Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Endelea Kumweka Yehova Mbele Yako Daima

Endelea Kumweka Yehova Mbele Yako Daima

Endelea Kumweka Yehova Mbele Yako Daima

“Nimemweka Yehova mbele yangu daima.”—ZAB. 16:8.

1. Masimulizi ya Biblia yanaweza kuwa na matokeo gani kwetu?

NENO la Yehova lililoandikwa limejaa masimulizi kuhusu shughuli za Mungu pamoja na wanadamu. Linawataja watu wengi walioshiriki kutimiza kusudi la Mungu. Bila shaka, maneno na matendo yao hayakuandikwa katika Biblia yawe hadithi tamu tu. Badala yake, masimulizi hayo yanaweza kutusaidia tumkaribie Mungu zaidi.—Yak. 4:8.

2, 3. Maneno ya Zaburi 16:8 yanamaanisha nini?

2 Sote tunaweza kujifunza mengi kutokana na mambo yaliyowapata watu fulani katika Biblia wanaojulikana sana kama vile Abrahamu, Sara, Musa, Ruthu, Daudi, Esta, mtume Paulo, na wengineo. Hata hivyo, masimulizi kuhusu watu fulani wasiojulikana sana yanaweza kutusaidia pia. Kutafakari kuhusu masimulizi ya Biblia kunaweza kutusaidia kutenda kupatana na maneno haya ya mtunga-zaburi: “Nimemweka Yehova mbele yangu daima. Kwa sababu yuko upande wa mkono wangu wa kuume, sitatikiswa.” (Zab. 16:8) Maneno hayo yanamaanisha nini?

3 Kwa kawaida, askari-jeshi alishika upanga wake kwa mkono wake wa kuume, hivyo upande wake wa kuume haukulindwa na ngao aliyobeba kwa mkono wake wa kushoto. Lakini, angelindwa ikiwa rafiki yake angepigana karibu naye akiwa upande wake wa kulia. Tukimweka Yehova akilini na tukifanya mapenzi yake, atatulinda. Hivyo, acheni tuone jinsi kuchunguza masimulizi ya Biblia kunavyoweza kuimarisha imani yetu ili ‘tuendelee kumweka Yehova sikuzote mbele yetu.’—Byington.

Yehova Anajibu Sala Zetu

4. Toa mfano wa Kimaandiko unaoonyesha kwamba Mungu anajibu sala.

4 Tukiendelea kumweka Yehova mbele yetu, atajibu sala zetu. (Zab. 65:2; 66:19) Kisa cha mtumishi wa Abrahamu aliyekuwa na umri mkubwa zaidi, ambaye huenda alikuwa Eliezeri, kinathibitisha jambo hilo. Abrahamu alimtuma huko Mesopotamia akamtafutie Isaka mke anayemwogopa Mungu. Eliezeri alisali apewe mwongozo wa Mungu, naye alitambua kwamba Mungu alimwongoza wakati Rebeka alipowanywesha ngamia wake. Kwa sababu alisali, Eliezeri alimpata yule ambaye baadaye alikuja kuwa mke mpendwa wa Isaka. (Mwa. 24:12-14, 67) Ni kweli kwamba mtumishi wa Abrahamu alikuwa na utume wa pekee. Lakini je, hatupaswi kuwa na uhakika kama huo kwamba Yehova anasikia sala zetu?

5. Kwa nini tunaweza kusema kwamba hata sala fupi ya kimyakimya inaweza kuwa na matokeo mazuri?

5 Nyakati nyingine, huenda tukahitaji kuomba msaada wa Mungu haraka. Pindi moja, Mfalme Artashasta wa Uajemi alitambua kwamba Nehemia, mnyweshaji wake alikuwa na huzuni. “Ni jambo gani hili unalotaka?” akauliza mfalme. “Mara moja [Nehemia] akasali kwa Mungu wa mbinguni.” Nehemia alitoa sala fupi ambayo inaelekea ilikuwa ya kimyakimya. Lakini, Mungu alimjibu, kwa sababu mfalme alimpa Nehemia msaada wa kujenga upya kuta za Yerusalemu. (Soma Nehemia 2:1-8.) Ndiyo, hata sala fupi ya kimyakimya inaweza kuwa na matokeo mazuri.

