Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tembea Katika Njia za Yehova

Tembea Katika Njia za Yehova

Tembea Katika Njia za Yehova

“Mwenye furaha ni kila mtu anayemwogopa Yehova. Anayetembea katika njia zake.”—ZAB. 128:1.

1, 2. Kwa nini tuna hakika kwamba furaha inaweza kupatikana?

FURAHA—kila mtu anaitaka. Lakini, hapana shaka utakubali kwamba kutamani furaha na hata kuitafuta si sawa na kuwa na furaha.

2 Hata hivyo, furaha inaweza kupatikana. “Mwenye furaha ni kila mtu anayemwogopa Yehova. Anayetembea katika njia zake,” inasema Zaburi 128:1. Tutapata furaha ikiwa tutamwabudu Mungu na kutembea katika njia zake kwa kufanya mapenzi yake. Hilo linaweza kuwa na uvutano gani juu ya mwenendo wetu na sifa tunazoonyesha?

Uwe Mwenye Kutegemeka

3. Kutegemeka kunahusiana namna gani na kujiweka wakfu kwa Mungu?

3 Wale wanaomwogopa Yehova ni wenye kutegemeka kama Yehova alivyo. Yehova alitimiza ahadi zote alizowapa Waisraeli wa kale. (1 Fal. 8:56) Ahadi ya kujiweka wakfu kwa Mungu ndiyo ahadi kubwa zaidi tunayoweza kutoa, na kusali kwa ukawaida kutatusaidia kuitimiza. Tunaweza kusali kama mtunga-zaburi Daudi alivyosali: “Wewe mwenyewe, Ee Mungu, umesikiliza nadhiri zangu. . . . Jina lako nitalipigia muziki milele, ili nipate kutimiza nadhiri zangu siku baada ya siku.” (Zab. 61:5, 8; Mhu. 5:4-6) Ili tuwe marafiki wa Mungu, ni lazima tuwe wenye kutegemeka.—Zab. 15:1, 4.

4. Yeftha na binti yake walitenda jinsi gani kuhusiana na nadhiri ya Yeftha kwa Yehova?

4 Katika siku za Waamuzi wa Israeli, Yeftha aliweka nadhiri kwamba ikiwa Yehova angempa ushindi juu ya Waamoni, yeye angemtolea Yehova “kuwa toleo la kuteketezwa” yeyote ambaye angekuwa wa kwanza kumpokea kutoka vitani. Binti yake, mtoto wake pekee, ndiye aliyekuwa wa kwanza kumpokea. Wakiwa na imani katika Yehova, Yeftha na binti yake ambaye hakuwa ameolewa walitimiza nadhiri hiyo. Ijapokuwa ndoa na kuzaa watoto kulithaminiwa sana katika Israeli, binti ya Yeftha alikubali kwa kupenda kubaki mseja, na hivyo akawa na pendeleo la kutoa utumishi mtakatifu katika patakatifu pa Yehova.—Amu. 11:28-40.

5. Hana alikuwa mwenye kutegemeka katika njia gani?

5 Hana, mwanamke aliyemwogopa Mungu alikuwa mwenye kutegemeka. Yeye, mume wake Mlawi aliyeitwa Elkana, na mke mwenzake aliyeitwa Penina, waliishi katika eneo lenye milima huko Efraimu. Penina alizaa watoto kadhaa na akamdhihaki Hana ambaye alikuwa tasa. Alimdhihaki hasa familia yao ilipoenda kwenye maskani. Pindi moja, Hana aliweka nadhiri kwamba iwapo angezaa mwana, angempa Yehova mwana huyo. Muda si muda, alipata mimba na kuzaa mvulana ambaye aliitwa Samweli. Baada ya kuachishwa kunyonya, Hana alimtoa kwa Mungu huko Shilo, akimwazima Samweli kwa Yehova “siku zote za maisha yake.” (1 Sam. 1:11) Hivyo akatimiza nadhiri yake hata ingawa hakujua kama angezaa watoto wengine baadaye.—1 Sam. 2:20, 21.

