Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wamehesabiwa Kuwa Wanastahili Kuupokea Ufalme

Wamehesabiwa Kuwa Wanastahili Kuupokea Ufalme

Wamehesabiwa Kuwa Wanastahili Kuupokea Ufalme

“Huo ni uthibitisho wa hukumu ya uadilifu ya Mungu, inayowaongoza ninyi kwenye hali ya kuhesabiwa kuwa mnastahili ufalme wa Mungu.”—2 THE. 1:5.

1, 2. Kusudi la Mungu ni nini kuhusiana na hukumu, na ni nani atakayetekeleza hukumu hiyo?

KATIKA mwaka wa 50 hivi Wakati Wetu wa Kawaida, mtume Paulo alikuwa huko Athene. Akiwa amekasirishwa na ibada ya sanamu iliyoenea, alichochewa kutoa ushahidi mzuri sana. Alimalizia hotuba yake kwa maneno yaliyovuta uangalifu wa wasikilizaji wake wapagani. Alisema hivi: “Sasa [Mungu] anawaambia wanadamu wote kila mahali kwamba wanapaswa kutubu. Kwa sababu ameweka siku ambayo katika hiyo anakusudia kuihukumu kwa uadilifu dunia inayokaliwa kupitia kwa mwanamume ambaye amemweka rasmi, naye ametoa uhakikisho kamili kwa watu wote kwa kuwa amemfufua kutoka kwa wafu.”—Mdo. 17:30, 31.

2 Ni jambo zito kama nini kutafakari juu ya uhakika wa kwamba Mungu ameweka siku atakayowahukumu wanadamu! Hukumu hiyo itatekelezwa na yule ambaye Paulo hakumtaja jina katika hotuba yake huko Athene. Hata hivyo, tunajua kwamba mtu huyo ni Yesu Kristo aliyefufuliwa. Kuhukumiwa na Yesu kutamaanisha ama uzima au kifo.

3. Kwa nini Yehova alifanya agano na Abrahamu, na ni nani aliye na sehemu ya pekee katika kutimizwa kwa agano hilo?

3 Siku ya Hukumu itakuwa na urefu wa miaka 1,000. Yesu ndiye atakayesimamia siku hiyo ya hukumu kwa jina la Yehova akiwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu, lakini hatakuwa peke yake. Yehova anachagua wengine kutoka kati ya wanadamu ili watawale pamoja na Yesu na kuhukumu wakati wa siku hiyo ya miaka 1,000. (Linganisha Luka 22:29, 30.) Karibu miaka 4,000 iliyopita, Yehova aliweka msingi kwa ajili ya Siku hiyo ya Hukumu alipofanya agano pamoja na mtumishi wake mwaminifu Abrahamu. (Soma Mwanzo 22:17, 18.) Kwa wazi, agano hilo lilianza kufanya kazi mwaka wa 1943 K.W.K. Bila shaka, Abrahamu hakuelewa kikamili kile ambacho agano hilo lingemaanisha kwa wanadamu. Hata hivyo, leo tunaweza kuona kupatana na masharti ya agano hilo kwamba uzao wa Abrahamu una sehemu ya pekee katika kutimizwa kwa kusudi la Mungu la kuwahukumu wanadamu.

4, 5. (a) Ni nani aliye sehemu ya msingi ya uzao wa Abrahamu, na alisema nini kuhusu Ufalme? (b) Tumaini la kushiriki katika Ufalme lilitolewa wakati gani?

4 Yesu ndiye sehemu ya msingi ya uzao wa Abrahamu. Katika mwaka wa 29 W.K. alitiwa mafuta kwa roho takatifu na hivyo akawa Masihi aliyeahidiwa, au Kristo. (Gal. 3:16) Yesu angetumia miaka mitatu na nusu iliyofuata akihubiri habari njema ya Ufalme kwa taifa la Wayahudi. Baada ya kukamatwa kwa Yohana Mbatizaji, Yesu alionyesha kwamba wengine wangekuwa na tumaini la kushiriki katika Ufalme huo aliposema hivi: “Tangu siku za Yohana Mbatizaji mpaka sasa ufalme wa mbinguni ndio mradi ambao watu wanajikaza kuufikia, na wale wanaojikaza wanaufikia.”—Mt. 11:12.

