Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kubali Maoni ya Wengine na Uwe Mwenye Usawaziko

Kubali Maoni ya Wengine na Uwe Mwenye Usawaziko

Kubali Maoni ya Wengine na Uwe Mwenye Usawaziko

“Endelea kuwakumbusha . . . wawe wenye usawaziko.”—TITO 3:1, 2.

1, 2. Maandiko yanasema nini kuhusu kuwa mwenye usawaziko, na kwa nini jambo hilo linafaa?

YEHOVA, Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo, ana hekima isiyo na kifani. Tukiwa viumbe wake, tunamtegemea ili atuongoze katika maisha yetu. (Zab. 48:14) Mwanafunzi Mkristo Yakobo anatuambia kwamba “hekima inayotoka juu kwanza kabisa ni safi kiadili, kisha yenye kufanya amani, yenye usawaziko [“yenye kukubali maoni ya wengine,” maelezo ya chini katika Reference Bible], tayari kutii, yenye kujaa rehema na matunda mema, haifanyi tofauti zenye ubaguzi, si ya kinafiki.”—Yak. 3:17.

2 Mtume Paulo anatuhimiza hivi: “Usawaziko wenu [“kukubali maoni ya wengine,” Kingdom Interlinear] na ujulikane kwa watu wote.” * (Flp. 4:5) Kristo Yesu ni Bwana na Kichwa cha kutaniko la Kikristo. (Efe. 5:23) Ni jambo la maana kama nini kwa kila mmoja wetu kutenda kwa usawaziko, kukubali mwongozo wa Kristo, na pia kuwa mwenye usawaziko anaposhughulika na wanadamu wengine!

3, 4. (a) Toa mfano unaoonyesha faida za kuwa wenye usawaziko. (b) Tutachunguza nini?

3 Tunafaidika tunapokuwa tayari kukubali maoni ya wengine kwa usawaziko. Kwa mfano: Baada ya njama ya ugaidi kugunduliwa nchini Uingereza, ilionekana kwamba wasafiri wengi walikuwa tayari kutii amri ya kutobeba vitu ambavyo hapo awali waliruhusiwa kubeba ndani ya ndege. Tunapoendesha gari, tunatambua umuhimu wa kuwa wenye usawaziko kuelekea madereva wengine, kama vile tunapoingia katika mizunguko ya barabara, ili kuhakikisha kwamba kila mtu yuko salama na magari yanasafiri kwa utaratibu.

4 Si rahisi kwa wengi wetu kuwa wenye usawaziko. Acheni tuchunguze mambo matatu yatakayotusaidia kuwa wenye usawaziko, yaani, nia yetu, mtazamo wetu kuelekea mamlaka, na kadiri tunavyopaswa kuwa wenye usawaziko.

Kwa Nini Uwe Mwenye Usawaziko?

5. Chini ya Sheria ya Musa, ni nini kingemchochea mtumwa kuendelea kukaa na bwana wake?

5 Mfano mmoja wa kabla ya Ukristo unakazia nia nzuri ya kuwa mwenye usawaziko. Chini ya Sheria ya Musa, Waebrania ambao walikuwa watumwa walipaswa kuwekwa huru katika mwaka wa saba wa utumwa wao au katika mwaka wa Yubile, mwaka ambao ungetangulia kati ya hiyo miwili. Lakini mtu angeweza kuamua kuendelea kuwa mtumwa. (Soma Kutoka 21:5, 6.) Ni nini kingemchochea kufanya uamuzi huo? Upendo ulimchochea mtumwa abaki katika hali hiyo, chini ya mamlaka ya bwana wake mwenye kujali.

6. Upendo unahusika jinsi gani katika kuwa wenye usawaziko?

6 Vivyo hivyo, kumpenda Yehova kunatuchochea kuweka maisha yetu wakfu kwake na kisha kuishi kulingana na wakfu wetu. (Rom. 14:7, 8) Mtume Yohana aliandika: “Kumpenda Mungu humaanisha hivi, kwamba tuzishike amri zake; na bado amri zake si mzigo mzito.” (1 Yoh. 5:3) Upendo huo hautafuti faida zake wenyewe. (1 Kor. 13:4, 5) Tunaposhughulika na wanadamu wengine, upendo kwa jirani unatuchochea kuwa wenye usawaziko na hivyo kutanguliza mahitaji yao. Badala ya kuruhusu uchoyo utuongoze, tunafikiria faida za wengine.—Flp. 2:2, 3.