6, 7. (a) Epafra aliweka mfano gani kuhusu sala? (b) Kwa nini tusali kwa ajili ya wengine?

6 Tunahimizwa “tusali kwa ajili ya mtu na mwenzake,” hata ikiwa hatuna uthibitisho wa papo hapo kwamba sala hizo zinajibiwa. (Yak. 5:16) Epafra, “mhudumu mwaminifu wa Kristo,” alisali kwa bidii kwa ajili ya waamini wenzake. Akiandika kutoka Roma, Paulo alisema: “Epafra, ambaye ni kutoka kati yenu [Wakolosai], mtumwa wa Kristo Yesu, anawatumia ninyi salamu zake, sikuzote akijikaza kwa ajili yenu katika sala zake, ili mwishowe msimame mkiwa kamili na kwa usadikisho imara katika mapenzi yote ya Mungu. Kwa kweli namtolea yeye ushahidi kwamba anajitahidi sana kwa ajili yenu na kwa ajili ya wale walioko Laodikia na wale walioko Hierapoli.”—Kol. 1:7; 4:12, 13.

7 Kolosai, Laodikia, na Hierapoli yalikuwa majiji katika eneo lilelile huko Asia Ndogo. Wakristo huko Hierapoli waliishi miongoni mwa waabudu wa mungu wa kike Cybele, roho ya kupenda mali ilitishia hali ya wale walioishi Laodikia, na hali ya Wakolosai ilihatarishwa na falsafa za wanadamu. (Kol. 2:8) Hivyo, haishangazi kwamba Epafra, ambaye alitoka Kolosai, ‘alijikaza katika sala’ kwa ajili ya waamini walioishi katika jiji hilo! Biblia haielezi jinsi sala za Epafra zilivyojibiwa, lakini hakuacha kusali kwa ajili ya waamini wenzake; sisi pia tusiache. Ijapokuwa ‘hatujiingizi katika mambo ya watu wengine,’ huenda tunajua kwamba mshiriki fulani wa familia au rafiki fulani anakabili jaribu kali la imani. (1 Pet. 4:15) Ingefaa kama nini kusali kibinafsi kwa ajili yake! Sala za wengine zilimsaidia Paulo, vivyo hivyo sala zetu zinaweza kuwa na matokeo mazuri sana.—2 Kor. 1:10, 11.

8. (a) Tunajua jinsi gani kwamba wazee ambao walitoka Efeso walitambua umuhimu wa sala? (b) Tunapaswa kuwa na mtazamo gani kuhusu kusali kwa Mungu?

8 Je, wengine wanatuona kuwa watu wanaothamini pendeleo la sala na wanaosali kwa ukawaida? Paulo alipokutana na wazee kutoka Efeso, ‘alipiga magoti pamoja nao wote na kusali.’ Kisha “wote wakalia sana, nao wakamwangukia Paulo shingoni na kumbusu kwa wororo, kwa sababu waliumizwa hasa na neno alilosema kwamba hawangemwona uso wake tena.” (Mdo. 20:36-38) Hatujui majina ya wazee hao wote, lakini hapana shaka kwamba walitambua umuhimu wa sala. Bila shaka, tunapaswa kuthamini pendeleo la kusali kwa Mungu na ‘kuinua mikono yenye ushikamanifu’ tukiamini kwamba Baba yetu wa mbinguni atatujibu.—1 Tim. 2:8.

Mtii Mungu Kikamilifu

9, 10. (a) Ni mfano gani uliowekwa na binti za Selofehadi? (b) Utii wa binti za Selofehadi unaweza kuwa na uvutano gani juu ya maoni ya Wakristo waseja kuhusu ndoa?

