Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unawaona Wengine Kama Yehova Anavyowaona?

Je, Unawaona Wengine Kama Yehova Anavyowaona?

Je, Unawaona Wengine Kama Yehova Anavyowaona?

“Kusiwe na mgawanyiko katika mwili . . . Viungo vyake vitunzane kwa njia ileile.”—1 KOR. 12:25.

1. Ulihisi namna gani ulipoingia katika paradiso ya kiroho?

TULIPOJITENGA na ulimwengu mbovu na kuanza kushirikiana na watu wa Yehova, inaelekea kwamba tulifurahia upendo mchangamfu na hangaiko la kweli kati yao. Hali hiyo ni tofauti kama nini na hali ya watu wakaidi, wenye chuki, na wagomvi ambao wanaongozwa na Shetani! Tuliingia katika paradiso ya kiroho ambayo imejaa amani na umoja.—Isa. 48:17, 18; 60:18; 65:25.

2. (a) Ni nini kinachoweza kutufanya tuwe na maoni mabaya juu ya wengine? (b) Huenda tukahitaji kufanya nini?

2 Hata hivyo, kwa sababu ya kutokamilika, kadiri wakati unavyopita huenda tukaanza kuwa na maoni yasiyofaa kuwahusu ndugu zetu. Kutokamilika kwetu kunaweza kutufanya tupanue sana makosa ya ndugu zetu badala ya kukazia fikira sifa zao za kiroho. Kwa maneno mengine, tunaacha kuwaona kama Yehova anavyowaona. Hilo likitukia, itafaa tuchunguze maoni yetu na kuyapatanisha na maoni yaliyo sawa ya Yehova.—Kut. 33:13.

Jinsi Yehova Anavyowaona Ndugu Zetu

3. Biblia inalinganisha kutaniko la Kikristo na nini?

3 Kama ilivyoandikwa katika 1 Wakorintho 12:2-26, mtume Paulo alilinganisha kutaniko la Wakristo watiwa-mafuta na mwili wenye “viungo vingi.” Kama vile viungo vya mwili vinavyotofautiana, ndivyo sifa na uwezo wa washiriki wa kutaniko unavyotofautiana. Lakini, Yehova anawakubali washiriki hao tofauti-tofauti wa kutaniko. Anampenda na kumthamini kila mshiriki. Hivyo, Paulo anawashauri washiriki wa kutaniko ‘watunzane kwa njia ileile.’ Huenda hilo likawa jambo gumu kwa sababu nyutu za wengine zinaweza kuwa tofauti na zetu.

4. Kwa nini huenda tukahitaji kubadili maoni yetu kuhusu ndugu zetu?

4 Huenda hata tukawa na mwelekeo wa kukazia fikira udhaifu wa ndugu zetu. Tunapofanya hivyo, ni kana kwamba tunatumia kamera inayoweza kupiga picha sehemu ndogo tu ya mtu. Hata hivyo, Yehova anaweza kuona eneo kubwa sana, anaweza kumwona mtu kikamili pamoja na mazingira yake. Huenda tuna mwelekeo wa kukazia fikira mambo yasiyotupendeza, lakini Yehova anamwona mtu kwa ujumla, kutia ndani sifa zake zote nzuri. Kadiri tunavyojitahidi kumwiga Yehova, ndivyo tutakavyochangia zaidi roho ya upendo na umoja katika kutaniko.—Efe. 4:1-3; 5:1, 2.

5. Kwa nini haifai kuwahukumu wengine?

5 Yesu alijua vizuri kwamba kwa kawaida wanadamu wasio wakamilifu wana mwelekeo wa kuwahukumu wengine. Alishauri hivi: “Acheni kuhukumu ili msihukumiwe.” (Mt. 7:1) Ona kwamba Yesu hakusema: “Msihukumu”; bali alisema: “Acheni kuhukumu.” Alijua kwamba wengi kati ya wasikilizaji wake walikuwa na tabia ya kuwachambua wengine. Je, inawezekana kwamba tumesitawisha tabia hiyo? Ikiwa tuna mwelekeo huo, tunapaswa kujitahidi kufanya mabadiliko, ili tusije kuhukumiwa vikali. Kwa kweli, tuna haki gani ya kumhukumu mtu ambaye Yehova amemweka rasmi kutanikoni au kusema kwamba hapaswi kuwa katika kutaniko? Huenda ndugu akawa na udhaifu, lakini ikiwa bado Yehova anamkubali, je, ingefaa kumkataa ndugu huyo? (Yoh. 6:44) Je, kweli tunaamini kwamba Yehova anaongoza watu wake na kwamba ikiwa marekebisho fulani yanahitajiwa, atachukua hatua kwa wakati wake mwenyewe?—Soma Waroma 14:1-4.

