Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yesu Kristo—Yule Mmishonari Mkuu Zaidi

Yesu Kristo—Yule Mmishonari Mkuu Zaidi

Yesu Kristo—Yule Mmishonari Mkuu Zaidi

“Mimi ni mwakilishi kutoka kwake, na Yeye alinituma.”—YOH. 7:29.

1, 2. Mmishonari ni nani, na ni nani anayeweza kuitwa Mmishonari mkuu zaidi?

UNAFIKIRIA nini unaposikia neno “mmishonari”? Watu fulani wanafikiria wamishonari wa dini zinazodai kuwa za Kikristo, ambao wengi wao wanajiingiza katika siasa na shughuli za kiuchumi za nchi ambako wanatumikia. Hata hivyo, ukiwa Shahidi wa Yehova, inaelekea unafikiria wamishonari ambao wanatumwa na Baraza Linaloongoza ili kuhubiri habari njema katika nchi mbalimbali ulimwenguni. (Mt. 24:14) Wamishonari hao wanatumia bila uchoyo wakati na jitihada zao katika kazi nzuri ya kuwasaidia watu wamkaribie Yehova Mungu na hivyo kuwa na uhusiano mzuri pamoja naye.—Yak. 4:8.

2 Maneno “mmishonari” na “wamishonari” hayapatikani katika maandishi makuu ya Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya. Hata hivyo, kuhusu Waefeso 4:11, maelezo ya chini katika Biblia ya Marejeo yanaonyesha kwamba neno la Kigiriki linalotafsiriwa “waeneza-injili” linaweza pia kutafsiriwa “wamishonari.” Yehova ndiye Mweneza-injili mkuu, lakini hawezi kuitwa Mmishonari mkuu, kwa sababu hakuwahi kutumwa na mtu yeyote. Lakini Yesu Kristo alisema hivi kuhusu Baba yake wa mbinguni: “Mimi ninamjua, kwa sababu mimi ni mwakilishi kutoka kwake, na Yeye alinituma.” (Yoh. 7:29) Ili kuonyesha kwamba aliupenda sana ulimwengu wa wanadamu, Yehova alimtuma Mwana wake mzaliwa-pekee duniani. (Yoh. 3:16) Yesu anaweza kuitwa Mmishonari mkuu zaidi, Mmishonari bora zaidi, kwa kuwa sababu moja iliyofanya atumwe duniani ilikuwa ‘kutoa ushahidi juu ya ile kweli.’ (Yoh. 18:37) Alifanikiwa kabisa kutangaza habari njema ya Ufalme, na bado tunafaidika na matokeo ya utumishi wake. Kwa mfano, tunaweza kuiga njia zake za kufundisha katika huduma yetu, iwe tunatumwa tukiwa wamishonari au hapana.

3. Tutachunguza maswali gani?

3 Daraka la Yesu akiwa mhubiri wa Ufalme linatokeza maswali kama haya: Yesu alipatwa na mambo gani duniani? Kwa nini mafundisho yake yalikuwa na matokeo mazuri? Na kwa nini huduma yake ilifanikiwa?

Kuwa Tayari Kusaidia Katika Mazingira Mapya

4-6. Taja mabadiliko fulani ambayo Yesu alikabiliana nayo alipotumwa duniani.

4 Wamishonari wa siku hizi na Wakristo fulani ambao wanahamia katika maeneo ambako kuna uhitaji mkubwa zaidi wa wahubiri wa Ufalme huenda wakahitaji kuishi maisha ya chini sana kuliko yale waliyozoea. Lakini hatuwezi hata kufikiria tofauti kati ya hali za Yesu duniani na zile za mbinguni, ambako aliishi pamoja na Baba yake katikati ya viumbe wa kimalaika ambao walimtumikia Yehova wakiwa na nia nzuri. (Ayu. 38:7) Ilikuwa tofauti kama nini kuwa katikati ya wanadamu wenye dhambi katika ulimwengu mpotovu! (Marko 7:20-23) Yesu hata alivumilia mashindano kati ya wanafunzi wake wa karibu zaidi. (Luka 20:46; 22:24) Bila shaka, alitenda kwa ukamilifu katika kila jambo alilokabili duniani.

5 Yesu hakuanza kuzungumza kimuujiza lugha ya wanadamu; alianza kujifunza lugha hiyo akiwa mtoto mchanga. Lilikuwa badiliko kubwa kama nini kwa mtu aliyekuwa akiwaongoza malaika mbinguni! Akiwa duniani, Yesu alitumia angalau lugha moja kati ya “lugha za wanadamu.” Lugha hiyo ilikuwa tofauti kabisa na ‘lugha za malaika.’ (1 Kor. 13:1) Hata hivyo, hakuna mwanadamu aliyesema maneno yenye kuvutia kama Yesu.—Luka 4:22.

