Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuwapo Kwa Kristo—kunamaanisha Nini Kwako?

Kuwapo Kwa Kristo—kunamaanisha Nini Kwako?

Kuwapo Kwa Kristo—kunamaanisha Nini Kwako?

“Ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo?”—MT. 24:3.

1. Mitume wa Yesu walimuuliza swali gani lenye kupendeza?

KARIBU miaka elfu mbili iliyopita, mitume wanne wa Yesu waliuliza swali walipokuwa wakizungumza faraghani na Bwana wao kwenye Mlima wa Mizeituni. Waliuliza hivi: “Mambo haya yatakuwa wakati gani, na ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo?” (Mt. 24:3) Walipouliza swali hilo, mitume hao walitumia semi mbili zenye kupendeza sana. Walitaja “kuwapo kwako” na “umalizio wa mfumo wa mambo.” Semi hizo zinamaanisha nini?

2. Neno “umalizio” linamaanisha nini?

2 Acheni tuanze na usemi wa pili. Fikiria neno “umalizio” ambalo limetafsiriwa kutokana na neno la Kigiriki syn·teʹlei·a. Katika Tafsiri ya Ulimwengu Mpya, neno hilo limetafsiriwa kotekote kuwa “umalizio,” lakini neno la Kigiriki te’los ambalo linahusiana nalo, limetafsiriwa kuwa “mwisho.” Tunaweza kuelewa tofauti ya maneno hayo mawili kwa kutumia mfano wa hotuba inayotolewa kwenye Jumba la Ufalme. Umalizio wa hotuba ni sehemu ya mwisho ya hotuba. Katika sehemu hiyo, msemaji anatumia muda mfupi kuwakumbusha wasikilizaji mambo ambayo amezungumzia halafu anawaeleza jinsi habari hiyo inavyowahusu. Mwisho wa hotuba ni wakati msemaji anapoondoka kwenye jukwaa. Vivyo hivyo, kulingana na Biblia, usemi “umalizio wa mfumo wa mambo” unamaanisha kipindi cha wakati kinachoongoza kwenye mwisho na kinatia ndani mwisho wa mfumo wa mambo.

3. Ni baadhi ya mambo gani yanayotukia wakati wa kuwapo kwa Yesu?

3 Mitume waliuliza kuhusu “kuwapo” gani? Neno hilo limetafsiriwa kutokana na neno la Kigiriki pa·rou·siʹa. * Pa·rou·siʹa au kuwapo kwa Kristo, kulianza Yesu alipowekwa rasmi kuwa Mfalme mbinguni mwaka wa 1914, na kungali kunaendelea, na kunatia ndani ile “dhiki kuu,” wakati atakapokuja kuwaharibu waovu. (Mt. 24:21) Mambo mbalimbali yanatukia wakati wa kuwapo kwa Yesu, kama vile “siku za mwisho” za mfumo huu mbovu wa mambo, kukusanywa kwa wale waliochaguliwa, na kufufuliwa kwenye uhai wa kimbingu. (2 Tim. 3:1; 1 Kor. 15:23; 1 The. 4:15-17; 2 The. 2:1) Tunaweza kusema kwamba kipindi cha “umalizio wa mfumo wa mambo” (syn·teʹlei·a) kinaenda sambamba na kipindi kinachoitwa kuwapo kwa Kristo (pa·rou·siʹa).

Kipindi Kirefu cha Wakati

4. Kuwapo kwa Yesu kunalingana jinsi gani na matukio ya siku za Noa?

4 Uhakika wa kwamba neno pa·rou·siʹa linamaanisha kipindi kirefu cha wakati unapatana na yale ambayo Yesu alisema kuhusu kuwapo kwake. (Soma Mathayo 24:37-39.) Ona kwamba Yesu hakulinganisha kuwapo kwake na kile kipindi kifupi wakati Gharika ilipokuja katika siku za Noa. Badala yake, alilinganisha kuwapo kwake na kipindi kirefu zaidi cha wakati kilichotangulia Gharika. Noa alijenga safina na kuhubiri katika kipindi hicho, mpaka Gharika ilipokuja. Matukio hayo yalitukia kwa makumi ya miaka. Vivyo hivyo, kuwapo kwa Kristo kunatia ndani matukio yanayotangulia na pia ile dhiki kuu.—2 The. 1:6-9.