5 Inapendeza kwamba kabla tu ya kusema kuhusu wale ambao ‘wangeufikia’ Ufalme wa mbinguni, Yesu alisema hivi: “Kwa kweli nawaambia ninyi, Kati ya wale waliozaliwa na wanawake hajatokea mkuu kuliko Yohana Mbatizaji; lakini mtu aliye mdogo zaidi katika ufalme wa mbinguni ni mkuu kuliko yeye.” (Mt. 11:11) Kwa nini ilikuwa hivyo? Kwa sababu tumaini la kushiriki katika mpango wa Ufalme halikuwa limetolewa kikamili kwa waaminifu mpaka roho takatifu ilipomiminwa katika Pentekoste ya 33 W.K. Kufikia wakati huo, Yohana Mbatizaji alikuwa tayari amekufa.—Mdo. 2:1-4.

Uzao wa Abrahamu Unatangazwa Kuwa Mwadilifu

6, 7. (a) Uzao wa Abrahamu ungekuwa “kama nyota za mbinguni” katika njia gani? (b) Abrahamu alipokea baraka gani, nao uzao wake unapokea baraka gani inayofanana na hiyo?

6 Abrahamu aliambiwa kwamba uzao wake ungeongezeka na kuwa “kama nyota za mbinguni” na chembe za mchanga zilizo kando ya bahari. (Mwa. 13:16; 22:17) Kwa maneno mengine, katika siku za Abrahamu wanadamu hawangeweza kujua hesabu ya wale ambao wangefanyiza uzao huo. Hata hivyo, mwishowe hesabu kamili ya uzao wake wa kiroho ilifunuliwa. Mbali na Yesu, hesabu yao ingekuwa 144,000.—Ufunuo 7:4; 14:1.

7 Kuhusu imani ya Abrahamu, Neno la Mungu linasema hivi: “[Abrahamu] akawa na imani katika Yehova; naye akamhesabia kuwa ni uadilifu.” (Mwa. 15:5, 6) Ni kweli kwamba hakuna mwanadamu aliye mwadilifu kabisa. (Yak. 3:2) Hata hivyo, kwa sababu ya imani ya pekee ya Abrahamu, Yehova alishughulika naye kana kwamba alikuwa mwadilifu na hata alimwita rafiki yake. (Isa. 41:8) Wale ambao pamoja na Yesu wanafanyiza uzao wa kiroho wa Abrahamu, wamehesabiwa pia kuwa waadilifu, na hilo linawaletea baraka nyingi zaidi hata kuliko zile alizopokea Abrahamu.

8. Ni baraka gani zinazotolewa kwa washiriki wa uzao wa Abrahamu?

8 Wakristo watiwa-mafuta wanahesabiwa kuwa waadilifu kwa sababu wana imani katika dhabihu ya fidia ya Yesu. (Rom. 3:24, 28) Machoni pa Yehova, wameondolewa hatia ya dhambi na wanaweza kutiwa mafuta kwa roho takatifu na kuwa wana wa kiroho wa Mungu, ndugu za Yesu Kristo. (Yoh. 1:12, 13) Wanaingizwa katika agano jipya na wanafanyiza taifa jipya, “Israeli wa Mungu.” (Gal. 6:16; Luka 22:20) Hilo ni pendeleo kubwa kama nini! Kwa sababu ya mambo yote hayo ambayo Mungu anawatendea, Wakristo watiwa-mafuta hawatumaini kuishi milele duniani. Wanadhabihu tumaini hilo kwa ajili ya shangwe isiyoelezeka ya kushirikiana na Yesu wakati wa Siku ya Hukumu na kutawala pamoja naye huko mbinguni.—Soma Waroma 8:17.

