Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Watu Wenye “Mwelekeo Unaofaa” Wanaitikia

Watu Wenye “Mwelekeo Unaofaa” Wanaitikia

Watu Wenye “Mwelekeo Unaofaa” Wanaitikia

“Wale wote waliokuwa na mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uzima wa milele wakawa waamini.”—MDO. 13:48.

1, 2. Wakristo wa mapema walitii jinsi gani unabii wa Yesu wa kwamba habari njema ingehubiriwa katika dunia yote inayokaliwa?

KITABU cha Biblia cha Matendo kina masimulizi yenye kusisimua kuhusu jinsi Wakristo wa mapema walivyotii unabii wa Yesu wa kuhubiri habari njema ya Ufalme katika dunia yote inayokaliwa. (Mt. 24:14) Wahubiri hao wenye bidii waliwawekea kielelezo wote ambao wangekuja baadaye. Kwa sababu ya bidii ya kuhubiri ya wanafunzi wa Yesu huko Yerusalemu, maelfu ya watu, kutia ndani “umati mkubwa wa makuhani,” walijiunga na kutaniko la karne ya kwanza.—Mdo. 2:41; 4:4; 6:7.

2 Wamishonari wa mapema waliwasaidia wengine wengi kukubali Ukristo. Kwa mfano, Filipo alienda Samaria ambako umati ulimsikiliza. (Mdo. 8:5-8) Paulo alisafiri kotekote akiwa na watu mbalimbali ili kuhubiri ujumbe wa Kikristo huko Kipro, maeneo ya Asia Ndogo, Makedonia, Ugiriki, na Italia. Katika majiji ambako alihubiri, umati mkubwa wa Wayahudi na Wagiriki wakawa waamini. (Mdo. 14:1; 16:5; 17:4) Tito alitimiza huduma fulani huko Krete. (Tito 1:5) Petro alihubiri sana huko Babiloni, na kufikia wakati alipoandika barua yake ya kwanza, kati ya mwaka wa 62 na 64 W.K. hivi, kazi ya Wakristo ilijulikana sana huko Ponto, Galatia, Kapadokia, Asia, na Bithinia. (1 Pet. 1:1; 5:13) Zilikuwa nyakati zenye kusisimua kama nini! Wahubiri hao Wakristo wa karne ya kwanza walihubiri kwa bidii sana hivi kwamba maadui wao walidai kwamba walikuwa “wameipindua dunia inayokaliwa.”—Mdo. 17:6; 28:22.

3. Watangazaji wa Ufalme wanapata matokeo gani leo katika kazi yao ya kuhubiri, na matokeo hayo yanakufanya uhisi namna gani?

3 Leo pia, kutaniko la Kikristo limebarikiwa na ongezeko kubwa ajabu. Je, hutiwi moyo unaposoma ripoti ya kila mwaka ya Mashahidi wa Yehova na kuona matokeo yanayopatikana ulimwenguni pote? Je, huchangamki kujua kwamba watangazaji wa Ufalme waliongoza mafunzo ya Biblia zaidi ya milioni sita katika mwaka wa utumishi wa 2007? Kwa kuongezea, hudhurio la Ukumbusho wa kifo cha Yesu Kristo mwaka uliopita linaonyesha kwamba watu milioni kumi hivi ambao si Mashahidi wa Yehova walipendezwa sana na habari njema hivi kwamba walihudhuria mwadhimisho huo muhimu. Hilo linaonyesha kwamba bado kuna kazi nyingi ya kufanya.

4. Ni nani wanaoitikia ujumbe wa Ufalme?

4 Leo, kama ilivyokuwa katika karne ya kwanza, watu ‘wote wenye mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uzima wa milele’ wanaitikia ujumbe wa kweli. (Mdo. 13:48) Yehova anawavuta watu kama hao waje katika tengenezo lake. (Soma Hagai 2:7.) Tunahitaji kudumisha mtazamo gani kuelekea huduma ya Kikristo ili tushiriki kikamili katika kazi hii ya kuwakusanya watu?

Hubiri Bila Ubaguzi

5. Yehova anawakubali watu wa aina gani?

5 Wakristo wa karne ya kwanza walielewa kwamba “Mungu hana ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye anamwogopa na kutenda uadilifu anakubalika kwake.” (Mdo. 10:34, 35) Mtu hawezi kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Yehova asipokuwa na imani katika dhabihu ya fidia ya Yesu. (Yoh. 3:16, 36) Na ni mapenzi ya Yehova kwamba “watu wa namna zote waokolewe na kupata ujuzi sahihi wa kweli.”—1 Tim. 2:3, 4.

