Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jifunze Kutokana na Makosa ya Waisraeli

Jifunze Kutokana na Makosa ya Waisraeli

Jifunze Kutokana na Makosa ya Waisraeli

WAISRAELI walipokuwa wakiingia katika Nchi ya Ahadi, walijua mambo ambayo Yehova alitaka wafanye. Mungu alikuwa amewaamuru hivi kupitia Musa: “Mnapaswa kuwafukuzia mbali wakaaji wote wa nchi hiyo kutoka mbele yenu na kuharibu maumbo yao yote ya mawe, nanyi mnapaswa kuziharibu sanamu zao zote za madini ya kuyeyusha, na mnapaswa kupaharibu mahali pao pote patakatifu.”—Hes. 33:52.

Waisraeli hawakupaswa kufanya agano lolote na wakaaji wa nchi hiyo, wala hawakupaswa kufanya mapatano yoyote ya ndoa pamoja nao. (Kum. 7:2, 3) Kwa kweli, watu hao waliochaguliwa na Mungu walionywa hivi: “Jiangalie usije ukafanya agano pamoja na wakaaji wa nchi hiyo unayoiendea, isije ikawa mtego katikati yako.” (Kut. 34:12) Hata hivyo, Waisraeli hawakumtii Mungu na hivyo wakanaswa na mtego huo. Kwa nini walinaswa na mtego? Ni mambo gani yenye kuonya tunayoweza kujifunza kutokana na kisa chao?—1 Kor. 10:11.

Kushirikiana na Watu wa Mataifa Kuliwaongoza Kwenye Ibada ya Sanamu

Waisraeli waliwashinda wakaaji wa Nchi ya Ahadi na kuimiliki. Hata hivyo, wana wa Israeli hawakutii amri za Mungu kikamilifu. Hawakuwafukuzia mbali maadui. (Amu. 1:1–2:10) Badala yake, Waisraeli walipoanza kukaa katikati ya “mataifa saba” ambayo yalikuwa katika nchi hiyo, walishirikiana kwa ukawaida na watu wa mataifa hayo na hivyo wakaanzisha urafiki nao. (Kum. 7:1) Matokeo yalikuwa nini kwa Waisraeli? Biblia inasema: “Wakaanza kuoa binti zao, na binti zao wenyewe wakawapa wana wao, nao wakaanza kuitumikia miungu yao. Basi wana wa Israeli wakafanya yaliyokuwa mabaya machoni pa Yehova, wakamsahau Yehova Mungu wao, wakatumikia Mabaali na miti mitakatifu.” (Amu. 3:5-7) Baada ya kushirikiana na watu wa nchi hiyo, Waisraeli walianza kuoana nao na kuabudu sanamu zao. Baada ya Waisraeli kufanya mapatano ya ndoa nao, ikawa vigumu sana kwa Waisraeli kuwafukuza wapagani hao kutoka katika nchi hiyo. Ibada ya kweli ilichafuliwa, na Waisraeli wenyewe walianza kuitumikia miungu ya uwongo.

Wakiwa marafiki wao, wakaaji wa Nchi ya Ahadi walihatarisha hata zaidi hali ya kiroho ya Waisraeli kuliko walipokuwa maadui wao. Fikiria jambo lingine ambalo huenda lilichafua ibada yao.

Uhusiano Kati ya Ukulima na Ibada ya Baali

Walipoingia katika Nchi ya Ahadi, wana wa Israeli waliacha maisha ya kuhamahama na wengi wakawa wakulima. Huenda walitumia njia za ukulima kama za watu walioilima nchi hiyo kabla yao. Inaonekana kwamba hawakufuata tu njia za ukulima za Wakanaani. Waliposhirikiana na wakaaji hao, Waisraeli walishawishiwa pia kukubali ibada yao iliyohusiana na ukulima.

Wakanaani waliabudu Mabaali wengi—miungu ambayo ilisemekana kwamba iliufanya udongo uwe na rutuba. Zaidi ya kulima na kuvuna mazao, baada ya muda Waisraeli walijiunga nao katika kuheshimu miungu ya Wakanaani ambayo walidai ilileta mazao mengi. Kwa hiyo, watu wengi wa Israeli walijifanya wanamwabudu Yehova, lakini kwa kweli walishiriki kabisa katika uasi-imani.

Onyo Kali Kwetu Leo

Haielekei kwamba Waisraeli walikusudia kushiriki katika ibada ya Baali na matendo yake mapotovu walipokutana kwa mara ya kwanza na wakaaji wa Nchi ya Ahadi. Hata hivyo, kushirikiana na watu hao kuliwaongoza katika mambo hayo. Tukishirikiana na watu ambao huenda ni wenye urafiki lakini hawafuati imani, maadili, na kanuni zetu za Kikristo, je, hatutapata madhara kama hayo? Bila shaka, huenda tukalazimika kushirikiana na watu wasio waamini katika mambo fulani kazini, shuleni, au labda hata nyumbani. Hata hivyo, mambo yaliyowapata Waisraeli ni onyo kwetu kwamba tukitafuta mashirika ya aina hiyo tunacheza na moto. Biblia inasema ukweli huu usioepukika: “Mashirika mabaya huharibu tabia nzuri.”—1 Kor. 15:33.

Leo, tunakabili matatizo mengi kama ya Waisraeli. Katika jamii ya leo, kuna vitu vingi na watu ambao wanaabudiwa kama sanamu. Wanaabudu pesa, watu mashuhuri katika burudani, wanamichezo, mifumo ya kisiasa, viongozi fulani wa kidini, na hata washiriki wa familia. Chochote ambacho mtu anaabudu kinaweza kuwa jambo kuu katika maisha yetu. Kusitawisha urafiki wa karibu pamoja na wale ambao hawampendi Yehova kunaweza kutudhuru kiroho.

Ngono haramu ilikuwa sehemu kuu ya ibada ya Baali na iliwavutia na kuwashawishi Waisraeli wengi. Watu wengi wa Mungu bado wananaswa na mitego kama hiyo. Kwa mfano, mtu mwenye hamu ya kujua mambo au asiye mwangalifu anaweza kuchafua dhamiri yake safi kwa kuangalia ponografia (picha au habari za ngono) kwenye Intaneti nyumbani mwake. Ingehuzunisha sana ikiwa Mkristo angeshawishiwa na ponografia kwenye Intaneti!

“Wenye Furaha Ni Wale Wanaoshika Vikumbusho Vyake”

Uamuzi wa kutii au kutotii yale ambayo Yehova anasema kuhusu mashirika ni wa kibinafsi. (Kum. 30:19, 20) Hivyo, tunahitaji kujiuliza hivi: ‘Ninashirikiana na nani katika tafrija na burudani? Wanafuata viwango gani vya maadili? Je, wanamwabudu Yehova? Je, nitakuwa Mkristo bora nikishirikiana nao?’

Mtunga-zaburi aliimba hivi: “Wenye furaha ni wale wasio na kosa katika njia yao, wale wanaotembea katika sheria ya Yehova. Wenye furaha ni wale wanaoshika vikumbusho vyake; wanaendelea kumtafuta kwa moyo wote.” (Zab. 119:1, 2) Kwa kweli, “mwenye furaha ni kila mtu anayemwogopa Yehova. Anayetembea katika njia zake.” (Zab. 128:1) Inapohusu kuchagua mashirika yetu, na tujifunze kutokana na makosa ya Waisraeli na hivyo tumtii Yehova kabisa.—Met. 13:20.

[Picha katika ukurasa wa 26]

Kushirikiana na watu ambao hawampendi Yehova kunaweza kutuongoza kwenye ibada ya sanamu