9, 10. (a) Wakristo walitiwa mafuta kwa roho takatifu mara ya kwanza wakati gani, na walitazamia mambo gani? (b) Wakristo watiwa-mafuta walipokea msaada gani?

9 Katika Pentekoste ya 33 W.K., kikundi cha wanadamu waaminifu kilipewa pendeleo la kuwa kati ya wale ambao wangetawala pamoja na Yesu wakati wa Siku ya Hukumu. Wanafunzi 120 hivi wa Yesu walibatizwa kwa roho takatifu na hivyo wakawa Wakristo wa kwanza watiwa-mafuta. Hata hivyo, huo ulikuwa mwanzo tu kwa Wakristo hao. Tangu hapo na kuendelea, walipaswa kuonyesha ushikamanifu wao kwa Yehova hata ingawa Shetani angewaletea majaribu mengi. Walipaswa kuendelea kuwa waaminifu mpaka kifo ili wapokee taji la uhai wa kimbingu.—Ufu. 2:10.

10 Ili kuwasaidia waendelee kuwa waaminifu, Yehova kupitia Neno lake na kutaniko la Kikristo aliwapa Wakristo watiwa-mafuta himizo na kitia-moyo ambacho walihitaji. Kwa mfano, mtume Paulo aliwaandikia hivi Wakristo watiwa-mafuta huko Thesalonike: ‘Kama baba anavyowatendea watoto wake, tuliendelea kumhimiza kila mmoja wenu, na kuwafariji na kuwatolea ninyi ushahidi, ili kwamba mwendelee kutembea kwa kumstahili Mungu anayewaita ninyi kwenye ufalme na utukufu wake.’—1 The. 2:11, 12.

11. Ni rekodi gani iliyoandikwa ambayo Yehova aliwapa “Israeli wa Mungu”?

11 Miaka mingi baada ya washiriki wa kwanza wa kutaniko la Wakristo watiwa-mafuta kuchaguliwa, Yehova aliona vema kuweka rekodi ya kudumu ya huduma ya Yesu ya kidunia na shughuli Zake na mashauri Yake kwa Wakristo watiwa-mafuta wa karne ya kwanza. Hivyo, zaidi ya Maandiko ya Kiebrania yaliyoongozwa na roho, Yehova aliongeza Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo ambayo pia yaliongozwa na roho. Maandiko ya Kiebrania yaliandikwa kwanza kwa ajili ya taifa la asili la Israeli wakati lilipokuwa na uhusiano wa pekee pamoja na Mungu. Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yaliandikwa hasa kwa ajili ya “Israeli wa Mungu,” wale watiwa-mafuta ambao ni ndugu za Kristo na wana wa kiroho wa Mungu. Bila shaka, watu wasio Waisraeli wangefaidika sana kwa kujifunza Maandiko ya Kiebrania. Vivyo hivyo, Wakristo wasiotiwa mafuta kwa roho takatifu wanafaidika sana kwa kujifunza na kuishi kulingana na mashauri yaliyo katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo.—Soma 2 Timotheo 3:15-17.

12. Paulo aliwakumbusha nini Wakristo watiwa-mafuta?

12 Wakristo wa karne ya kwanza walitangazwa kuwa waadilifu na kutiwa mafuta kwa roho takatifu ili waweze kupokea urithi wao wa kimbingu. Kutiwa mafuta hakukuwafanya wawe wafalme juu ya Wakristo wenzao watiwa-mafuta wakiwa bado duniani. Kwa wazi, Wakristo fulani wa mapema walisahau uhakika huo nao wakaanza kutafuta isivyo lazima umashuhuri kati ya ndugu zao katika kutaniko. Kwa sababu hiyo, Paulo alichochewa kuuliza hivi: “Ninyi tayari mmepata shibe yenu, sivyo? Ninyi tayari ni matajiri, sivyo? Mmeanza kutawala mkiwa wafalme bila sisi, sivyo? Nami ningalipenda kwamba muwe mmeanza kutawala mkiwa wafalme, ili sisi pia tutawale pamoja nanyi tukiwa wafalme.” (1 Kor. 4:8) Kwa hiyo, Paulo aliwakumbusha hivi watiwa-mafuta wa siku zake: “Si kwamba sisi ndio mabwana juu ya imani yenu, bali sisi ni wafanyakazi wenzi kwa shangwe yenu.”—2 Kor. 1:24.