9 Kuendelea kumweka Yehova akilini daima kutatusaidia kumtii, na hivyo tutapata baraka nyingi. (Kum. 28:13; 1 Sam. 15:22) Kwa hiyo, tunapaswa kuwa na roho ya utii. Fikiria mtazamo wa dada watano, binti za Selofehadi, walioishi katika siku za Musa. Miongoni mwa Waisraeli, kwa kawaida wana walipewa urithi na baba zao. Selofehadi alikufa bila wana, na Yehova akaagiza wanawake hao watano wapewe urithi wote, lakini akawawekea takwa moja. Walipaswa kuolewa na wana wa Manase ili urithi huo ubaki katika kabila lilelile.—Hes. 27:1-8; 36:6-8.

10 Binti za Selofehadi waliamini kwamba mambo yangewaendea vema ikiwa wangemtii Mungu. “Kama vile Yehova alivyokuwa amemwamuru Musa, hivyo ndivyo binti za Selofehadi walivyofanya,” inasema Biblia. “Basi Mala, Tirsa na Hogla na Milka na Noa, binti za Selofehadi, wakawa wake za wana wa ndugu za baba yao. Wakawa wake za baadhi ya familia za wana wa Manase mwana wa Yosefu, ili urithi wao uendelee kuwa pamoja na kabila la familia ya baba yao.” (Hes. 36:10-12) Wanawake hao watiifu walifanya kile ambacho Yehova aliamuru. (Yos. 17:3, 4) Wakiwa na imani kama hiyo, Wakristo waliokomaa kiroho wanamtii Mungu kwa kuoa au kuolewa “katika Bwana tu.”—1 Kor. 7:39.

11, 12. Kalebu alionyesha kwa njia gani kwamba alikuwa na uhakika katika Mungu?

11 Tunahitaji kumtii Yehova kikamilifu kama alivyofanya Mwisraeli aliyeitwa Kalebu. (Kum. 1:36) Baada ya Waisraeli kukombolewa kutoka Misri katika karne ya 16 K.W.K., Musa aliwatuma wanaume 12 wakapeleleze nchi ya Kanaani, lakini wapelelezi 2 tu, yaani, Kalebu na Yoshua, ndio waliowahimiza watu wamtegemee Mungu kikamilifu na kuingia katika nchi hiyo. (Hes. 14:6-9) Miaka 40 hivi baadaye, bado Yoshua na Kalebu walikuwa hai na walikuwa wakimfuata Yehova kikamilifu, naye Mungu alimtumia Yoshua kuwaongoza Waisraeli kuingia katika Nchi ya Ahadi. Hata hivyo, ni wazi kwamba wapelelezi kumi wasio na imani walikufa katika kipindi cha miaka 40, Waisraeli walipokuwa wakitangatanga nyikani.—Hes. 14:31-34.

12 Akiwa mwokokaji mwenye umri mkubwa zaidi wa mambo yaliyowapata Waisraeli nyikani, Kalebu angeweza kusimama mbele za Yoshua na kusema: “Nilimfuata kikamilifu Yehova Mungu wangu.” (Soma Yoshua 14:6-9.) Kalebu ambaye wakati huo alikuwa na umri wa miaka 85 aliomba apewe eneo lenye milima ambalo Yehova alikuwa amemwahidi, ijapokuwa lilikuwa limekaliwa na maadui walioishi katika majiji makubwa yenye ngome.—Yos. 14:10-15.

13. Hata tukikabili majaribu gani, tutabarikiwa tukifanya nini?

13 Kama Kalebu ambaye alikuwa mwaminifu na mtiifu, Yehova atatutegemeza iwapo ‘tutamfuata kikamilifu.’ Tukikabili matatizo makubwa, tutabarikiwa ‘tukimfuata Yehova kikamilifu.’ Lakini huenda ikawa vigumu kufanya hivyo siku zote za maisha yetu, kama Kalebu alivyofanya. Mwanzoni Mfalme Sulemani alimfuata Yehova, hata hivyo alipokuwa mzee, wake zake waliugeuza moyo wake ukaifuata miungu ya uwongo, naye “hakumfuata Yehova kikamilifu kama Daudi baba yake.” (1 Fal. 11:4-6) Hata tukikabili majaribu gani, acheni sikuzote tumtii Mungu kikamilifu na tuendelee kumweka mbele yetu daima.

Mtegemee Yehova Sikuzote

14, 15. Umejifunza nini kutokana na kisa cha Naomi kuhusu uhitaji wa kumtegemea Mungu?