7. Usawaziko unahusika namna gani katika huduma yetu?

7 Hatupaswi kuwakwaza wengine kwa usemi au matendo yetu. (Efe. 4:29) Kwa kweli, upendo utatuchochea kuepuka kufanya jambo lolote ambalo linaweza kuwazuia watu wa malezi na tamaduni mbalimbali wasifanye maendeleo na kumtumikia Yehova. Mara nyingi, hilo linahitaji tuwe wenye usawaziko. Kwa mfano, dada wamishonari waliozoea kujipodoa au kuvaa mtindo fulani wa mavazi hawasisitizi kwamba wanapaswa kuvaa hivyo katika maeneo ambako watu wanaweza kufikiri kwamba wana maadili mapotovu na hivyo kuwakwaza wengine.—1 Kor. 10:31-33.

8. Kumpenda Mungu kunaweza kutusaidia jinsi gani kujiendesha kama ‘walio wadogo zaidi’?

8 Kumpenda Yehova kunatusaidia kushinda kiburi. Baada ya wanafunzi kubishana kuhusu ni nani aliyekuwa mkubwa zaidi, Yesu alimsimamisha mtoto mchanga katikati yao. Aliwaambia hivi: “Yeyote yule anayempokea mtoto huyu mchanga kwa msingi wa jina langu ananipokea mimi pia, na yeyote anayenipokea, anampokea pia yule aliyenituma. Kwa maana anayejiendesha kama aliye mdogo zaidi kati yenu nyote ndiye aliye mkuu.” (Luka 9:48; Marko 9:36) Huenda ikawa vigumu sana kwa kila mmoja wetu kujiendesha kama “aliye mdogo zaidi.” Kutokamilika tulikorithi na mwelekeo wa kuwa na kiburi unaweza kutuchochea kutafuta umashuhuri, lakini unyenyekevu utatusaidia kuwa wenye usawaziko.—Rom. 12:10.

9. Ili tuwe wenye usawaziko, tunapaswa kutambua nini?

9 Ili tuwe wenye usawaziko, tunapaswa kutambua mamlaka ya wale waliowekwa rasmi na Mungu. Wakristo wote wa kweli wanatambua umuhimu wa kanuni ya ukichwa. Mtume Paulo aliwaonyesha Wakorintho kanuni hiyo waziwazi: “Nataka mjue kwamba kichwa cha kila mwanamume ni Kristo; nacho kichwa cha mwanamke ni mwanamume; nacho kichwa cha Kristo ni Mungu.”—1 Kor. 11:3.

10. Kukubali mamlaka ya Yehova kunaonyesha nini?

10 Kukubali mamlaka ya Mungu kunaonyesha kwamba tunamtegemea na kumtumaini akiwa Baba yetu mwenye upendo. Anajua yote yanayotukia na hivyo anaweza kututhawabisha. Kujua hivyo kutatusaidia kuwa wenye usawaziko wengine wanapokosa kututendea kwa heshima au wanapokasirika na kuwaka kwa ghadhabu. Paulo aliandika: “Ikiwezekana, kwa kadiri inavyowategemea ninyi, iweni wenye kufanya amani na watu wote.” Paulo alikazia shauri hilo kwa kutoa mwongozo huu: “Wapendwa, msijilipizie kisasi wenyewe bali iachieni nafasi ghadhabu; kwa maana imeandikwa: ‘Kisasi ni changu; mimi nitalipa, asema Yehova.’”—Rom. 12:18, 19.