6. Wahubiri wa Ufalme hawapaswi kufanya nini, na kwa nini?

6 Haingefaa watangazaji wa habari njema wawabague watu kwa sababu ya kabila, cheo, sura, dini, au jambo lingine lolote. Tua kidogo na ufikirie jambo hili: Je, huthamini kwamba mtu ambaye alizungumza nawe kwa mara ya kwanza kuhusu kweli za Kimaandiko hakukubagua? Basi, kwa nini ukatae kumpa mtu yeyote ujumbe ambao unaweza kuokoa uhai wake ikiwa atausikiliza?—Soma Mathayo 7:12.

7. Kwa nini hatupaswi kuwahukumu wale tunaowahubiria?

7 Yehova amemweka rasmi Yesu awe Hakimu; kwa hivyo, hatuna haki ya kumhukumu mtu yeyote. Na hilo linafaa kwa sababu tofauti na Yesu, sisi tunaweza kuhukumu tu ‘kulingana na sura inayoonekana kwa macho yetu tu,’ au ‘kulingana tu na jambo lililosikiwa na masikio yetu,’ lakini Yesu anaweza kujua mawazo ya ndani na fikira za moyo.—Isa. 11:1-5; 2 Tim. 4:1.

8, 9. (a) Sauli alikuwa mtu wa aina gani kabla ya kuwa Mkristo? (b) Mfano wa mtume Paulo unapaswa kutufundisha nini?

8 Watu wa malezi mbalimbali wamekuwa watumishi wa Yehova. Mfano mmoja unaojulikana sana ni Sauli wa Tarso, ambaye baadaye aliitwa mtume Paulo. Sauli, ambaye alikuwa Farisayo, aliwapinga vikali Wakristo. Alilitesa kutaniko la Kikristo kwa sababu aliamini kabisa kwamba hawakuwa waabudu wa kweli. (Gal. 1:13) Hakuna mwanadamu yeyote ambaye angefikiri kwamba Sauli angekuwa Mkristo. Hata hivyo, Yesu aliona sifa fulani nzuri katika moyo wa Sauli naye akamchagua ili atimize kazi ya pekee. Kwa hiyo, Sauli akawa kati ya washiriki watendaji na wenye bidii zaidi wa kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza.

9 Mfano wa mtume Paulo unatufundisha nini? Huenda kuna watu ambao wanaonekana wanapinga vikali ujumbe wetu katika eneo letu. Ingawa huenda tukawa na shaka kwamba hawatakuwa kamwe Wakristo wa kweli, tunapaswa kuendelea kujitahidi kuwahubiria. Nyakati nyingine, hata watu ambao wanaonekana kuwa hawapendezwi hata kidogo wanaitikia. Kazi yetu ni kuendelea kuwahubiria wote “bila kuacha.”—Soma Matendo 5:42.

Baraka Zinawangojea Wale Wanaohubiri “Bila Kuacha”

10. Kwa nini hatupaswi kukataa kuwahubiria watu ambao wanaonekana kuwa wenye kutisha? Simulia mambo ya kwenu.

10 Sura ya nje inaweza kudanganya. Kwa mfano, Ignacio, * alianza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova alipokuwa gerezani katika nchi moja ya Amerika Kusini. Watu walimwogopa kwa sababu alikuwa mjeuri sana. Basi, wafungwa ambao walitengeneza vitu na kuwauzia wafungwa wengine walimtumia Ignacio kukusanya madeni kutoka kwa wale ambao hawakutaka kulipa haraka. Hata hivyo, kadiri Ignacio alivyofanya maendeleo ya kiroho na kutumia mambo aliyokuwa akijifunza, ndivyo mtu huyo aliyekuwa mkatili na mjeuri alivyozidi kuwa mwenye fadhili. Sasa hakuna yeyote anayemtumia kukusanya madeni, hata hivyo, Ignacio ameridhika kwamba kweli za Biblia na roho ya Mungu imebadili utu wake. Pia, anafurahi kwa kuwa wahubiri wa Ufalme ambao walijitahidi kujifunza naye hawakuwa na ubaguzi.

11. Kwa nini tunaendelea kuwatembelea watu?

11 Moja ya sababu zinazofanya tuendelee kuwatembelea watu ambao tayari tumewahubiria habari njema ni kwamba hali na mitazamo yao inaweza kubadilika na kwa kweli inabadilika. Tangu tulipowatembelea mara ya mwisho, huenda wengine wao wamepatwa na ugonjwa mbaya, wamepoteza kazi, au wamefiwa na mpendwa wao. (Soma Mhubiri 9:11.) Matukio ya ulimwengu yanaweza kuwachochea watu wafikirie kwa uzito kuhusu wakati wao ujao. Matukio hayo yanaweza kumfanya mtu ambaye hakupendezwa au hata aliyepinga akubali ujumbe wetu. Hivyo, hatupaswi kukosa kuwahubiria wengine habari njema katika kila nafasi inayofaa.