Kukamilisha Hesabu Iliyotabiriwa

13. Mwito wa watiwa-mafuta uliendelea namna gani baada ya mwaka wa 33 W.K.?

13 Wakristo watiwa-mafuta 144,000 hawakuchaguliwa wote katika karne ya kwanza. Mwito wao uliendelea katika kipindi chote cha mitume na inaelekea kwamba katika karne zilizofuata ni wachache tu waliochaguliwa. Hata hivyo, kuchaguliwa huko kumeendelea kwa karne nyingi mpaka nyakati za kisasa. (Mt. 28:20) Mwishowe, baada ya Yesu kuanza kutawala mwaka wa 1914, mambo yalisonga haraka.

14, 15. Ni jambo gani limetukia wakati wetu kuhusu mwito wa watiwa-mafuta?

14 Kwanza, Yesu alisafisha mbingu kwa kuondoa upinzani wote kuelekea utawala wa Mungu. (Soma Ufunuo 12:10, 12.) Kisha, akaelekeza fikira zake kwenye kazi ya kukusanya washiriki waliobaki wa serikali yake ya Ufalme ili kukamilisha hesabu ya wale 144,000. Katikati ya miaka ya 1930, ni wazi kwamba kazi hiyo ilikuwa karibu kukamilika na wengi wa wale waliokubali ujumbe wa Ufalme hawakuwa na tamaa ya kwenda mbinguni. Roho haikuwa ikishuhudia pamoja nao kwamba walikuwa wana wa Mungu. (Linganisha Waroma 8:16.) Badala yake, walijitambulisha wenyewe kuwa “kondoo wengine,” ambao wana tumaini la kuishi milele katika paradiso duniani. (Yoh. 10:16) Hivyo, baada ya mwaka wa 1935, kazi ya kuhubiri ilikazia hasa kukusanywa kwa “umati mkubwa,” wale ambao mtume Yohana aliona katika maono na ambao wangeokoka “ile dhiki kuu.”—Ufu. 7:9, 10, 14.

15 Hata hivyo, kwa muda mrefu tangu miaka ya 1930, watu wachache tu ndio wamechaguliwa ili kuwa na tumaini la kimbingu. Kwa nini? Nyakati nyingine, inawezekana kwamba walichukua nafasi za watu waliochaguliwa zamani lakini ambao hawakuendelea kuwa waaminifu. (Linganisha Ufunuo 3:16.) Paulo alizungumza hata kuhusu watu fulani ambao aliwajua kibinafsi, na ambao waliacha kweli. (Flp. 3:17-19) Yehova angechagua nani ili kuchukua nafasi zao? Bila shaka, huo ni uamuzi wake. Hata hivyo, ni jambo linalopatana na akili kufikiri kwamba hangechagua waamini wapya, lakini angechagua watu ambao tayari wamethibitisha ushikamanifu wao kwa kadiri fulani, kama wale wanafunzi ambao Yesu alizungumza nao alipoanzisha mwadhimisho wa Ukumbusho. *Luka 22:28.