11. Tunaweza kuonyesha jinsi gani kwamba tunakubali ukichwa wa Kristo?

11 Tunapaswa pia kutambua mamlaka ya Mungu katika kutaniko la Kikristo. Ufunuo sura ya 1 inaonyesha Kristo Yesu akiwa na “nyota” za kutaniko katika mkono wake wa kuume. (Ufu. 1:16, 20) Kwa ujumla, “nyota” hizo zinawakilisha mabaraza ya wazee, au waangalizi katika makutaniko. Waangalizi hao waliowekwa rasmi wanakubali uongozi wa Kristo na wanaiga njia yake yenye fadhili ya kushughulika na wengine. Wote katika kutaniko wanajitiisha chini ya mpango ambao Yesu aliweka wa “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” wa kuandaa chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa. (Mt. 24:45-47) Leo, kuwa tayari kujifunza na kutumia mambo tunayojifunza kunaonyesha kwamba sisi binafsi tunakubali ukichwa wa Kristo, jambo ambalo linaendeleza amani na umoja.—Rom. 14:13, 19.

Tunapaswa Kuwa Wenye Usawaziko kwa Kadiri Gani?

12. Kwa nini usawaziko una mipaka?

12 Hata hivyo, kuwa mwenye usawaziko hakumaanishi kulegeza msimamo wetu wa imani au kanuni za kimungu. Wakristo wa mapema walichukua msimamo gani walipoamriwa na viongozi wa kidini waache kufundisha kwa msingi wa jina la Yesu? Petro na mitume wengine walisema hivi kwa ujasiri: “Lazima tumtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.” (Mdo. 4:18-20; 5:28, 29) Vivyo hivyo leo, wenye mamlaka wa serikali wanapojaribu kutulazimisha tuache kuhubiri habari njema, hatuachi, ingawa huenda tukabadili mbinu zetu na kuhubiri kwa busara. Tukizuiwa tusihubiri nyumba kwa nyumba, huenda tukatafuta njia nyingine za kuwafikia wenye nyumba na hivyo kuendelea kufanya kazi tuliyopewa na Mungu. Vivyo hivyo, wakati “mamlaka zilizo kubwa” zinapopiga marufuku mikutano yetu, tunakutana kwa siri katika vikundi vidogo.—Rom. 13:1; Ebr. 10:24, 25.

13. Yesu alisema nini kuhusu kuwatii wenye mamlaka?

13 Katika Mahubiri yake ya Mlimani, Yesu alionyesha umuhimu wa kuwatii wenye mamlaka: “Ikiwa mtu anataka kwenda mahakamani pamoja nawe na kulichukua vazi lako la ndani, acha alichukue vazi lako la nje pia; na mtu fulani aliye na mamlaka akikulazimisha uingie katika utumishi wa kilometa moja, nenda pamoja naye kilometa mbili.” (Mt. 5:40, 41) * Kuwajali wengine na pia tamaa ya kutaka kuwasaidia inatuchochea kufanya mengi zaidi ya yale tunayoombwa tufanye.—1 Kor. 13:5; Tito 3:1, 2.

14. Kwa nini tunapaswa kukataa uasi-imani?

14 Ingawa tunatamani kuwa wenye usawaziko, hatupaswi kamwe kulegeza msimamo ili kuwapendeza waasi-imani. Msimamo wetu ulio wazi na thabiti ni muhimu ili kulinda usafi wa ile kweli na umoja wa kutaniko. Kuhusu “ndugu wa uwongo,” Paulo aliandika hivi: “Kwa hao sisi hatukuwaachia nafasi kwa kujitiisha, hapana, hata kwa saa moja, ili kweli ya habari njema iendelee kuwa pamoja nanyi.” (Gal. 2:4, 5) Uasi-imani unatokea mara chache, lakini Wakristo washikamanifu wanabaki imara kwa yale yaliyo sawa.