6 Fikiria mabadiliko mengine ambayo Mwana wa Mungu alihitaji kukabiliana nayo alipokuja duniani. Ingawa Yesu hakurithi dhambi kutoka kwa Adamu, alikuja kuwa mwanadamu, kama wale ambao baadaye wangekuja kuwa “ndugu” zake au wafuasi wake watiwa-mafuta. (Soma Waebrania 2:17, 18.) Usiku wa mwisho wa maisha yake duniani, Yesu alijizuia kumwomba Baba yake wa mbinguni atume “vikosi zaidi ya kumi na viwili vya malaika.” Lakini fikiria viumbe wa kimalaika ambao alikuwa na mamlaka juu yao akiwa Mikaeli yule Malaika Mkuu! (Mt. 26:53; Yuda 9) Ndiyo, Yesu alifanya miujiza; hata hivyo, yale aliyofanya alipokuwa duniani yalikuwa si kitu yakilinganishwa na yale ambayo angeweza kutimiza huko mbinguni.

7. Wayahudi walitenda jinsi gani kuhusiana na Sheria?

7 Kabla ya kuwa mwanadamu, akiwa “Neno,” huenda Yesu alikuwa Msemaji wa Mungu ambaye aliwaongoza Waisraeli nyikani. (Yoh. 1:1; Kut. 23:20-23) Hata hivyo, ‘walipokea Sheria kama ilivyopitishwa na malaika lakini hawakuishika.’ (Mdo. 7:53; Ebr. 2:2, 3) Kwa kweli, viongozi wa dini ya Kiyahudi walishindwa kutambua kusudi la Sheria. Kwa mfano, fikiria sheria kuhusu Sabato. (Soma Marko 3:4-6.) Waandishi na Mafarisayo ‘walipuuza mambo mazito zaidi ya Sheria, yaani, haki na rehema na uaminifu.’ (Mt. 23:23) Hata hivyo, Yesu hakukata tamaa na kuacha kutangaza ile kweli.

8. Kwa nini Yesu anaweza kutusaidia?

8 Yesu alikuwa tayari kusaidia. Alichochewa na upendo kuelekea watu na alitaka sana kuwasaidia. Hakupoteza kamwe roho ya kueneza injili. Na kwa sababu ya uaminifu wake kwa Yehova alipokuwa duniani, Yesu alikuja kuwa “mwenye daraka la wokovu wa milele kwa wale wote wanaomtii.” Zaidi ya hayo, “kwa kuwa yeye mwenyewe ameteseka alipokuwa akijaribiwa, anaweza kuwasaidia wale [kama sisi] wanaojaribiwa.”—Ebr. 2:18; 5:8, 9.

Alizoezwa Vizuri Kuwa Mwalimu

9, 10. Ni mazoezi ya aina gani ambayo Yesu alipata kabla ya kutumwa duniani?

9 Leo, kabla ya Wakristo kutumwa wakiwa wamishonari, Baraza Linaloongoza linafanya mipango ili wazoezwe. Je, Yesu Kristo alizoezwa? Ndiyo, lakini hakuhudhuria shule za kirabi kabla ya kutiwa mafuta kwa roho na kuwa Masihi; wala hakufundishwa na mmoja wa viongozi mashuhuri wa kidini. (Yoh. 7:15; linganisha Matendo 22:3.) Basi, kwa nini Yesu alikuwa na sifa za kustahili kufundisha?

10 Haidhuru Yesu alijifunza nini kutoka kwa mama yake, Maria, na baba yake mlezi, Yosefu, yeye alipata mazoezi yaliyokuwa muhimu zaidi kwa ajili ya huduma kutoka Chanzo cha juu zaidi. Yesu alisema hivi kuhusu mazoezi hayo: “Sijasema kutokana na msukumo wangu mwenyewe, bali Baba mwenyewe aliyenituma amenipa amri kuhusu jambo la kutangaza na la kusema.” (Yoh. 12:49) Ona kwamba Mwana alipewa maagizo hususa kuhusu yale aliyopaswa kufundisha. Kabla ya kuja duniani, bila shaka Yesu alitumia wakati mwingi kusikiliza maagizo ya Baba yake. Je, kuna mazoezi mengine bora kuliko hayo aliyopokea?