12. Tunapaswa kuwa na maoni gani kuelekea watu tunaowahubiria, na kwa nini?

12 Inaonekana wanadamu wana mwelekeo wa kuwahukumu na kuwabagua wengine. Lakini Yehova anamkazia uangalifu mtu mmoja-mmoja. Anaona sifa nzuri za kila mtu. (Soma 1 Samweli 16:7.) Tunapaswa kujitahidi kufanya vivyo hivyo katika huduma yetu. Mambo mengi yaliyoonwa yanaonyesha matokeo mazuri ya kuwa na maoni yanayofaa kuelekea watu wote tunaowahubiria.

13, 14. (a) Kwa nini painia mmoja alikuwa na maoni yasiyofaa kumhusu mwanamke aliyekutana naye katika huduma? (b) Tunajifunza nini kutokana na jambo hilo?

13 Dada mmoja painia anayeitwa Sandra, alipokuwa akihubiri nyumba kwa nyumba katika kisiwa kimoja cha Karibea alikutana na Ruth, ambaye alikuwa akijishughulisha sana na mashindano fulani. Ruth alishinda mara mbili tuzo la malkia wa taifa wa mashindano hayo. Alipendezwa sana na yale ambayo Sandra alikuwa akimwambia, basi funzo la Biblia likapangwa. Sandra anakumbuka hivi: “Nilipoingia katika nyumba yake, niliona picha kubwa ya Ruth akiwa amevalia mavazi ya mashindano hayo, vilevile niliona vikombe alivyokuwa ameshinda. Nilifikiri kimakosa kwamba mtu aliyekuwa maarufu na aliyejishughulisha sana na mashindano hangependezwa na kweli. Kwa hiyo, nikaacha kumtembelea.”

14 Baada ya muda, Ruth alikuja kwenye Jumba la Ufalme, na mkutano ulipomalizika, alimuuliza Sandra hivi, “Kwa nini uliacha kuja kujifunza na mimi?” Sandra aliomba msamaha naye akapanga kuanza tena kujifunza naye. Ruth alifanya maendeleo haraka, akaondoa picha zake za mashindano ukutani, akaanza kushiriki katika utendaji wote wa kutaniko, kisha akaweka maisha yake wakfu kwa Yehova. Bila shaka, Sandra alitambua kwamba maoni aliyokuwa nayo kumhusu Ruth yalikuwa mabaya.

15, 16. (a) Mhubiri mmoja alipata matokeo gani alipomhubiria mtu wake wa ukoo? (b) Kwa nini hatupaswi kusitasita kumhubiria mtu wa ukoo anayeshikilia sana imani ya kidini?

15 Wahubiri wengi wamepata matokeo mazuri kwa kuwahubiria washiriki wa familia yao wasio waamini, hata ilipofikiriwa kwamba hawangeikubali kweli. Kwa mfano, mfikirie Joyce, dada mmoja Mkristo huko Marekani. Shemeji yake alikuwa amefungwa na kuachiliwa mara nyingi kutoka gerezani tangu akiwa kijana. Joyce anaeleza hivi: “Watu walisema kwamba maisha yake yalikuwa yameharibika kabisa kwa sababu alijishughulisha na dawa za kulevya, alikuwa mwizi, na alifanya mambo mengine mengi mabaya. Hata hivyo, jambo la kushangaza ni kwamba niliendelea kuzungumza naye kweli za Biblia kwa miaka 37.” Jitihada zake za kumsaidia mtu wake wa ukoo kwa subira zilithawabishwa sana mtu huyo alipoamua mwishowe kuanza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova na kufanya mabadiliko makubwa katika maisha yake. Hivi karibuni, Shemeji huyo wa Joyce alibatizwa akiwa na umri wa miaka 50 katika kusanyiko la wilaya huko California, Marekani. Joyce anasema hivi: “Nililia kwa shangwe. Ninafurahi sana kwamba sikuchoka kumsaidia!”

16 Huenda ukasitasita kuongea na watu fulani wa ukoo kuhusu kweli za Biblia kwa sababu ya malezi yao. Hata hivyo, Joyce hakusitasita kuongea na shemeji yake. Kwa kweli, mtu anaweza kujua namna gani yale yaliyo katika moyo wa mtu mwingine? Huenda mtu huyo anatafuta kwa unyoofu kweli ya kidini. Kwa hivyo, usimnyime nafasi ya kuipata kweli hiyo.—Soma Methali 3:27.

