitahidi kuwasaidia wengine. Ukifanya hivyo, utapata nguvu za kuvumilia hata unapovunjika moyo.—Gal. 6:1, 2.

Kuokoka Ile Dhiki na Kuingia Katika Ulimwengu Mpya

13. Ni kazi gani inayowangojea wale watakaookoka Har–Magedoni?

13 Baada ya Har–Magedoni, watu wengi wasio waadilifu ambao watafufuliwa watahitaji kufundishwa njia za Yehova. (Mdo. 24:15) Watahitaji kufundishwa kuhusu dhabihu ya fidia ya Yesu; zaidi ya hayo, ni lazima wafundishwe kuwa na imani katika dhabihu hiyo ili iwafaidi. Watahitaji kukataa mawazo yao ya zamani ya dini za uwongo na kuacha mwenendo wao wa zamani. Watalazimika kujifunza kuvaa utu mpya ambao unawatambulisha Wakristo wa kweli. (Efe. 4:22-24; Kol. 3:9, 10) Kondoo wengine ambao wataokoka Har–Magedoni watakuwa na kazi nyingi sana. Itakuwa shangwe kama nini kumtumikia Yehova bila uvutano na vikengeusha-fikira vya ulimwengu huu mbovu!

14, 15. Eleza jinsi mazungumzo yatakavyokuwa kati ya waokokaji wa ile dhiki kuu na waadilifu watakaofufuliwa.

14 Watumishi waaminifu wa Yehova waliokufa kabla ya huduma ya Yesu ya kidunia, watakuwa pia na mengi ya kujifunza wakati huo. Watajifunza Masihi aliyeahidiwa ni nani, yule ambaye walimtumaini lakini hawakuwahi kamwe kumwona. Walipokuwa hai, walionyesha kwamba walikuwa tayari kufundishwa na Yehova. Fikiria itakuwa shangwe na pendeleo kama nini—kwa mfano, kuwasaidia kumweleza Danieli utimizo wa unabii mbalimbali alioandika lakini ambao hakuelewa!—Dan. 12:8, 9.

15 Bila shaka, ingawa watakaofufuliwa watakuwa na mengi ya kujifunza kutoka kwetu, sisi pia tutakuwa na maswali mengi ya kuwauliza. Watatueleza mambo mengi kuhusu matukio yanayotajwa katika Biblia lakini ambayo hayaelezwi kwa undani. Fikiria jinsi itakavyosisimua kujifunza mambo madogo-madogo ya kibinafsi kumhusu Yesu kutoka kwa binamu yake Yohana Mbatizaji! Bila shaka, mambo tutakayojifunza kutoka kwa mashahidi hao waaminifu yatatusaidia kuelewa hata zaidi Neno la Mungu kuliko tunavyolielewa sasa. Watumishi waaminifu wa Yehova waliokufa, kutia ndani wale wa umati mkubwa ambao walikufa wakati wa mwisho, watapokea “ufufuo ulio bora.” Walianza kumtumikia Yehova katika ulimwengu uliotawaliwa na Shetani. Itakuwa shangwe kama nini kwao kuendelea na utumishi wao katika mazingira mazuri zaidi ya ulimwengu mpya!—Ebr. 11:35; 1 Yoh. 5:19.

16. Kulingana na unabii, Siku ya Hukumu itakuwa namna gani?

16 Wakati fulani katika Siku ya Hukumu, vitabu vya kukunjwa vitafunguliwa. Vitabu hivyo pamoja na Biblia, ndivyo vitakavyotumiwa kama msingi wa kuwahukumu wote walio hai ili kujua ikiwa wanastahili kupata uzima wa milele. (Soma Ufunuo 20:12, 13.) Mwishoni mwa Siku ya Hukumu, kila mtu atakuwa amepewa nafasi ya kutosha kuonyesha anaunga mkono upande gani wa lile suala la enzi kuu ya ulimwengu wote. Je, ataunga mkono mpango wa Ufalme na kumruhusu Mwana-Kondoo amwongoze kwenye “chemchemi za maji ya uzima”? Au atapinga na kukataa kujitiisha chini ya Ufalme wa Mungu? (Ufu. 7:17; Isa. 65:20) Kufikia wakati huo, watu wote wanaoishi duniani watakuwa na nafasi ya kufanya uamuzi wa kibinafsi, bila kuzuiwa na dhambi iliyorithiwa au mazingira yenye uovu. Hakuna mtu atakayeweza kutilia shaka haki ya hukumu ya mwisho ya Yehova. Waovu tu ndio watakaoharibiwa milele.—Ufu. 20:14, 15.

17, 18. Wakristo watiwa-mafuta na kondoo wengine wanatazamia nini kwa shangwe wakati wa Siku ya Hukumu?

17 Leo, tayari Wakristo watiwa-mafuta wamehesabiwa kuwa wanastahili kuupokea Ufalme, na hivyo wanangojea kwa hamu kutawala wakati wa Siku ya Hukumu. Watakuwa na pendeleo kubwa kama nini! Tumaini hilo linawachochea kufuata shauri ambalo Petro aliwapa ndugu zake wa karne ya kwanza: “Fanyeni hata zaidi yote mnayoweza ili kufanya mwito na kuchaguliwa kwenu kuwe hakika kwa ajili yenu wenyewe; kwa maana mkiendelea kufanya mambo hayo hamtashindwa hata kidogo. Kwa kweli, hivyo ndivyo mtakavyowezeshwa kwa wingi kuingia katika ufalme wa milele wa Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo.”—2 Pet. 1:10, 11.

18 Kondoo wengine wanashangilia pamoja na ndugu zao watiwa-mafuta. Wameazimia kuwategemeza. Wakiwa marafiki wa Mungu, wanachochewa kufanya yote wanayoweza katika utumishi wa Mungu. Wakati wa Siku ya Hukumu, watafurahi kutegemeza kwa moyo wote mipango ya Mungu wakati Yesu anapowaongoza kwenye chemchemi za maji ya uzima. Kisha, watahesabiwa mwishowe kwamba wanastahili kuwa watumishi wa kidunia wa Yehova kwa umilele wote!—Rom. 8:20, 21; Ufu. 21:1-7.

Je, Unakumbuka?

• Mali za Yesu zinatia ndani nini?

• Washiriki wa umati mkubwa wanawategemeza kwa njia gani ndugu zao watiwa-mafuta?

• Ni mapendeleo na tumaini gani ambalo washiriki wa umati mkubwa wanafurahia?

• Una maoni gani kuhusu Siku ya Hukumu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 25]

Wale wa umati mkubwa wamefua kanzu zao na kuzifanya nyeupe katika damu ya Mwana-Kondoo

[Picha katika ukurasa wa 27]

Unatazamia kujifunza nini kutoka kwa waaminifu watakaofufuliwa?