14 Tunapaswa kumtegemea Mungu hasa tunaposhuka moyo kwa sababu ya kukosa tumaini. Mfikirie Naomi aliyezeeka, ambaye alimpoteza mume wake na wanawe wawili kupitia adui kifo. Alipotoka Moabu na kurudi Yuda, aliomboleza hivi: “Msiniite Naomi [“Uzuri Wangu”]. Niiteni Mara [“Uchungu”], kwa maana Mweza-Yote amenifanya kuwa na uchungu sana. Nilikuwa nimejaa nilipoenda, naye Yehova amenifanya nirudi mikono mitupu. Kwa nini mniite Naomi, hali Yehova ndiye amenifedhehesha na Mweza-Yote ndiye amenisababishia msiba?”—Rut. 1:20, 21.

15 Ijapokuwa Naomi alifadhaika sana, tukisoma kitabu cha Ruthu kwa makini tutaona kwamba aliendelea kumtegemea Yehova. Na hali yake ilibadilika kama nini! Ruthu, binti-mkwe wa Naomi, ambaye pia alikuwa mjane aliolewa na Boazi na kumzaa mwana. Naomi akawa mlezi wa mtoto huyo, na simulizi hilo linasema: “Wanawake majirani wakampa jina, wakisema: ‘Naomi amepata mwana.’ Nao wakamwita Obedi. Yeye ndiye baba ya Yese, baba ya Daudi.” (Rut. 4:14-17) Naomi atakapofufuliwa aishi duniani, atajulishwa kwamba Ruthu, ambaye pia atakuwepo duniani, alikuwa nyanya ya Yesu, yule Masihi. (Mt. 1:5, 6, 16) Sawa na Naomi, hatuwezi kujua kwa hakika hali mbaya tunazokabili zitabadilika jinsi gani. Hivyo, acheni tumtegemee Mungu sikuzote, kama tunavyohimizwa katika Methali 3:5, 6: “Mtegemee Yehova kwa moyo wako wote wala usitegemee uelewaji wako mwenyewe. Mtambue yeye katika njia zako zote, naye atanyoosha mapito yako.”

Itegemee Roho Takatifu

16. Roho takatifu ya Mungu iliwasaidia kwa njia gani wanaume fulani wazee katika Israeli la kale?

16 Tukiendelea kumweka Yehova mbele yetu daima, atatuongoza kwa roho yake takatifu. (Gal. 5:16-18) Roho ya Mungu ilikuwa juu ya wale wanaume wazee 70 waliochaguliwa kumsaidia Musa “kuubeba mzigo wa watu” wa Israeli. Eldadi na Medadi tu ndio tunaojua majina yao, lakini roho hiyo iliwawezesha wote kutimiza majukumu yao. (Hes. 11:13-29) Hapana shaka kwamba walikuwa wanaume wenye uwezo, waliomwogopa Mungu, wenye kutegemeka, na wanyoofu—kama tu wale waliokuwa wamechaguliwa mapema. (Kut. 18:21) Sifa kama hizo zinaonyeshwa na wazee Wakristo leo.

17. Roho takatifu ya Yehova ilihusika jinsi gani katika ujenzi wa ile maskani?

17 Roho takatifu ya Yehova ilisaidia sana katika ujenzi wa ile maskani nyikani. Yehova alimweka rasmi Bezaleli awe fundi na mjenzi mkuu wa maskani, na akaahidi ‘kumjaza roho ya Mungu katika hekima na katika uelewaji na katika ujuzi na katika kila aina ya ufundi.’ (Kut. 31:3-5) Wanaume waliokuwa na ‘moyo wenye hekima’ walimsaidia Bezaleli na Oholiabu msaidizi wake katika kazi hiyo ya pekee sana. Zaidi ya hilo, roho ya Yehova iliwachochea watu waliokuwa na moyo wenye nia watoe michango kwa ukarimu. (Kut. 31:6; 35:5, 30-34) Roho hiyohiyo inawachochea watumishi wa Mungu leo wafanye yote wanayoweza ili kutegemeza kazi ya Ufalme. (Mt. 6:33) Huenda tukawa na vipawa fulani, lakini ili tufanye kazi ambayo Yehova amewapa watu wake katika siku zetu, tunahitaji kusali tupewe roho takatifu na kuiruhusu ituongoze.—Luka 11:13.