6. Tikiko alionyesha jinsi gani kwamba alikuwa mwenye kutegemeka?

6 Tikiko, Mkristo aliyeishi katika karne ya kwanza alikuwa mwanamume mwenye kutegemeka na “mhudumu mwaminifu.” (Kol. 4:7) Tikiko alisafiri pamoja na mtume Paulo kutoka Ugiriki hadi Makedonia, na kuingia Asia Ndogo, na huenda hata alifika Yerusalemu. (Mdo. 20:2-4) Huenda Tikiko ndiye “ndugu ambaye” alimsaidia Tito kugawa zile zawadi kwa waamini wenzao waliokuwa na uhitaji huko Yudea. (2 Kor. 8:18, 19; 12:18) Paulo alipofungwa gerezani huko Roma mara ya kwanza, Tikiko akiwa mwakilishi wake mwenye kutegemeka alipeleka barua za Paulo kwa waamini wenzake huko Efeso na Kolosai. (Efe. 6:21, 22; Kol. 4:8, 9) Alipofungwa mara ya pili huko Roma, Paulo alimtuma Tikiko huko Efeso. (2 Tim. 4:12) Sisi pia tukiwa wenye kutegemeka, tutapata baraka katika utumishi wa Yehova.

7, 8. Kwa nini tunaweza kusema kwamba Daudi na Yonathani walikuwa marafiki wa kweli?

7 Mungu anataka tuwe marafiki wenye kutegemeka. (Met. 17:17) Yonathani, mwana wa Mfalme Sauli, alikuwa rafiki ya Daudi. Yonathani aliposikia kwamba Daudi alikuwa amemuua Goliathi, “nafsi ya Yonathani ikashikamana na nafsi ya Daudi, na Yonathani akaanza kumpenda kama nafsi yake mwenyewe.” (1 Sam. 18:1, 3) Yonathani hata alimwonya Daudi Sauli alipotaka kumuua. Daudi alipokimbia, Yonathani alikutana naye na kufanya agano pamoja naye. Karibu Sauli amuue Yonathani alipomwambia kumhusu Daudi, lakini marafiki hao wawili walikutana na kuanzisha tena urafiki wao. (1 Sam. 20:24-41) Walipokutana mara ya mwisho, Yonathani aliutia nguvu mkono wa Daudi “kuhusiana na Mungu.”—1 Sam. 23:16-18.

8 Yonathani alikufa katika vita dhidi ya Wafilisti. (1 Sam. 31:6) Katika maombolezo yake, Daudi aliimba hivi: “Nimesikitika kwa ajili yako, Yonathani ndugu yangu, ulinipendeza sana. Upendo wako kwangu ulikuwa wa ajabu sana kuliko upendo kutoka kwa wanawake.” (2 Sam. 1:26) Upendo huo ulikuwa wa kirafiki wala haukuwa wa kimahaba. Daudi na Yonathani walikuwa marafiki wa kweli.

Sikuzote Uwe ‘Mnyenyekevu Katika Akili’

9. Umuhimu wa unyenyekevu unaonyeshwa namna gani katika Waamuzi sura ya 9?

9 Ili tuwe marafiki wa Mungu, ni lazima tuwe “wanyenyekevu katika akili.” (1 Pet. 3:8; Zab. 138:6) Umuhimu wa unyenyekevu unaonyeshwa katika Waamuzi sura ya 9. Yothamu, mwana wa Gideoni alisema hivi: “Hapo zamani za kale, miti ilienda kumtia mafuta mfalme juu yao.” Mzeituni, mtini, na mzabibu ulitajwa. Miti hiyo iliwakilisha watu waliostahili lakini ambao hawakutafuta kuwatawala Waisraeli wenzao. Lakini mkwamba, ambao haufai kwa kazi yoyote ile ila kwa kuni, uliwakilisha utawala wa Abimeleki mwenye kiburi, muuaji aliyetamani kuwatawala wenzake. Ingawa ‘alijitwalia ukuu juu ya Israeli kwa miaka mitatu,’ alikufa kifo cha mapema. (Amu. 9:8-15, 22, 50-54) Ni vizuri kama nini kuwa “wanyenyekevu katika akili”!