5. Maneno ya Ufunuo sura ya 6 yanaonyesha namna gani kwamba kuwapo kwa Yesu ni kipindi kirefu cha wakati?

5 Unabii mwingine wa Biblia unaonyesha wazi kwamba kuwapo kwa Kristo kunamaanisha kipindi kirefu cha wakati wala si kuja kwake tu kuwaharibu waovu. Katika kitabu cha Ufunuo Yesu anaonekana akiendesha farasi mweupe na akipewa taji. (Soma Ufunuo 6:1-8.) Baada ya kuvishwa taji na kuwa Mfalme mwaka wa 1914, Yesu anaonekana akienda ‘akishinda na kukamilisha ushindi wake.’ Kisha, simulizi hilo linaonyesha kwamba anafuatwa na wapanda-farasi wanaoendesha farasi wenye rangi mbalimbali. Wapanda-farasi hao wa kinabii wanafananisha vita, upungufu wa chakula, na tauni au magonjwa ya kuambukiza. Hali hizo zote zimetukia katika kipindi hiki kirefu cha wakati ambacho kinaitwa “siku za mwisho.” Tunaona unabii huo ukitimizwa katika siku zetu.

6. Ufunuo sura ya 12 inatusaidia kuelewa nini kuhusu kuwapo kwa Kristo?

6 Ufunuo sura ya 12 inaeleza mambo zaidi kuhusu kusimamishwa kwa Ufalme wa Mungu mbinguni. Andiko hilo linataja vita vilivyotukia katika makao ya roho. Mikaeli, ambaye ni Yesu Kristo katika cheo chake cha kimbingu, na malaika wake wanapigana na Ibilisi na roho wake waovu. Matokeo ni kwamba Shetani Ibilisi na majeshi yake wanatupwa duniani. Simulizi hilo linatuambia kwamba Ibilisi anapotupwa chini ana hasira kali “akijua kwamba ana kipindi kifupi cha wakati.” (Soma Ufunuo 12:7-12.) Basi ni wazi kwamba baada ya Ufalme wa Kristo kusimamishwa mbinguni kunakuwa na kipindi ambacho “ole” inaongezeka duniani na kwa watu wanaokaa humo.

7. Zaburi ya pili inazungumza kuhusu nini, na watu wanapewa nafasi gani katika zaburi hiyo?

7 Pia, zaburi ya pili inazungumza kinabii kuhusu kuwekwa kwa Yesu kuwa Mfalme juu ya Mlima Sinai wa kimbingu. (Soma Zaburi 2:5-9; 110:1, 2.) Hata hivyo, zaburi hiyo inaonyesha pia kwamba kuna kipindi cha wakati ambacho watawala wa dunia, pamoja na raia wao, wanapewa nafasi ya kujitiisha kwa utawala wa Kristo. Wanahimizwa ‘waonyesha ufahamu’ na kukubali “kurekebishwa.” Ndiyo, wakati huo, “wenye furaha ni wale wote wanaomkimbilia [Mungu]” kwa kumtumikia Yehova na Mfalme wake aliyewekwa rasmi. Hivyo basi, watawala na raia wana nafasi ya kubadilika wakati wa kuwapo kwa Yesu akiwa katika mamlaka ya kifalme.—Zab. 2:10-12.

Kuitambua Ishara

8, 9. Ni nani ambao wangetambua ishara ya kuwapo kwa Kristo na kuelewa maana yake?