Waangalizi Wanahitaji Kuwa Wenye Usawaziko

15. Waangalizi Wakristo wanaweza jinsi gani kuwa wenye usawaziko wanapokutana?

15 Mojawapo ya sifa za kustahili za wale wanaowekwa rasmi kutumika wakiwa waangalizi ni kuwa mwenye usawaziko. Paulo aliandika: “Mwangalizi anapaswa kuwa . . . mwenye usawaziko,” au mwenye kukubali maoni ya wengine. (1 Tim. 3:2, 3) Hilo ni muhimu hasa wanaume waliowekwa rasmi wanapokutana ili kuzungumzia mambo yanayohusu kutaniko. Kabla ya kufikia uamuzi fulani, kila mzee ana uhuru wa kutoa maoni yake waziwazi, hata ingawa si lazima kila mzee atoe maoni. Wakati wa mazungumzo, mzee anaweza kubadili maoni anaposikia wengine wakitaja kanuni za Kimaandiko zinazohusika. Badala ya kupinga na kushikilia maoni yake, mzee mkomavu anakubali maoni ya wengine. Mwanzoni mwa mazungumzo, huenda kukawa na maoni yenye kutofautiana, lakini kufikiria mambo na kusali kunasaidia kudumisha umoja kati ya wazee wenye kiasi na usawaziko.—1 Kor. 1:10; Soma Waefeso 4:1-3.

16. Ni mtazamo gani ambao mwangalizi Mkristo anapaswa kuonyesha?

16 Katika utendaji wake wote, mzee Mkristo anapaswa kujitahidi kufuata utaratibu wa Kitheokrasi. Mtazamo huo unapaswa kuonekana wazi hata anapolichunga kundi, na unamsaidia kuwajali na kuwatendea wengine kwa upole. Petro aliandika hivi: “Lichungeni kundi la Mungu lililo chini ya uangalizi wenu, si kwa kulazimishwa, bali kwa kupenda; wala si kwa kupenda pato lisilo la haki, bali kwa hamu.”—1 Pet. 5:2.

17. Wote kutanikoni wanaweza kuonyesha jinsi gani mtazamo wenye usawaziko wanaposhughulika na wengine?

17 Washiriki waliozeeka wa kutaniko wanathamini msaada mkubwa wa vijana na wanawatendea kwa heshima. Vivyo hivyo, vijana wanawaheshimu wale waliozeeka ambao wana miaka mingi ya uzoefu katika utumishi wa Yehova. (1 Tim. 5:1, 2) Wazee Wakristo wanatafuta wanaume walio na sifa za kustahili wanaoweza kupewa madaraka fulani na kuwazoeza ili wasaidie kulitunza kundi la Mungu. (2 Tim. 2:1, 2) Kila Mkristo anapaswa kulithamini shauri hili la Paulo ambalo liliongozwa na roho: “Watiini wale wanaoongoza katikati yenu na mnyenyekee [mjitiishe], kwa maana wanaendelea kuzilinda nafsi zenu kama wale watakaotoa hesabu; ili wafanye hivyo kwa shangwe na si kwa kuugua, kwa maana kufanya hivyo kungewadhuru ninyi.”—Ebr. 13:17.

Uwe Mwenye Usawaziko Katika Familia

18. Kwa nini mtazamo wa usawaziko unafaa katika familia?

18 Mtazamo wa usawaziko unahitajiwa pia katika familia. (Soma Wakolosai 3:18-21.) Biblia inaonyesha wajibu wa washiriki mbalimbali wa familia ya Kikristo. Baba ni kichwa cha mke wake na ndiye hasa aliye na daraka la kuwaongoza watoto. Mke anapaswa kutambua mamlaka ya mwenzi wake, na watoto wanapaswa kujitahidi kuwa watiifu, jambo ambalo linampendeza vema Bwana wetu. Kila mshiriki wa familia anaweza kuchangia umoja na amani ya familia kwa kukubali maoni ya wengine kwa njia inayofaa na yenye usawaziko. Biblia ina mifano inayosaidia kuelewa jambo hilo.

19, 20. (a) Tofautisha mfano wa Eli na wa Yehova katika kuwa mwenye usawaziko. (b) Wazazi wanaweza kujifunza masomo gani kutokana na mifano hiyo?