10. Umejifunza nini kutokana na tendo la Herode la ‘kutompa Mungu utukufu’?

10 Katika karne ya kwanza W.K., uhusiano uliharibika kati ya Mfalme Herode Agripa wa Yudea, ambaye alikuwa na kiburi, na wakaaji wa Tiro na Sidoni, ambao walitaka kufanya amani naye. Pindi moja Herode alipokuwa akitoa hotuba, wakaaji hao walipaaza sauti hivi: “Ni sauti ya mungu, wala si ya mwanadamu!” Herode hakukataa kutukuzwa, na malaika wa Yehova akampiga naye akafa kifo kibaya kwa sababu “hakumpa Mungu utukufu.” (Mdo. 12:20-23) Namna gani ikiwa sisi ni wasemaji au walimu stadi wa kweli za Biblia? Na tumtukuze Mungu kwa mambo ambayo anaturuhusu kufanya.—1 Kor. 4:6, 7; Yak. 4:6.

Uwe Hodari na Mwenye Nguvu

11, 12. Kisa cha Enoko kinaonyesha namna gani kwamba Yehova anawapa watumishi wake uhodari na nguvu?

11 Tukitembea katika njia za Yehova kwa unyenyekevu, atatuwezesha kuwa hodari na wenye nguvu. (Kum. 31:6-8, 23) Enoko, mtu wa saba kutoka kwa Adamu, alitembea pamoja na Mungu kwa uhodari kwa kufuatia unyoofu katikati ya kizazi kiovu cha siku zake. (Mwa. 5:21-24) Yehova alimpa Enoko nguvu za kuwatangazia watu hao ujumbe mzito kwa sababu ya maneno na matendo yao ya kutomwogopa Mungu. (Soma Yuda 14, 15.) Je, una uhodari unaohitajiwa ili kutangaza hukumu za Mungu?

12 Kupitia Gharika ya siku za Noa, Yehova alitekeleza hukumu yake juu ya watu wasiomwogopa Mungu. Lakini unabii wa Enoko unatutia moyo kwa kuwa hivi karibuni makumi ya maelfu ya watakatifu wa Mungu watawaharibu watu wa siku zetu ambao hawamwogopi Mungu. (Ufu. 16:14-16; 19:11-16) Yehova anajibu sala zetu kwa kutupa uhodari wa kutangaza ujumbe wake, iwe unahusu hukumu au baraka zake chini ya utawala wa Ufalme.

13. Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba Mungu anaweza kutupa uhodari na nguvu tunazohitaji ili kukabiliana na matatizo yenye kushusha moyo?

13 Ili kukabiliana na matatizo yenye kushusha moyo tunahitaji kitia-moyo na nguvu kutoka kwa Mungu. Esau alipochukua wanawake wawili Wahiti wawe wake zake, wake hao “walikuwa chanzo cha uchungu wa roho kwa [wazazi wake] Isaka na Rebeka.” Hata Rebeka alilalamika hivi: “Nimekuja kuyachukia sana haya maisha yangu kwa sababu ya binti za Hethi. Yakobo [mwana wetu] akichukua mke kutoka kwa binti za Hethi kama hawa kutoka kwa binti za hii nchi, basi maisha yana faida gani kwangu?” (Mwa. 26:34, 35; 27:46) Isaka alichukua hatua na kumtuma Yakobo akatafute mke kati ya waabudu wa Yehova. Ijapokuwa Isaka na Rebeka hawangeweza kubadili kile ambacho Esau alikuwa amefanya, Mungu aliwapa hekima, uhodari, na nguvu za kuendelea kuwa waaminifu Kwake. Tukisali tupewe msaada tunaohitaji, Yehova atatutendea vivyo hivyo.—Zab. 118:5.

14. Msichana mdogo Mwisraeli alionyesha uhodari kwa njia gani?

14 Karne kadhaa baadaye, msichana mdogo Mwisraeli alichukuliwa mateka na kikundi cha waporaji na kuwa kijakazi katika nyumba ya Naamani mwenye ukoma aliyekuwa mkuu wa jeshi la Siria. Msichana huyo alikuwa amesikia kuhusu miujiza ya Mungu iliyofanywa na nabii Elisha, hivyo kwa uhodari akamwambia mke wa Naamani: ‘Ikiwa bwana wangu angeenda Israeli, nabii wa Yehova angemponya ukoma wake.’ Naamani alienda Israeli, naye akaponywa kimuujiza. (2 Fal. 5:1-3) Msichana huyo aliwawekea mfano mzuri kama nini vijana wanaomtegemea Yehova awape uhodari wa kuwatolea ushahidi walimu, wanashule wenzao, na watu wengine!

