Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Marko

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Marko

Neno la Yehova Liko Hai

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Marko

INJILI ya Marko ndiyo fupi zaidi kati ya zile Injili nne. Iliandikwa na Yohana Marko miaka 30 baada ya kufa na kufufuliwa kwa Yesu Kristo. Inasimulia matukio mengi sana yenye kusisimua kuhusu huduma ya Yesu ya miaka mitatu na nusu.

Inaonekana kwamba kitabu cha Marko kiliandikwa kwa ajili ya watu wasio Wayahudi, hasa Waroma. Kitabu hicho kinaonyesha Yesu akiwa Mwana mfanya-miujiza wa Mungu. Pia, Yesu anaonyeshwa akiendesha kwa bidii kampeni ya kuhubiri. Kinakazia zaidi mambo ambayo Yesu alifanya badala ya yale ambayo alifundisha. Kukazia uangalifu Injili ya Marko kutatia nguvu imani yetu katika Masihi na kutuchochea tuwe watangazaji wenye bidii wa ujumbe wa Mungu katika huduma ya Kikristo.—Ebr. 4:12.

HUDUMA YA PEKEE HUKO GALILAYA

(Marko 1:1–9:50)

Marko anazungumzia utendaji wa Yohana Mbatizaji na pia kukaa kwa Yesu nyikani kwa siku 40 katika mistari 14 tu, kisha anaanza kusimulia kwa njia yenye kusisimua kuhusu huduma ya Yesu huko Galilaya. Maneno “mara moja” ambayo yanarudiwa-rudiwa yanaonyesha uharaka wa masimulizi hayo.—Marko 1:10, 12.

Yesu anakamilisha kampeni tatu za kuhubiri huko Galilaya kwa miaka isiyozidi mitatu. Marko anafuata hasa utaratibu wa wakati wa matukio katika masimulizi yake. Mahubiri ya Mlimani hayatajwi, na vilevile hotuba nyingine ndefu za Yesu.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

1:15—Ni “wakati uliowekwa” wa nini ambao ulitimizwa? Yesu alikuwa akisema kwamba wakati uliowekwa wa kuanza huduma yake ulikuwa umetimia. Ufalme wa Mungu ulikuwa umekaribia kwa sababu alikuwepo akiwa Mfalme Aliyechaguliwa. Watu wenye mioyo minyoofu wangeweza kukubali ujumbe aliokuwa akihubiri na kuchukua hatua ambazo zingewafanya wakubaliwe na Mungu.

1:44; 3:12; 7:36—Kwa nini Yesu hakutaka miujiza yake itangazwe? Yesu hakutaka watu wakate kauli wakitegemea ripoti zenye kusisimua au zilizotiwa chumvi, alitaka wajionee wenyewe kwamba alikuwa Kristo na wafanye uamuzi wa kibinafsi wakitegemea uthibitisho huo. (Isa. 42:1-4; Mt. 8:4; 9:30; 12:15-21; 16:20; Luka 5:14) Alimruhusu tu mtu aliyekuwa na roho waovu katika nchi ya Wagerasene atangaze. Yesu alimwambia aende nyumbani na kuwajulisha watu wake wa ukoo. Yesu alikuwa amesihiwa aondoke katika eneo hilo, kwa hiyo hangekutana na watu wengi wa huko. Kuwapo na pia ushuhuda wa mtu ambaye Yesu alikuwa amemfanyia jambo jema kungepinga habari zozote mbaya kuhusu nguruwe walioangamia.—Marko 5:1-20; Luka 8:26-39.

2:28—Kwa nini Yesu anaitwa “Bwana hata wa sabato”? Mtume Paulo aliandika hivi: “Sheria ina kivuli cha mambo mema yatakayokuja.” (Ebr. 10:1) Kulingana na Sheria, Sabato ilikuja baada ya siku sita za kazi, na Yesu aliwaponya watu wengi siku hiyo. Hilo lilionyesha kimbele pumziko lenye amani na baraka nyingine ambazo wanadamu watapata chini ya Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo baada ya utawala wenye kuonea wa Shetani kuondolewa. Kwa hiyo, Mfalme wa Ufalme huo ni “Bwana wa sabato” pia.—Mt. 12:8; Luka 6:5.