6. Yehova anawaona watumishi wake jinsi gani?

6 Jambo lenye kustaajabisha sana kumhusu Yehova ni kwamba anaweza kuona uwezo kamili ambao Wakristo mmoja-mmoja watakuwa nao watakapofikia ukamilifu katika ulimwengu mpya. Pia, anajua maendeleo ya kiroho ambayo tayari wamefanya. Hivyo, hana sababu yoyote ya kukazia fikira kila kasoro waliyo nayo. Tunasoma hivi katika Zaburi 103:12: “Kama vile mashariki ilivyo mbali sana na magharibi, ndivyo ameweka makosa yetu mbali sana na sisi.” Sisi binafsi tunapaswa kuwa wenye shukrani kama nini kwa sababu ya jambo hilo!—Zab. 130:3.

7. Tunajifunza nini kutokana na maoni ya Yehova kumhusu Daudi?

7 Maandiko yanathibitisha kwamba Yehova ana uwezo wa pekee wa kukazia fikira sifa nzuri za mtu. Mungu alisema hivi kumhusu Daudi: “Mtumishi wangu Daudi, aliyeshika amri zangu na kunifuata kwa moyo wake wote kwa kufanya yaliyokuwa sawa tu machoni pangu.” (1 Fal. 14:8) Bila shaka, tunajua kwamba Daudi alifanya makosa. Hata hivyo, Yehova aliamua kukazia fikira sifa nzuri za Daudi kwa sababu alijua kwamba alikuwa na moyo mnyoofu.—1 Nya. 29:17.

Waone Ndugu Zako Kama Yehova Anavyowaona

8, 9. (a) Tunaweza kuwa kama Yehova katika njia gani? (b) Toa mfano unaoonyesha jambo hilo, na ueleze somo tunalojifunza.

8 Yehova anaweza kusoma mioyo, lakini sisi hatuwezi. Hiyo ni sababu nzuri ya kutuzuia tusiwahukumu wengine. Hatujui mambo yote kuhusu nia ya mtu mwingine. Tunapaswa kujitahidi kumwiga Yehova kwa kutokazia fikira kutokamilika kwa wanadamu wenzetu, ambako mwishowe kutatoweka. Je, haingefaa kujitahidi kumwiga katika jambo hilo? Kufanya hivyo kutachangia sana mahusiano yenye amani pamoja na ndugu na dada zetu.—Efe. 4:23, 24.

9 Kwa mfano, fikiria nyumba ambayo imeharibika—mabati yake yameng’oka, madirisha yamevunjika, na dari lake limeharibiwa na maji. Huenda watu wengi wakatazama nyumba hiyo na kukata kauli kwamba inapaswa kubomolewa; haivutii hata kidogo. Lakini mtu mwingine anaweza kuitazama na kuwa na maoni tofauti kabisa. Badala ya kukazia fikira kasoro za kijuu-juu tu, huenda akachunguza kwa makini na kuona kwamba nyumba hiyo ni imara na inaweza kurekebishwa. Anainunua kisha anajitahidi kuirekebisha na kuifanya ivutie. Baada ya hapo, wapita-njia wanasema kwamba inapendeza sana. Je, tunaweza kuwa kama mtu huyo anayejitahidi kuirekebisha au kuiboresha nyumba hiyo? Badala ya kukazia fikira kasoro za kijuu-juu tu za ndugu zetu, je, tunaweza kutambua sifa zao nzuri na uwezekano wao wa kufanya maendeleo ya kiroho? Tukifanya hivyo, tutawapenda ndugu zetu kwa sababu ya uzuri wao wa kiroho, kama Yehova anavyowapenda.—Soma Waebrania 6:10.

10. Shauri la Wafilipi 2:3, 4 linaweza kutusaidia namna gani?

10 Mtume Paulo alitoa shauri linaloweza kutusaidia katika uhusiano wetu na watu wote katika kutaniko. Aliwahimiza Wakristo hivi: “[Msifanye] jambo lolote kwa ugomvi au kwa kujisifu, bali kwa unyenyekevu wa akili mkiwaona wengine kuwa ni bora kuliko ninyi, mkiendelea kuangalia, si faida za kibinafsi za mambo yenu wenyewe tu, bali pia faida za kibinafsi za wengine.” (Flp. 2:3, 4) Unyenyekevu utatusaidia kuwa na maoni yanayofaa kuhusu wengine. Kupendezwa na wengine na pia kutafuta sifa zao nzuri kutatusaidia kuwaona kama Yehova anavyowaona.

11. Ni hali gani ambazo zimebadili makutaniko fulani?

11 Katika nyakati za karibuni, watu wengi wamehamia maeneo mengine kwa sababu ya hali zinazobadilika ulimwenguni pote. Majiji fulani yana watu kutoka nchi mbalimbali. Watu fulani ambao wamehamia eneo letu, wamependezwa na kweli ya Biblia na wamejiunga nasi katika kumwabudu Yehova. Watu hao ‘wanatoka katika mataifa yote na makabila na vikundi vya watu na lugha.’ (Ufu. 7:9) Kwa sababu hiyo, mengi ya makutaniko yetu yana watu kutoka mataifa mbalimbali.