15. Obadia, msimamizi-nyumba wa Ahabu alichukua hatua gani ya uhodari?

15 Uhodari tunaopewa na Mungu unatusaidia kuvumilia mateso. Mfikirie Obadia, msimamizi-nyumba wa Mfalme Ahabu, ambaye aliishi katika siku za Eliya. Malkia Yezebeli alipoagiza manabii wote wa Mungu wachinjwe, Obadia aliwaficha manabii 100 “wakiwa vikundi viwili vya watu 50 pangoni.” (1 Fal. 18:13; 19:18) Je, ungewasaidia kwa uhodari Wakristo wenzako wanaoteswa, kama Obadia alivyowasaidia manabii wa Yehova?

16, 17. Aristarko na Gayo walifanya nini walipoteswa?

16 Tunapoteswa, tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova atakuwa pamoja nasi. (Rom. 8:35-39) Katika jumba fulani la maonyesho huko Efeso, Aristarko na Gayo, wafanyakazi wenzi wa Paulo, walishambuliwa na umati ambao huenda ulikuwa na maelfu ya watu. Demetrio, yule fundi wa fedha, aliwachochea watu wafanye ghasia. Yeye pamoja na mafundi wengine walitengeneza madhabahu za fedha za mungu wa kike Artemi, na biashara yao iliyowaletea faida kubwa ilihatarishwa kwa sababu kazi ya kuhubiri ya Paulo iliwafanya wakaaji wengi wa jiji hilo waache ibada ya sanamu. Umati huo uliwakokota Aristarko na Gayo ndani ya jumba hilo la maonyesho na kuendelea kupaaza sauti hivi: “Artemi wa Waefeso ni mkuu!” Huenda Aristarko na Gayo walifikiri wangeuawa, lakini karani wa jiji aliutuliza umati.—Mdo. 19:23-41.

17 Ikiwa ungekabili hali kama hiyo, je, ungetafuta maisha matulivu zaidi? Hakuna jambo linaloonyesha kwamba Aristarko na Gayo waliacha kuwa hodari. Aristarko, ambaye alitoka Thesalonike, alijua kwamba kutangaza habari njema kungetokeza mateso. Muda fulani mapema, ghasia zilitokea Paulo alipokuwa akihubiri katika eneo hilo. (Mdo. 17:5; 20:4) Kwa kuwa Aristarko na Gayo walitembea katika njia za Yehova, aliwapa nguvu na uhodari ili wavumilie mateso.

Endelea Kuangalia Faida za wengine

18. Priska na Akila ‘waliendelea kuangalia’ faida za wengine kwa njia gani?

18 Iwe tunateswa au hatuteswi, tunapaswa kuwahangaikia Wakristo wenzetu. Priska na Akila ‘waliendelea kuangalia’ faida za wengine. (Soma Wafilipi 2:4.) Huenda wenzi hao wa ndoa walioweka mfano mzuri walimpa Paulo makao alipokuwa Efeso, ambako Demetrio, yule fundi wa fedha, alichochea ghasia iliyotajwa mapema. Pengine hali hiyo ndiyo iliyowafanya Akila na Priska ‘wahatarishe shingo zao wenyewe’ kwa ajili ya Paulo. (Rom. 16:3, 4; 2 Kor. 1:8) Leo, kuwahangaikia ndugu zetu wanaoteswa kunatufanya tuwe wenye “kujihadhari kama nyoka.” (Mt. 10:16-18) Tunajihadhari tunapofanya kazi yetu nasi tunakataa kuwasaliti ndugu zetu kwa kuwapa watesaji majina yao au habari nyingine.