8 Yesu alipoulizwa na Mafarisayo kuhusu wakati ambapo Ufalme ungekuja, aliwajibu kwamba haungekuja “kwa wonyesho wenye kutokeza sana” kama walivyofikiri. (Luka 17:20, 21) Watu wasio waamini hawangeelewa. Wangeelewa namna gani ikiwa hata hawakumtambua Yesu kuwa Mfalme wao wa wakati ujao! Basi ni nani ambao wangetambua ishara ya kuwapo kwa Kristo na kuelewa maana yake?

9 Yesu aliendelea kusema kwamba wanafunzi wake wangeona ishara hiyo waziwazi kama wanavyoona ‘umeme, unapowaka, na kung’aa kutoka sehemu moja chini ya mbingu mpaka sehemu nyingine.’ (Soma Luka 17:24-29.) Inapendeza kuona kwamba Mathayo 24:23-27 linahusianisha jambo hilohilo na ishara ya kuwapo kwa Kristo.

Kizazi Kinachoona Ile Ishara

10, 11. (a) Ni maelezo gani yaliyotolewa wakati uliopita kuhusu kile “kizazi” kinachotajwa katika Mathayo 24:34? (b) Ni nani ambao bila shaka wanafunzi wa Yesu walielewa kwamba wangekuwa sehemu ya “kizazi” hicho?

10 Wakati uliopita, gazeti hili lilieleza kwamba katika karne ya kwanza, “kizazi hiki” kinachotajwa katika Mathayo 24:34 kilimaanisha “kizazi cha Wayahudi wasioamini ambao waliishi wakati huo.” * Ilionekana kwamba maelezo hayo yalipatana na akili kwa sababu pindi nyingine zote ambazo Yesu alitumia neno “kizazi” halikuwa na maana nzuri, na mara nyingi, Yesu alitumia kivumishi cha sifa mbaya kama vile “kiovu,” ili kufafanua kizazi alichokuwa akizungumzia. (Mt. 12:39; 17:17; Marko 8:38) Hivyo, ilieleweka kwamba katika utimizo wa leo, Yesu alikuwa akizungumza kuhusu kizazi kiovu cha wasio waamini ambao wangeona ishara ya “umalizio wa mfumo wa mambo” (syn·teʹlei·a) na ya mwisho wa mfumo (teʹlos).

11 Ni kweli kwamba Yesu aliposema “kizazi” kiovu, alikuwa akizungumza na au kuhusu watu waovu wa siku zake. Lakini je, ni lazima “kizazi” anachozungumzia katika Mathayo 24:34 kiwe kilimaanisha watu waovu walioishi siku zake? Kumbuka kwamba wanafunzi wanne wa Yesu walimkaribia “faraghani.” (Mt. 24:3) Kwa kuwa Yesu hakutumia maneno au vivumishi vya sifa mbaya alipozungumza nao kuhusu “kizazi hiki,” bila shaka mitume hao wangeelewa kwamba wao pamoja na wanafunzi wenzao wangekuwa sehemu ya “kizazi” ambacho hakingepitilia mbali kamwe “mpaka mambo yote hayo yatukie.”

12. Kulingana na mistari mingine katika Mathayo sura ya 24, Yesu alikuwa akizungumza kuhusu nani alipotumia neno “kizazi”?

12 Tunakata kauli hiyo kwa msingi gani? Kwa kuchunguza kwa uangalifu mistari mingine katika sura hiyo. Kulingana na Mathayo 24:32, 33, Yesu alisema hivi: “Basi jifunzeni jambo hili kutokana na mtini kama mfano: Mara tu tawi lake changa linapokuwa jororo na kutoa majani, mnajua kwamba kiangazi kiko karibu. Vivyo hivyo ninyi pia, mnapoona mambo yote hayo, jueni kwamba yuko karibu milangoni.” (Linganisha Marko 13:28-30; Luka 21:30-32.) Kisha, tunasoma hivi kwenye Mathayo 24:34: “Kwa kweli ninawaambia ninyi kwamba kizazi hiki hakitapitilia mbali kamwe mpaka mambo yote hayo yatukie.”