11. Yesu alionyesha kwa kadiri gani mtazamo wa Baba yake kuelekea wanadamu?

11 Tangu alipoumbwa, Mwana huyo alikuwa na uhusiano wa karibu sana pamoja na Baba yake. Kabla ya kuwa mwanadamu, Yesu alitambua mtazamo wa Mungu kuelekea wanadamu kwa kuchunguza jinsi Yehova alivyoshughulika nao. Mwana huyo alionyesha upendo kama wa Mungu kuwaelekea wanadamu kwa kadiri kubwa hivi kwamba akiwa hekima inayofananishwa na mtu, angeweza kusema hivi: “Vitu nilivyopenda sana vilihusiana na wana wa binadamu.”—Met. 8:22, 31.

12, 13. (a) Yesu alijifunza namna gani kwa kuchunguza jinsi Baba yake alivyoshughulika na Waisraeli? (b) Yesu alitumia jinsi gani mazoezi aliyopata?

12 Pia, mazoezi ambayo Mwana huyo alipata yalitia ndani kuchunguza jinsi Baba yake alivyoshughulikia hali ngumu. Kwa mfano, fikiria jinsi Yehova alivyoshughulika na Waisraeli waasi. Andiko la Nehemia 9:28 linasema hivi: “Mara tu walipopata kupumzika, wakatenda tena mabaya mbele zako [Yehova], nawe ukawaacha mkononi mwa adui zao, ambao waliwakanyagia chini. Kisha wakawa wanarudi na kukulilia wapate msaada, nawe ukasikia kutoka mbinguni kwenyewe na kuwakomboa kulingana na rehema zako nyingi, tena na tena.” Akitumika pamoja na Yehova na akimchunguza, Yesu alisitawisha huruma kama ya Yehova kuwaelekea watu wa eneo lake.—Yoh. 5:19.

13 Yesu alitumia mazoezi aliyopata kwa kuwashughulikia wanafunzi wake kwa huruma. Usiku kabla ya kifo chake, mitume wote ambao aliwapenda sana ‘walimwacha na kukimbia.’ (Mt. 26:56; Yoh. 13:1) Mtume Petro hata alimkana Kristo mara tatu! Hata hivyo, Yesu alifungua njia ili mitume wamrudie. Alimwambia Petro: “Nimeomba dua kwa ajili yako ili imani yako isififie; na wewe, mara tu utakapokuwa umerudi, watie nguvu ndugu zako.” (Luka 22:32) Israeli la kiroho limejengwa juu ya “mitume na manabii,” na msingi wa mawe wa ukuta wa Yerusalemu Mpya una majina ya mitume waaminifu 12 wa Mwana-Kondoo, Yesu Kristo. Mpaka leo hii, Wakristo watiwa-mafuta pamoja na washiriki wao waliojiweka wakfu, wale “kondoo wengine,” wanasitawi wakiwa tengenezo linalohubiri kuhusu Ufalme chini ya mkono wenye nguvu wa Mungu na uongozi wa Mwana wake mpendwa.—Efe. 2:20; Yoh. 10:16; Ufu. 21:14.

Jinsi Yesu Alivyofundisha

14, 15. Ni katika njia gani mafundisho ya Yesu yalitofautiana na yale ya waandishi na Mafarisayo?

14 Yesu alitumia jinsi gani mazoezi yake katika kuwafundisha wafuasi wake? Tunaona wazi jinsi njia ya Yesu ya kufundisha ilivyokuwa bora zaidi tunapoilinganisha na ile ya viongozi wa dini ya Kiyahudi. Waandishi na Mafarisayo ‘walilibatilisha neno la Mungu kwa sababu ya mapokeo yao.’ Tofauti na watu hao, mambo ambayo Yesu alisema hayakutokana naye; sikuzote alifundisha neno au ujumbe wa Mungu. (Mt. 15:6; Yoh. 14:10) Tunahitaji pia kufanya hivyo.

15 Kuna jambo lingine ambalo lilimfanya Yesu awe tofauti kabisa na viongozi wa kidini. Alisema hivi kuhusu waandishi na Mafarisayo: “Mambo yote wanayowaambia ninyi, yafanyeni na kuyashika, lakini msifanye kulingana na matendo yao, kwa maana wao husema lakini hawatendi.” (Mt. 23:3) Yesu aliishi kulingana na mambo aliyofundisha. Acheni tuchunguze mfano mmoja ambao unathibitisha ukweli wa jambo hilo.