Mheshimu Yehova wa Majeshi Sikuzote

18, 19. (a) Roho takatifu ya Mungu inatuwezesha kuwa na mtazamo gani? (b) Umejifunza nini kutokana na mfano wa Simeoni na Ana?

18 Roho takatifu inatuwezesha kuwa na mtazamo wa kumheshimu Yehova na hivyo kuendelea kumweka mbele yetu daima. Watu wa kale wa Mungu waliambiwa hivi: “Yehova wa majeshi ndiye mnayepaswa kumheshimu akiwa mtakatifu.” (Isa. 8:13, Byington) Katika karne ya kwanza, wazee wawili waliomheshimu Mungu huko Yerusalemu ni Simeoni na Ana. (Soma Luka 2:25-38.) Simeoni aliamini unabii kumhusu Masihi na alikuwa “akingojea faraja ya Israeli.” Mungu alimwaga roho yake takatifu juu ya Simeoni na akamhakikishia kwamba hangekufa kabla ya kumwona Masihi. Na hilo lilitukia. Siku moja katika mwaka wa 2 K.W.K., Maria mama ya Yesu na Yosefu baba yake mlezi walimpeleka mtoto huyo mchanga hekaluni. Akichochewa na roho takatifu, Simeoni alisema maneno ya kinabii kumhusu Masihi na akatabiri huzuni ambayo ingempata Maria, ambaye alihuzunika Yesu alipotundikwa kwenye mti wa mateso. Lakini wazia furaha ambayo Simeoni alikuwa nayo alipombeba mikononi mwake “Kristo wa Yehova”! Na Simeoni aliwawekea watumishi wa Mungu leo mfano mzuri kama nini wa kumheshimu Mungu!

19 Ana, mjane mwenye umri wa miaka 84 ambaye alimheshimu Mungu, “alikuwa hakosi kamwe kuwa katika hekalu.” Alimtolea Yehova utumishi mtakatifu usiku na mchana kwa “kufunga na dua.” Ana alikuwepo pia mtoto mchanga Yesu alipoletwa hekaluni. Alishukuru kama nini kumwona yule ambaye angekuwa Masihi! Kwa kweli, ‘alianza kumshukuru Mungu akisema juu ya mtoto huyo kwa wale wote waliokuwa wakiungojea ukombozi wa Yerusalemu.’ Ana hangejizuia kuwatangazia wengine habari njema hiyo! Kama Simeoni na Ana, leo Wakristo waliozeeka wanashangilia sana kwamba hata watu wakiwa wamezeeka kadiri gani, bado wanaweza kumtumikia Yehova wakiwa Mashahidi wake.

20. Tunapaswa kufanya nini haidhuru tuna umri gani, na kwa nini?

20 Tunapaswa kuendelea kumweka Yehova mbele yetu daima haidhuru tuna umri gani. Tukifanya hivyo, atabariki jitihada zetu za unyenyekevu za kuwatangazia wengine kuhusu Ufalme wake na kuhusu kazi zake za ajabu. (Zab. 71:17, 18; 145:10-13) Lakini ili tumheshimu Yehova, ni lazima tuwe na sifa za kimungu. Tunaweza kujifunza nini kuhusu sifa kama hizo kwa kuchunguza masimulizi mengine ya Biblia?

Ungetoa Jibu Gani?

• Tunajua jinsi gani kwamba Yehova anajibu sala?

• Kwa nini tumtii Mungu kikamilifu?

• Kwa nini tunapaswa kumtegemea Yehova sikuzote hata tunaposhuka moyo?

• Roho takatifu ya Mungu inawasaidia watu wake kwa njia gani?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 4]

Sala ya Nehemia kwa Yehova ilikuwa na matokeo mazuri

[Picha katika ukurasa wa 5]

Kukumbuka baraka ambazo Naomi alipata kutatusaidia kumtegemea Yehova