13, 14. Kwa nini tunaweza kusema kwamba ni lazima kile “kizazi” ambacho Yesu alizungumzia kilikuwa wanafunzi wake?

13 Yesu alisema kwamba wanafunzi wake, ambao punde si punde wangetiwa mafuta kwa roho takatifu, ndio wangeweza kukata kauli fulani walipoona “mambo yote hayo” yakitukia. Kwa hiyo, lazima Yesu awe alikuwa akizungumza kuhusu wanafunzi wake aliposema hivi: “Kizazi hiki hakitapitilia mbali kamwe mpaka mambo yote hayo yatukie.”

14 Tofauti na watu wasio waamini, wanafunzi wa Yesu wangeona ile ishara na pia wangeelewa maana ya ishara hiyo. ‘Wangejifunza’ kutokana na matukio ya ishara hiyo na ‘kujua’ kikweli maana yake. Wangetambua kabisa kwamba “yuko karibu, milangoni.” Ni kweli kwamba Wayahudi wasio waamini na pia Wakristo watiwa-mafuta waaminifu waliona maneno ya Yesu yakitimia kwa kadiri fulani katika karne ya kwanza, lakini ni wafuasi wake watiwa-mafuta tu walioishi wakati huo ndio wangejifunza kutokana na matukio hayo na kuelewa kikweli maana ya mambo waliyokuwa wakiona.

15. (a) Ni nani wanaofanyiza “kizazi” cha siku zetu ambacho Yesu alizungumzia? (b) Kwa nini hatuwezi kuhesabu urefu kamili wa “kizazi hiki”? (Ona sanduku kwenye ukurasa wa 25.)

15 Leo, watu ambao hawaelewi kweli ya Mungu wanafikiri kwamba ishara ya kuwapo kwa Yesu haijatokea kwa “wonyesho wenye kutokeza sana.” Wanasema kwamba mambo yote yanaendelea sawasawa tangu zamani. (2 Pet. 3:4) Kwa upande mwingine, ndugu waaminifu watiwa-mafuta wa Kristo, yaani, jamii ya Yohana ya leo, wametambua ishara hiyo kama umeme unaowaka nao wameelewa maana yake ya kweli. Wakiwa kikundi, watiwa-mafuta hao wanafanyiza “kizazi” cha siku zetu, jamii ambayo haitapitilia mbali kamwe “mpaka mambo yote hayo yatukie.” * Hilo linadokeza kwamba wengine kati ya ndugu za Kristo watiwa-mafuta bado watakuwa hai duniani wakati dhiki kuu iliyotabiriwa itakapoanza.

“Endeleeni Kukesha”

16. Ni lazima wanafunzi wote wa Kristo wafanye nini?

16 Hata hivyo, ni lazima tufanye mengi zaidi ya kuitambua ile ishara. Yesu aliendelea kusema hivi: “Lile ninalowaambia ninyi ninawaambia wote, Endeleeni kukesha.” (Marko 13:37) Hilo ni jambo la maana sana kwetu sote leo tuwe watiwa-mafuta au umati mkubwa. Miaka zaidi ya 90 imepita tangu Yesu alipowekwa rasmi kuwa Mfalme mbinguni mwaka wa 1914. Ni lazima tuwe tayari na kuendelea kukesha hata ingawa si rahisi kufanya hivyo. Kujua kwamba Kristo yupo na anatawala akiwa Mfalme bila kuonekana kunatusaidia kufanya hivyo. Pia, kunatusaidia kutambua kwamba hivi karibuni atakuja kuwaharibu maadui wake ‘katika saa tusiyotazamia.’—Luka 12:40.