12. Tunahitaji kuendelea kuwa na maoni gani kuwahusu wengine, na kwa nini inaweza kuwa vigumu kufanya hivyo?

12 Huenda tukahitaji kujitahidi zaidi kuendelea kuwa na maoni mazuri kuwahusu wengine katika kutaniko letu. Hivyo, tunapaswa kufikiria shauri la mtume Petro kuhusu kuonyesha “upendo wa kindugu usio na unafiki” na ‘kupendana sana kutoka moyoni.’ (1 Pet. 1:22) Inaweza kuwa vigumu kusitawisha upendo wa kweli katika kikundi cha watu kutoka mataifa mbalimbali. Elimu, hali za kiuchumi, malezi, na tamaduni za waabudu wenzetu zinaweza kuwa tofauti sana na zetu. Je, unaona ni vigumu kuelewa mawazo au matendo ya wengine? Huenda wao pia wakashindwa kukuelewa. Hata hivyo, sote tunaagizwa hivi: “Upendeni ushirika mzima wa akina ndugu.”—1 Pet. 2:17.

13. Huenda tukahitaji kufanya marekebisho gani katika kufikiri kwetu?

13 Huenda tukahitaji kufanya marekebisho fulani katika kufikiri kwetu ili tuweze kupanuka katika upendo wetu kuwaelekea ndugu zetu wote. (Soma 2 Wakorintho 6:12, 13.) Je, tunajikuta tukisema hivi, “Sina ubaguzi, lakini . . . ” kisha tunaanza kuzungumzia zile tunazoona kuwa sifa mbaya zinaonyeshwa na watu wengi wa kabila fulani? Maoni kama hayo yanaweza kufunua kwamba tunahitaji kung’oa hisia za ndani za ubaguzi ambazo bado tunazo. Tunaweza kujiuliza, ‘Je, ninajitahidi kwa ukawaida kuwafahamu watu wa utamaduni tofauti na wangu?’ Kujichunguza kwa njia hiyo kunaweza kutusaidia kufanya marekebisho ili kuwakubali na kuwathamini ndugu zetu kutoka mataifa mbalimbali.

14, 15. (a) Toa mifano ya watu waliorekebisha maoni yao kuhusu wengine. (b) Tunaweza kuwaiga jinsi gani?

14 Biblia ina mifano mizuri ya wale ambao walifanya marekebisho. Mmoja wao ni mtume Petro. Kwa kuwa alikuwa Myahudi, Petro angeepuka kuingia katika nyumba ya mtu asiye Myahudi. Hebu wazia jinsi alivyohisi alipoambiwa aende nyumbani kwa Kornelio, mtu asiye Myahudi na ambaye hakuwa ametahiriwa! Petro alifanya marekebisho, akitambua kwamba yalikuwa mapenzi ya Mungu watu wa mataifa yote wawe sehemu ya kutaniko la Kikristo. (Mdo. 10:9-35) Pia Sauli, aliyekuja kuwa mtume Paulo, alihitaji kufanya marekebisho na kuacha ubaguzi. Alikiri kuwa aliwachukia Wakristo sana hivi kwamba ‘kufikia hatua ya kuzidi mno aliendelea kulitesa kutaniko la Mungu na kuliangamiza.’ Hata hivyo, Bwana Yesu alipomsahihisha, Paulo alifanya mabadiliko makubwa na hata akaanza kufuata mwongozo kutoka kwa wale ambao alikuwa akiwatesa hapo zamani.—Gal. 1:13-20.

15 Hapana shaka kwamba tunaweza kufanya marekebisho kwa msaada wa roho ya Yehova. Tukigundua kwamba bado hisia fulani za ubaguzi zimefichika ndani yetu, na tujitahidi kuzing’oa na “kuushika umoja wa roho katika kifungo chenye kuunganisha cha amani.” (Efe. 4:3-6) Biblia inatuhimiza ‘tujivike upendo, kwa maana huo ni kifungo kikamilifu cha muungano.’—Kol. 3:14.

Kumwiga Yehova Katika Huduma Yetu

16. Mapenzi ya Mungu ni nini kuwahusu watu?

16 “Hakuna ubaguzi kwa Mungu,” akaandika mtume Paulo. (Rom. 2:11) Yehova anakusudia kwamba watu kutoka mataifa yote wajiunge na mpango wake wa ibada. (Soma 1 Timotheo 2:3, 4.) Ili kutimiza kusudi hilo, Yehova amefanya mipango “habari njema ya milele” itangazwe “kwa kila taifa na kabila na lugha na watu.” (Ufu. 14:6) Yesu alisema: “Shamba ni ulimwengu.” (Mt. 13:38) Hilo linamaanisha nini kwako wewe na familia yako?