3:5; 7:34; 8:12—Marko alijua jinsi gani mambo mengi kuhusu hali ya kihisia ya Yesu? Marko hakuwa mmoja wa wale mitume 12 wala hakuwa mshiriki wa karibu wa Yesu. Mapokeo ya zamani yanadai kwamba mwandamani wa karibu wa Marko, mtume Petro, ndiye aliyempa Marko habari nyingi.—1 Pet. 5:13.

6:51, 52—Ni nini “maana ya ile mikate” ambayo wanafunzi hawakufahamu? Saa chache tu mapema, Yesu alikuwa amelisha wanaume 5,000 bila kuhesabu wanawake na watoto kwa mikate mitano na samaki wawili tu. “Maana ya ile mikate” ambayo wanafunzi walipaswa kufahamu kutokana na tukio hilo ni kwamba Yehova Mungu alikuwa amempa Yesu nguvu za kufanya miujiza. (Marko 6:41-44) Ikiwa wangeelewa Yesu alipewa nguvu nyingi kadiri gani, hawangeshangaa alipotembea juu ya maji kimuujiza.

8:22-26—Kwa nini Yesu alimponya kwa hatua mbili mtu aliyekuwa kipofu? Huenda Yesu alifanya hivyo kwa sababu alimjali mtu huyo. Kwa muda mrefu mtu huyo alizoea giza, kwa hiyo kumponya hatua kwa hatua kulimwezesha kuzoea mwangaza wa jua.

Mambo Tunayojifunza:

2:18; 7:11; 12:18; 13:3. Marko anaeleza desturi, maneno, imani, na mahali ambapo huenda wasomaji wasio Wayahudi hawakujua. Anaeleza wazi kwamba Mafarisayo “walikuwa na zoea la kufunga,” kwamba korbani ni “zawadi iliyowekwa wakfu kwa Mungu,” kwamba masadukayo “husema hakuna ufufuo,” na kwamba hekalu lilikuwa “linaonekana” kutoka kwenye “Mlima wa Mizeituni.” Kwa kuwa ukoo wa Masihi ungewapendeza hasa Wayahudi, Marko hauzungumzii hata kidogo. Hivyo, Marko anatuwekea mfano. Tunapaswa kufikiria malezi ya wasikilizaji wetu tunaposhiriki katika huduma ya Kikristo au tunapotoa hotuba katika mikutano ya kutaniko.

3:21. Watu wa jamaa ya Yesu hawakuwa waamini. Hivyo, anawahurumia wale ambao kwa sababu ya imani yao wanapingwa au kudhihakiwa na watu wao wa jamaa ambao si waamini.

3:31-35. Alipobatizwa, Yesu akawa Mwana wa kiroho wa Mungu, na mama yake alikuwa “Yerusalemu la juu.” (Gal. 4:26) Tangu wakati huo na kuendelea, Yesu alithamini na kuwa na uhusiano wa karibu zaidi na wanafunzi wake kuliko watu wake wa ukoo. Hilo linatufundisha kwamba tunapaswa kutanguliza mambo ya kiroho katika maisha yetu.—Mt. 12:46-50; Luka 8:19-21.

8:32-34. Tunapaswa kutambua na kukataa mara moja fadhili yoyote isiyofaa tunayoonyeshwa na wengine. Mfuasi wa Kristo anapaswa kuwa tayari ‘kujikana mwenyewe,’ yaani, kujinyima na kukataa tamaa na miradi ya kichoyo. Anapaswa kuwa tayari “kuuchukua mti wake wa mateso,” yaani, kuteseka ikiwa ni lazima, kuaibishwa, kuteswa, au hata kuuawa kwa sababu ya kuwa Mkristo. Ni lazima ‘amfuate Yesu sikuzote,’ afuate kielelezo Chake cha maisha. Tukiwa wanafunzi ni lazima tusitawishe na kudumisha roho ya kujidhabihu kama ya Kristo Yesu.—Mt. 16:21-25; Luka 9:22, 23.