Kitabu Chenye Matokeo cha Kujifunzia Biblia

17, 18. (a) Ripoti kutoka ulimwenguni pote zinaonyesha nini kuhusu faida za kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? (b) Umepata matokeo gani mazuri kwa kutumia kitabu hicho?

17 Ripoti kutoka nchi nyingi ulimwenguni pote zinaonyesha kwamba watu wengi wenye mioyo minyoofu wanafurahia sana kitabu cha kujifunzia Biblia kinachoitwa Biblia Inafundisha Nini Hasa? Dada painia anayeitwa Penni, huko Marekani, alianzisha mafunzo kadhaa akitumia kitabu hicho. Wawili walikuwa wazee kwa umri na walikuwa washiriki wenye bidii katika makanisa yao. Penni hakujua jinsi ambavyo wangeitikia kweli za Kimaandiko zilizo katika kitabu Biblia Inafundisha. Hata hivyo, anaandika hivi: “Kwa sababu habari imeelezwa kwa njia iliyo wazi, inayopatana na akili, na inayoeleweka kwa urahisi, walikubali haraka kwamba mambo waliyokuwa wakijifunza ni ya kweli. Hawakubisha wala kukasirika.”

18 Pat, mhubiri aliye nchini Uingereza, alianza kujifunza Biblia pamoja na mwanamke ambaye ni mkimbizi kutoka katika nchi moja ya Asia. Mwanamke huyo alilazimika kukimbia kutoka katika nchi yao baada ya mume wake na wanawe kuchukuliwa na askari-jeshi waasi na kutoweka kabisa. Alitishwa kwamba angeuawa, nyumba yake ilikuwa imeteketezwa, naye alikuwa amelalwa kinguvu na genge la wanaume. Mambo yote hayo yalifanya maisha yake yakose kusudi, na mara nyingi alifikiria kujiua. Hata hivyo, kujifunza Biblia kulimpa tumaini. Pat anaandika hivi: “Maelezo na mifano rahisi ya kitabu Biblia Inafundisha ilimgusa moyo sana.” Mwanafunzi huyo alifanya maendeleo ya haraka, akastahili kuwa mhubiri ambaye hajabatizwa, naye akaomba kubatizwa katika kusanyiko lililofuata. Ni shangwe kama nini kuwasaidia watu wanyoofu kuelewa na kuthamini tumaini linalotolewa na Maandiko!

“Tusife Moyo Katika Kufanya Yaliyo Mema”

19. Kwa nini kazi ya kuhubiri ni muhimu sana?

19 Kazi yetu ya kuhubiri na kufanya wanafunzi inazidi kuwa muhimu sana kadiri siku zinavyopita. Maelfu ya watu wenye mwelekeo unaofaa wanaitikia ujumbe wetu kila mwaka. Lakini, “ile siku kuu ya Yehova iko karibu,” kwa hivyo, wale ambao wanaendelea kukaa katika giza la kiroho ‘wanapepesuka wakielekea kuchinjwa.’—Sef. 1:14; Met. 24:11.

20. Kila mmoja wetu anapaswa kuazimia kufanya nini?

20 Bado tunaweza kuwasaidia watu kama hao. Lakini ili tuwasaidie, ni muhimu tuwaige Wakristo wa karne ya kwanza ambao ‘waliendelea bila kuacha kufundisha na kutangaza habari njema juu ya Kristo, Yesu.’ (Mdo. 5:42) Fuata mfano wao kwa kuendelea hata unapokabili matatizo. Kazia uangalifu ‘ufundi wako wa kufundisha,’ na uwahubirie watu wote bila ubaguzi! “Tusife moyo katika kufanya yaliyo mema,” kwa kuwa tukiendelea, tutavuna baraka nyingi sana za kukubaliwa na Mungu.—2 Tim. 4:2; soma Wagalatia 6:9.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 10 Baadhi ya majina yamebadilishwa.

Ungetoa Jibu Gani?

• Ni nani wanaokubali habari njema?

• Kwa nini hatupaswi kuwabagua wale tunaowahubiria?

• Kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kina matokeo gani mazuri?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 13]

Maelfu ya watu wenye mioyo minyoofu wanaitikia

[Picha katika ukurasa wa 15]

Mabadiliko ambayo mtume Paulo alifanya yanatufunza nini?

[Picha katika ukurasa wa 16]

Watangazaji wa habari njema hawabagui watu