17. Tunaweza kuwasaidia jinsi gani watu wa namna zote?

17 Si kila mtu anayeweza kwenda katika maeneo ya mbali ya ulimwengu ili kuwapelekea wengine ujumbe wa Ufalme. Hata hivyo, tunaweza kuwapelekea ujumbe huo watu kutoka sehemu zote za dunia ambao wanaishi katika eneo letu. Je, tuko macho kutumia nafasi zote kuwatolea ushahidi watu na namna zote, mbali na wale ambao tumekuwa tukiwahubiria kwa miaka mingi? Kwa nini usiazimie kuwahubiria wale ambao hawajatolewa ushahidi kikamili?—Rom. 15:20, 21.

18. Yesu alionyesha hangaiko gani kuwaelekea watu?

18 Yesu alitambua kabisa uhitaji wa kuwasaidia watu wote. Hakuhubiri katika eneo moja tu. Simulizi moja la Biblia linatuambia kwamba ‘aliondoka ili kutembelea majiji na vijiji vyote.’ Kisha, “alipouona umati akawasikitikia” naye akaonyesha uhitaji wa kuwasaidia.—Mt. 9:35-37.

19, 20. Tunaweza kuonyesha kwa njia gani hangaiko kama lile ambalo Yehova na Yesu wanalo kuelekea watu wa namna zote?

19 Unaweza kuonyesha mtazamo kama wa Yesu katika njia gani? Wengine wamejitahidi kuhubiri katika maeneo ambayo hayajahubiriwa kwa ukawaida. Hayo yanatia ndani maeneo ya biashara, bustani, vituo vya magari, au mbele ya majengo yenye ulinzi mkali. Wengine wamejitahidi kujifunza lugha mpya ili wawahubirie watu wa makabila fulani ambao sasa wanaishi katika eneo lao au makabila ambayo hayajahubiriwa kwa ukawaida. Kujifunza kuwasalimu watu hao katika lugha yao wenyewe kunaweza kusaidia kuonyesha unapendezwa sana na hali yao njema. Ikiwa hali zetu hazituruhusu kujifunza lugha nyingine, je, tunaweza kuwatia moyo wale wanaofanya hivyo? Bila shaka, haingefaa kuwavunja moyo au kutilia shaka nia yao ya kujitahidi kuwahubiria watu kutoka nchi nyingine. Uhai wa kila mtu ni wenye thamani machoni pa Mungu na tungependa kuwa na maoni kama yake.—Kol. 3:10, 11.

20 Pia, kuwa na maoni kama ya Mungu kuhusu watu kunatia ndani kuwahubiria wote, haidhuru hali zao. Huenda wengine hawana makao, ni wachafu, au wanaishi maisha yasiyo safi kiadili. Watu fulani wasipotutendea kwa fadhili, hatupaswi kuwa na maoni mabaya kuhusu taifa au kabila lao. Paulo alitendewa vibaya na watu wa jamii fulani, lakini hakuruhusu hilo limzuie asiwahubirie watu wa jamii hiyo. (Mdo. 14:5-7, 19-22) Aliamini kwamba watu mmoja-mmoja wangeitikia kwa uthamini.

21. Kuwa na maoni kama ya Yehova kuwahusu wengine kunaweza kukusaidia jinsi gani?

21 Sasa tunaona wazi zaidi kwamba tunahitaji kuwa na maoni yanayofaa—maoni ya Yehova—tunaposhughulika na ndugu katika kutaniko letu, undugu wetu wa kimataifa, na watu tunaowahubiria. Kadiri tunavyoiga maoni ya Yehova, ndivyo tutakavyozidi kuchangia amani na umoja. Na tutastahili zaidi kuwasaidia wengine wamthamini Yehova, Mungu ambaye “hajaonyesha upendeleo,” anayewapenda na kuwajali wote, “kwa maana wao wote ni kazi ya mikono yake.”—Ayu. 34:19.

Je, Unaweza Kujibu?

• Tunapaswa kuepuka kuwa na maoni gani kuwahusu ndugu zetu?

• Tunaweza kumwiga Yehova jinsi gani kuhusu namna tunavyowaona ndugu zetu?

• Umejifunza nini kuhusu maoni yetu kuelekea undugu wetu wa kimataifa?

• Tunaweza kuiga jinsi gani maoni ya Yehova kuhusu watu tunapokuwa katika huduma?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 26]

Unaweza kufanya nini ili uwafahamu watu wa tamaduni nyingine?

[Picha katika ukurasa wa 28]

Unaweza kufanya nini ili uwahubirie watu wengi zaidi habari njema?