Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wahitimu wa Gileadi Wahimizwa “Waanze Kuchimba”

Wahitimu wa Gileadi Wahimizwa “Waanze Kuchimba”

Kuhitimu Kwa Darasa la 123 la Gileadi

Wahitimu wa Gileadi Wahimizwa “Waanze Kuchimba”

JUMAMOSI (Siku ya Posho), Septemba 8, 2007 (8/9/2007), umati wa watu 6,352 kutoka nchi 41 ulihudhuria programu ya kuhitimu ya darasa la 123 la Shule ya Gileadi. Saa nne asubuhi, mwenyekiti wa programu hiyo, Anthony Morris wa Baraza Linaloongoza, aliwakaribisha wasikilizaji. Baada ya kutoa maelezo machache ya utangulizi, alimkaribisha msemaji wa kwanza, Gary Breaux wa Halmashauri ya Tawi ya Marekani.

Ndugu Breaux aliwahakikishia wanafunzi kwamba Yehova anavutiwa na wale wanaofanya mapenzi yake bila kujali sura yao ya nje. (Yer. 13:11) Aliwahimiza wahitimu hao wadumishe uzuri huo. Kisha, Gerrit Lösch wa Baraza Linaloongoza akakazia kwamba inafaa kutumaini kupata thawabu tunapomtumikia Yehova. (Ebr. 11:6) Hata hivyo, nia yetu inapaswa kuwa upendo usio na ubinafsi.

Kisha, mwangalizi wa Idara ya Shule za Kitheokrasi, William Samuelson, akawahimiza wahitimu washikamane na mgawo wao wenye kuheshimika wa kumtangaza Mfalme ambaye anatawala na kuonyesha heshima yao kwa mwenendo wao mzuri. * Sam Roberson, mwangalizi-msaidizi wa Idara ya Shule za Kitheokrasi, aliwahimiza wahitimu hao watafute sikuzote sifa nzuri za wengine. Ikiwa watafanya hivyo, wataweza ‘kuupenda zaidi ushirika mzima wa akina ndugu.’—1 Pet. 2:17.

Baada ya hotuba hizo zenye kuchochea, mwalimu wa Shule ya Gileadi Mark Noumair aliwahoji wahitimu kadhaa ambao walisimulia mambo waliyoona waliposhiriki katika utumishi wa shambani wakati wa shule hiyo. Masimulizi yao yaliwathibitishia wasikilizaji kwamba wahitimu hao wanapenda huduma na wanatamani kuwasaidia wengine. Halafu Kent Fischer wa Ofisi ya Betheli ya Patterson akawahoji washiriki wa Halmashauri za Tawi kutoka katika nchi tatu ambazo zina wamishonari. Maneno ya ndugu hao wazuri yaliwahakikishia wasikilizaji, kutia ndani wazazi wengi wa wahitimu, kwamba wamishonari wapya wanatunzwa vizuri katika migawo yao. Kisha, Izak Marais wa Idara ya Utumishi wa Kutafsiri aliwahoji wamishonari fulani wa muda mrefu. Masimulizi yao yaliwasaidia wahitimu kuona shangwe watakayopata.

Hotuba kuu ya programu, ambayo ilitolewa na Geoffrey Jackson wa Baraza Linaloongoza, ilikuwa na kichwa “Mtafanya Nini Baada ya Kusikia Mambo Yote Hayo?” Ndugu Jackson, ambaye alitumika akiwa mmishonari kwa miaka karibu 25 huko Pasifiki ya Kusini, alizungumzia sehemu ya mwisho ya Mahubiri ya Mlimani. Katika hotuba hiyo, Yesu alizungumza kuhusu watu wawili waliojenga nyumba, mmoja alikuwa mwenye busara na yule mwingine mpumbavu. Msemaji huyo alitaja kwamba huenda nyumba hizo mbili zilijengwa katika eneo lilelile. Hata hivyo, yule mtu mpumbavu alijenga juu ya mchanga, lakini yule mwenye busara alichimba chini kabisa mpaka alipoufikia mwamba ili ajenge juu yake. Mvua kubwa iliponyesha, nyumba iliyojengwa juu ya mwamba haikuporomoka lakini ile iliyojengwa juu ya mchanga iliporomoka.—Mt. 7:24-27; Luka 6:48.

Yesu alieleza kwamba yule mtu mpumbavu alifananisha watu ambao walisikiliza tu mafundisho yake lakini hawakutenda. Yule mwenye hekima alifananisha wale waliomsikiliza Yesu na kutenda kupatana na maneno yake. Ndugu Jackson aliwaambia hivi wahitimu, “Mnapotumia katika eneo lenu la umishonari mambo mliyojifunza kupitia funzo la Biblia, mtakuwa kama yule mtu mwenye busara.” Hivyo, alimalizia kwa kuwahimiza wahitimu hao “waanze kuchimba” katika migawo yao ya umishonari.

Mwishowe, wahitimu walipokea diploma na migawo yao, kisha Ndugu Morris akawapa mashauri ya kumalizia. Aliwatia moyo wahitimu hao wamfuate Yesu sikuzote na wasikose kamwe kumtegemea Yehova ili awape nguvu. Programu ya kuhitimu ikafikia mwisho.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Idara ya Shule za Kitheokrasi ambayo iko chini ya uangalizi wa Halmashauri ya Kufundisha, inasimamia shule ya Gileadi, shule ya washiriki wa Halmashauri za Tawi, na shule ya waangalizi wanaosafiri.

[Sanduku katika ukurasa wa 31]

TAKWIMU ZA DARASA

Idadi ya nchi ambazo zimewakilishwa: 10

Idadi ya nchi ambako wametumwa: 24

Idadi ya wanafunzi: 56

Wastani wa umri: 33.5

Wastani wa miaka katika kweli: 17.9

Wastani wa miaka katika huduma ya wakati wote: 13.8

[Picha katika ukurasa wa 32]

Darasa la 123 Lililohitimu la Shule ya Gileadi

Katika orodha iliyo chini, nambari za safu zinaanzia mbele kuelekea nyuma, na majina yameorodheshwa kuanzia kushoto kuelekea kulia katika kila safu.

(1) Esparza, E.; Papaya, S.; Bilal, A.; Suárez, M.; Evers, E.; Dimichino, K. (2) Rosa, M.; Fujii, R.; Ratey, O.; Leveton, J.; Van Leemputten, M. (3) Boscaino, A.; Beck, K.; Budanov, H.; Braz, C.; Peltz, K.; Siaw, A. (4) Leveton, S.; Santikko, H.; Conte, S.; Wilson, J.; Rylatt, J.; Pierce, S.; Fujii, K. (5) Rosa, D.; Boscaino, M.; Austin, V.; Rodiel, P.; Bilal, P.; Dimichino, P. (6) Ratey, B.; Czyzyk, D.; Clarke, C.; Riedel, A.; Esparza, F.; Siaw, P.; Van Leemputten, T.(7) Rodiel, J.; Evers, J.; Green, J.; Czyzyk, J.; Santikko, M.; Rylatt, M. (8) Peltz, L.; Austin, D.; Riedel, T.; Beck, M.; Pierce, W.; Conte, S.; Green, S. (9) Suárez, J.; Clarke, J.; Papaya, S.; Budanov, M.; Wilson, R.; Braz, R.