16. Kuhusu watiwa-mafuta, kwa nini sisi ni wenye shukrani, na tunaweza kuamini nini kwa uhakika?

16 Hata hivyo, inaonekana kwamba wengine kati ya wale walioitwa kwa ajili ya tumaini la kimbingu tangu miaka ya 1930 hawachukui nafasi za wale walioacha kweli. Ni wazi kwamba Yehova amehakikisha kutakuwa na Wakristo watiwa-mafuta kati yetu katika siku za mwisho za mfumo huu wa mambo mpaka wakati wa uharibifu wa “Babiloni Mkubwa.” * (Ufu. 17:5) Na tunaweza kuwa na hakika kwamba hesabu kamili ya washiriki 144,000 itakamilishwa kwa wakati uliowekwa na Yehova na kwamba mwishowe wote watachukua nafasi zao katika serikali ya Ufalme. Pia, tunaweza kuliamini Neno la kinabii linaloonyesha kwamba washiriki wa umati mkubwa ambao wanaendelea kuongezeka, wataendelea kujithibitisha kuwa waaminifu wakiwa kikundi. Hivi karibuni umati mkubwa ‘utatoka katika ile dhiki kuu’ itakayoletwa juu ya ulimwengu wa Shetani na kusonga mbele kwa shangwe kuingia katika ulimwengu mpya wa Mungu.

Serikali ya Mungu ya Kimbingu Inakaribia Kukamilika!

17. Kulingana na 1 Wathesalonike 4:15-17 na Ufunuo 6:9-11, Wakristo watiwa-mafuta ambao wamekufa wakiwa waaminifu wamepokea nini?

17 Tangu mwaka wa 33 W.K., makumi ya maelfu ya Wakristo watiwa-mafuta wameonyesha imani yenye nguvu na wamevumilia kwa uaminifu mpaka kifo. Wakristo hao tayari wamehesabiwa kuwa wanastahili kuupokea Ufalme, na ni wazi kwamba tangu mwanzoni mwa kuwapo kwa Kristo, wamekuwa wakipokea thawabu yao ya kimbingu.—Soma 1  Wathesalonike 4:15-17; Ufunuo 6:9-11.

18. (a) Watiwa-mafuta ambao wangali duniani wana uhakika gani? (b) Kondoo wengine wanawaona jinsi gani ndugu zao Wakristo watiwa-mafuta?

18 Watiwa-mafuta ambao wangali duniani wana hakika kabisa kwamba wakiendelea kuwa waaminifu, hivi karibuni wao pia watapokea thawabu yao ya kimbingu. Mamilioni ya kondoo wengine, wanapotafakari imani ya ndugu zao watiwa-mafuta, wanakubaliana na maneno haya ya mtume Paulo, ambaye alisema hivi kuhusu ndugu watiwa-mafuta wa Thesalonike: “Sisi wenyewe tunajivunia ninyi kati ya makutaniko ya Mungu kwa sababu ya uvumilivu wenu na imani katika mateso yenu yote na dhiki mnazovumilia. Huo ni uthibitisho wa hukumu ya uadilifu ya Mungu, inayowaongoza ninyi kwenye hali ya kuhesabiwa kuwa mnastahili ufalme wa Mungu, ambao mnateseka kwa ajili yake.” (2 The. 1:3-5) Mshiriki wa mwisho wa watiwa-mafuta atakapokufa na kutoka duniani, haidhuru hilo litatokea wakati gani, serikali ya Mungu ya kimbingu itakuwa imekamilika. Itakuwa shangwe kama nini mbinguni na duniani!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 15 Ona gazeti la Mnara wa Mlinzi la Machi 1, 1992 (1/3/1992), ukurasa wa 20, fungu la 17.

^ fu. 16 Ona “Maswali Kutoka kwa Wasomaji” katika Mnara wa Mlinzi la Mei 1, 2007 (1/5/2007).

Je, Unaweza Kueleza?

• Mungu alimfunulia Abrahamu jambo gani linalohusiana na Siku ya Hukumu?

• Kwa nini Abrahamu alitangazwa kuwa mwadilifu?

• Kutangazwa kuwa waadilifu kuna matokeo gani kwa wale ambao ni uzao wa Abrahamu?

• Wakristo wote wana uhakika gani?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 20]

Yesu aliwatia moyo wafuasi wake wajitahidi kuufikia Ufalme

[Picha katika ukurasa wa 21]

Katika Pentekoste ya 33 W.K., Yehova alianza kuchagua washiriki wa sehemu ya pili ya uzao wa Abrahamu

[Picha katika ukurasa wa 23]

Kondoo wengine wanashukuru kwamba Wakristo watiwa-mafuta wamekuwa pamoja nao katika siku hizi za mwisho