16. Kwa nini ungesema kwamba Yesu aliishi kulingana na maneno yake yaliyo katika Mathayo 6:19-21?

16 Yesu aliwahimiza wanafunzi wake ‘wajiwekee hazina mbinguni.’ (Soma Mathayo 6:19-21.) Je, Yesu mwenyewe aliishi kulingana na himizo hilo? Ndiyo, kwa kuwa angeweza kusema hivi kwa unyoofu kujihusu: “Mbweha wana mapango na ndege wa mbinguni wana viota, lakini Mwana wa binadamu hana mahali popote pa kulaza kichwa chake.” (Luka 9:58) Yesu aliishi maisha rahisi. Alijishughulisha hasa na kazi ya kutangaza habari njema ya Ufalme, na alionyesha maana ya kuishi bila mahangaiko yanayotokana na kujiwekea hazina duniani. Yesu alionyesha umuhimu wa kujiwekea hazina mbinguni, “ambako nondo na kutu havili, na ambako wezi hawavunji na kuiba.” Je, unafuata himizo la Yesu la kujiwekea hazina mbinguni?

Sifa Zilizomfanya Yesu Apendwe na Watu

17. Ni sifa gani zilizomfanya Yesu awe mweneza-injili asiye na kifani?

17 Ni sifa gani zilizomfanya Yesu awe mweneza-injili asiye na kifani? Sifa moja ilikuwa mtazamo wake kuelekea watu aliowasaidia. Yesu aliiga sifa nzuri za Yehova kama vile unyenyekevu, upendo, na huruma. Ona jinsi sifa hizo zilivyowavuta watu wengi kwa Yesu.

18. Kwa nini inaweza kusemwa kwamba Yesu alikuwa mnyenyekevu?

18 Kwa kukubali mgawo wa kuja duniani, Yesu “alijiondolea mwenyewe hali yake na kuchukua umbo la mtumwa na kuwa kama wanadamu.” (Flp. 2:7) Hilo lilikuwa tendo la unyenyekevu. Zaidi ya hayo, Yesu hakuwadharau watu. Hakuwaambia watu, ‘Nilitoka mbinguni, kwa hiyo mnapaswa kunisikiliza.’ Tofauti na wale waliojitangaza wenyewe kwa uwongo kuwa masihi, Yesu hakujitutumua kwa sababu ya cheo chake cha kuwa Masihi wa kweli. Nyakati nyingine, aliwakataza watu wasiwaambie wengine yeye alikuwa nani au yale aliyokuwa amefanya. (Mt. 12:15-21) Yesu alitaka watu wafanye uamuzi wao wa kumfuata kwa msingi wa yale ambayo walijionea wenyewe. Wanafunzi wake walitiwa moyo kama nini kwa sababu Bwana wao hakuwatazamia wawe kama malaika wakamilifu ambao alishirikiana nao huko mbinguni!

19, 20. Sifa kama upendo na huruma zilimchochea Yesu jinsi gani kuwasaidia watu?

19 Pia, Yesu Kristo alionyesha upendo, sifa kuu ya Baba yake wa mbinguni. (1 Yoh. 4:8) Yesu aliwafundisha wasikilizaji wake kwa sababu aliwapenda. Kwa mfano, fikiria hisia zake kumhusu mtawala fulani kijana. (Soma Marko 10:17-22.) Yesu ‘alimpenda’ na alitaka kumsaidia, lakini mtawala huyo kijana hakutaka kuachana na mali zake nyingi ili awe mfuasi wa Kristo.

20 Sifa nyingine ambayo ilimfanya Yesu apendwe ni huruma. Kama wanadamu wote wasio wakamilifu, wale waliokubali mafundisho yake walikuwa wamelemewa na matatizo. Yesu alijua hilo, hivyo aliwafundisha kwa huruma na pia aliwasikitikia. Kwa mfano: Pindi moja, Yesu na mitume wake walikuwa na shughuli nyingi hivi kwamba hawakupata wakati wa kula chakula. Hata hivyo, Yesu alifanya nini alipoona umati wa watu umekusanyika? “Akawasikitikia, kwa sababu walikuwa kama kondoo wasio na mchungaji. Naye akaanza kuwafundisha mambo mengi.” (Marko 6:34) Yesu alitambua hali yenye kusikitisha ya watu wa eneo lake naye akajitahidi sana kuwafundisha na kufanya miujiza kwa faida yao. Wengine walivutiwa na sifa zake nzuri, wakachochewa na maneno yake, nao wakawa wanafunzi wake.

21. Tutachunguza nini katika habari inayofuata?

21 Tunaweza kujifunza mengi zaidi kuhusu huduma ya Yesu ya kidunia, kama itakavyoonyeshwa na habari inayofuata. Tunaweza kumwiga Yesu Kristo, yule Mmishonari mkuu zaidi, katika njia gani nyingine?

Ungetoa Jibu Gani?

• Yesu alipata mazoezi gani kabla ya kuja duniani?

• Njia ya Yesu ya kufundisha ilikuwa bora kuliko ile ya waandishi na Mafarisayo jinsi gani?

• Ni sifa gani zilizomfanya Yesu apendwe na watu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 15]

Yesu aliufundisha umati jinsi gani?