Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ahadi ya Maana Sana

Ahadi ya Maana Sana

Ahadi ya Maana Sana

NIMETOA ahadi ya maana sana. Acheni niwaeleze kile kilichonifanya nitoe ahadi hiyo nikiwa mama kijana Mhispania.

Hatukuwa na amani na upatano nyumbani kwa wazazi wetu. Familia yetu ilihuzunika sana wakati ndugu yangu mdogo alipokufa katika msiba mbaya sana wa barabarani akiwa na umri wa miaka minne. Zaidi ya hilo, ilikuwa vigumu sana kwa mama yangu kupata furaha katika ndoa kwa sababu ya tabia mbaya za baba yangu. Hata hivyo, matatizo hayo hayakumzuia mama asinifundishe mimi na ndugu yangu mkubwa viwango vya maadili.

Muda si muda, ndugu yangu alioa, na mimi pia nikaolewa. Muda mfupi baadaye, iligunduliwa kuwa mama yangu ana kansa, ambayo mwishowe ilisababisha kifo chake. Lakini kabla hajafa, alitupa hazina.

Mmoja wa rafiki zake alikuwa amezungumza naye kuhusu tumaini la Kimaandiko la ufufuo, na mama akakubali kujifunza Biblia. Katika siku za mwisho za maisha yake, ujumbe wa tumaini ulio katika Biblia ulimletea furaha na kusudi maishani.

Tulipoona matokeo mazuri ya ujumbe wa Biblia katika maisha yake, mimi na ndugu yangu tulianza kujifunza Neno la Mungu. Nilibatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova mwezi mmoja kabla mtoto wangu wa pili hajazaliwa, msichana mrembo ambaye tulimwita Lucía.

Siku niliyobatizwa ilikuwa ya maana sana kwangu. Sababu moja ilikuwa kwamba sasa nilikuwa mali ya Yehova, baada ya kujiweka wakfu kwake ili nimtumikie milele. Sababu nyingine ilikuwa kwamba ningeweza kumfundisha mwana na binti yangu mpendwa kuhusu imani yangu.

Hata hivyo, punde si punde, jambo la pili ambalo liliniletea furaha lilikatizwa. Lucía alipokuwa na umri wa miaka minne, alianza kupata maumivu makali ya tumbo. Baada ya kupimwa mara kadhaa, daktari anayepiga picha za eksirei alieleza kwamba ini lake lilikuwa na uvimbe wenye ukubwa kama wa chungwa. Daktari huyo alisema kwamba Lucía alikuwa na uvimbe wa kansa ambao unakua haraka sana (neuroblastoma). Hivyo ndivyo Lucía alivyoanza kupambana na kansa. Alipambana na ugonjwa huo kwa miaka saba, na alilazwa hospitalini kwa vipindi virefu.

Roho ya Kujinyima

Katika miaka hiyo migumu, mara nyingi Lucía alinikumbatia kwa uchangamfu na kunipiga busu ili kunitia moyo. Wafanyakazi wa hospitali walivutiwa sana walipoona jinsi alivyokabiliana na ugonjwa huo. Sikuzote alikuwa tayari kushirikiana na wauguzi, akiwasaidia kuwagawia watoto wengine wagonjwa vitu kama vile mtindi na maji ya machungwa, katika vyumba vilivyo karibu. Wauguzi hata walimpa Lucía koti jeupe na beji yenye maneno “msaidizi wa wauguzi.”

“Lucía alinigusa moyo,” anakumbuka mfanyakazi mmoja wa hospitali hiyo. “Alikuwa mtoto mwenye bidii na mwenye akili, naye alipenda kuchora picha. Alikuwa mchangamfu na mkomavu, mkomavu sana.”

Lucía alipata nguvu na usawaziko kutoka katika Neno la Mungu. (Ebr. 4:12) Alisadiki kwamba katika ulimwengu mpya, “kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena,” kama Neno la Mungu linavyoahidi. (Ufu. 21:4) Alipendezwa na wengine hivi kwamba alitumia kila nafasi aliyopata ili kuzungumza nao kuhusu ujumbe wa Biblia. Tumaini imara la Lucía katika ufufuo lilimsaidia kuwa mtulivu na mchangamfu sana hata ingawa hakutarajia kupona. (Isa. 25:8) Aliendelea kuwa na mtazamo huo mpaka siku ambayo alikufa kutokana na kansa hiyo.