17. Kuelewa maana ya kuwapo kwa Kristo kunatufanya tuhisi namna gani, na tunapaswa kuazimia kufanya nini?

17 Kuelewa maana ya kuwapo kwa Kristo kunatusaidia tuwe macho tukifikiria uharaka wa nyakati. Tunajua kwamba tayari Yesu yupo naye amekuwa akitawala akiwa Mfalme mbinguni bila kuonekana tangu 1914. Hivi karibuni, atakuja kuwaharibu waovu na kuleta mabadiliko makubwa katika dunia yote. Kwa hiyo, tunapaswa kuazimia kuliko wakati mwingine wowote kushiriki kwa bidii katika kazi ambayo Yesu alitabiri aliposema: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho [teʹlos] utakapokuja.”—Mt. 24:14.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Maana ya neno pa·rou·siʹa inaonyeshwa na 2 Wakorintho 10:10, 11 na Wafilipi 2:12 ambapo “kuwapo” na “kutokuwapo” kwa mtume Paulo kunatofautishwa. Kwa habari zaidi, ona Insight on the Scriptures, Buku la 2, ukurasa wa 676-679 au Étude perspicace des Écritures, Buku la 2, ukurasa wa 648-651.

^ fu. 10 Ona Mnara wa Mlinzi, Novemba 1, 1995, ukurasa wa 11-15, 19, 30, 31.

^ fu. 15 Inaonekana kwamba kizazi hiki kinaishi wakati wa kutimizwa kwa maono ya kwanza ya kitabu cha Ufunuo. (Ufu. 1:10–3:22) Sehemu hiyo ya siku ya Bwana inaanza mwaka wa 1914 mpaka mshiriki wa mwisho mtiwa-mafuta aliye mwaminifu atakapokufa na kufufuliwa.—Ona Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu!, ukurasa wa 24, fungu la 4.

Ungetoa Jibu Gani?

• Tunajua jinsi gani kwamba kuwapo kwa Yesu ni kipindi kirefu cha wakati?

• Ni nani wanaotambua ishara ya kuwapo kwa Yesu na kuelewa maana yake?

• Ni nani wanaofanyiza kizazi cha siku zetu kinachotajwa katika Mathayo 24:34?

• Kwa nini hatuwezi kuhesabu urefu kamili wa “kizazi hiki”?

[Maswali ya Funzo]

[Sanduku katika ukurasa wa 25]

Je, Tunaweza Kuhesabu Urefu wa “Kizazi Hiki”?

Kwa kawaida, neno “kizazi” linamaanisha watu wenye umri mbalimbali ambao wanaishi katika kipindi fulani cha wakati au tukio fulani. Kwa mfano, andiko la Kutoka 1:6 linatuambia hivi: “Mwishowe Yosefu akafa, na pia ndugu zake wote na kizazi hicho chote.” Yosefu na ndugu zake walikuwa na umri mbalimbali, lakini waliona mambo yaleyale katika kipindi kilekile cha wakati. “Kizazi hicho” kilitia ndani baadhi ya ndugu za Yosefu ambao walizaliwa kabla yake. Wengine wao waliishi muda mrefu zaidi ya Yosefu. (Mwa. 50:24) Watu fulani wa “kizazi hicho,” kama vile Benyamini, walizaliwa baada ya Yosefu kuzaliwa na huenda waliendelea kuishi baada ya Yosefu kufa.

Kwa hiyo, neno “kizazi” linapotumiwa kuwahusu watu wanaoishi katika kipindi fulani, urefu kamili wa kipindi hicho hauwezi kujulikana lakini kipindi hicho kina mwisho na hakiwezi kuwa kirefu kupita kiasi. Kwa hivyo, Yesu alipotumia usemi “kizazi hiki” katika Mathayo 24:34, hakuwapa wanafunzi wake njia ya kuhesabu na kujua “siku za mwisho” zingekwisha wakati gani. Badala yake, Yesu alikazia kwamba hawangejua “siku ile na saa ile.”—2 Tim. 3:1; Mt. 24:36.

[Picha katika ukurasa wa 22, 23]

Baada ya kuvishwa taji na kuwa Mfalme mwaka wa 1914, Yesu anaonyeshwa “akishinda”

[Picha katika ukurasa wa 24]

“Kizazi hiki hakitapitilia mbali kamwe mpaka mambo yote hayo yatukie”