19 Samweli alipokuwa mvulana tu, Eli alikuwa kuhani mkuu katika Israeli. Hata hivyo, Hofni na Finehasi, wana wa Eli, walikuwa “watu wasiofaa kitu” ambao “hawakumtambua Yehova.” Eli alisikia ripoti mbaya kuwahusu, kutia ndani habari za kwamba walikuwa wakifanya uasherati na wanawake waliokuwa wakitumika kwenye lango la hema la mkutano. Alifanya nini? Eli aliwaambia kwamba ikiwa walikuwa wakimtendea Yehova dhambi, hakuna mtu angesali kwa ajili yao. Lakini hakuwarekebisha wala kuwatia nidhamu. Kwa sababu hiyo, wana wa Eli waliendelea katika njia yao mbaya. Mwishowe, Yehova aliamua kwa haki kwamba walistahili adhabu ya kifo. Alipopata habari kwamba wamekufa, Eli mwenyewe alikufa. Hayo yalikuwa matokeo yenye kuhuzunisha kama nini! Kwa wazi, Eli alitenda isivyofaa kwa kuachilia matendo yao maovu na kuwaacha waendelee na mwenendo wao.—1 Sam. 2:12-17, 22-25, 34, 35; 4:17, 18.

20 Tofauti na hilo, fikiria jinsi Mungu alivyoshughulika na wanawe wa kimalaika. Nabii Mikaya aliona maono ya ajabu ya mkutano wa Yehova pamoja na malaika Wake. Yehova aliuliza ni malaika gani ambaye angemdanganya Mfalme Ahabu wa Israeli ili mfalme huyo mwovu aanguke. Yehova alisikiliza mapendekezo ya wanawe mbalimbali wa roho. Kisha malaika mmoja akasema kwamba angemdanganya. Yehova alimuuliza angemdanganya jinsi gani. Baada ya kutosheka na jibu lake, Yehova alimtuma malaika huyo afanye hivyo. (1 Fal. 22:19-23) Je, washirikiwa familia hawajifunzi kuwa wenye usawaziko kutokana na simulizi hilo? Ni vizuri mume na baba Mkristo atilie maanani maoni na mapendekezo ya mke na watoto wake. Kwa upande mwingine, wake na watoto wanapaswa kujua kwamba ikiwa wametoa maoni au mapendekezo, huenda wakahitaji kuwa wenye usawaziko ili kufuata mwongozo wa mume kwa sababu Maandiko yanampa mamlaka ya kuamua.

21. Tutachunguza nini katika habari inayofuata?

21 Tunathamini kama nini vikumbusho vya Yehova vyenye upendo na hekima kuhusu kuwa wenye usawaziko! (Zab. 119:99) Habari inayofuata itachunguza jinsi kukubali maoni ya wengine kwa usawaziko kunavyoweza kuchangia shangwe katika ndoa.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Mtume Paulo alitumia neno ambalo ni gumu kutafsiri kwa kutumia neno moja tu la Kiswahili. Kitabu kimoja kinasema hivi: “Usawaziko unatia ndani kuwa tayari kudhabihu haki zetu, kuwajali wengine, na kuwatendea kwa upole.” Hivyo, neno hilo linamaanisha kukubali maoni ya wengine, kutosisitiza sheria ifuatwe bila kunyumbulika au kudai haki zako.

^ fu. 13 Ona habari ‘Ukilazimishwa Uingie Katika Utumishi,’ katika Mnara wa Mlinzi la Februari 15, 2005 (15/2/2005), ukurasa wa 23-26.

Ungetoa Jibu Gani?

• Kukubali maoni ya wengine kunaleta matokeo gani mazuri?

• Waangalizi wanaweza kuonyesha jinsi gani mtazamo wa usawaziko?

• Kwa nini mtazamo wa usawaziko ni muhimu katika familia?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 4]

Wazee wanaiga njia ya fadhili ya Kristo ya kushughulika na wengine

[Picha katika ukurasa wa 6]

Katika mkutano wa wazee wa kutaniko, kufikiria, kusali, na kuwa na mtazamo wa usawaziko kunachangia umoja