Hiyo ndiyo siku niliyotoa ile ahadi ya maana sana. Lucía hangeweza kufumbua macho yake. Baba yake aliushika mkono wake mmoja nami nikaushika ule mwingine. Nilimnong’onezea hivi: “Usiwe na wasiwasi, sitakuacha. Pumua polepole tu. Utakapoamka, utakuwa sawa. Hutahisi maumivu tena, nitakuwa pamoja nawe.”

Sasa ni lazima nitimize ahadi hiyo. Ninajua kwamba kipindi cha kungoja hakitakuwa rahisi. Lakini pia ninajua kwamba nikimtegemea Yehova kwa subira na kuendelea kuwa mtimilifu kwake, nitakuwapo Lucía atakapofufuliwa.

Urithi Ambao Lucía Alituachia

Mfano wa ujasiri wa Lucía, na pia bidii yake nyingi ya kulitegemeza kutaniko, ilimvutia sana mume wangu ambaye hakuwa Shahidi wa Yehova. Siku ambayo Lucía alikufa, mume wangu aliniambia kwamba anapaswa ajichunguze. Majuma machache baadaye, alizungumza na mzee wa kutaniko na kuomba funzo la Biblia. Muda si muda, mume wangu alianza kuhudhuria mikutano yote. Kwa msaada wa Yehova, aliacha kuvuta sigara, zoea ambalo alikuwa ameshindwa kuacha kabla ya hapo.

Bado ninahuzunika kwa sababu ya kifo cha Lucía, hata hivyo, ninamshukuru Yehova kwa sababu ya urithi ambao Lucía alituachia. Mimi na mume wangu tunafarijiana kwa tumaini zuri ajabu la ufufuo, hata tunawazia wakati ambapo tutamwona tena Lucía, tutaona tena macho yake ya mviringo yaliyo maangavu na mashavu yake yakibonyea kwa tabasamu.

Msiba uliompata binti yangu ulimgusa moyo hasa jirani fulani. Jumamosi moja asubuhi (Siku ya Posho) mvua ilipokuwa ikinyesha, mwanamke mmoja ambaye mwana wake alisomea shule moja na Lucía alikuja nyumbani kwetu. Mwanamke huyo alikuwa amefiwa na mtoto wake mwenye umri wa miaka 11 aliyeugua ugonjwa huohuo. Mwanamke huyo alipopata habari kumhusu Lucía, alitafuta tulikoishi naye akaja kututembelea. Alitaka kujua jinsi nilivyokuwa nikikabiliana na kifo cha Lucía naye akapendekeza tuanzishe kikundi cha kusaidiana ili tuwafariji akina mama walio katika hali kama zetu.

Nilimweleza kwamba mimi binafsi nilikuwa nimefarijiwa kikweli na ahadi moja ya Biblia, ahadi ambayo ni bora kuliko ahadi yoyote ambayo wanadamu wanaweza kutoa. Macho yake yaling’aa nilipomsomea maneno ya Yesu katika Yohana 5:28, 29. Alikubali funzo la Biblia na muda si muda akaanza kuhisi “amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote.” (Flp. 4:7) Mara nyingi tunapojifunza Biblia pamoja, tunatua na kuwazia tukiwa katika ulimwengu mpya, tukiwapokea wapendwa wetu wakati wa ufufuo.

Ndiyo, maisha mafupi ya Lucía yametuachia urithi wa kudumu. Imani yake imesaidia kuunganisha familia yetu katika utumishi wa Mungu, na imetia nguvu azimio langu la kubaki thabiti katika imani. Bila shaka, sote ambao tumefiwa na wapendwa wetu ambao tunatazamia watafufuliwa, tuna ahadi ya maana sana ya kutimiza.

[Picha katika ukurasa wa 20]

Picha ya paradiso iliyochorwa na Lucía