9:24. Hatupaswi kuona haya kuwaambia wengine kuhusu imani yetu au kuomba tupewe imani zaidi.—Luka 17:5.

MWEZI WA MWISHO

(Marko 10:1–16:8)

Kuelekea mwishoni mwa mwaka wa 32 W.K., Yesu anakuja kwenye “mipaka ya Yudea na ng’ambo ya Yordani,” na umati unamjia tena. (Marko 10:1) Baada ya kuhubiri huko, anaelekea Yerusalemu.

Mnamo Nisani 8, Yesu yuko Bethania. Ameketi kwenye mlo, na mwanamke mmoja anaingia na kumimina mafuta yenye marashi juu ya kichwa chake. Matukio yote kuanzia Yesu anapoingia kwa ushindi Yerusalemu mpaka ufufuo wake yanasimuliwa kulingana na wakati yalipotukia.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

10:17, 18—Kwa nini Yesu alimsahihisha mtu fulani aliyemwita “Mwalimu Mwema”? Kwa kukataa cheo hicho cha kumsifu, Yesu alielekeza utukufu kwa Yehova na kuonyesha kwamba Mungu wa kweli ndiye chanzo cha vitu vyote vyema. Zaidi ya hayo, Yesu alikazia fikira kweli ya msingi ya kwamba Muumba wa vitu vyote, Yehova Mungu, ndiye peke yake aliye na haki ya kuweka viwango vya mema na mabaya.—Mt. 19:16, 17; Luka 18:18, 19.

14:25—Yesu alimaanisha nini alipowaambia hivi mitume wake waaminifu: “Sitakunywa tena kamwe divai ya mzabibu mpaka siku ile nitakapokunywa ikiwa mpya katika ufalme wa Mungu”? Yesu hakuwa akidokeza kwamba kuna divai halisi mbinguni. Hata hivyo, kwa kuwa nyakati nyingine divai inafananisha kushangilia, Yesu alikuwa akizungumzia shangwe ya kuwa katika Ufalme pamoja na wafuasi wake watiwa-mafuta waliofufuliwa.—Zab. 104:15; Mt. 26:29.

14:51, 52—Ni kijana gani ‘aliyekimbia akiwa uchi’? Ni Marko peke yake anayetaja kisa hiki, kwa hiyo ni jambo linalopatana na akili kukata kauli kwamba alikuwa akizungumza kuhusu kisa chake mwenyewe.

15:34—Je, maneno haya ya Yesu: “Mungu wangu, Mungu wangu, kwa nini umeniacha?” yanaonyesha kwamba hakuwa na imani? Hapana. Ingawa hatujui kwa uhakika Yesu alikuwa na nia gani aliposema maneno hayo, huenda yanaonyesha kwamba Yesu alitambua kuwa Yehova alikuwa ameondoa ulinzi Wake ili utimilifu wa Mwana Wake ujaribiwe kikamili. Inawezekana pia kwamba Yesu alisema hivyo kwa sababu alitaka kutimiza unabii wa Zaburi 22:1 ambao ulimhusu.—Mt. 27:46.

Mambo Tunayojifunza:

10:6-9. Kusudi la Mungu ni kwamba wenzi wa ndoa wasiachane kamwe. Kwa hiyo, badala ya kukimbilia kutafuta talaka, waume na wake wanapaswa kujitahidi kutumia kanuni za Biblia kutatua matatizo yoyote ambayo yanaweza kutokea katika ndoa.—Mt. 19:4-6.

12:41-44. Mfano wa mjane maskini unatufundisha kwamba tunapaswa kutegemeza ibada ya kweli bila uchoyo.

[Picha katika ukurasa wa 29]

Kwa nini Yesu alimwambia mtu huyu awajulishe watu wake wa ukoo mambo aliyomtendea?