19. Dorkasi aliwatendea wengine matendo gani mema?

19 Tunaweza kuendelea kuangalia faida za wengine katika njia nyingine mbalimbali. Wakristo fulani wana uhitaji, na huenda tuna uwezo wa kuwatimizia mahitaji hayo. (Efe. 4:28; Yak. 2:14-17) Katika kutaniko la Yopa la karne ya kwanza, kulikuwa na mwanamke mkarimu aliyeitwa Dorkasi. (Soma Matendo 9:36-42.) Dorkasi “alizidi katika matendo mema na zawadi za rehema” ambazo kwa wazi zilitia ndani kuwashonea mavazi wajane wenye uhitaji. Alipokufa mwaka wa 36 W.K., wajane hao walihuzunika sana. Mungu alimtumia mtume Petro kumfufua Dorkasi, na pana uwezekano mkubwa kwamba baada ya hapo alitumia maisha yake hapa duniani akihubiri habari njema kwa furaha na kuwatendea wengine matendo mema. Tunafurahi kama nini kuwa na wanawake Wakristo wasio na ubinafsi miongoni mwetu leo!

20, 21. (a) Kutia moyo kunahusiana namna gani na kuangalia faida za wengine? (b) Unaweza kufanya nini ili uwe mwenye kutia moyo?

20 Tunaangalia faida za wengine kwa kuwatia moyo. (Rom. 1:11, 12) Sila, mfanyakazi mwenzi wa Paulo alikuwa chanzo cha kitia-moyo. Karibu mwaka wa 49 W.K., baada ya uamuzi kufanywa kuhusu kutahiriwa, baraza linaloongoza la Yerusalemu lilituma wawakilishi wawapelekee barua waamini waliokuwa katika maeneo mengine. Sila, Yuda, Barnaba, na Paulo walipeleka barua huko Antiokia. Wakiwa huko, Sila na Yuda ‘waliwatia moyo akina ndugu kwa hotuba nyingi na kuwatia nguvu.’—Mdo. 15:32.

21 Baadaye, Paulo na Sila walifungwa gerezani huko Filipi lakini wakawekwa huru tetemeko la nchi lilipotokea. Walifurahi kama nini kutoa ushahidi na kushuhudia mlinzi wa gereza hilo na watu wa nyumbani mwake wakikubali kuwa waamini! Kabla ya kuondoka katika jiji hilo, Sila na Paulo waliwatia moyo akina ndugu. (Mdo. 16:12, 40) Kama Paulo na Sila, jitahidi kuwatia moyo wengine kupitia maelezo, hotuba, na bidii yako katika utumishi wa shambani. Na unapokuwa na ‘neno la kitia-moyo,’ usikose kamwe ‘kulisema.’—Mdo. 13:15.

Endelea Kutembea Katika Njia za Yehova

22, 23. Tunaweza jinsi gani kufaidika kikweli kutokana na masimulizi ya Biblia?

22 Tunapaswa kushukuru kama nini kwa sababu ya masimulizi ya watu halisi yaliyo katika Neno la Yehova, yule “Mungu wa kitia-moyo chote”! (2 Kor. 1:3, Byington) Ili tufaidike kutokana na masimulizi hayo, ni lazima tutumie maishani mwetu mambo tunayojifunza kutoka katika Biblia na kukubali roho takatifu ya Mungu ituongoze.—Gal. 5:22-25.

23 Kutafakari kuhusu masimulizi ya Biblia kutatusaidia kuonyesha sifa za kimungu. Kutatia nguvu uhusiano wetu na Yehova, ambaye anatupa “hekima na ujuzi na furaha.” (Mhu. 2:26) Kisha, tutaweza kuufanya moyo wa Mungu wenye upendo ushangilie. (Met. 27:11) Na tuazimie kufanya hivyo kwa kuendelea kutembea katika njia za Yehova.

Ungetoa Jibu Gani?

• Unaweza kuonyesha jinsi gani kwamba unategemeka?

• Kwa nini tunapaswa kuwa “wanyenyekevu katika akili”?

• Masimulizi ya Biblia yanaweza kutusaidia namna gani kuwa hodari?

• Tunaweza jinsi gani kuangalia faida za wengine?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 8]

Yeftha aliyekuwa mwenye kutegemeka pamoja na binti yake walitimiza nadhiri ya Yeftha, ijapokuwa haikuwa rahisi kufanya hivyo

[Picha katika ukurasa wa 10]

Vijana, mmejifunza nini kutokana na yule msichana Mwisraeli?

[Picha katika ukurasa wa 11]

Dorkasi alitimiza jinsi gani mahitaji ya Wakristo wenzake?